Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Methali

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Methali

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Methali

MFALME SULEMANI wa Israeli la kale “alikuwa na uwezo wa kusema methali elfu tatu.” (1 Wafalme 4:32) Je, tunaweza kupata maneno yake yenye hekima? Naam, tunaweza. Kitabu cha Biblia cha Methali kilichokamilishwa yapata mwaka wa 717 K.W.K., kina methali nyingi za Sulemani. Sura mbili za mwisho tu ndizo zilizoandikwa na waandishi wengine, yaani, Aguri mwana wa Yake na Mfalme Lemueli. Lakini wengine wanaamini kwamba Lemueli ni jina lingine la Sulemani.

Maneno yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu ambayo yamekusanywa katika kitabu cha Methali yana makusudi mawili, yaani, “ili mtu ajue hekima na nidhamu.” (Methali 1:2) Maneno hayo hutusaidia kupata hekima ambayo ni uwezo wa kuona mambo waziwazi na kutumia ujuzi ili kutatua matatizo. Kupitia maneno hayo, tunapata nidhamu au mafundisho ya maadili. Kuchunguza kwa makini methali hizo na kutii mashauri yake kunaweza kugusa moyo wetu, kutupa furaha, na kutuwezesha kufanikiwa.—Waebrania 4:12.

‘JIPATIE HEKIMA NA USHIKE NIDHAMU’

(Methali 1:1–9:18)

Sulemani anasema: “Hekima ya kweli huendelea kulia kwa sauti kubwa barabarani.” (Methali 1:20) Kwa nini tusikilize sauti yake kubwa na iliyo wazi? Sura ya pili inataja faida nyingi za kupata hekima. Sura ya tatu inazungumzia jinsi ya kuwa na urafiki wa karibu pamoja na Yehova. Kisha Sulemani anasema: “Hekima ndilo jambo kuu. Jipatie hekima; na pamoja na vyote unavyojipatia, jipatie uelewaji. Shika nidhamu; usiiache.”—Methali 4:7, 13.

Ni nini kitakachotusaidia kukataa njia zisizo za adili za ulimwengu? Sura ya tano ya Methali inajibu hivi: Tumia uwezo wa kufikiri na utambue njia zenye kushawishi za ulimwengu. Fikiria pia matokeo mabaya ya kuhusika katika ukosefu wa adili. Sura inayofuata inaonya juu ya mazoea na mitazamo inayohatarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova. Sura ya saba inafafanua vizuri matendo ya mtu asiye na maadili. Sura ya nane inaeleza thamani na ubora wa hekima kwa njia yenye kuvutia. Sura ya tisa ambayo ni umalizio wenye kusisimua wa methali zilizotangulia, ina mfano unaotuchochea kuwa wenye hekima.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:7; 9:10—Ni katika njia gani kumwogopa Yehova ni “mwanzo wa ujuzi” na “mwanzo wa hekima”? Bila kumwogopa Yehova hakuwezi kuwa na ujuzi kwa kuwa yeye ni Muumba wa vitu vyote na Mtungaji wa Maandiko. (Waroma 1:20; 2 Timotheo 3:16, 17) Yeye ndiye Chanzo cha ujuzi wote wa kweli. Hivyo, ujuzi huanza kwa kumwogopa Yehova. Pia, kumwogopa Mungu ni mwanzo wa hekima kwa sababu hakuwezi kuwa na hekima bila ujuzi. Isitoshe, mtu asiyemwogopa Yehova hawezi kutumia ujuzi wowote alio nao ili kumheshimu Muumba.

5:3—Kwa nini kahaba anaitwa “mwanamke mgeni”? Andiko la Methali 2:16, 17 linamfafanua “mwanamke mgeni” kuwa mtu “ambaye amelisahau agano la Mungu wake.” Mtu yeyote aliyeabudu miungu ya uwongo au kupuuza Sheria ya Musa, kutia ndani kahaba, aliitwa mgeni.—Yeremia 2:25; 3:13.

7:1, 2—Ni nini kinachohusishwa katika “maneno yangu” na “amri zangu”? Zaidi ya mafundisho ya Biblia, hayo yanatia ndani sheria au masharti ya familia ambayo wazazi wanaweka kwa faida ya familia. Watoto wanapaswa kutii sheria hizo na mafundisho ya Biblia ambayo wanapata kutoka kwa wazazi wao.

8:30—“Stadi wa kazi” ni nani? Hekima iliyopewa utu inajiita stadi wa kazi. Lugha hiyo ya mfano inatumiwa kueleza sifa za hekima na kumrejelea Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu, Yesu Kristo, kabla ya kuwa mwanadamu. Muda mrefu kabla ya kuzaliwa akiwa mwanadamu duniani, ‘alitokezwa akiwa mwanzo wa njia ya Mungu.’ (Methali 8:22) Akiwa “stadi wa kazi,” alifanya kazi kwa bidii pamoja na Baba yake wakati wa uumbaji wa vitu vyote.—Wakolosai 1:15-17.

9:17—Ni nini kinachomaanishwa na “maji ya kuibwa,” na kwa nini ni “matamu”? Kwa kuwa Biblia inafananisha kufurahia ngono katika ndoa na kunywa maji yenye kuburudisha yaliyotekwa katika kisima, maji ya kuibwa yanafananisha mahusiano haramu ya ngono yanayofanywa kwa siri. (Methali 5:15-17) Wazo la kufanya jambo na kuepuka kujulikana ndilo linalofanya maji hayo yaonekane kuwa matamu.

Mambo Tunayojifunza:

1:10-14. Tunapaswa kuepuka kushawishiwa na ahadi za utajiri za watenda-dhambi ambazo zitatuongoza kufuata njia zao mbaya.

3:3. Tunapaswa kuthamini sana fadhili zenye upendo na kweli na kuzionyesha waziwazi kama mkufu wenye thamani. Pia, tunapaswa kuandika sifa hizo moyoni mwetu, kwa kuzifanya ziwe sehemu muhimu ya maisha yetu.

4:18. Ujuzi wa kiroho huongezeka hatua kwa hatua. Ili tudumu katika nuru, ni lazima tuendelee kuwa wanyenyekevu na wapole.

5:8. Tunapaswa kujiepusha na mambo yasiyo ya adili iwe kupitia muziki, burudani, Intaneti, au vitabu na magazeti.

5:21. Je, mtu anayempenda Yehova ataharibu uhusiano wake pamoja na Mungu wa kweli ili kupata furaha ya muda? Hapana! Kichocheo kikuu cha kudumisha usafi wa kiadili ni kutambua kwamba Yehova anaona njia zetu na atatutoza hesabu.

6:1-5. Tunapata shauri zuri kama nini katika mistari hiyo kuhusu ‘kuwa mdhamini’ au kufanya makubaliano ya kifedha kwa niaba ya wengine bila kutumia hekima! Ikiwa baada ya kuchunguza jambo hilo kwa makini tunaona kwamba hatukutumia hekima, tunapaswa ‘kumsihi sana mwenzetu’ tena na tena na kufanya yote tuwezayo kusuluhisha mambo bila kukawia.

6:16-19. Mistari hiyo inataja mambo saba ya msingi ambayo yanahusisha karibu kila aina ya dhambi. Tunapaswa kuyachukia.

6:20-24. Kupata mazoezi ya kiroho tangu utotoni, kunaweza kumlinda mtu asinaswe na mtego wa ukosefu wa adili katika ngono. Wazazi hawapaswi kupuuza kuwazoeza watoto wao.

7:4. Tunapaswa kupenda hekima na uelewaji.

METHALI MOJA MOJA ZA KUTUONGOZA

(Methali 10:1–29:27)

Methali zilizobaki za Sulemani ni methali moja moja zinazoeleza mambo kwa ufupi. Zinaonyesha tofauti kati ya mambo na kuyalinganisha, nazo zina masomo muhimu kuhusu mwenendo, usemi, na mtazamo.

Sura ya 10 hadi ya 24 zinakazia umuhimu wa kumwogopa na kumheshimu Yehova. Methali zilizo katika sura ya 25 hadi ya 29 ziliandikwa na “watu wa Hezekia, mfalme wa Yuda.” (Methali 25:1) Methali hizo zinatufundisha kumtegemea Yehova na pia mambo mengine muhimu.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

10:6—‘Kinywa cha waovu hufunikaje jeuri’? Huenda ikawa hivyo katika maana ya kwamba waovu hutumia maneno matamu kuficha nia yao mbaya ya kuwadhuru wengine. Au kwa kuwa kwa kawaida waovu hutendewa kwa chuki, ukatili wanaotendewa na wengine huwanyamazisha.

10:10—Mtu “anayekonyeza jicho lake” hutokezaje maumivu? Zaidi ya kusema “maneno mapotovu,” “mtu asiyefaa kitu” anaweza pia kujaribu kuficha nia yake kwa ishara za mwili kama vile ‘kukonyeza jicho lake.’ (Methali 6:12, 13) Udanganyifu huo unaweza kumtaabisha sana kiakili yule anayetendewa hivyo.

10:29—“Njia ya Yehova” inamaanisha nini? Hiyo inamaanisha njia ambayo Yehova hushughulika na wanadamu, bali si jinsi tunavyopaswa kuishi. Jinsi Mungu anavyoshughulika na wanadamu huwawezesha wasio na lawama kupata usalama na waovu kuharibiwa.

11:31—Kwa nini mwovu anapata thawabu kubwa zaidi kuliko mwadilifu? Thawabu inayotajwa hapa ni adhabu ambayo kila mmoja wao anapata. Mwadilifu anapotenda dhambi, thawabu anayopata kwa makosa yake ni nidhamu. Mwovu hufanya dhambi kimakusudi na kukataa kutenda mema. Hivyo, anastahili na anapata adhabu kali.

12:23—Mtu ‘hufunikaje ujuzi’? Kufunika ujuzi hakumaanishi mtu hapaswi kuuonyesha. Badala yake, kunamaanisha kuuonyesha kwa busara, bali si kujionyesha au kujivuna kwa sababu ya kuwa nao.

14:17—Ni katika maana gani “mtu mwenye uwezo wa kufikiri huchukiwa”? Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “uwezo wa kufikiri” linaweza kumaanisha ufahamu au mawazo maovu. Bila shaka, mtu mwenye mawazo maovu huchukiwa. Mtu mwenye ufahamu anayetumia uwezo wake wa kufikiri na kuamua ‘kutokuwa sehemu ya ulimwengu’ huchukiwa pia.—Yohana 15:19.

18:19—Ni kwa njia gani “ndugu aliyekosewa ni mgumu kuliko mji wenye nguvu”? Kama mji wenye nguvu uliozingirwa, mtu huyo anaweza kukataa kusamehe. Ugomvi kati yake na yule aliyemkosea unaweza kuwa kizuizi kama vile “pingo la mnara wa makao.”

Mambo Tunayojifunza:

10:11-14. Ili maneno yetu yawe yenye kutia moyo, akili zetu zinapaswa kujazwa ujuzi sahihi, moyo wetu uchochewe na upendo, na tunapaswa kuongozwa na hekima tunapoongea.

10:19; 12:18; 13:3; 15:28; 17:28. Tunapaswa kufikiri kabla ya kuzungumza, na maneno yetu yawe machache.

11:1; 16:11; 20:10, 23. Yehova anataka tuwe wanyoofu katika shughuli zetu za kibiashara.

11:4. Ni upumbavu kutafuta utajiri huku tukipuuza funzo la kibinafsi la Biblia, kuhudhuria mikutano, kusali, na kuhubiri.

13:4. “Kutamani” pendeleo fulani kutanikoni au uzima katika ulimwengu mpya hakutoshi. Tunapaswa pia kuwa wenye bidii na kujitahidi sana kutimiza matakwa.

13:24; 29:15, 21. Mzazi mwenye upendo hambembelezi mtoto wake wala kupuuza makosa yake. Badala yake, baba au mama huchukua hatua za kusahihisha makosa kabla hayajasitawi.

14:10. Kwa kuwa hatuwezi kueleza hisia zetu za ndani kwa usahihi kila wakati wala watu wanaotutazama hawawezi kuzielewa, faraja ambayo wengine wanaweza kutoa ina mipaka. Huenda tukalazimika kuvumilia matatizo fulani kwa kumtegemea Yehova tu.

15:7. Hatupaswi kumwambia mtu kila kitu tunachojua mara moja, kama vile mkulima hamwagi mbegu zote mahali pamoja. Mtu mwenye hekima hutawanya ujuzi wake hatua kwa hatua kulingana na uhitaji.

15:15; 18:14. Kuwa na mtazamo mzuri wa akili kutatusaidia tuwe na shangwe hata tunapokabili hali ngumu.

17:24. Tofauti na “mjinga” ambaye macho yake na akili zake hutangatanga badala ya kukazia fikira mambo muhimu, tunapaswa kutafuta uelewaji ili tutende kwa hekima.

23:6-8. Tunapaswa kuepuka kuonyesha ukarimu kwa unafiki.

27:21. Kusifiwa kunaweza kufunua utu wetu. Unyenyekevu hufunuliwa ikiwa kusifiwa kunatuchochea kutambua kwamba tuna wajibu mbele za Yehova na kututia moyo tuendelee kumtumikia. Wakati sifa inapomchochea mtu kujihisi kuwa bora kuliko wengine, hiyo hufunua kwamba hana unyenyekevu.

27:23-27. Kwa kuzungumzia kazi ya uchungaji, methali hizo zinakazia umuhimu wa kuridhika na maisha rahisi kwa kufanya kazi kwa bidii. Zinapaswa hasa kutuonyesha uhitaji wa kumtegemea Mungu. *

28:5. ‘Tukimtafuta Yehova’ kupitia sala na kujifunza Neno lake, tunaweza “kuelewa kila jambo” linalohitajiwa ili kumtumikia kwa njia inayofaa.

“UJUMBE MZITO”

(Methali 30:1–31:31)

Kitabu cha Biblia cha Methali kinamalizia kwa sura mbili zenye “ujumbe mzito.” (Methali 30:1; 31:1) Kwa kutumia ulinganifu unaotuchochea kufikiri, ujumbe wa Aguri unaonyesha jinsi ambavyo pupa haiwezi kutoshelezwa na jinsi njia za mwanamume anayemshawishi mwanamwali zisivyoweza kujulikana. * Pia, ujumbe huo unaonya dhidi ya kujiinua na kuongea kwa hasira.

Ujumbe mzito ambao Lemueli alipokea kutoka kwa mama yake una mashauri mazuri kuhusu kutumia divai na kileo na pia kuhukumu kwa uadilifu. Ufafanuzi wa mke mwema unamalizika kwa maneno haya: “Mpeni baadhi ya matunda ya mikono yake, nazo kazi zake na zimsifu malangoni.”—Methali 31:31.

Pata hekima, kubali nidhamu, sitawisha kumwogopa Mungu, mtegemee Yehova. Methali zilizoongozwa kwa roho ya Mungu zina mafundisho yenye thamani kama nini! Basi, acheni tutumie mashauri ya methali hizo ili tupate furaha ya “mtu anayemwogopa Yehova.”—Zaburi 112:1.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 50 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 1991, ukurasa wa 31.

^ fu. 54 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1992, ukurasa wa 31.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yehova ndiye Chanzo cha ujuzi wote wa kweli

[Picha katika ukurasa wa 18]

‘Kutawanya ujuzi’ kunamaanisha nini?