Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alipendezwa na Sheria ya Yehova

Alipendezwa na Sheria ya Yehova

Alipendezwa na Sheria ya Yehova

ALBERT D. SCHROEDER, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alikufa mnamo Jumatano, Machi 8, 2006 akiwa na tumaini la kwenda mbinguni. Alikuwa na umri wa miaka 94 na alikuwa mtumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 73.

Ndugu Schroeder alizaliwa huko Saginaw, Michigan, Marekani, mwaka wa 1911. * Akiwa mtoto, alijifunza mambo mengi kuhusu Biblia kutoka kwa nyanya yake wa upande wa mama, ambaye alimchochea kupenda kusoma Neno la Yehova. Alijifunza Kilatini, Kijerumani, na uinjinia wa umeme kwenye Chuo Kikuu cha Michigan. Hata hivyo, alipozidi kuthamini Maandiko, aliacha masomo yake ili kufanya kazi ya kuhubiri wakati wote kuhusu Ufalme. Mwaka wa 1932 akawa mshiriki wa familia ya Betheli huko Brooklyn, New York.

Mwaka wa 1937, akiwa na umri wa miaka 26, Ndugu Schroeder aliwekwa rasmi kusimamia kazi ya Mashahidi wa Yehova huko Uingereza. Bidii yake katika kazi ya kuhubiri iliwatia moyo wengi huko Uingereza kuanza utumishi wa wakati wote. Kijana mmoja aliyeshirikiana naye katika Betheli ya London alikuwa John E. Barr. Baadaye, walitumika pamoja kwa miaka mingi katika Baraza Linaloongoza.

Kazi ambayo Ndugu Schroeder alifanya kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova ilitambuliwa katika miaka ya vita. Mnamo Agosti 1942, alifukuzwa Uingereza. Baada ya safari ngumu wakati wa vita kupitia Bahari ya Atlantiki, alifika Brooklyn mwezi wa Septemba.

Wakati huo, watumishi wa Yehova walikuwa wanatazamia kwamba kazi kubwa ingehitaji kufanywa baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Ndugu Schroeder alishangaa na kufurahi alipopokea mgawo mwingine, yaani, kusaidia kuanzisha Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Kwa miaka kadhaa alikuwa mwalimu wa shule hiyo, akisaidia kuwazoeza wamishonari. Wanafunzi ambao alifundisha katika Shule ya Gileadi na baadaye katika Shule ya Huduma ya Ufalme wanakumbuka sana jinsi alivyowafundisha. Alifurahia kuwachochea wanafunzi wake kupenda sheria za Mungu, na alikazia umuhimu wa kumjua Yehova.

Mwaka wa 1956, Ndugu Schroeder alimwoa Charlotte Bowin, na mwaka wa 1958, mwana wao Judah Ben akazaliwa. Ndugu Schroeder alikuwa mume na baba Mkristo mwema. Mwaka wa 1974 alianza kutumikia katika Baraza Linaloongoza, ambako ufahamu wake ulithaminiwa sana. Alikuwa mtu mwenye fadhili na mnyenyekevu ambaye alitaka hasa kulitukuza jina kuu la Mungu. Tuna uhakika kwamba Ndugu Schroeder amepokea thawabu yake huko mbinguni akiwa Mkristo mtiwa-mafuta ambaye ‘alipendezwa na sheria ya Yehova.’—Zaburi 1:2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Simulizi la maisha la Ndugu Schroeder lilichapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1988.