Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Tatu na cha Nne cha Zaburi

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Tatu na cha Nne cha Zaburi

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Tatu na cha Nne cha Zaburi

MTUNGA-ZABURI anauliza hivi katika sala kwa Mungu: “Je, fadhili zako zenye upendo zitatangazwa katika kaburi, na uaminifu wako katika mahali pa maangamizi?” (Zaburi 88:11) Bila shaka hapana. Bila uhai, hatuwezi kumsifu Yehova. Kumsifu Yehova ni sababu nzuri ya kuendelea kuishi, na kuwa na uhai kunapaswa kutuchochea kumsifu.

Zaburi ya 73 hadi ya 106 zinapatikana katika Kitabu cha Tatu na cha Nne cha Zaburi. Zaburi hizo zinatupa sababu nyingi za kumsifu Muumba na kulibariki jina lake. Kutafakari zaburi hizo kunapaswa kuimarisha uthamini wetu wa “neno la Mungu” na kutuchochea kuzidisha na kuboresha jinsi tunavyomsifu. (Waebrania 4:12) Acheni kwanza tuchunguze kwa makini Kitabu cha Tatu cha Zaburi.

“KUMKARIBIA MUNGU NI KWEMA KWANGU”

(Zaburi 73:1–89:52)

Zaburi 11 za kwanza katika mkusanyo wa tatu zilitungwa na Asafu au washiriki wa nyumba ya Asafu. Wimbo wa kwanza unaeleza kilichomsaidia Asafu asipotoshwe kwa kufikiri isivyofaa. Amefikia mkataa unaofaa. Anaimba hivi: “Lakini mimi, kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.” (Zaburi 73:28) Zaburi ya 74. ni maombolezo kuhusu uharibifu wa Yerusalemu. Zaburi ya 75, 76, na 77 zinamfafanua Yehova kuwa Mwamuzi mwadilifu, Mwokoaji wa wapole, na Msikiaji wa sala. Zaburi ya 78 inazungumzia maisha ya Waisraeli tangu siku za Musa hadi siku za Daudi. Zaburi ya 79 ni maombolezo juu ya uharibifu wa hekalu. Zaburi ya 80 ni sala kwa ajili ya watu wa Mungu waliorudishwa. Zaburi ya 81 inatuhimiza tumtii Yehova. Zaburi ya 82 na ya 83 ni sala ya kumwomba Mungu awahukumu waamuzi wafisadi na adui za Mungu.

Wimbo wa wana wa Kora unasema: “Nafsi yangu imetamani sana na pia imedhoofika kwa kutamani nyua za Yehova.” (Zaburi 84:2) Katika Zaburi ya 85, Mungu anaombwa awabariki wale waliorudi kutoka uhamishoni. Zaburi hiyo inakazia kwamba baraka za kiroho zina thamani sana kuliko baraka za kimwili. Katika Zaburi ya 86, Daudi anamwomba Mungu amlinde na kumfundisha. Zaburi ya 87 ni wimbo kuhusu Sayuni na waliozaliwa humo, nayo inafuatwa na sala kwa Yehova katika Zaburi ya 88. Fadhili zenye upendo za Yehova kama zinavyoonyeshwa katika agano la Daudi, zinatiliwa mkazo katika Zaburi ya 89 iliyotungwa na Ethani. Huenda Ethani alikuwa mmoja wa wanaume wanne wenye hekima katika siku za Sulemani.—1 Wafalme 4:31.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

73:9—Ni katika maana gani waovu “wameweka kinywa chao mbinguni, nao ulimi wao hutembea huku na huku duniani”? Kwa kuwa waovu hawamheshimu yeyote mbinguni wala duniani, wao humdhihaki Mungu kwa kinywa chao. Wao pia huwachongea wanadamu kwa ulimi wao.

74:13, 14—Ni wakati gani ambapo Yehova ‘alivunja vichwa vya wanyama wakubwa wa baharini katika maji na kuponda vipande-vipande vichwa vya Lewiathani’? “Farao, mfalme wa Misri,” anaitwa “yule mnyama mkubwa wa baharini anayelala akiwa amejinyoosha katikati ya mifereji yake ya Nile.” (Ezekieli 29:3) Huenda Lewiathani akawakilisha watu wenye nguvu wa Farao. (Zaburi 74:14) Kuponda vipande-vipande vichwa vyao yaelekea kunarejelea kushindwa kwa Farao na majeshi yake wakati Yehova alipowakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri.

75:4, 5, 10—Neno “pembe” linamaanisha nini? Pembe za mnyama ni silaha yenye nguvu. Hivyo, kwa njia ya mfano, neno “pembe” linamaanisha mamlaka au nguvu. Yehova huinua pembe za watu wake, akiwafanya wainuliwe, lakini ‘anazikata pembe za waovu.’ Tunaonywa dhidi ya ‘kuinua pembe zetu juu,’ yaani, tusiwe wenye kujisifu au wenye kiburi. Kwa kuwa Yehova ndiye anayewainua watu, madaraka kutanikoni yanapaswa kuonwa kuwa yanatoka kwake.—Zaburi 75:7.

76:10—“Ghadhabu ya mwanadamu” inaweza kumsifuje Yehova? Huenda kukawa na matokeo mazuri Mungu anapowaruhusu wanadamu watutendee kwa ghadhabu kwa sababu sisi ni watumishi wake. Tatizo lolote ambalo huenda tukapata linaweza kutuzoeza kwa njia fulani. Yehova huruhusu tuteseke ikiwa tu mateso hayo yanaweza kutuzoeza. (1 Petro 5:10) ‘Mungu hujifunga ghadhabu iliyobaki ya mwanadamu.’ Namna gani tukiteseka hadi kifo? Hilo pia linaweza kumsifu Yehova kwa sababu wale wanaotuona tukivumilia kwa uaminifu wanaweza kumtukuza Mungu.

78:24, 25Kwa nini mana inaitwa “nafaka ya mbinguni” na “mkate wa wenye nguvu”? “Wenye nguvu” wanaotajwa hapa ni malaika wa mbinguni. Hata hivyo, maneno hayo hayamaanishi kwamba mana ilikuwa chakula cha malaika. Ilikuwa “nafaka ya mbinguni” kwa sababu ilitoka mbinguni. (Zaburi 105:40) Kwa kuwa malaika au “wenye nguvu” wanaishi mbinguni, maneno “mkate wa wenye nguvu” huenda yakamaanisha kwamba mana iliandaliwa na Mungu anayeishi mbinguni. (Zaburi 11:4) Huenda pia Yehova aliwatumia malaika kuwaandalia Waisraeli mana.

82:1, 6—Ni nani wanaoitwa “miungu” na “wana wa Aliye Juu Zaidi”? Maneno yote hayo yanawarejelea waamuzi wa Israeli. Maneno hayo yaliwafaa kwa sababu walipaswa kumtumikia Mungu wakiwa wasemaji na wawakilishi wake.—Yohana 10:33-36.

83:2—‘Kuinua kichwa’ kunamaanisha nini? Hiyo ni ishara ya kuonyesha kwamba mtu yuko tayari kutumia mamlaka au kuchukua hatua, kwa kawaida ili kupinga, kupigana, au kunyanyasa.

Mambo Tunayojifunza:

73:2-5, 18-20, 25, 28. Hatupaswi kuwaonea wivu waovu kwa sababu ya ufanisi wao wala kuiga njia zao mbaya. Waovu wako kwenye udongo unaoteleza. Hakika ‘wataanguka kwenye uharibifu.’ Isitoshe, kwa kuwa uovu hauwezi kuondolewa na utawala wa wanadamu wasio wakamilifu, kujaribu kuuondoa ni kazi bure. Tutakuwa wenye hekima tukikabiliana na uovu kama Asafu kwa “kumkaribia Mungu” na kufurahia uhusiano wa karibu pamoja Naye.

73:3, 6, 8, 27. Tunapaswa kujilinda dhidi ya kujisifu, majivuno, dhihaka, na upunjaji. Lazima tufanye hivyo ingawa sifa hizo huenda zikaonekana kuwa zenye faida.

73:15-17. Tunapochanganyikiwa, tunapaswa kujizuia tusitoe maoni yetu hadharani. Kusimulia “hadithi kama hiyo” kutawavunja wengine moyo. Tunapaswa kutafakari kwa utulivu kuhusu mahangaiko yetu na kuyasuluhisha kwa kushirikiana na waamini wenzetu.—Methali 18:1.

73:21-24. Kuwa na ‘uchungu moyoni’ kwa sababu ya ufanisi wa waovu hufananishwa na kutenda kama wanyama wasiotumia akili. Mtu anapokuwa na uchungu moyoni anatenda bila kufikiri, naye huongozwa na hisia. Lakini, tunapaswa kuongozwa na shauri la Yehova, tukiwa na uhakika kwamba ‘ataushika mkono wetu wa kuume’ na kutusaidia. Isitoshe, Yehova ‘atatupeleka kwenye utukufu,’ yaani, tutakuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye.

77:6. Kuhangaikia kweli za kiroho na kuzitafuta kwa makini kunahitaji wakati wa kujifunza na kutafakari. Ni muhimu kutenga wakati wa kuwa peke yetu!

79:9. Yehova husikia sala zetu hasa ikiwa zinahusiana na kutakaswa kwa jina lake.

81:13, 16. Kusikiliza sauti ya Yehova na kutembea katika njia zake huleta baraka nyingi.—Methali 10:22.

82:2, 5Ukosefu wa haki hufanya ‘misingi ya dunia’ itikisike. Matendo yasiyo ya haki huvuruga jamii.

84:1-4, 10-12. Kwa kuthamini mahali pa ibada ya Yehova na kufurahia utumishi wao wa pekee, watunga-zaburi wanatuwekea kielelezo kizuri.

86:5. Tunashukuru sana kwa kuwa Yehova yuko “tayari kusamehe”! Yeye anatafuta uthibitisho wowote unaoweza kumpa sababu ya kumwonyesha rehema mkosaji anayetubu.

87:5, 6Je, wale watakaoishi katika dunia Paradiso watajua majina ya wale wanaofufuliwa kuishi mbinguni? Mistari hiyo inaonyesha kwamba huenda ikawa hivyo.

88:13, 14. Ikiwa tumesali kwa Yehova kuhusu tatizo fulani na hatujajibiwa, huenda hilo likaonyesha kwamba Yehova anataka tuonyeshe ikiwa tunajitoa kwake kwa unyoofu.

“MTOLEENI SHUKRANI, LIBARIKINI JINA LAKE”

(Zaburi 90:1–106:48)

Fikiria sababu mbalimbali za kumtukuza Yehova zinazotajwa katika mkusanyo wa nne wa zaburi. Katika Zaburi ya 90, Musa analinganisha kuwapo kwa “Mfalme wa umilele” na maisha mafupi ya mwanadamu. (1 Timotheo 1:17) Kulingana na Zaburi 91:2, Musa anamwita Yehova ‘kimbilio na ngome yake,’ yaani, Chanzo cha usalama wake. Zaburi chache zinazofuata zinazungumzia sifa nzuri za Mungu, fikira zake zilizotukuka, na kazi zake za ajabu. Nyimbo tatu zinaanza kwa maneno haya, ‘Yehova mwenyewe amekuwa mfalme.’ (Zaburi 93:1; 97:1; 99:1) Kwa kusema kwamba Yehova ni Mtengenezaji wetu, mtunga-zaburi anatualika ‘tumtolee shukrani na kulibariki jina lake.’—Zaburi 100:4.

Mtawala anayemwogopa Yehova anapaswa kusimamiaje mambo? Zaburi ya 101 iliyoandikwa na Mfalme Daudi inajibu. Zaburi inayofuata inasema kwamba Yehova “hakika ataielekea sala ya wale waliovuliwa kila kitu, naye hataidharau sala yao.” (Zaburi 102:17) Zaburi ya 103 huonyesha fadhili zenye upendo na rehema za Yehova. Akirejelea vitu vingi vya Mungu hapa duniani, mtunga-zaburi anasema hivi kwa mshangao: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima.” (Zaburi 104:24) Nyimbo mbili za mwisho za Kitabu cha Nne zinamtukuza Yehova kwa kazi zake za ajabu.—Zaburi 105:2, 5; 106:7, 22.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

91:1, 2—“Mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi” ni wapi, nasi tunaweza ‘kukaaje’ hapo? Ni mahali pa mfano penye usalama wa kiroho, yaani, kulindwa kutokana na madhara ya kiroho. Ni mahali pa siri kwa sababu wale wasiomtumaini Mungu hawajui mahali hapo. Tunamfanya Yehova kuwa makao yetu kwa kumtegemea akiwa kimbilio letu na ngome yetu, kwa kumsifu akiwa Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, na kwa kuhubiri habari njema za Ufalme. Tunahisi tukiwa salama kiroho kwa sababu tunajua kwamba sikuzote Yehova yuko tayari kutusaidia.—Zaburi 90:1.

92:12—Ni katika njia gani mwadilifu ‘huchanua kama mtende’? Mtende unajulikana kwa kuzaa sana. Mtu mwadilifu ni kama mtende kwa kuwa yeye ni mnyoofu machoni pa Yehova naye huendelea kuzaa “matunda mazuri” yanayotia ndani kazi nzuri.—Mathayo 7:17-20.

Mambo Tunayojifunza:

90:7, 8, 13, 14. Mara nyingi makosa yetu huharibu uhusiano wetu na Mungu wa kweli. Yeye huona dhambi zinazofanywa kwa siri. Hata hivyo, tukitubu kikweli na kuacha mwenendo mbaya, Yehova atatukubali tena, ‘akitushibisha kwa fadhili zake zenye upendo.’

90:10, 12. Kwa kuwa maisha ni mafupi, tunapaswa “kuzihesabu siku zetu.” Jinsi gani? Kwa “kuuingiza moyo wa hekima” au kuwa na hekima ili tusitumie vibaya siku zetu zilizobaki, bali tuzitumie kwa njia inayompendeza Yehova. Hiyo inamaanisha tutangulize mambo ya kiroho na kutumia wakati wetu kwa hekima.—Waefeso 5:15, 16; Wafilipi 1:10.

90:17. Ni jambo linalofaa kumwomba Yehova ‘aifanye imara kazi ya mikono yetu’ na abariki jitihada zetu katika utumishi.

92:14, 15. Kwa kujifunza Neno la Mungu kwa bidii na kushirikiana kwa ukawaida na watu wa Yehova, walio wazee kwa umri huendelea kuwa “wanono na wabichi” wakiwa wenye nguvu kiroho na hivyo kuwa wenye thamani kubwa kutanikoni.

94:19. Hata sababu ya ‘fikira zetu zinazofadhaisha’ iwe nini, kusoma na kutafakari “faraja” zinazopatikana katika Biblia kunatufariji.

95:7, 8Kusikiliza shauri la Kimaandiko, kulitilia maanani, na kulitii kutatuzuia tusiwe na mioyo migumu.—Waebrania 3:7, 8.

106:36, 37. Mistari hii inahusianisha ibada ya sanamu na kutoa dhabihu kwa roho waovu. Hilo linamaanisha kwamba mtu anayetumia sanamu anaweza kuwa chini ya uvutano wa roho waovu. Biblia inatusihi hivi: “Jilindeni na sanamu.”—1 Yohana 5:21.

“Msifuni Yah!”

Nyimbo tatu za mwisho katika Kitabu cha Nne cha Zaburi zinamalizia kwa kusihi hivi: “Msifuni Yah!” Zaburi ya mwisho pia inaanza kwa maneno hayo. (Zaburi 104:35; 105:45; 106:1, 48) Maneno “Msifuni Yah!” yanapatikana mara nyingi katika Kitabu cha Nne cha Zaburi.

Bila shaka, tuna sababu za kumsifu Yehova. Zaburi ya 73 hadi ya 106 zimetupa mambo mengi ya kutafakari na kujaza mioyo yetu shukrani kwa Baba yetu wa mbinguni. Tunapofikiria yale ambayo ametufanyia na atakayotufanyia wakati ujao, je, hatuchochewi ‘kumsifu Yah’ kwa nguvu zetu zote?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kama Asafu, tunaweza kukabiliana na uovu kwa “kumkaribia Mungu”

[Picha katika ukurasa wa 11]

Farao ashindwa katika Bahari Nyekundu

[Picha katika ukurasa wa 11]

Je, unajua ni kwa nini mana inaitwa “mkate wa wenye nguvu”?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Ni nini hutusaidia kuondoa ‘fikira zinazotufadhaisha’?