Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tukio la Mfano” Ambalo Ni Muhimu Kwetu

“Tukio la Mfano” Ambalo Ni Muhimu Kwetu

“Tukio la Mfano” Ambalo Ni Muhimu Kwetu

INGEKUWA vigumu kama nini kutambua maana kamili ya masimulizi fulani katika Biblia ikiwa hayangefafanuliwa katika sehemu nyingine za Biblia! Masimulizi ya kihistoria katika Neno la Mungu yanaweza kueleweka kijuu-juu tu. Lakini baadhi ya masimulizi hayo yana kweli nzito ambazo kwa kawaida hazionekani wazi unaposoma mara ya kwanza. Mfano mmoja ni simulizi la wanawake wawili katika familia ya mzee wa ukoo Abrahamu. Mtume Paulo aliliita simulizi hilo “tukio la mfano.”—Wagalatia 4:24.

Tunapaswa kupendezwa na tukio hilo kwa sababu mambo ambayo linawakilisha yana umuhimu mkubwa kwa wote wanaotamani kupata baraka za Yehova Mungu. Kabla ya kuchunguza kwa nini mambo yako hivyo, acheni tuone hali zilizomchochea Paulo afunue maana ya tukio hilo.

Kulikuwa na tatizo fulani miongoni mwa Wakristo wa karne ya kwanza huko Galatia. Baadhi yao walikuwa ‘wanashika kwa uangalifu mwingi siku na miezi na majira na miaka,’ yaani, mambo yaliyoamuriwa na Sheria ya Musa. Watu hao walidai kwamba waamini walipaswa kutii Sheria hiyo ili kupata kibali cha Mungu. (Wagalatia 4:10; 5:2, 3) Hata hivyo, Paulo alijua kwamba Wakristo hawakuhitaji kufuata sherehe kama hizo. Ili kuthibitisha hilo, alizungumzia simulizi lililojulikana na wote waliokuwa na malezi ya Kiyahudi.

Paulo aliwakumbusha Wagalatia kwamba Abrahamu, baba ya taifa la Wayahudi, aliwazaa Ishmaeli na Isaka. Ishmaeli alizaliwa na msichana mjakazi Hagari, na Isaka akazaliwa na mwanamke huru Sara. Bila shaka, wale waliokuwa wakiwahimiza wengine huko Galatia kutii Sheria ya Musa, walifahamu simulizi kuhusu jinsi Sara alivyokuwa tasa hapo mwanzoni na jinsi alivyompa Abrahamu mjakazi wake Hagari ili amzalie mtoto. Yaelekea walijua kwamba baada ya kupata mimba ya Ishmaeli, Hagari alianza kumdharau bimkubwa wake, Sara. Hata hivyo, kulingana na ahadi ya Mungu, mwishowe katika uzee wake Sara alimzaa Isaka. Baadaye, Abrahamu alimfukuza Hagari na Ishmaeli kwa sababu Ishmaeli alikuwa akimtesa Isaka.—Mwanzo 16:1-4; 17:15-17; 21:1-14; Wagalatia 4:22, 23.

Wanawake Wawili, Maagano Mawili

Paulo alifafanua maana ya sehemu mbalimbali za ‘tukio hilo la mfano.’ Aliandika hivi: “Wanawake hawa wanamaanisha maagano mawili, moja kutoka Mlima Sinai, ambalo huzaa watoto kwa ajili ya utumwa, na ambalo ni Hagari. . . . Naye analingana na Yerusalemu la leo, kwa maana liko katika utumwa pamoja na watoto wake.” (Wagalatia 4:24, 25) Hagari aliwakilisha Israeli halisi, ambalo jiji lake kuu lilikuwa Yerusalemu. Taifa la Wayahudi liliunganishwa na Yehova kupitia agano la Sheria lililoanzishwa kwenye Mlima Sinai. Chini ya agano la Sheria, mara kwa mara Waisraeli walikumbushwa kwamba walikuwa watumwa wa dhambi na kwamba walihitaji kukombolewa.—Yeremia 31:31, 32; Waroma 7:14-24.

Hivyo basi, “mwanamke huru” Sara na mwana wake, Isaka, waliwakilisha nani? Paulo alionyesha kwamba Sara, “mwanamke tasa,” alifananisha mke wa Mungu, sehemu ya kimbingu ya tengenezo lake. Mwanamke huyo wa kimbingu alikuwa tasa katika maana ya kwamba kabla ya Yesu kuja duniani, mwanamke huyo hakuwa na “watoto” wa kidunia waliotiwa mafuta kwa roho. (Wagalatia 4:27; Isaya 54:1-6) Hata hivyo, kwenye Pentekoste 33 W.K., roho takatifu ilimiminwa juu ya kikundi cha wanaume na wanawake ambao walikuwa wamezaliwa mara ya pili wakiwa watoto wa mwanamke huyo wa kimbingu. Watoto hao waliotokezwa na tengenezo hilo walifanywa kuwa wana wa Mungu na warithi pamoja na Kristo Yesu chini ya uhusiano wa agano jipya. (Waroma 8:15-17) Mtume Paulo, akiwa mmoja wa watoto hao, aliandika hivi: “Yerusalemu la juu liko huru, nalo ni mama yetu.”—Wagalatia 4:26.

Watoto wa Wanawake Hao

Kulingana na simulizi la Biblia, Ishmaeli alimtesa Isaka. Vivyo hivyo, katika karne ya kwanza W.K., watoto wa Yerusalemu lililokuwa katika utumwa waliwadhihaki na kuwatesa watoto wa Yerusalemu la juu. Paulo alifafanua hivi: “Kama ilivyokuwa wakati huo, yule aliyezaliwa katika namna ya mwili [Ishmaeli] alianza kumtesa yule aliyezaliwa katika namna ya roho [Isaka], ndivyo ilivyo pia na sasa.” (Wagalatia 4:29) Yesu Kristo alipokuja duniani na kuanza kutangaza Ufalme, viongozi wa dini ya Kiyahudi walitenda kama vile Ishmaeli mwana wa Hagari alivyomtendea mrithi halisi wa Abrahamu, yaani, Isaka. Walimdhihaki na kumtesa Yesu Kristo, na yaelekea waliona kwamba wao ndio warithi halisi wa Abrahamu na kwamba Yesu ni mrithi bandia.

Yesu alisema hivi muda mfupi kabla ya kuuawa na viongozi wa taifa la asili la Israeli: “Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na ambaye huwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwake,—ni mara ngapi nilitaka kuwakusanya watoto wako, kama vile kuku anavyokusanya vifaranga vyake chini ya mabawa yake! Lakini hamkutaka. Tazama! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.”—Mathayo 23:37, 38.

Masimulizi yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu kuhusu matukio ya karne ya kwanza yanaonyesha kwamba taifa la kimwili lililowakilishwa na Hagari halikutokeza wana ambao wangekuwa warithi pamoja na Yesu kwa msingi wa ukoo. Wayahudi ambao waliamini kwa kiburi kwamba walikuwa na haki ya urithi huo kwa msingi wa ukoo wao walitupiliwa mbali, na wakakataliwa na Yehova. Bila shaka, baadhi ya Waisraeli wa asili walipata kuwa warithi pamoja na Kristo. Hata hivyo, walipewa pendeleo hilo kwa msingi wa imani yao katika Yesu na si kwa sababu ya ukoo wao.

Baadhi ya wale ambao wangekuwa warithi pamoja na Kristo walionekana wazi kwenye Pentekoste 33 W.K. Wakati ulivyoendelea kusonga, Yehova aliwatia wengine mafuta ili wawe wana wa Yerusalemu la juu.

Kusudi la Paulo la kufafanua ‘tukio hilo la mfano’ lilikuwa kuonyesha ubora wa agano jipya juu ya agano la Sheria ambalo lilipatanishwa na Musa. Hakuna mtu ambaye angepata kibali cha Mungu kupitia matendo ya Sheria ya Musa, kwa kuwa wanadamu wote si wakamilifu, na Sheria ilikazia tu kwamba walikuwa watumwa wa dhambi. Hata hivyo, kama Paulo alivyosema, Yesu alikuja ili “awaachilie huru kwa kuwanunua wale walio chini ya sheria.” (Wagalatia 4:4, 5) Hivyo, imani katika thamani ya dhabihu ya Kristo ilileta uhuru kutokana na hukumu ya Sheria.—Wagalatia 5:1-6.

Umuhimu wa Tukio Hilo Kwetu

Kwa nini tupendezwe na jinsi Paulo alivyofafanua tukio hilo kupitia uongozi wa roho ya Mungu? Sababu moja ni kwamba tukio hilo linatusaidia kufahamu maana ya Kimaandiko ambayo hatungeelewa iwapo halingefafanuliwa. Ufafanuzi huo unaimarisha uhakika wetu kwamba Biblia ina umoja na inapatana.—1 Wathesalonike 2:13.

Isitoshe, mambo yanayofananishwa na tukio hilo ni muhimu kwa ajili ya furaha yetu ya wakati ujao. Ikiwa wana wa Yerusalemu la juu hawangetokezwa, tungeendelea tu kuwa katika utumwa wa dhambi na kifo. Hata hivyo, kupitia usimamizi wenye upendo wa Kristo na warithi wenzake wa ahadi ya Mungu kwa Abrahamu, “mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki.” (Mwanzo 22:18) Hilo litatukia wakati wanadamu watakapowekwa huru kabisa kutokana na matokeo ya dhambi, kutokamilika, huzuni, na kifo. (Isaya 25:8, 9) Lo! Huo utakuwa wakati mzuri!

[Picha katika ukurasa wa 11]

Agano la Sheria lilianzishwa kwenye Mlima Sinai

[Picha zimetolewa na]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

[Picha katika ukurasa wa 12]

“Tukio la mfano” linalotajwa na mtume Paulo linamaanisha nini?