Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tuliazimia Kumtumikia Yehova

Tuliazimia Kumtumikia Yehova

Simulizi la Maisha

Tuliazimia Kumtumikia Yehova

LIMESIMULIWA NA RAIMO KUOKKANEN

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilianza mwaka wa 1939 huko Ulaya, na Muungano wa Sovieti ukashambulia nchi yetu ya Finland. Baba yangu alienda vitani akiwa mwanajeshi wa Finland. Baada ya muda, ndege za kivita za Urusi ziliangusha mabomu katika jiji tulimoishi. Kwa sababu hiyo, mama yangu alinihamisha na kunipeleka kwa nyanya yangu ambapo palikuwa salama.

MNAMO 1971, nilikuwa mmishonari huko Uganda, Afrika Mashariki. Siku moja nilipokuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba, watu wengi wenye wasiwasi walinipita wakikimbia. Nilisikia mlio wa risasi na nikaanza kukimbia kuelekea nyumbani. Mlio huo ulipokaribia, niliingia ndani ya mtaro uliopita kando ya barabara. Nilitambaa kuelekea nyumbani kwetu huku risasi zikipita juu ya kichwa changu.

Singeweza kuepuka madhara ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, lakini kwa nini mimi na mke wangu tulihatarisha maisha yetu huko Afrika Mashariki? Jibu linapatana sana na azimio letu la kumtumikia Yehova.

Jinsi Nilivyotiwa Moyo Kuazimia Kumtumikia Mungu

Nilizaliwa mwaka wa 1934 huko Helsinki, Finland. Baba yangu alikuwa mpaka-rangi, na siku moja alipaka rangi nyumba iliyotumiwa kama ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Finland. Mashahidi walimwambia kuhusu mikutano ya kutaniko. Alipofika nyumbani, alimweleza mama yangu kuhusu mikutano hiyo. Mama hakuanza kuhudhuria mikutano hiyo wakati huo, lakini baadaye alianza kujifunza Biblia pamoja na mfanyakazi mwenzake aliyekuwa Shahidi. Baada ya muda, mama alichukua kwa uzito mambo aliyojifunza na akabatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mwaka wa 1940.

Kabla tu ya wakati huo, nyanya yangu alikuwa amenipeleka kwake mashambani wakati Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokuwa vikiendelea. Akiwa Helsinki, mama yangu alimwandikia nyanya na mama yangu mdogo kuhusu imani ya Mashahidi wa Yehova. Nyanya yangu na mama yangu mdogo walipendezwa na wakanieleza mambo waliyojifunza. Wawakilishi waliosafiri wa Mashahidi wa Yehova walitutembelea nyumbani kwa nyanya na wakatutia moyo, lakini sikuwa nimeazimia kumtumikia Mungu.

Mazoezi Yaliyonisaidia Kumtumikia Yehova

Vita vilipoisha mwaka wa 1945, nilirudi Helsinki na Mama akaanza kunipeleka kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Wakati mwingine badala ya kwenda mikutanoni, nilienda kutazama sinema. Lakini Mama alikuwa akinieleza kuhusu hotuba iliyotolewa mkutanoni, na mara nyingi alikazia jambo moja: Har–Magedoni imekaribia sana. Nilisadikishwa na jambo hilo na nikaanza kuhudhuria mikutano yote. Kadiri nilivyoelewa kweli ya Biblia, ndivyo tamaa yangu ya kushiriki katika utendaji wote wa kutaniko ilivyoongezeka.

Nilifurahia hasa kuhudhuria makusanyiko. Mnamo 1948, nilipokuwa likizoni wakati wa majira ya kiangazi, nilihudhuria kusanyiko la wilaya lililofanywa karibu na nyumbani kwa nyanya. Rafiki yangu alikuwa anabatizwa katika kusanyiko hilo na akanitia moyo nibatizwe pia. Nilimwambia kwamba sikubeba mavazi ya kuogelea, lakini akapendekeza kwamba baada ya yeye kubatizwa, ninaweza kutumia mavazi yake. Nilikubali na nikabatizwa Juni 27, 1948, nikiwa na umri wa miaka 13.

Baada ya kusanyiko, rafiki za mama walimwambia kwamba nilikuwa nimebatizwa. Tulipoonana, alitaka kujua ni kwa nini nilichukua hatua hiyo muhimu bila kumjulisha. Nilimweleza kwamba nilielewa mafundisho ya msingi ya Biblia na kwamba nilijua mimi ndiye nitakayetoa hesabu kwa Yehova kuhusiana na mwenendo wangu.

Azimio Langu Laimarika

Ndugu kutanikoni walinisaidia kuimarisha azimio langu la kumtumikia Yehova. Waliambatana nami katika huduma ya nyumba kwa nyumba na walinipa migawo mikutanoni karibu kila juma. (Matendo 20:20) Nikiwa na umri wa miaka 16, nilitoa hotuba ya watu wote kwa mara ya kwanza. Muda mfupi baadaye, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa funzo la Biblia katika kutaniko letu. Utendaji wote huo wa kiroho ulinisaidia kukomaa. Lakini bado nilihitaji kushinda tatizo la kuwaogopa wanadamu.

Wakati huo, tulitumia mabango makubwa ya kutangaza hotuba ya watu wote ya kusanyiko la wilaya. Kila bango lilikuwa na sehemu mbili zilizounganishwa kwa kamba ambazo zilining’inia kwenye mabega ya mtu. Sehemu moja ilining’inizwa upande wa mbele na ile nyingine mgongoni.

Wakati mmoja nilipokuwa kwenye kona ya barabara nikiwa na bango langu, niliona wanafunzi wenzangu wakija. Niliogopa sana nilipoona jinsi walivyonitazama. Nilimwomba Yehova anipe ujasiri na nikasimama tuli nikiwa na bango langu. Kushinda tatizo la kuwaogopa wanadamu wakati huo kulinitayarisha kwa ajili ya majaribu makubwa ya kudumisha kutokuwamo kwa Kikristo.

Baadaye, mimi na vijana wengine Mashahidi, tuliamuriwa na serikali tujiandikishe jeshini. Tulienda kwenye kituo cha jeshi kama tulivyokuwa tumeamuriwa, lakini tukakataa kuvaa mavazi ya kijeshi. Wasimamizi walituzuilia katika kituo hicho, na muda mfupi baadaye, tukahukumiwa kifungo cha miezi sita gerezani. Pia, tulifungwa kwa miezi minane, muda ambao tungetumikia jeshini. Hivyo, tukatumia jumla ya miezi 14 gerezani kwa sababu ya msimamo wetu wa kutokuwamo.

Tukiwa gerezani, tulikutana kila siku ili kuzungumzia Biblia. Wengi wetu tulisoma Biblia mara mbili katika miezi hiyo. Kifungo chetu kilipokwisha, wengi wetu tulikuwa tumeazimia hata zaidi kumtumikia Yehova. Hadi leo, wengi miongoni mwa kikundi hicho cha vijana Mashahidi, wanamtumikia Yehova kwa uaminifu.

Baada ya kutoka gerezani, nilirudi kuishi na wazazi wangu. Muda mfupi baadaye, nikamfahamu Veera, Shahidi mwenye bidii aliyekuwa amebatizwa karibuni. Kisha tukafunga ndoa mwaka wa 1957.

Jioni Iliyobadili Maisha Yetu

Jioni moja tulipowatembelea ndugu waliosimamia kazi katika ofisi ya tawi, mmoja wao alituuliza ikiwa tungependa kufanya kazi ya mzunguko. Baada ya kusali usiku kucha, nilipiga simu kwenye ofisi ya tawi na kuwaambia kwamba tumekubali. Ili kuanza utumishi wa wakati wote nilihitaji kuacha kazi yenye mshahara mnono. Hata hivyo, tulikuwa tumeazimia kutanguliza Ufalme maishani mwetu. Nilikuwa na umri wa miaka 23 na Veera alikuwa na umri wa miaka 19 tulipoanza kazi ya mzunguko mnamo Desemba 1957. Kwa miaka mitatu tulifurahia kutembelea na kutia moyo makutaniko ya watu wa Yehova nchini Finland.

Mwishoni mwa mwaka wa 1960, nilialikwa kuhudhuria Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) huko Brooklyn, New York. Ndugu watatu kutoka Finland kutia ndani mimi tulikuwa twende kupata mazoezi ya pekee kwa miezi kumi kuhusiana na kusimamia ofisi ya tawi. Wake zetu walibaki Finland ambapo walifanya kazi katika ofisi ya tawi.

Kabla tu ya kukamilisha shule, niliambiwa niende katika ofisi ya Nathan H. Knorr, aliyekuwa msimamizi wa kazi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Ndugu Knorr alinipa mimi na mke wangu mgawo wa umishonari katika Jamhuri ya Malagasi, inayojulikana sasa kama Madagaska. Nilimwandikia Veera na kumuuliza maoni yake kuhusu mgawo huo, naye alijibu mara moja, “Ndiyo.” Niliporudi Finland, tulifanya haraka kujitayarisha kwa ajili ya maisha huko Madagaska.

Shangwe na Kukata Tamaa

Mnamo Januari 1962 tulipanda ndege kwenda Antananarivo, jiji kuu la nchi hiyo. Tulikuwa tumevalia kofia zenye manyoya na makoti mazito, kwa kuwa tuliondoka Finland katika majira ya baridi kali. Tulibadili mavazi yetu upesi kwa sababu ya hali ya joto ya Madagaska. Makao yetu ya kwanza ya wamishonari yalikuwa madogo na yenye chumba kimoja cha kulala. Tayari kulikuwa na wenzi wa ndoa wamishonari katika makao hayo, kwa hiyo mimi na Veera tulilala ukumbini.

Tulianza kujifunza Kifaransa, lugha rasmi ya Madagaska. Haikuwa rahisi kwa kuwa tulizungumza lugha tofauti na ya mwalimu wetu, Dada Carbonneau. Alitufundisha Kifaransa akitumia Kiingereza, lakini Veera hakuwa anajua Kiingereza. Hivyo, nilimtafsiria Veera maagizo ya Dada Carbonneau katika Kifini. Kisha, tukagundua kwamba Veera alielewa mambo magumu ya lugha alipoelezwa kwa Kiswedi. Hivyo, nilimfafanulia sarufi ya Kifaransa kwa kutumia Kiswedi. Baada ya muda mfupi, tulifanya maendeleo mazuri katika Kifaransa, kisha tukaanza kujifunza lugha ya wenyeji ya Kimalagasi.

Mtu wa kwanza niliyejifunza Biblia naye nchini Madagaska alikuwa mwanamume ambaye alizungumza Kimalagasi pekee. Nilisoma mistari katika Biblia yangu ya Kifini kisha tukachunguza mistari hiyo katika Biblia ya Kimalagasi. Ingawa sikuweza kumwelezea mengi kuhusu maandiko hayo, muda si muda mwanamume huyo alianza kuthamini kweli ya Biblia, akafanya maendeleo na kubatizwa.

Katika mwaka wa 1963, Milton Henschel wa makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, alitembelea Madagaska. Muda mfupi baadaye, ofisi mpya ya tawi ilianzishwa nchini Madagaska, nami nikawekwa kuwa mwangalizi wa tawi, mbali na mgawo wangu wa kuwa mwangalizi wa mzunguko na wa wilaya. Wakati huo wote, Yehova alitubariki sana. Kuanzia mwaka wa 1962 mpaka 1970, idadi ya wahubiri wa Ufalme nchini Madagaska iliongezeka kutoka 85 mpaka 469.

Siku moja mnamo 1970, tuliporudi kutoka mahubiri, tulipata barua mlangoni iliyoamuru wamishonari wote wa Mashahidi wa Yehova wafike kwenye ofisi ya waziri wa mambo ya ndani. Tukiwa huko, ofisa mmoja alituambia kwamba serikali ilikuwa imetoa amri tuondoke nchini mara moja. Nilipouliza kosa linalofanya nifukuzwe, ofisa huyo aliniambia hivi: “Bwana Kuokkanen, hujafanya kosa lolote.”

Nikamwambia: “Tumekuwa hapa kwa miaka minane. Huku ndiko nyumbani. Hatuwezi kuondoka ghafula bila sababu yoyote.” Licha ya jitihada zetu, wamishonari wote walilazimika kuondoka katika kipindi cha juma moja. Ofisi ya tawi ilifungwa, na Shahidi mwenyeji akaanza kusimamia kazi ya kuhubiri. Kabla ya kuwaacha ndugu zetu wapendwa wa Madagaska, tulipata mgawo mpya nchini Uganda.

Tunaanza Mgawo Mpya

Siku chache baada ya kuondoka Madagaska, tulifika Kampala, jiji kuu la Uganda. Bila kukawia tulianza kujifunza Kiganda, lugha nzuri inayosikika kama wimbo inapozungumzwa, lakini iliyo ngumu sana kujifunza. Wamishonari wengine walimsaidia Veera kujifunza Kiingereza kwanza, na lugha hiyo ilitusaidia kuhubiri kwa matokeo.

Afya ya Veera ilidhoofishwa na joto la Kampala. Basi tukatumwa mji wa Mbarara, huko Uganda, ambao una halihewa ya wastani. Sisi ndio tuliokuwa Mashahidi wa kwanza huko, na siku yetu ya kwanza katika mahubiri, tulipata jambo lenye kutia moyo. Nilipokuwa nikizungumza na mwanamume mmoja nyumbani kwake, mke wake alitoka jikoni. Mwanamke huyo aliitwa Margaret, naye alikuwa amesikiliza mahubiri yangu. Veera alianza kumfundisha Margaret Biblia, naye akafanya maendeleo mazuri ya kiroho. Alibatizwa na kuwa mhubiri wa Ufalme mwenye bidii.

Mapigano Mitaani

Mnamo 1971, vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivuruga amani nchini Uganda. Siku moja vita vilitokea karibu na makao yetu ya wamishonari huko Mbarara. Wakati huo ndipo nilipopatwa na mambo niliyotaja mwanzoni mwa simulizi hili.

Tayari Veera alikuwa katika makao ya wamishonari nilipofika baada ya kutambaa kwa muda mrefu ndani ya mtaro, nikijificha askari wasinione. Tulitumia godoro na vyombo vya mbao kutengeneza “ngome” katika kona moja ya nyumba. Kwa muda wa juma moja, tulikaa nyumbani tukisikiliza habari kwenye redio. Wakati mwingine risasi ziligonga kuta huku tukijificha ndani ya ngome yetu. Usiku hatukuwasha taa kwa kuwa hatukutaka watu wajue kwamba tulikuwa nyumbani. Wakati mmoja askari walikuja kwenye mlango wa mbele na kupaaza sauti. Tulikaa tuli na kusali kwa Yehova kimyakimya. Baada ya mapigano kumalizika, majirani wetu walikuja kutushukuru kwa sababu ya usalama wao. Waliamini kwamba Yehova alikuwa ametulinda sote, nasi tukakubaliana nao.

Hali ya utulivu iliendelea mpaka asubuhi moja tuliposikia kwenye redio kwamba Mashahidi wa Yehova wamepigwa marufuku na serikali ya Uganda. Mtangazaji alisema kwamba Mashahidi wa Yehova walipaswa kurudi katika dini zao za awali. Nilijaribu kuzungumza na maofisa wa serikali bila mafanikio. Kisha nikaenda kwa ofisi ya Rais Idi Amin ili kuomba nizungumze naye. Mpokea-wageni akaniambia kwamba rais alikuwa na shughuli nyingi. Nilirudi mara nyingi, lakini sikupata kumwona rais. Mwishowe, tulilazimika kuondoka Uganda mnamo Julai 1973.

Mwaka Mmoja Unakuwa Miaka Kumi

Tulihuzunika sana tulipowaacha ndugu zetu wapendwa huko Uganda kama vile tulivyohuzunika tulipofukuzwa Madagaska. Kabla ya kwenda katika mgawo wetu mpya huko Senegal, tulienda Finland. Tukiwa huko, mgawo wetu wa kwenda Senegal ulifutwa na tukaambiwa tukae Finland. Ni kana kwamba mgawo wetu wa umishonari ulikuwa umekwisha. Tukiwa Finland tulikuwa mapainia wa pekee na tulifanya pia kazi ya mzunguko.

Kufikia mwaka wa 1990 upinzani kuelekea kazi ya kuhubiri huko Madagaska ulikuwa umepungua, nasi tulishangaa wakati makao makuu ya Brooklyn yalipotuomba twende kutumikia huko Madagaska kwa mwaka mmoja. Tulitaka kwenda, lakini tulikabili vizuizi viwili vikubwa. Baba yangu ambaye alikuwa amezeeka alihitaji kutunzwa, na Veera alikuwa na matatizo ya afya. Nilihuzunika baba yangu alipokufa mnamo Novemba 1990, lakini kwa kuwa Veera alipata nafuu, tulikuwa na tumaini la kurudia kazi ya umishonari. Tulirudi Madagaska mnamo Septemba 1991.

Mgawo wetu huko Madagaska ulikuwa wa mwaka mmoja, lakini uliendelea kwa miaka kumi. Wakati huo, idadi ya wahubiri iliongezeka kutoka 4,000 hadi 11,600. Nilifurahia sana kutumika nikiwa mmishonari. Hata hivyo, wakati mwingine nilivunjika moyo nikifikiria kwamba nilikuwa nikipuuza mahitaji ya kimwili na ya kihisia ya mke wangu mpendwa. Yehova alitupa sote wawili nguvu za kuendelea. Mwishowe katika mwaka wa 2001, tulirudi Finland ambapo tumekuwa tukifanya kazi katika ofisi ya tawi. Bado tuna bidii katika kazi ya Ufalme, na tungali tunakumbuka Afrika. Tumeazimia kufanya mapenzi ya Yehova popote pale atakapotutuma.—Isaya 6:8.

[Ramani katika ukurasa wa 12]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

FINLAND

ULAYA

[Ramani katika ukurasa wa 14]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

AFRIKA

MADAGASKA

[Ramani katika ukurasa wa 15]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

AFRIKA

UGANDA

[Picha katika ukurasa wa 14]

Siku yetu ya arusi

[Picha katika ukurasa wa 14, 15]

Katika kazi ya mzunguko huko Finland mnamo 1960 . . .

. . . kisha kazi ya umishonari huko Madagaska mnamo 1962

[Picha katika ukurasa wa 16]

Nikiwa na Veera leo