Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kutaniko lina daraka gani ikiwa Mkristo anayeendesha gari anahusika katika msiba wa barabarani unaosababisha kifo cha watu wengine?

Msiba wa barabarani unapotokea, uwezekano wa kuwa na hatia ya damu unapaswa kuchunguzwa kwa sababu kutaniko linahitaji kuepuka daraka la kijamii la hatia ya damu. (Kumbukumbu la Torati 21:1-9; 22:8) Dereva anayesababisha msiba barabarani ambao unasababisha kifo anaweza kuwa na hatia ya damu ikiwa hakuwa mwangalifu au alivunja kimakusudi mojawapo ya sheria za Kaisari za usalama barabarani. (Marko 12:14) Lakini kuna mambo mengine ya kufikiria.

Muuaji aliyekimbilia mojawapo ya majiji ya makimbilio ya Israeli alipaswa kuhukumiwa. Ikiwa ingegunduliwa kwamba mauaji hayo hayakuwa ya kukusudiwa, angeruhusiwa kubaki katika jiji hilo akiwa salama kutoka kwa mlipiza-kisasi cha damu. (Hesabu 35:6-25) Hivyo, ikiwa Mkristo anasababisha kifo cha mtu katika msiba wa barabarani, wazee wanapaswa kuchunguza kisa hicho ili kuhakikisha iwapo kuna hatia ya damu kwa kadiri fulani. Maoni ya serikali au uamuzi wa mahakama peke yake haupaswi kutumiwa kuamua hatua ambayo itachukuliwa na kutaniko.

Kwa mfano, mahakama inaweza kuamua kwamba mtu huyo ana hatia ya kuvunja sheria fulani za barabarani, lakini wazee wanaochunguza kesi hiyo wanaweza kuamua kwamba mtu huyo hana hatia ya damu kwa sababu hangeweza kuzuia hali zilizosababisha msiba huo. Kwa upande mwingine, hata mahakama ikitupilia mbali kesi hiyo, huenda wazee wakaamua kwamba mtu huyo ana hatia ya damu.

Uamuzi wa wazee wanaochunguza kesi hiyo unapaswa kutegemea Maandiko na mambo ya hakika yaliyothibitishwa, yaani, ikiwa dereva amekubali kwamba ana hatia na/au ushuhuda wa mashahidi wawili au watatu waliojionea kisa hicho. (Kumbukumbu la Torati 17:6; Mathayo 18:15, 16) Ikithibitishwa kwamba ana hatia ya damu, halmashauri ya hukumu inapaswa kuundwa. Halmashauri hiyo ikiona kwamba mtu huyo mwenye hatia ya damu ametubu, atapewa karipio la Kimaandiko linalofaa, naye hatakubaliwa kuwa na mapendeleo kutanikoni. Hataendelea kutumikia akiwa mzee au mtumishi wa huduma. Huenda pia akawekewa vizuizi vingine. Isitoshe, atatoa hesabu mbele za Mungu kwa sababu ya kukosa uangalifu, kuwa mzembe, au kukosa kuwa makini na hivyo kusababisha msiba na kifo.—Wagalatia 6:5, 7.

Kwa mfano: Ikiwa hali ya hewa ilikuwa mbaya wakati wa msiba huo, dereva alipaswa kuwa makini sana. Ikiwa alikuwa na usingizi, angesimamisha gari ili apumzike mpaka usingizi uishe, au angemwomba mtu mwingine aendeshe gari hilo.

Tuseme dereva alikuwa anaendesha gari kwa kasi mno. Mkristo yeyote akipitisha mwendo unaokubalika kisheria, basi anakosa kumpa “Kaisari vitu vya Kaisari.” Pia, hilo linaonyesha kwamba haheshimu utakatifu wa uhai kwa sababu anaweza kusababisha kifo. (Mathayo 22:21) Kuhusiana na suala hilo, fikiria jambo lingine. Mzee anayepuuza sheria za barabarani za Kaisari au kuzivunja kimakusudi analiwekea kundi kielelezo gani?—1 Petro 5:3.

Wakristo hawapaswi kuwaomba wengine wafike mahali fulani kwa wakati ambao utawafanya walazimike kuendesha gari kwa kasi sana na hivyo kupitisha mwendo unaokubalika kisheria. Kwa kawaida, inafaa kuanza safari mapema vya kutosha au kubadili ratiba ili kuwa na wakati wa kutosha wa kusafiri. Mkristo anapofanya hivyo, hatashawishiwa kuendesha gari kwa mwendo wa kuvunja sheria, lakini ataweza kutii sheria za barabarani za “mamlaka zilizo kubwa” za kiserikali. (Waroma 13:1, 5) Jambo hilo litamwezesha dereva kuepuka kusababisha kifo na uwezekano wa kuwa na hatia ya damu. Pia, litamwezesha kuweka kielelezo kizuri na kudumisha dhamiri njema.—1 Petro 3:16.