Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Onyesha Upendo na Heshima kwa Kuzuia Ulimi Wako

Onyesha Upendo na Heshima kwa Kuzuia Ulimi Wako

Onyesha Upendo na Heshima kwa Kuzuia Ulimi Wako

“Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”—WAEFESO 5:33.

1, 2. Watu wote waliofunga ndoa wanapaswa kujiuliza swali gani muhimu, na kwa nini?

TUSEME umepata kifurushi chenye zawadi ambacho kina maandishi haya: “Tunza Vizuri.” Utakishughulikiaje kifurushi hicho? Bila shaka, utajitahidi sana kuepuka kukiharibu. Namna gani zawadi ya ndoa?

2 Yule mjane Mwisraeli Naomi aliwaambia hivi wasichana walioitwa Orpa na Ruthu: “Yehova na awape zawadi, na mpate mahali pa kupumzika kila mmoja katika nyumba ya mume wake.” (Ruthu 1:3-9) Biblia inasema hivi kuhusu mke mwema: “Urithi kutoka kwa akina baba ni nyumba na mali, lakini mke mwenye busara hutoka kwa Yehova.” (Methali 19:14) Ikiwa umefunga ndoa, unahitaji kumwona mwenzi wako kuwa zawadi kutoka kwa Mungu. Unaishughulikiaje zawadi ambayo umepewa na Mungu?

3. Ni shauri gani la Paulo ambalo waume na wake wanapaswa kutii?

3 Mtume Paulo alisema hivi alipowaandikia Wakristo wa karne ya kwanza: “Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33) Fikiria jinsi waume na wake wanavyoweza kutii shauri hilo kuhusiana na usemi wao.

Jihadhari na “Kitu Kitundu Chenye Kudhuru”

4. Ulimi unaweza kuwaje na matokeo mazuri au mabaya?

4 Mwandikaji wa Biblia Yakobo anasema kwamba ulimi ni “kitu kitundu chenye kudhuru” na kwamba “umejaa sumu yenye kuua.” (Yakobo 3:8) Yakobo alijua ukweli huu muhimu: Ulimi mtundu husababisha madhara. Bila shaka, alijua methali ya Biblia inayosema kwamba maneno yanayotamkwa bila kufikiri ni kama “upanga unaochoma.” Kwa upande mwingine, methali hiyohiyo inasema kuwa “ulimi wa mwenye hekima huponya.” (Methali 12:18) Naam, maneno yana nguvu sana. Yanaweza kuumiza, au kuponya. Mwenzi wako wa ndoa huhisije kuhusu maneno yako? Ikiwa ungemuuliza swali hilo, angejibuje?

5, 6. Ni mambo gani yanayofanya iwe vigumu kwa wengine kuuzuia ulimi?

5 Ikiwa mmeanza kutumia maneno yenye kuumiza katika ndoa yenu, mnaweza kuboresha hali hiyo. Hata hivyo, mnahitaji kujitahidi. Kwa nini? Kwanza, tunahitaji kupambana na hali yetu ya kutokamilika. Dhambi tuliyorithi huathiri jinsi tunavyofikiri kuhusu wengine na jinsi tunavyozungumza nao. Yakobo aliandika hivi: “Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu, anayeweza kuuongoza kwa lijamu mwili wake wote pia.”—Yakobo 3:2.

6 Zaidi ya hali ya wanadamu ya kutokamilika, malezi ambayo mtu alipata huchangia matumizi mabaya ya ulimi. Watu fulani walilelewa katika familia zenye wazazi ‘wasiotaka makubaliano yoyote, wasiojizuia, na wakali.’ (2 Timotheo 3:1-3) Mara nyingi, watoto wanaolelewa katika familia hizo huwa na tabia hizohizo wanapokuwa watu wazima. Ni kweli kwamba kutokamilika au malezi mabaya hayapaswi kuwa kisingizio cha kutumia maneno yenye kuumiza. Lakini kujua mambo hayo kunatusaidia kuelewa kwa nini watu fulani huona ni vigumu kuzuia ulimi usiseme mambo yenye kuumiza.

‘Ondoeni Masengenyo’

7. Petro alimaanisha nini alipowashauri Wakristo ‘waondoe namna zote za masengenyo’?

7 Hata sababu iwe nini, kutumia maneno yenye kuumiza katika ndoa kunaweza kuonyesha kwamba mtu hampendi wala hamheshimu mwenzi wake. Petro alikuwa na sababu nzuri ya kuwashauri Wakristo ‘waondoe namna zote za masengenyo.’ (1 Petro 2:1) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “masengenyo” linamaanisha “matusi.” Linaonyesha wazo la ‘kuwashambulia watu kwa maneno.’ Hilo linaonyesha vizuri sana madhara ya ulimi mtundu!

8, 9. Kutumia maneno yenye kuumiza kunaweza kusababisha nini, na kwa nini wenzi wa ndoa wanapaswa kuepuka kufanya hivyo?

8 Huenda kutumia matusi kusionekane kuwa jambo zito, lakini fikiria yale yanayotukia wakati mume au mke anapotumia matusi. Kumwita mwenzi wa ndoa mjinga, mvivu, au mchoyo kunaonyesha kwamba utu wake unaweza kufafanuliwa kwa neno moja tu la dharau. Huo ni ukatili. Namna gani maneno yaliyotiwa chumvi yanayokazia kasoro za mwenzi wa ndoa? Je, mtu hatii chumvi anaposema hivi, “Wewe huchelewa kila wakati” au “Wewe hunisikilizi kamwe”? Yaelekea maneno hayo yatamfanya mwenzi wako atake kujitetea, nayo yanaweza kusababisha mabishano makali.—Yakobo 3:5.

9 Mazungumzo yaliyojaa matusi husababisha mkazo katika ndoa, na hilo pia linaweza kusababisha matokeo mabaya. Andiko la Methali 25:24 linasema hivi: “Ni afadhali kukaa pembeni mwa paa kuliko kukaa pamoja na mke mgomvi, ingawa ni katika nyumba moja.” Bila shaka, hilo linamhusu mume mgomvi pia. Hatua kwa hatua, maneno yenye kuumiza yanayosemwa na mwenzi yeyote yanaweza kuharibu uhusiano, na labda kumfanya mume au mke ahisi kwamba hapendwi au hata hastahili kupendwa. Ni wazi kwamba ni muhimu kuuzuia ulimi. Lakini hilo linaweza kufanywaje?

‘Ongoza Ulimi’

10. Kwa nini ni muhimu kuuzuia ulimi?

10 Andiko la Yakobo 3:8 linasema hivi: “Ulimi, hakuna hata mmoja wa wanadamu anayeweza kuufuga.” Hata hivyo, kama vile mwendeshaji wa farasi anavyotumia lijamu ili kumwongoza mnyama huyo, tunapaswa kujitahidi tuwezavyo kuuongoza ulimi wetu. “Ikiwa mtu yeyote anajiona kuwa mwabudu anayeshikilia vizuri namna ya ibada na bado hauongozi ulimi wake, bali anaendelea kuudanganya moyo wake mwenyewe, namna ya ibada ya mtu huyo ni ya ubatili.” (Yakobo 1:26; 3:2, 3) Maneno hayo yanaonyesha kwamba jinsi unavyotumia ulimi wako ni jambo zito. Jambo hilo haliathiri tu uhusiano wako pamoja na mwenzi wako bali pia uhusiano wako pamoja na Yehova Mungu.—1 Petro 3:7.

11. Ni mambo gani yanayoweza kufanywa ili kuzuia hali ya kutoelewana isigeuke kuwa mabishano makali?

11 Ni jambo la hekima kufikiria jinsi unavyozungumza na mwenzi wako. Mkazo unapotokea, jaribu kuupunguza. Fikiria hali iliyotokea kati ya Isaka na mke wake Rebeka, kama inavyosimuliwa kwenye Mwanzo 27:46–28:4. “Rebeka akawa akimwambia Isaka: ‘Nimekuja kuyachukia sana haya maisha yangu kwa sababu ya binti za Hethi. Yakobo akichukua mke kutoka kwa binti za Hethi kama hawa kutoka kwa binti za hii nchi, basi maisha yana faida gani kwangu?’” Hakuna jambo lolote linaloonyesha kwamba Isaka alijibu kwa ukali. Badala yake, alimtuma mwana wao Yakobo atafute mke anayemwogopa Mungu ambaye hangemtaabisha Rebeka. Tuseme hali ya kutoelewana imetokea kati ya mume na mke wake. Unaweza kuzuia jambo hilo lisigeuke kuwa mabishano makali kwa kutumia busara na kubadili neno “wewe” liwe “mimi.” Kwa mfano, badala ya kusema “Wewe hutumii wakati pamoja nami kamwe!” unaweza kusema, “Mimi ningefurahia ikiwa tungeweza kutumia wakati mwingi pamoja.” Kazia fikira tatizo lenyewe bali si mtu mwenyewe tu. Epuka kujaribu kuonyesha ni nani aliye na kosa na ni nani asiye na kosa. Andiko la Waroma 14:19 linasema hivi: “Tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani na mambo ambayo ni ya kujengana.”

Ondolea Mbali ‘Uchungu Wenye Uovu, Hasira, na Ghadhabu’

12. Ili kuzuia ulimi, tunapaswa kusali kwa ajili ya nini, na kwa nini?

12 Mengi yanahusika katika kuzuia ulimi kuliko tu kujihadhari kuhusu mambo tunayosema. Kwa kweli, maneno yetu hutoka moyoni bali si kinywani. Yesu alisema: “Mtu mwema hutokeza mema katika hazina njema ya moyo wake, lakini mtu mwovu hutokeza maovu katika hazina yake mbovu; kwa maana kutokana na wingi wa moyo kinywa chake husema.” (Luka 6:45) Hivyo, ili kuzuia ulimi wako, huenda ukahitaji kusali hivi kama alivyofanya Daudi: “Uumbe moyo safi ndani yangu, Ee Mungu, na kuweka ndani yangu roho mpya, iliyo imara.”—Zaburi 51:10.

13. Uchungu wenye uovu, hasira, na ghadhabu zinaweza kusababishaje matukano?

13 Paulo aliwahimiza Waefeso waepuke maneno yenye kuumiza na hata hisia zinazoyachochea. Aliandika hivi: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.” (Waefeso 4:31) Ona kwamba kabla ya kutaja “kupiga kelele na matukano,” Paulo alitaja “uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu.” Ghadhabu inayochemka ndani ya mtu ndiyo hutaka kulipuka na kumfanya aropoke maneno yenye kuumiza. Basi, jiulize hivi: ‘Je, mimi huendelea kuwa na uchungu na ghadhabu moyoni? Je, mimi nina “mwelekeo wa ghadhabu”?’ (Methali 29:22) Ikiwa wewe hufanya hivyo, sali Mungu akusaidie kushinda mielekeo hiyo na kujizuia ili uweze kuepuka milipuko ya hasira. Zaburi 4:4 inasema: “Fadhaikeni, lakini msitende dhambi. Semeni moyoni mwenu, kitandani mwenu, na kunyamaza.” Ukiona hasira inazidi na unaogopa kwamba hutaweza kujizuia, fuata shauri hili la Methali 17:14: “Kabla mabishano hayajalipuka, jiondokee.” Epuka hali hiyo kwa muda mfupi mpaka hasira ipungue.

14. Kinyongo kinaweza kuathirije ndoa?

14 Si rahisi kuzuia ghadhabu na hasira hasa ikiwa inatokana na kile ambacho Paulo anakiita “uchungu wenye uovu.” Neno la Kigiriki ambalo Paulo alitumia limefafanuliwa kuwa “roho ya kuweka kinyongo ambayo hukataa kusuluhisha mambo” na ‘roho mbaya ya kuhesabu makosa.’ Nyakati nyingine, uhasama huwa kama ukuta mkubwa kati ya mume na mke na hali hiyo inaweza kuendelea kwa muda mrefu. Hali ya kutoelewana isipotatuliwa kabisa, hilo linaweza kusababisha dharau. Lakini ni ubatili kuweka kinyongo kwa sababu ya makosa ya zamani. Maji yakimwagika hayazoleki. Mtu akisamehe kosa la mwingine, anapaswa kulisahau. Upendo “hauweki hesabu ya ubaya.”—1 Wakorintho 13:4, 5.

15. Ni jambo gani litakalowasaidia wale waliozoea kutumia maneno makali kufanya mabadiliko?

15 Namna gani ikiwa ulilelewa katika familia ambamo maneno makali yalitumiwa na umezoea kuyatumia? Unaweza kufanya mabadiliko. Tayari umejiwekea mipaka kuhusu mambo fulani maishani, na kuna mambo ambayo huwezi kukubali kuyafanya. Utaweka mpaka wapi kuhusiana na usemi wako? Je, utanyamaza kabla maneno yako hayajageuka kuwa matusi? Huenda ungependa kujiwekea mpaka unaotajwa kwenye Waefeso 4:29: “Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu.” Ili ufanye hivyo, unahitaji ‘kuvua utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na ujivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba.’—Wakolosai 3:9, 10.

Ni Lazima Muwe na “Mazungumzo ya Siri”

16. Kwa nini kukataa kuzungumza na mwenzi wa ndoa husababisha madhara katika ndoa?

16 Mume au mke hatimizi lolote anapokataa kuongea na mwenzi wake, badala yake kufanya hivyo kunaweza kusababisha madhara. Nyakati nyingine mtu hafanyi hivyo ili kumwadhibu mwenzi wake. Huenda akafanya hivyo kwa sababu ya kufadhaika au kuvunjika moyo. Lakini kukataa kuzungumza na mwenzi wako huongeza tu mkazo na si suluhisho kwa tatizo lenyewe. Mke mmoja alisema hivi: “Tunapoanza kuzungumza tena, huwa hatujasuluhisha tatizo lenyewe.”

17. Wakristo wanaokabili mkazo katika ndoa wanapaswa kufanya nini?

17 Mkazo katika ndoa unapoendelea, hakuna njia ya mkato ya kusuluhisha mambo. Andiko la Methali 15:22 linasema hivi: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri, lakini katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.” Unahitaji kuketi pamoja na mwenzi wako wa ndoa na kuzungumzia jambo hilo. Jitahidi sana kumsikiliza mwenzi wako ukiwa na maoni yanayofaa. Ikiwa haiwezekani kufanya hivyo, kwa nini usiwaendee wazee katika kutaniko la Kikristo? Wanajua Maandiko na wana uzoefu wa kutumia kanuni za Biblia. Wanaume hao ni “kama mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua.”—Isaya 32:2.

Unaweza Kushinda Pambano Hilo

18. Ni pambano gani linalozungumziwa kwenye Waroma 7:18-23?

18 Tunahitaji kupambana ili kuongoza ulimi wetu. Tunahitaji kupambana pia ili kuongoza matendo yetu. Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu tatizo alilokabili: “Najua kwamba ndani yangu, yaani, ndani ya mwili wangu, halikai jambo lolote jema; kwa maana nina uwezo wa kutaka, bali uwezo wa kufanya yaliyo mazuri haupo. Kwa maana lile jema ninalotaka silifanyi, bali lile baya nisilotaka ndilo ninalozoea kulifanya. Basi, ikiwa lile nisilotaka ndilo ninalofanya, anayelifanya hilo si mimi tena, bali ni ile dhambi inayokaa ndani yangu.” Kwa sababu ya “sheria ya dhambi iliyo ndani ya viungo [vyetu],” tuna mwelekeo wa kutumia vibaya ulimi wetu na viungo vingine vya mwili. (Waroma 7:18-23) Hata hivyo, ni lazima tupambane, na tunaweza kushinda kwa msaada wa Mungu.

19, 20. Kielelezo cha Yesu kinaweza kuwasaidiaje waume na wake kuongoza ulimi wao?

19 Watu walio katika uhusiano wenye upendo na heshima hawatasema bila kufikiri wala kutumia maneno makali. Fikiria kielelezo cha Yesu Kristo kuhusiana na jambo hilo. Yesu hakuwatusi kamwe wanafunzi wake. Hata usiku wa mwisho wa maisha yake hapa duniani wakati mitume wake walipokuwa wakibishana kuhusu ni nani kati yao aliye mkuu zaidi, Mwana wa Mungu hakuwagombeza. (Luka 22:24-27) Biblia inashauri hivi: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.”—Waefeso 5:25.

20 Namna gani mke? Anapaswa “kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33) Je, mke anayemheshimu mume wake anaweza kumfokea na kumtukana? Paulo aliandika hivi: “Nataka mjue kwamba kichwa cha kila mwanamume ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Wakorintho 11:3) Wake wanapaswa kujitiisha kwa kichwa chao kama vile Kristo anavyojitiisha kwa Kichwa chake. (Wakolosai 3:18) Ingawa hakuna mwanadamu asiye mkamilifu anayeweza kumwiga Yesu kwa ukamili, kujitahidi ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu’ kutawasaidia waume na wake kushinda pambano dhidi ya kutumia ulimi vibaya.—1 Petro 2:21.

Umejifunza Nini?

• Ulimi mtundu unaweza kuharibuje ndoa?

• Kwa nini ni vigumu kuongoza ulimi?

• Ni nini kinachotusaidia kuzuia ulimi wetu?

• Unapaswa kufanya nini unapokabili mkazo katika ndoa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24]

Wazee hutoa msaada kupitia Biblia