Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tunzeni Akili Zenu Kwa Ukamili”

“Tunzeni Akili Zenu Kwa Ukamili”

“Tunzeni Akili Zenu Kwa Ukamili”

“Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—METHALI 14:15.

1, 2. (a) Tunajifunza nini kutokana na yaliyompata Loti huko Sodoma? (b) Maneno “tunzeni akili zenu” yanamaanisha nini?

ABRAHAMU alipompa Loti nafasi ya kwanza ya kuchagua nchi, Loti alivutiwa na eneo lenye maji mengi lililokuwa “kama bustani ya Yehova.” Huenda Loti aliona eneo hilo kuwa sehemu bora kabisa kwa ajili ya familia yake, kwa kuwa ‘alijichagulia Wilaya yote ya Yordani’ na kupiga kambi karibu na Sodoma. Hata hivyo, mambo ambayo Loti aliona kijuujuu yalimpumbaza, kwa kuwa karibu na eneo hilo ndiko walikoishi “watu wa Sodoma [ambao] walikuwa wabaya nao walikuwa wakimtendea Yehova dhambi nzito.” (Mwanzo 13:7-13) Muda si muda, Loti na familia yake walipata hasara kubwa sana. Hatimaye, hali ya maisha ya Loti na binti zake ilizorota sana hivi kwamba wakaishi pangoni. (Mwanzo 19:17, 23-26, 30) Hali ambazo Loti aliziona kuwa nzuri sana mwanzoni, zilibadilika kuwa tofauti kabisa.

2 Watumishi wa Mungu leo wanaweza kujifunza kutokana na simulizi hilo kumhusu Loti. Tunapokabili maamuzi, tunapaswa kuwa macho kuona hatari zinazoweza kutokea na kujihadhari tusidanganywe na mambo tunayoona kijuujuu. Ndiyo sababu Neno la Mungu linatuhimiza hivi: “Tunzeni akili zenu kwa ukamili.” (1 Petro 1:13) Katika mstari huo, neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “tunzeni akili zenu” linamaanisha “kuwa timamu katika akili.” Kulingana na msomi wa Biblia R.C.H. Lenski, utimamu huo wa akili ni “hali ya kutulia akilini daima ambayo hutuwezesha kupima na kuchanganua mambo vizuri na hivyo kufanya uamuzi unaofaa.” Hebu tuzungumzie hali fulani ambazo zinahitaji tuwe na utimamu wa akili.

Kufikiria Mradi wa Kibiashara

3. Kwa nini tunahitaji kuwa waangalifu mtu fulani anapotaka kutuingiza katika biashara fulani?

3 Tuseme mtu fulani anayeheshimika, kama vile mwabudu mwenzako wa Yehova, anataka kukuingiza katika biashara fulani. Anasadiki kwamba biashara hiyo itafanikiwa, naye anakutia moyo ufanye haraka ili usikose mafanikio hayo. Huenda ukaanza kuwazia jinsi wewe na familia yako mtakavyokuwa na maisha mazuri zaidi na kwamba biashara hiyo itakuwezesha uwe na wakati zaidi kwa ajili ya mambo ya kiroho. Hata hivyo, andiko la Methali 14:15 linatoa onyo hili: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” Kwa sababu ya msisimuko wa kuanzisha biashara, inaweza kuwa rahisi kupuuza uwezekano wa kupata hasara, hatari zinazohusika, na hali ya wakati ujao ya biashara hiyo. (Yakobo 4:13, 14) Katika hali kama hiyo, ni muhimu sana utunze akili zako kwa ukamili!

4. Tunaweza ‘kuzifikiriaje hatua zetu’ wakati mtu anapotuomba tujiunge naye katika biashara fulani?

4 Kabla ya kufanya uamuzi, mtu mwenye hekima huchunguza mambo kwa uangalifu wakati anapoombwa aingie katika biashara fulani. (Methali 21:5) Mara nyingi, kuchunguza mambo hufunua hatari zisizoonekana wazi. Fikiria hali hii: Mtu fulani anatafuta pesa ili aanzishe biashara, naye anakuahidi kwamba atakupa faida kubwa ukimkopesha pesa hizo. Huenda ahadi hiyo ikaonekana kuwa yenye kuvutia, lakini kuna hatari gani? Je, yule anayekopa pesa ameahidi kulipa pesa hizo hata biashara isipofaulu, au atalipa tu ikiwa biashara itafaulu? Kwa maneno mengine, je, unaweza kukubali kupoteza pesa zako biashara hiyo isipofaulu? Unaweza pia kuuliza hivi: “Kwa nini watu binafsi wanaombwa pesa? Je, benki zinaona kwamba huenda biashara hiyo haitafaulu?” Kufikiria hatari kwa uangalifu kutakusaidia kuchanganua mambo vizuri unapoombwa uingie katika biashara hiyo.—Methali 13:16; 22:3.

5. (a) Yeremia alichukua hatua gani ya hekima aliponunua shamba? (b) Kwa nini kuna faida kuandika mapatano yote ya kibiashara katika hati rasmi ya mapatano?

5 Nabii Yeremia aliponunua shamba kutoka kwa binamu yake, ambaye alikuwa mwabudu mwenzake wa Yehova, aliandika hati ya mapatano mbele ya mashahidi. (Yeremia 32:9-12) Leo, mtu mwenye hekima atahakikisha kwamba mapatano yote ya kibiashara anayofanya, kutia ndani yale anayofanya pamoja na watu wa ukoo na waamini wenzake, yameandikwa katika hati rasmi ya mapatano. * Kuwa na hati ya mapatano iliyoandikwa na kutayarishwa vizuri huzuia hali ya kutoelewana na hudumisha umoja. Kwa upande mwingine, nyakati nyingine watumishi wa Yehova hukosa kuelewana kuhusu mambo ya kibiashara hasa kwa sababu ya kutoandika hati ya mapatano. Kwa kusikitisha, hali hiyo inaweza kusababisha huzuni na chuki, na hata kudhoofisha hali ya kiroho.

6. Kwa nini tunahitaji kujihadhari na pupa?

6 Ni lazima pia tujihadhari na pupa. (Luka 12:15) Uwezekano wa kupata faida kubwa unaweza kumpofusha mtu asione hatari za biashara isiyofaa. Hata wengine ambao wamefurahia mapendeleo mazuri katika utumishi wa Yehova wamenaswa na mtego huo. Neno la Mungu linatuonya hivi: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa.” (Waebrania 13:5) Mkristo anapofikiria kuingia katika biashara fulani, inafaa ajiulize, ‘Je, ni lazima nijihusishe na biashara hii?’ Kuishi maisha rahisi ya kutanguliza ibada ya Yehova kutatulinda na “mambo mabaya ya namna zote.”—1 Timotheo 6:6-10.

Matatizo Ambayo Wakristo Waseja Hukabili

7. (a) Wakristo wengi waseja hukabili matatizo gani? (b) Uchaguzi wetu wa mwenzi wa ndoa unahusianaje na ushikamanifu wetu kwa Mungu?

7 Watumishi wengi wa Yehova wanatamani kufunga ndoa, lakini bado hawajapata mwenzi anayefaa. Katika nchi fulani, watu huchochewa sana na jamii yao wafunge ndoa. Lakini, huenda isiwe rahisi kumpata mtu ambaye ungependa kufunga ndoa naye kati ya waamini wenzako. (Methali 13:12) Hata hivyo, Wakristo wanatambua kwamba kutii amri ya Biblia ya kuoa au kuolewa “katika Bwana tu” huonyesha ushikamanifu wao kwa Yehova. (1 Wakorintho 7:39) Ni lazima Wakristo waseja watunze akili zao kwa ukamili ili wasimame imara dhidi ya mikazo na vishawishi wanavyokabili.

8. Msichana mmoja Mshulami alikabili mkazo gani, na wanawake Wakristo leo wanaweza kukabilije hali kama hiyo?

8 Katika Wimbo wa Sulemani, msichana mmoja wa mashambani wa hali ya chini anayeitwa Mshulami anamvutia mfalme. Ingawa msichana huyo tayari anampenda kijana mwingine, mfalme anajaribu kumvutia kwa kumwonyesha utajiri mwingi, umashuhuri wake, na kwa kutumia maneno matamu. (Wimbo wa Sulemani 1:9-11; 3:7-10; 6:8-10, 13) Ikiwa wewe ni mwanamke Mkristo, huenda mtu fulani akavutiwa nawe, ingawa wewe hufurahii jambo hilo. Mtu fulani kazini, labda mwenye cheo, anaweza kuanza kukusifu-sifu, kukufanyia mambo mazuri, na kutafuta njia za kuwa pamoja nawe. Jihadhari mtu anapokufanyia hivyo. Ingawa katika visa fulani huenda mtu anayefanya hivyo asiwe na nia ya kuanzisha uhusiano wa kimahaba au kufanya ukosefu wa adili, katika visa vingi wengi huwa na nia hiyo. Uwe “ukuta,” kama yule mwanamwali Mshulami. (Wimbo wa Sulemani 8:4, 10) Kataa katakata mtu fulani anapokuambia kwamba angependa kuwa na uhusiano wa kimahaba pamoja nawe ikiwa wewe hutaki. Kuanzia siku yako ya kwanza kazini, wajulishe wafanyakazi wenzako kwamba wewe ni Shahidi wa Yehova, na utumie kila nafasi kuwahubiria. Hilo litakulinda.

9. Kuna hatari gani za kuanzisha uhusiano kwenye Intaneti pamoja na mtu usiyemjua? (Ona pia sanduku kwenye ukurasa wa 25.)

9 Vituo vya Intaneti vinavyokusudiwa kuwasaidia waseja kupata mwenzi wa ndoa vinazidi kupendwa. Wengine huona vituo hivyo kuwa njia ya kuwajua watu ambao hawawezi kukutana nao. Hata hivyo, kuanzisha uhusiano pamoja na mtu usiyemjua ni hatari sana. Kwenye Intaneti, ni vigumu kujua mambo ya kweli na yasiyo ya kweli. (Zaburi 26:4) Wengine wanadai kuwa watumishi wa Yehova, kumbe sivyo. Isitoshe, watu wanapochumbiana kwa kutumia Intaneti wanaweza kusitawisha uhusiano wa karibu haraka, na hilo linaweza kumzuia mtu asifikiri vizuri. (Methali 28:26) Si jambo la hekima kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na mtu ambaye humjui vizuri, iwe ni kupitia Intaneti au kupitia njia nyingine.—1 Wakorintho 15:33.

10. Wakristo waseja wanaweza kutiwaje moyo na waamini wenzao?

10 Yehova “ni mwenye upendo mwororo sana” kwa watumishi wake. (Yakobo 5:11) Anajua kwamba nyakati nyingine Wakristo ambao ni waseja kwa sababu ya hali huvunjika moyo kutokana na matatizo ambayo wanakabili, naye anathamini ushikamanifu wao. Wengine wanaweza kuwatiaje moyo? Tunapaswa kuwapongeza kwa ukawaida kwa utii wao na roho yao ya kujidhabihu. (Waamuzi 11:39, 40) Pia, tunaweza kuwaalika tunapopangia pindi za kushirikiana na kujengana. Je, umefanya hivyo karibuni? Zaidi ya hayo, tunaweza kusali kwa ajili yao na kumwomba Yehova awasaidie kuendelea kuwa thabiti kiroho na kupata shangwe wanapomtumikia. Acheni tuonyeshe kwamba tunawathamini washikamanifu hao kama Yehova anavyofanya, kwa kuwajali kikweli.—Zaburi 37:28.

Kushughulikia Matatizo ya Afya

11. Ni hali gani ngumu zinazosababishwa na matatizo makubwa ya afya?

11 Inasikitisha sana wakati sisi au wapendwa wetu wanapokuwa wagonjwa sana! (Isaya 38:1-3) Ingawa sisi hutafuta matibabu yanayofaa, ni muhimu tushikamane na kanuni za Biblia. Kwa mfano, Wakristo hutii amri ya Biblia ya kujiepusha na damu, nao huepuka njia za kupima au kutibu magonjwa ambazo zinahusisha kuwasiliana na pepo. (Matendo 15:28, 29; Wagalatia 5:19-21) Hata hivyo, wale ambao hawajui mambo ya tiba wanaweza kutatizika au hata kuogopa kuchanganua matibabu mbalimbali. Ni nini kinachoweza kutusaidia kutunza akili zetu kwa ukamili?

12. Mkristo anaweza kudumishaje usawaziko anapofikiria matibabu mbalimbali?

12 “Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake” kwa kufanya utafiti katika Biblia na vichapo vya Kikristo. (Methali 14:15) Katika sehemu za dunia ambako hakuna madaktari wengi au hospitali nyingi, huenda matibabu yanayopatikana ni yale ya kienyeji tu, ambayo yanahusisha kutumia mitishamba. Ikiwa tunafikiria kupata matibabu hayo, tunaweza kupata habari zitakazotusaidia katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1987, ukurasa wa 26-29. Gazeti hilo linatuonyesha hatari tunazoweza kukabili. Kwa mfano, huenda tukahitaji kujua mambo haya: Je, daktari huyo wa kienyeji huwasiliana na pepo? Je, matibabu hayo yanategemea imani ya kwamba magonjwa na kifo husababishwa kwa sababu miungu (au roho za mababu waliokufa) imeudhika au husababishwa na maadui wanaotumia uchawi? Je, dhabihu, nyimbo za uchawi, au desturi nyingine za kuwasiliana na pepo hutumiwa wakati wa kutengeneza au kutumia dawa? (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Utafiti huo utatusaidia kutii shauri hili lililoandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu: “Hakikisheni mambo yote; shikeni sana yaliyo mazuri.” * (1 Wathesalonike 5:21) Tukifanya hivyo, tutakuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu matibabu.

13, 14. (a) Tunaweza kuonyeshaje usawaziko tunapotunza afya yetu ya kimwili? (b) Kwa nini usawaziko unahitajiwa tunapozungumza na wengine kuhusu mambo ya afya na matibabu?

13 Usawaziko unahitajiwa katika mambo yote maishani, kutia ndani kutunza afya yetu. (Wafilipi 4:5) Kutunza afya kwa usawaziko kunaonyesha kwamba tunathamini zawadi ya uhai yenye thamani. Tunapopata matatizo ya afya, inafaa tuyashughulikie. Hata hivyo, hatuwezi kuwa na afya kamilifu hadi wakati wa Mungu ufike wa “kuponya mataifa.” (Ufunuo 22:1, 2) Tunapaswa kujihadhari tusije tukajishughulisha sana na afya yetu ya kimwili na kupuuza mahitaji yetu ya kiroho ambayo ndiyo ya maana zaidi.—Mathayo 5:3; Wafilipi 1:10.

14 Pia, tunahitaji kuwa wenye usawaziko tunapozungumza na wengine kuhusu mambo ya afya na matibabu. Hatupaswi kuzungumzia sana mambo hayo tunapokutana kwa ajili ya ushirika wa kiroho kwenye mikutano na makusanyiko ya Kikristo. Isitoshe, mara nyingi maamuzi kuhusu matibabu huhusiana na kanuni za Biblia, dhamiri ya mtu, na uhusiano wake pamoja na Yehova. Hivyo, si jambo la upendo kusisitiza mwamini mwenzetu afuate maoni yetu au kumshurutisha apuuze dhamiri yake. Ingawa Wakristo wakomavu katika kutaniko wanaweza kuombwa mashauri, ni lazima kila Mkristo ‘aubebe mzigo wake mwenyewe’ kulingana na maamuzi anayofanya, na “kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”—Wagalatia 6:5; Waroma 14:12, 22, 23.

Tunapofadhaika

15. Tunaweza kuathiriwaje na hali zenye kufadhaisha?

15 Hali zenye kufadhaisha zinaweza kuwafanya hata watumishi washikamanifu wa Yehova kusema au kutenda bila hekima. (Mhubiri 7:7) Ayubu alipokabili jaribu kali, alikosa usawaziko na alihitaji kurekebishwa. (Ayubu 35:2, 3; 40:6-8) Ingawa “Musa alikuwa mpole zaidi kuliko watu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi,” wakati fulani alikasirika na kusema bila kufikiri. (Hesabu 12:3; 20:7-12; Zaburi 106:32, 33) Daudi alijizuia sana ili asimuue Mfalme Sauli, lakini wakati Nabali alipomtukana na kuwatusi watu wake, Daudi alipandwa na hasira na akakosa ufahamu. Daudi alianza kufikiri vizuri tena wakati Abigaili alipoingilia kati, naye akaponea chupuchupu kufanya kosa ambalo lingesababisha msiba.—1 Samweli 24:2-7; 25:9-13, 32, 33.

16. Ni nini kinachoweza kutusaidia tuepuke kutenda haraka bila kufikiri?

16 Sisi pia tunaweza kukabili hali zenye kufadhaisha ambazo zinaweza kutufanya tutende bila kufikiri. Kufikiria kwa makini maoni ya wengine, kama vile Daudi alivyofanya, kunaweza kutusaidia tuepuke kutenda haraka bila kufikiri na kutumbukia katika dhambi. (Methali 19:2) Isitoshe, Neno la Mungu linatushauri hivi: “Fadhaikeni, lakini msitende dhambi. Semeni moyoni mwenu, kitandani mwenu, na kunyamaza.” (Zaburi 4:4) Inapowezekana, ni jambo la hekima kungoja hadi tunapotulia kabla ya kuchukua hatua au kufanya maamuzi. (Methali 14:17, 29) Tunaweza kusali kwa Yehova kwa bidii, “na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo [yetu] na nguvu [zetu] za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Utulivu huo kutoka kwa Mungu utatusaidia kufikiri vizuri na kutunza akili zetu kwa ukamili.

17. Kwa nini tunahitaji kumtegemea Yehova ili tutunze akili zetu kwa ukamili?

17 Licha ya jitihada zetu nyingi za kutenda kwa hekima na kuepuka hatari, sote hukosea. (Yakobo 3:2) Huenda tuko karibu kujikwaa vibaya bila sisi kujua. (Zaburi 19:12, 13) Isitoshe, kwa kuwa sisi ni wanadamu, hatuna uwezo wala haki ya kuongoza hatua zetu bila msaada wa Yehova. (Yeremia 10:23) Tunashukuru sana kwamba anatuhakikishia hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” (Zaburi 32:8) Naam, kwa msaada wa Yehova, tunaweza kutunza akili zetu kwa ukamili.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kwa habari zaidi kuhusu kuandika hati ya mapatano ya kibiashara, ona magazeti ya Mnara wa Mlinzi ya Agosti 1, 1997, ukurasa wa 30-31; Novemba 15, 1986, ukurasa wa 16-17; na gazeti la Amkeni! la Agosti 8, 1984, ukurasa wa 13-15, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 12 Kufanya hivyo kutawasaidia hata wale wanaofikiria matibabu mengine yenye kutiliwa shaka.

Ungejibuje?

Tunaweza kutunzaje akili zetu

• tunapoahidiwa biashara fulani?

• tunapotafuta mwenzi wa ndoa?

• tunapokabili matatizo ya afya?

• tunapofadhaika?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 25]

Je, Unaweza Kuiamini?

Tahadhari zifuatazo hutolewa kwenye vituo vya Intaneti vilivyokusudiwa kuwasaidia waseja wapate mwenzi wa ndoa:

“Licha ya jitihada zetu, hatuwezi kuhakikisha utambulisho wa kweli wa mtu.”

“Hatuwezi kuhakikisha kwamba habari zote zinazotolewa kupitia huduma hii ni sahihi, kamili, au zenye faida.”

“Maoni, mashauri, taarifa, ahadi, au habari nyingine zozote zinazopatikana kupitia huduma [hii] zimetayarishwa na watu walioziandika . . . na huenda hazitegemeki.”

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake”

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Wanawake Wakristo wanaweza kumwigaje mwanamwali Mshulami?

[Picha katika ukurasa wa 26]

“Hakikisheni mambo yote; shikeni sana yaliyo mazuri”