Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kifo Kinaogopesha!

Kifo Kinaogopesha!

Kifo Kinaogopesha!

“KUANZIA wakati mwanadamu anapozaliwa kuna uwezekano wa kwamba anaweza kufa wakati wowote,” akaandika mwanahistoria Mwingereza, Arnold Toynbee. Aliongeza hivi: “Ni wazi kwamba kila mtu atakufa mwishowe.” Kifo huleta huzuni nyingi sana wakati mtu wa familia tunayempenda sana au rafiki wa karibu anapokufa!

Kifo kimewaogopesha wanadamu kwa maelfu ya miaka. Sisi huwa hoi mpendwa wetu anapokufa. Isitoshe, watu wote hupatwa na huzuni inayosababishwa na kifo. Hakuna mtu anayeweza kuepuka kifo. “Hata iwe tuna elimu au hatuna, huzuni hutufanya tuwe kama watoto wadogo na hututatanisha. Hata wenye hekima hushindwa la kufanya.” Ndivyo alivyoandika mwandishi wa karne ya 19. Kifo hutufanya tuwe kama watoto wadogo walio hoi ambao hawana uwezo wa kubadili mambo. Hasara inayosababishwa na kifo haiwezi kuondolewa na mali wala mamlaka. Wenye hekima na wenye akili hawawezi kufanya lolote. Wote hulia, wawe wenye nguvu au dhaifu.

Mfalme Daudi wa Israeli la kale alihisi hivyo wakati Absalomu mwana wake alipokufa. Alipopata habari kwamba mwana wake amekufa, mfalme alianza kulia na kusema hivi: “Mwanangu Absalomu, mwanangu, mwanangu Absalomu! Laiti mimi mwenyewe ningekufa badala yako, Absalomu mwanangu, mwanangu!” (2 Samweli 18:33) Mfalme huyo mwenye nguvu aliyekuwa ameshinda maadui wenye nguvu alijihisi hoi na kutamani kwamba ni afadhali yeye mwenyewe angeshindwa na ‘adui wa mwisho, kifo,’ badala ya mwana wake.—1 Wakorintho 15:26.

Je, kuna suluhisho la kifo? Ikiwa lipo, wafu wana tumaini gani? Je, tutaweza kuwaona tena wapendwa wetu? Makala inayofuata inatoa majibu ya Kimaandiko kwa maswali hayo.