Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukombolewa kwa “Damu Yenye Thamani”

Kukombolewa kwa “Damu Yenye Thamani”

“Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala Kuliko Wanadamu”

Kukombolewa kwa “Damu Yenye Thamani”

YEHOVA alionyesha upendo mkubwa sana kwa kumtuma Mwana wake wa pekee ili atoe uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kuwa fidia. Tukiwa wanadamu wenye dhambi, tunahitaji ukombozi wa namna hiyo kwa kuwa hakuna mwanadamu asiye mkamilifu “anayeweza kumkomboa hata ndugu, wala kumpa Mungu fidia kwa ajili yake . . . kwamba yeye aendelee kuishi milele.” (Zaburi 49:6-9) Tunashukuru sana kwamba Mungu ‘alimtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele’!—Yohana 3:16.

Fidia inatukomboaje? Acheni tuzungumzie mambo manne ambayo yanaonyesha jinsi ambavyo tunapata uhuru kwa sababu ya tendo hilo kubwa la upendo wa Yehova Mungu.

Kukombolewa kwa Fidia

Kwanza, dhabihu ya Yesu inaweza kutukomboa kutokana na dhambi tuliyorithi. Sote tunazaliwa katika dhambi. Naam, sisi ni wenye dhambi hata kabla hatujaweza kuvunja sheria ya Yehova. Jinsi gani? Andiko la Waroma 5:12 linasema: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.” Tukiwa watoto wa Adamu aliyetenda dhambi, tumerithi hali yake ya kutokamilika. Hata hivyo, kulipwa kwa fidia kumetuwezesha kuwekwa huru kutokana na utumwa wa dhambi tuliyorithi. (Waroma 5:16) Yesu ‘alionja kifo kwa ajili ya kila mwanadamu’ na kuchukua matokeo ya dhambi kwa niaba ya wazao wa Adamu.—Waebrania 2:9; 2 Wakorintho 5:21; 1 Petro 2:24.

Pili, fidia inaweza kutuweka huru kutokana na madhara ya dhambi. “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Adhabu ya dhambi ni kifo. Kupitia dhabihu ya Mwana wa Mungu, wanadamu watiifu wanaweza kupata uzima wa milele. Kwa kweli, “yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele; yule asiyemtii Mwana hataona uzima.”—Yohana 3:36.

Ona kwamba tunaweza kukombolewa kutokana na madhara ya dhambi ikiwa tu tunamwamini Mwana wa Mungu. Hiyo inatia ndani kufanya marekebisho maishani mwetu na kuyapatanisha na mapenzi ya Mungu. Tunapaswa kukataa mwenendo wowote mbaya ambao huenda tumekuwa nao, kisha tuchukue hatua ya kufanya mambo yanayompendeza Mungu. Mtume Petro alisema kwamba tunahitaji ‘kutubu na kugeuka ili dhambi zetu zipate kufutwa.’—Matendo 3:19.

Tatu, dhabihu ambayo Yesu alitoa inatuweka huru kutokana na dhamiri yenye hatia. Wote wanaojiweka wakfu kwa Yehova na kuwa wanafunzi waliobatizwa wa Mwana wake hupata faraja. (Mathayo 11:28-30) Licha ya kutokamilika kwetu, tunapata shangwe nyingi tunapomtumikia Mungu tukiwa na dhamiri safi. (1 Timotheo 3:9; 1 Petro 3:21) Kwa kutubu na kuacha dhambi zetu, tunaonyeshwa rehema na tunaacha kusumbuliwa na dhamiri.—Methali 28:13.

Fidia Inatoa Msaada na Tumaini

Hatimaye, imani katika fidia hutuwezesha tuache kuwa na wasiwasi kuhusu msimamo wetu mbele za Mungu. Mtume Yohana aliandika hivi: “Yeyote akitenda dhambi, tuna msaidizi kwa Baba, Yesu Kristo.” (1 Yohana 2:1) Kuhusiana na sehemu ya Yesu akiwa msaidiaji, mtume Paulo aliandika hivi: “Yeye anaweza pia kuwaokoa kwa ukamili wale wanaomkaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu yeye yuko hai sikuzote ili kuwaombea.” (Waebrania 7:25) Maadamu tuna doa la dhambi, tunahitaji huduma za Kuhani Mkuu Yesu Kristo ili atusaidie kuwa na msimamo mzuri mbele za Mungu. Yesu alitendaje kama kuhani mkuu kwa niaba yetu?

Siku 40 baada ya kufufuliwa mwaka wa 33 W.K., Yesu alipaa mbinguni ambapo aliwasilisha thamani ya ‘damu yake yenye thamani’ kwa Mungu. Kwa hiyo, karibuni Yesu atawaweka huru wanadamu watiifu kutokana na dhambi na kifo. * (1 Petro 1:18, 19) Basi, je, hukubali kwamba tunapaswa kumpenda na kumtii Yesu Kristo?

Isitoshe, tunapaswa kumpenda na kumtii Yehova Mungu. Kwa upendo alifanya iwezekane ‘tuachiliwe huru kupitia fidia.’ (1 Wakorintho 1:30) Yeye ndiye ametupa uhai tulio nao sasa na pia tumaini la kupata uzima wa milele. Kwa hiyo, tuna kila sababu ya ‘kumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’—Matendo 5:29.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Ona Kalenda ya Mashahidi wa Yehova 2006, Machi/Aprili.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

JE, ULIJUA?

• Yesu alipaa mbinguni kutoka Mlima wa Mizeituni.—Matendo 1:9, 12.

• Ni mitume waaminifu tu wa Yesu ndio waliomwona akipaa.—Matendo 1:2, 11-13.