Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ayubu

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ayubu

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ayubu

MZEE wa ukoo Ayubu aliishi katika nchi ya Usi, ambayo sasa iko Arabia. Wakati huo, Waisraeli wengi walikuwa wakiishi Misri. Ingawa hakuwa Mwisraeli, Ayubu alikuwa mwabudu wa Yehova Mungu. Biblia inasema hivi kumhusu: “Hakuna yeyote aliye kama yeye duniani, mtu asiye na lawama na mnyoofu, mwenye kumwogopa Mungu na kujiepusha na ubaya.” (Ayubu 1:8) Hicho kilikuwa kipindi kati ya siku za Yosefu mwana wa Yakobo na siku za nabii Musa, ambao walikuwa watumishi wa Yehova wenye sifa nzuri.

Musa, anayedhaniwa kuwa ndiye aliyeandika kitabu cha Ayubu, huenda alipata habari kumhusu Ayubu alipokuwa huko Midiani kwa muda wa miaka 40. Midiani iko karibu na nchi ya Usi. Yaelekea Musa alipata habari kuhusu miaka ya mwisho-mwisho ya maisha ya Ayubu wakati Waisraeli walipokuwa karibu na Usi, mwishoni mwa miaka 40 ya safari yao nyikani. * Mambo yaliyompata Ayubu yanaelezwa vizuri sana katika kitabu cha Ayubu hivi kwamba masimulizi hayo yanatajwa kuwa uandishi bora. Hata hivyo, zaidi ya yote simulizi hilo linajibu maswali haya: Kwa nini watu wema huteseka? Kwa nini Yehova anaruhusu uovu? Je, wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kudumisha utimilifu wao kwa Mungu? Ujumbe wa kitabu cha Ayubu ni sehemu ya Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho na uko hai na una nguvu hata leo.—Waebrania 4:12.

“NA IANGAMIE ILE SIKU NILIYOZALIWA”

(Ayubu 1:1–3:26)

Siku moja Shetani alitilia shaka utimilifu wa Ayubu mbele za Mungu. Yehova alikubali madai hayo naye akamruhusu Shetani alete mfululizo wa misiba juu ya Ayubu. Hata hivyo, Ayubu alikataa ‘kumlaani Mungu.’—Ayubu 2:9.

Marafiki watatu wa Ayubu walikuja “kumsikitikia.” (Ayubu 2:11) Walikaa pamoja naye bila kusema neno lolote hadi Ayubu alipokatiza kimya hicho kwa kusema: “Na iangamie ile siku niliyozaliwa.” (Ayubu 3:3) Alitamani kuwa “kama watoto ambao hawajaona nuru,” au kama watoto ambao hufa kabla ya kuzaliwa.—Ayubu 3:11, 16.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:4—Je, watoto wa Ayubu walisherehekea siku ya kuzaliwa? La. Maneno ya lugha ya awali kuhusu “siku” na “sikukuu ya kuzaliwa” yanatofautiana, kila moja likiwa na maana yake. (Mwanzo 40:20) Kwenye Ayubu 1:4, neno “siku” linatumiwa ili kuonyesha kipindi cha wakati tangu kuchomoza kwa jua hadi jua kutua. Yaonekana kwamba wana saba wa Ayubu walifanya karamu ya familia kwa siku saba mara moja kwa mwaka. Kila mwana alikuwa na “siku yake mwenyewe” ya kuwakaribisha ndugu na dada zake nyumbani kwake kwa ajili ya karamu.

1:6; 2:1—Ni nani aliyeruhusiwa kuingia mbele za Yehova? Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, yule Neno; malaika waaminifu; na ‘wana wa Mungu’ wa kimalaika walioasi, kutia ndani Shetani Ibilisi, walikuwa kati ya wale waliosimama mbele za Yehova. (Yohana 1:1, 18) Wakati huo, Shetani na roho wake waovu walikuwa bado hawajafukuzwa mbinguni. Walifukuzwa muda mfupi baada ya kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu mwaka wa 1914. (Ufunuo 12:1-12) Kwa kuwaruhusu waingie mbele zake, Yehova aliwafunulia viumbe wote wa roho dai la Shetani na masuala yaliyotokezwa.

1:7; 2:2—Je, Yehova alizungumza na Shetani moja kwa moja? Biblia haisemi mambo mengi kuhusu jinsi Yehova anavyozungumza na viumbe wa roho. Hata hivyo, katika maono, nabii Mikaya aliona malaika mmoja akizungumza na Yehova moja kwa moja. (1 Wafalme 22:14, 19-23) Kwa hiyo, huenda Yehova alizungumza na Shetani moja kwa moja.

1:21—Ni katika njia gani Ayubu angerudi ‘tumboni mwa mama yake’? Kwa kuwa Yehova Mungu alimfanya mtu “kutoka katika mavumbi ya nchi,” neno “mama” linatumiwa hapa katika maana ya mfano ili kurejelea dunia.—Mwanzo 2:7.

2:9—Huenda ni nini kilichomfanya mke wa Ayubu amwambie mume wake amlaani Mungu na kufa? Mke wa Ayubu alipatwa na hasara zilezile kama mume wake. Huenda ilimhuzunisha sana kuona mume wake aliyekuwa na afya nzuri akiteseka kutokana na ugonjwa mbaya sana. Alikuwa amefiwa na watoto wake wapendwa. Huenda alifadhaika sana kwa sababu ya mambo yote hayo hivi kwamba hakufikiria jambo lililokuwa muhimu kabisa, yaani, uhusiano wao pamoja na Mungu.

Mambo Tunayojifunza:

1:8-11; 2:3-5. Kama inavyoonyeshwa katika kisa cha Ayubu, mbali na matendo na usemi unaofaa, ili mtu awe mtimilifu anahitaji kumtumikia Yehova akiwa na nia nzuri.

1:21, 22. Tukiwa washikamanifu kwa Yehova wakati wa hali nzuri na hali mbaya pia, tunaweza kumthibitisha Shetani kuwa mwongo.—Methali 27:11.

2:9, 10. Kama Ayubu, tunapaswa kuendelea kuwa imara katika imani hata ikiwa watu wa familia hawathamini mambo ya kiroho au wanafanya yote wawezayo ili tubadili msimamo wetu au tuache imani yetu.

2:13. Marafiki wa Ayubu hawakusema jambo lolote lenye kufariji kuhusu Mungu na ahadi zake kwa sababu hawakuwa na maoni kama ya Mungu.

“SITAJIONDOLEA UTIMILIFU WANGU!”

(Ayubu 4:1–31:40)

Marafiki watatu wa Ayubu walidai kwamba Ayubu alipokea adhabu hiyo kali kutoka kwa Mungu kwa sababu huenda alikuwa amefanya jambo fulani baya sana. Elifazi ndiye aliyeongoza mazungumzo, na Bildadi akafuata kwa kutumia maneno ya dhihaka zaidi. Sofari ndiye aliyekuwa mwenye dharau hata zaidi.

Ayubu hakukubaliana na mawazo yenye kupotoka ya marafiki wake. Kwa kuwa hakuelewa kwa nini Mungu aliruhusu ateseke, Ayubu alitaka kujitetea tu. Hata hivyo, Ayubu alimpenda Mungu naye akasema: “Mpaka nitakapokata pumzi, sitajiondolea utimilifu wangu!”—Ayubu 27:5.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

7:1; 14:14—“Kazi ya lazima” au ‘kazi ya kulazimishwa’ inamaanisha nini? Ayubu alitaabika sana hivi kwamba akakata kauli kuwa maisha yalikuwa magumu kama kazi ngumu ya lazima. (Ayubu 10:17) Ayubu alilinganisha kazi ya kulazimishwa na kipindi ambacho mtu hulazimika kukaa Sheoli, yaani, tangu wakati wa kifo hadi ufufuo.

7:9, 10; 10:21; 16:22—Je, maneno hayo yanaonyesha kwamba Ayubu hakuamini ufufuo? Ayubu anazungumza mambo ambayo yangetukia ikiwa angekufa. Kwa hiyo, alimaanisha nini? Huenda maneno yake yanamaanisha kwamba iwapo angekufa, watu walioishi katika siku zake hawangemwona tena. Hawangemtambua wala yeye hangeweza kurudi nyumbani kwake wala kutambuliwa tena hadi wakati wa Mungu uliowekwa. Pia, huenda Ayubu alimaanisha kwamba hakuna mtu anayeweza kutoka Sheoli bila kusaidiwa. Maneno ya Ayubu 14:13-15 yanaonyesha wazi kwamba Ayubu aliamini kutakuwa na ufufuo siku zijazo.

10:10—Yehova ‘alimmwagaje Ayubu kama maziwa na kumgandisha kama jibini’? Hayo ni maneno ya kishairi yanayoeleza jinsi Ayubu alivyoumbwa katika tumbo la mama yake.

19:20—Ayubu alimaanisha nini aliposema “ninaponyoka na ngozi ya meno yangu”? Ayubu aliposema kwamba aliponyoka na ngozi ya meno, ambayo kwa kawaida huonekana kwamba hayana ngozi, huenda alimaanisha kwamba aliponyoka bila kitu chochote.

Mambo Tunayojifunza:

4:7, 8; 8:5, 6; 11:13-15. Hatupaswi kukata kauli haraka kwamba mtu fulani aliye katika hali ya kufadhaika anavuna kile alichopanda na kwamba hana kibali cha Mungu.

4:18, 19; 22:2, 3Mashauri yetu yanapaswa kutegemea Neno la Mungu, wala si maoni yetu wenyewe.—2 Timotheo 3:16.

10:1. Kuudhika kulimpofusha Ayubu hivi kwamba hakufikiria sababu nyingine ambazo zilisababisha mateso yake. Hatupaswi kuudhika tunapoteseka, hasa kwa kuwa tunaelewa vizuri masuala yanayohusika.

14:7, 13-15; 19:25; 33:24. Tumaini la ufufuo linaweza kututegemeza wakati wa jaribu lolote lile ambalo Shetani anaweza kutuletea.

16:5; 19:2. Maneno yetu yanapaswa kuwatia wengine moyo na kuwaimarisha, wala si kuwakasirisha.—Methali 18:21.

22:5-7. Shauri linalotolewa kwa msingi wa shutuma zisizo na uthibitisho halina maana na ni lenye madhara.

27:2; 30:20, 21. Hatuhitaji kuwa wakamilifu ili kudumisha utimilifu. Ayubu alimlaumu Mungu isivyo haki.

27:5. Ni Ayubu mwenyewe tu ambaye angeweza kujiondolea utimilifu wake kwa sababu utimilifu unategemea upendo wa mtu kwa Mungu. Kwa hiyo, tunapaswa kumpenda Yehova sana ili tudumishe utimilifu wetu.

28:1-28. Mwanadamu anajua mahali hazina za dunia hupatikana. Anapozitafuta, ustadi wake humwongoza kwenye vijia vilivyochimbwa chini ya ardhi ambavyo haviwezi kuonekana na ndege yeyote mwenye kuwinda aliye na uwezo wa kuona mbali. Hata hivyo, hekima ya Mungu, hupatikana kwa kumwogopa Yehova.

29:12-15. Tunapaswa kuwa tayari kuonyesha fadhili zenye upendo kwa wale walio katika uhitaji.

31:1, 9-28. Ayubu alituwekea kielelezo kizuri kwa kuwa aliepuka kuwachezea wengine kimapenzi. Pia, aliepuka uzinzi, ukosefu wa haki, kuwatendea wengine bila huruma, kupenda vitu vya kimwili, na ibada ya sanamu.

“NINATUBU KATIKA MAVUMBI NA MAJIVU”

(Ayubu 32:1–42:17)

Kijana mmoja mtazamaji aliyeitwa Elihu alikuwa akisikiliza kwa subira mjadala huo. Kisha akaanza kuzungumza kwa ujasiri. Alimkosoa Ayubu na watesi wake watatu.

Punde tu baada ya Elihu kumaliza, Yehova alijibu kupitia dhoruba ya upepo. Hakueleza kwa nini Ayubu anateseka. Hata hivyo, kwa kuuliza mfululizo wa maswali, Mweza-Yote alimjulisha Ayubu kuhusu nguvu Zake zenye kutia hofu na hekima Yake nyingi. Ayubu alikubali kwamba alisema bila kuelewa, naye akasema hivi: “Ninayatangua niliyosema, nami ninatubu katika mavumbi na majivu.” (Ayubu 42:6) Jaribu la Ayubu lilipokoma, alipata thawabu kwa sababu ya utimilifu wake.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

32:1-3—Elihu alifika wakati gani? Kwa kuwa Elihu alisikiliza mazungumzo yote, huenda alikuwa ameketi kando mapema kabla ya Ayubu kuanza kusema na kukomesha kimya cha siku saba cha marafiki wake watatu.—Ayubu 3:1, 2.

34:7—Ayubu alikuwaje kama mtu “ambaye hunywa dharau kama maji”? Katika hali yake ya kufadhaika, Ayubu aliona kwamba wageni wake watatu walikuwa wanamdhihaki, ingawa kwa kweli walikuwa wakisema vibaya kumhusu Mungu. (Ayubu 42:7) Hivyo, alikubali kunywa dharau kama vile mtu anavyofurahia kunywa maji.

Mambo Tunayojifunza:

32:8, 9Mtu hawi na hekima kwa sababu tu ana umri mkubwa. Hekima inatokana na uelewaji wa Neno la Mungu na mwongozo wa roho yake.

34:36. Utimilifu wetu huonekana “tunapojaribiwa mpaka ukomo.”

35:2. Elihu alisikiliza kwa makini na kutambua tatizo hususa kabla ya kusema. (Ayubu 10:7; 16:7; 34:5) Kabla ya kutoa shauri, wazee Wakristo wanapaswa kusikiliza kwa makini, kuwa na uthibitisho, na kuelewa waziwazi mambo yote yanayohusika.—Methali 18:13.

37:14; 38:1–39:30. Kutafakari juu ya kazi za ajabu za Yehova, yaani, mambo yanayoonyesha nguvu zake na hekima, hutunyenyekeza na kutusaidia tutambue kwamba kutetewa kwa enzi yake kuu ndilo jambo muhimu zaidi kuliko mapendezi yetu.—Mathayo 6:9, 10.

40:1-4. Tunapohisi kwamba tunataka kumlaumu Mweza-Yote, tunapaswa ‘kuuweka mkono wetu juu ya kinywa chetu.’

40:15–41:34. Behemothi (kiboko) na Lewiathani (mamba) wana nguvu nyingi sana! Ili kuvumilia katika utumishi wa Mungu, sisi pia tunahitaji nguvu kutoka kwa Muumba wa wanyama hao wenye nguvu nyingi, anayetutia nguvu.—Wafilipi 4:13.

42:1-6. Kusikiliza neno la Yehova na kukumbushwa kuhusu mambo yanayoonyesha nguvu zake kulimsaidia Ayubu ‘kumwona Mungu,’ au kuona ukweli kumhusu. (Ayubu 19:26) Hilo lilirekebisha namna yake ya kufikiri. Tunapopata rekebisho kutoka katika Biblia, tunapaswa kutambua kwa haraka kosa letu na kufanya marekebisho.

Kusitawisha “Uvumilivu wa Ayubu”

Kitabu cha Ayubu kinaonyesha waziwazi kwamba si Mungu anayewatesa wanadamu. Shetani ndiye anayewatesa. Kwa kuruhusu uovu duniani, Mungu hutupa nafasi ya kuonyesha tunaunga mkono upande gani katika suala la enzi kuu ya Yehova na la utimilifu wetu.

Kama Ayubu, wote wanaompenda Yehova watajaribiwa. Simulizi kuhusu Ayubu hutupa uhakika wa kwamba tunaweza kuvumilia. Linatukumbusha kwamba matatizo yetu hayatadumu milele. Andiko la Yakobo 5:11 linasema hivi: “Mmesikia juu ya uvumilivu wa Ayubu nanyi mmeona matokeo ambayo Yehova alileta.” Yehova alimpa Ayubu thawabu kwa kuwa alidumisha utimilifu wake. (Ayubu 42:10-17) Mbele yetu tuna tumaini zuri sana, yaani, uzima wa milele katika Paradiso duniani! Kama Ayubu, acheni tuazimie kudumisha utimilifu wetu.—Waebrania 11:6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kitabu cha Ayubu kinasimulia mambo ya kipindi cha miaka zaidi ya 140, kati ya mwaka wa 1657 na 1473 K.W.K.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Tunaweza kujifunza nini kutokana na “uvumilivu wa Ayubu”?