Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Hatuwezi Kuacha Kusema Juu ya Yesu’

‘Hatuwezi Kuacha Kusema Juu ya Yesu’

“Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala Kuliko Wanadamu”

‘Hatuwezi Kuacha Kusema Juu ya Yesu’

NI MWAKA wa 33 W.K., na tukio lenyewe linatukia katika chumba cha kifahari cha mahakama ya kitaifa ya Wayahudi huko Yerusalemu. Sanhedrini iko karibu kusikiliza kesi ya wafuasi 12 wa Yesu Kristo. Kwa nini? Kwa sababu wamekuwa wakihubiri kuhusu Yesu. Mtume Petro na Yohana wako mbele ya mahakama hiyo kwa mara ya pili. Lakini ni mara ya kwanza kwa mitume wale wengine kufikishwa katika mahakama hiyo.

Kuhani mkuu anawaambia mitume hao 12 kuhusu agizo lililotolewa na mahakama hiyo katika kesi iliyotangulia. Wakati huo, mtume Petro na Yohana waliagizwa waache kufundisha kumhusu Yesu, nao wakajibu hivi: “Kama ni jambo la uadilifu mbele za macho ya Mungu kuwasikiliza ninyi badala ya Mungu, hukumuni ninyi wenyewe. Lakini sisi hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” Baada ya kusali wapate ujasiri, wanafunzi wa Yesu waliendelea kuhubiri habari njema.—Matendo 4:18-31.

Akitambua kwamba vitisho vyake vya awali havikufanikiwa, kuhani mkuu anasema hivi katika kesi hii ya pili: “Hakika tuliwaagiza msiendelee kufundisha juu ya msingi wa jina hili, na bado, tazameni! mmejaza Yerusalemu fundisho lenu, nanyi mnaazimia kuileta damu ya mtu huyu juu yetu.”—Matendo 5:28.

Azimio Thabiti

Wakijibu kwa ujasiri, Petro na wale mitume wengine wanasema: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Kwa kweli, badala ya kuwatii wanadamu, ni lazima tumtii Yehova wakati wanadamu wanapodai mambo yasiyopatana na amri zake. *

Maneno ya mitume yanayoonyesha ushikamanifu wao kwa Mungu yanapaswa kuwasadikisha washiriki wa Sanhedrini. Iwapo wangeulizwa kuhusu kumtii Mungu, viongozi hao wa Wayahudi wangepaswa kujibu hivi kwa sauti moja: “Mtii Mungu.” Wangepaswa kujibu hivyo kwa sababu waliamini kwamba Mungu ndiye Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote.

Labda akizungumza kwa niaba ya mitume wote, Petro anasema kwamba katika mambo yanayohusiana na huduma yao, wanamtii Mungu kuliko wanadamu. Hivyo, anakanusha mashtaka ya kwamba mitume hawatii. Kutokana na historia ya taifa lao, washiriki wa Sanhedrini wanajua kwamba kuna wakati ambapo inafaa kabisa kumtii Mungu kuliko wanadamu. Wazalishaji wawili huko Misri walimwogopa Mungu badala ya Farao, kwa kuwahifadhi watoto wa kiume waliozaliwa na wanawake Waebrania. (Kutoka 1:15-17) Mfalme Hezekia aliposhurutishwa kujisalimisha, alimtii Yehova badala ya kumtii Mfalme Senakeribu. (2 Wafalme 19:14-37) Maandiko ya Kiebrania ambayo washiriki wa Sanhedrini wanayajua, yanakazia kwamba Yehova anatarajia watu wake wamtii.—1 Samweli 15:22, 23.

Wapata Thawabu kwa Kutii

Angalau mshiriki mmoja wa mahakama hiyo kuu anaguswa moyo na maneno haya, “lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” Gamalieli, mwamuzi anayeheshimiwa sana katika Sanhedrini, anashawishi mahakama isikilize shauri la hekima analotoa katika kikao cha faragha. Akitaja mifano ya kale, Gamalieli anaonyesha kwamba si jambo la hekima kuingilia kazi ya mitume. Anamalizia kwa kusema: “Msijiingize katika mambo ya watu hawa, bali waacheni; . . . ama sivyo, huenda mkaonwa kuwa kwa kweli mnapigana na Mungu.”—Matendo 5:34-39.

Maneno yenye usawaziko ya Gamalieli yanasadikisha mahakama kuu kuwaachilia mitume. Ingawa wanapigwa viboko, mitume hawatishwi kamwe na tukio hilo. Badala yake Biblia inasema hivi: “Kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.”—Matendo 5:42.

Mitume walibarikiwa kama nini kwa kuonyesha waziwazi kwamba Mungu ndiye mwenye mamlaka kubwa zaidi! Wakristo wa kweli leo wana mtazamo huohuo. Mashahidi wa Yehova wanaendelea kumwona Yehova kuwa Mtawala wao Mkuu Zaidi. Wanapoamuriwa kutenda kinyume cha maagizo ya Mungu, wao husema kama mitume walivyosema: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona Kalenda ya Mashahidi wa Yehova 2006, Septemba/Oktoba.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

JE, UMEWAHI KUJIULIZA?

Luka, mwandikaji wa Biblia, alijuaje maneno ambayo Gamalieli alisema katika kikao cha faragha cha Sanhedrini? Huenda Luka alifunuliwa maneno hayo kupitia roho ya Mungu. Labda Paulo (aliyekuwa mmoja wa wanafunzi wa Gamalieli) alimjulisha Luka kuhusu maneno ya Gamalieli. Au huenda Luka aliwasiliana na mshiriki wa mahakama kuu aliyeunga mkono maoni ya mitume.