Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wakaita Pamoja Sanhedrini”

“Wakaita Pamoja Sanhedrini”

“Wakaita Pamoja Sanhedrini”

KUHANI mkuu na watawala wa Wayahudi hawakujua la kufanya. Wangefanya nini ili kunyamazisha msisimuko uliotokea kuhusu Yesu Kristo? Walikuwa wamefanikiwa kumuua, lakini sasa wanafunzi wa Yesu walikuwa wakizungumza kuhusu ufufuo wake kotekote Yerusalemu. Wangenyamazishwaje? Ili kuamua, kuhani mkuu na wasaidizi wake ‘waliita pamoja Sanhedrini,’ mahakama kuu zaidi ya Wayahudi.—Matendo 5:21.

Katika karne ya kwanza huko Israeli, Gavana Mroma Pontio Pilato alikuwa na mamlaka kubwa. Lakini Sanhedrini ilishirikianaje na Pilato? Sanhedrini ilikuwa na mamlaka gani? Ilifanyizwa na washiriki wangapi? Nayo ilifanyaje kazi?

Jinsi Sanhedrini Ilivyotokea

Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “Sanhedrini” linamaanisha “kuketi chini pamoja na.” Neno hilo lilitumiwa kumaanisha kusanyiko au mkutano. Katika desturi za Kiyahudi, lilimaanisha baraza au mahakama ya kidini ya hukumu.

Waandikaji wa Talmud, ambayo ilikamilishwa katika karne zilizofuatia uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K., walionyesha kwamba Sanhedrini ilikuwa baraza la kale. Walifikiri kwamba sikuzote Sanhedrini ilifanyizwa na wasomi ambao walikutanika ili kujadili sheria ya Kiyahudi, nao waliamini kwamba ilianzishwa wakati Musa alipokusanya wanaume wazee 70 ili wamsaidie kuongoza Israeli. (Hesabu 11:16, 17) Wanahistoria hawakubaliani na wazo hilo. Wanasema kwamba baraza linalofanana na Sanhedrini ya karne ya kwanza lilianzishwa wakati Waajemi walipotawala Israeli. Pia, wanahistoria wanasema kuwa maoni ya waandikaji wa Talmud kwamba hilo lilikuwa baraza la wasomi ni kama yanafafanua mabaraza ya marabi ya karne ya pili na ya tatu kuliko Sanhedrini ya karne ya kwanza. Hivyo basi, Sanhedrini ilitokea wakati gani?

Biblia inasema kwamba wahamishwa waliorudi Yuda kutoka Babiloni mwaka wa 537 K.W.K., walikuwa na mfumo wa kitaifa wa usimamizi. Nehemia na Ezra wanataja wakuu, wanaume wazee, watu wenye vyeo, na watawala-wasaidizi, na huenda huo ndio uliokuwa mwanzo wa ile ambayo baadaye iliitwa Sanhedrini.—Ezra 10:8; Nehemia 5:7.

Wayahudi walikabili msukosuko tangu Maandiko ya Kiebrania yalipokamilishwa hadi wakati Injili ya Mathayo ilipoandikwa. Katika mwaka wa 332 K.W.K., Aleksanda Mkuu alianza kutawala Yudea. Baada ya kifo cha Aleksanda, Yudea ikawa chini ya falme zake mbili za Ugiriki, kwanza ufalme wa ukoo wa Ptolemy kisha ufalme wa ukoo wa Seleuko. Katika masimulizi kuhusu utawala wa ukoo wa Seleuko ulioanza mwaka wa 198 K.W.K., baraza la Wayahudi linatajwa kwa mara ya kwanza. Yaelekea baraza hilo halikuwa na mamlaka kamili, lakini lilifanya Wayahudi wahisi kwamba wanajitawala.

Mwaka wa 167 K.W.K., Mfalme Antioko wa Nne (Epifane) wa ukoo wa Seleuko alijaribu kuwalazimisha Wayahudi wafuate utamaduni wa Wagiriki. Alinajisi hekalu la Yerusalemu kwa kutoa dhabihu ya nguruwe kwa mungu Zeu kwenye madhabahu. Hilo lilisababisha uasi na wakati huo Wamakabayo walikomesha utawala wa ukoo wa Seleuko na kuanzisha utawala wa ukoo wa Wahasmoni. * Wakati huohuo, waandishi na Mafarisayo, ambao walikuwa viongozi wa watu waliounga mkono uasi huo, walipata mamlaka ya kusimamia taifa na hivyo makuhani wakapoteza mamlaka yao.

Sanhedrini inayotajwa katika Maandiko ya Kigiriki ilikuwa ikisitawi. Baadaye, Sanhedrini ingekuwa baraza la kitaifa la usimamizi na mahakama kuu ya hukumu ya kufasiri sheria ya Kiyahudi.

Kugawa Mamlaka

Kufikia karne ya kwanza, Roma ilikuwa ikitawala Yudea. Hata hivyo, Wayahudi walikuwa na uhuru wa kiasi fulani. Kulingana na sera yao, Waroma waliwapa watu waliokuwa chini yao uhuru wa kuchagua serikali yao. Kwa hiyo, maofisa Waroma hawakuingilia kazi zilizofanywa na mahakama za maeneo mengine, na hivyo wakaepuka matatizo ambayo yangetokea kwa sababu ya tofauti katika utamaduni. Kusudi lilikuwa kuendeleza amani na ushikamanifu miongoni mwa watu walioishi katika maeneo hayo kwa kuwaruhusu kufuata desturi zao na kujitawala. Zaidi ya kumweka rasmi na kumwondoa kuhani mkuu—ambaye alikuwa msimamizi wa Sanhedrini—na kutoza kodi, Waroma waliingilia shughuli za Wayahudi wakati tu ilipokuwa lazima. Kama kesi ya Yesu inavyoonyesha, inaonekana kwamba Waroma walidumisha mamlaka yao ya kutoa hukumu ya kifo.—Yohana 18:31.

Hivyo, Sanhedrini ilisimamia mambo mengi ya ndani ya Wayahudi. Ilikuwa na maofisa wa kuwakamata watu. (Yohana 7:32) Mahakama za chini zilisikiliza kesi za mashtaka madogo ya uhalifu na kesi za madai bila Roma kuingilia. Wakati mahakama za chini ziliposhindwa kuamua kesi, kesi hiyo ilipelekwa mbele ya Sanhedrini, ambayo ilitoa uamuzi wa mwisho.

Ili kudumisha mamlaka yake, ilibidi Sanhedrini iendeleze amani na kuunga mkono utawala wa Roma. Lakini Waroma walipofikiri kwamba sheria fulani zilivunjwa, waliingilia na kuchukua hatua. Mfano mmoja ni wakati mtume Paulo alipokamatwa.—Matendo 21:31-40.

Washiriki wa Mahakama

Sanhedrini ilikuwa na washiriki 71, yaani, kuhani mkuu na wanaume 70 mashuhuri wa taifa. Katika siku za Waroma, Sanhedrini ilifanyizwa na makuhani wenye vyeo (hasa Masadukayo), watu wa tabaka la juu ambao hawakuwa makuhani, na waandishi wenye elimu wa chama cha Mafarisayo. Makuhani wa tabaka la juu ambao waliungwa mkono na watu wa kawaida ndio waliokuwa na uvutano mkubwa katika mahakama hiyo. * Ingawa Masadukayo walishikilia sana maoni yao, Mafarisayo walikuwa tayari kukubali maoni mapya na walikuwa hasa watu wa kawaida ambao walikuwa na uvutano mkubwa juu ya watu. Kulingana na mwanahistoria Yosefo, Masadukayo hawakukubali kwa urahisi maoni ya Mafarisayo. Paulo alitumia tofauti kati ya vikundi hivyo viwili na tofauti za mafundisho yao alipojitetea mbele ya Sanhedrini.—Matendo 23:6-9.

Kwa kuwa Sanhedrini ilikuwa hasa na watu wa tabaka la juu, inaonekana kwamba washiriki wake walikuwa wa kudumu, na wakati washiriki wapya walipohitajiwa, waliwekwa rasmi na wale wa zamani. Kulingana na Mishnah, washiriki wapya walipaswa kuwa “makuhani, Walawi, na Waisraeli ambao binti zao waliruhusiwa kuolewa na makuhani,” yaani, Wayahudi ambao wangeweza kuthibitisha kupitia maandishi kwamba ukoo wao haukuwa umechanganyika na ukoo mwingine. Kwa kuwa mahakama kuu ilisimamia mfumo wa hukumu wa nchi yote, yaelekea watu waliokuwa na sifa nzuri katika mahakama za chini walipandishwa cheo kuwa washiriki wa Sanhedrini.

Mamlaka Yake

Wayahudi waliheshimu sana Sanhedrini na waamuzi wa mahakama za chini walipaswa kukubali maamuzi yake, la sivyo wangehukumiwa kifo. Mahakama hiyo hasa ilichunguza sifa za kustahili za makuhani na kusimamia mambo yaliyohusu Yerusalemu, hekalu lake, na ibada katika hekalu. Kwa ujumla, Sanhedrini ilisimamia eneo la Yudea peke yake. Lakini, kwa kuwa Sanhedrini ilionwa kuwa yenye mamlaka kuu zaidi ya kufafanua Sheria, iliweka kanuni za maadili zilizopaswa kufuatwa na jamii za Wayahudi ulimwenguni pote. Kwa mfano, kuhani mkuu na baraza lake waliwaagiza viongozi wa masinagogi huko Damasko waunge mkono kukamatwa kwa wafuasi wa Kristo. (Matendo 9:1, 2; 22:4, 5; 26:12) Pia, yaelekea Wayahudi walioenda Yerusalemu kwa ajili ya sherehe walipeleka habari nyumbani kwao kuhusu maamuzi ya Sanhedrini.

Kulingana na Mishnah, Sanhedrini ilikuwa na mamlaka pekee juu ya masuala muhimu ya kitaifa, mamlaka ya kuwachukulia hatua waamuzi ambao walipinga maamuzi yake, na mamlaka ya kuwahukumu manabii wa uwongo. Yesu na Stefano walipelekwa mbele ya mahakama hiyo wakishtakiwa kuwa wakufuru, Petro na Yohana walishtakiwa kuwa wanapindua taifa, naye Paulo akashtakiwa kuwa mnajisi wa hekalu.—Marko 14:64; Matendo 4:15-17; 6:11; 23:1; 24:6.

Hukumu Dhidi ya Yesu na Wanafunzi Wake

Vikao vya Sanhedrini vilifanywa kila siku kutoka wakati wa dhabihu ya asubuhi hadi wakati wa toleo la jioni isipokuwa siku ya Sabato na siku takatifu. Kesi zilisikilizwa mchana peke yake. Kwa kuwa hukumu ya kifo ilitolewa siku iliyofuatia kusikilizwa kwa kesi, kesi kama hizo hazikupaswa kusikilizwa siku iliyotangulia Sabato au sherehe. Mashahidi walionywa vikali kuhusu uzito wa kumwaga damu isiyo na hatia. Kwa hiyo, kesi na hukumu dhidi ya Yesu iliyofanywa usiku katika nyumba ya Kayafa siku iliyotangulia sherehe ilikuwa haramu. Isitoshe, waamuzi wenyewe walitafuta mashahidi wa uwongo na kumshawishi Pilato aagize kuuawa kwa Yesu.—Mathayo 26:57-59; Yohana 11:47-53; 19:31.

Kulingana na Talmud, waamuzi wa kesi ya kifo walijitahidi kumwokoa mshtakiwa kwa kusikiliza kesi kwa makini katika vikao mbalimbali. Lakini kesi ya Stefano, kama ya Yesu pia, haikuwa hivyo. Kujitetea kwake mbele ya Sanhedrini kulifanya apigwe mawe na umati wa watu. Mtume Paulo pia angeuawa kwa njia hiyo kama Waroma hawangeingilia kati. Isitoshe, waamuzi wa Sanhedrini walipanga njama ya kumuua.—Matendo 6:12; 7:58; 23:6-15.

Angalau washiriki wachache wa mahakama hiyo walikuwa wanyoofu. Huenda kijana mmoja Myahudi mtawala, ambaye alizungumza na Yesu, alikuwa mshiriki wa Sanhedrini. Ingawa utajiri wa mtu huyo ulimzuia asichukue hatua, haikosi alikuwa na sifa nzuri kwa kuwa Yesu alimwalika awe mfuasi Wake.—Mathayo 19:16-22; Luka 18:18, 22.

Nikodemo, “mtawala wa Wayahudi” alimtembelea Yesu usiku, labda kwa sababu aliogopa maoni ya waamuzi wenzake. Hata hivyo, Nikodemo alimtetea Yesu mbele ya Sanhedrini kwa kuuliza hivi: “Je, sheria yetu humhukumu mtu isipokuwa kwanza iwe imesikia kutoka kwake na kujua analofanya?” Baadaye, Nikodemo alitoa “msokoto wa manemane na udi” ili mwili wa Yesu utayarishwe kwa ajili ya maziko.—Yohana 3:1, 2; 7:51, 52; 19:39.

Kwa ujasiri, Yosefu wa Arimathea, mshiriki mwingine wa Sanhedrini, alimwomba Pilato mwili wa Yesu, naye akauzika katika kaburi lake jipya. Yosefu alikuwa “akiungojea ufalme wa Mungu,” lakini kwa sababu aliogopa Wayahudi, hakujitambulisha kuwa mwanafunzi wa Yesu. Lakini Yosefu anastahili kusifiwa kwa sababu hakupiga kura kuunga mkono njama ya Sanhedrini ya kumuua Yesu.—Marko 15:43-46; Mathayo 27:57-60; Luka 23:50-53; Yohana 19:38.

Gamalieli, mshiriki wa Sanhedrini, aliwashauri kwa hekima waamuzi wenzake wawaache wanafunzi wa Yesu. Alisema hivi: “Ama sivyo, huenda mkaonwa kuwa kwa kweli mnapigana na Mungu.” (Matendo 5:34-39) Ni jambo gani lililozuia mahakama kuu isitambue kwamba Yesu na wanafunzi wake walitegemezwa na Mungu? Badala ya kukubali miujiza ya Yesu, Sanhedrini ilisema hivi: “Tufanye nini, kwa sababu mtu huyu anafanya ishara nyingi? Tukimwacha hivyo, hao wote watamwamini, na Waroma watakuja na kuondolea mbali mahali petu na taifa letu pia.” (Yohana 11:47, 48) Tamaa ya mamlaka ilizuia haki isitekelezwe na mahakama kuu ya Wayahudi. Pia, badala ya kufurahi wakati wanafunzi wa Yesu walipowaponya watu, viongozi wa dini ‘walijawa na wivu.’ (Matendo 5:17) Wakiwa waamuzi, walipaswa kumwogopa Mungu na kutenda haki, lakini, wengi wao walikuwa wafisadi na hawakuwa wanyoofu.—Kutoka 18:21; Kumbukumbu la Torati 16:18-20.

Hukumu ya Mungu

Kwa kuwa Waisraeli hawakutii Sheria ya Mungu na walimkataa Masihi, mwishowe Yehova alikataa taifa lao na hakuwaona tena kuwa watu wake. Mwaka wa 70 W.K., Waroma waliliharibu jiji la Yerusalemu na hekalu lake na kukomesha mfumo wote wa mambo wa Wayahudi na hatimaye Sanhedrini yenyewe.

Akiwa Mwamuzi aliyewekwa rasmi na Yehova, Yesu Kristo ataamua ikiwa yeyote wa washiriki wa Sanhedrini ya karne ya kwanza anastahili kufufuliwa na ni nani kati yao aliyetenda dhambi dhidi ya roho takatifu. (Marko 3:29; Yohana 5:22) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu atatenda kwa haki kamili atakapofanya maamuzi hayo.—Isaya 11:3-5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kuhusiana na Wamakabayo na Wahasmoni, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1998, ukurasa wa 21-24, na Juni 15, 2001, ukurasa wa 27-30.

^ fu. 16 Biblia inapozungumza kuhusu “wakuu wa makuhani,” inamaanisha makuhani wakuu wa sasa na wa zamani na watu wa familia hizo waliostahili kutumikia katika vyeo vikuu vya ukuhani baadaye.—Mathayo 21:23.