Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Zawadi ya Milele Kutoka kwa Muumba

Zawadi ya Milele Kutoka kwa Muumba

Zawadi ya Milele Kutoka kwa Muumba

JE, HUSHANGAI kwamba hali ambazo wanasayansi wanaamini kuwa ni muhimu kwa uhai katika sayari yoyote ile zinatajwa au kuzungumziwa moja kwa moja katika sura ya kwanza ya Biblia? Ni hali gani hizo?

Ili uhai usitawi, lazima kuwe na maji mengi sana kama inavyotajwa katika Mwanzo 1:2. Lazima kuwe na kiwango kinachofaa kabisa cha joto kwenye sayari hiyo ili maji yaendelee kuwa majimaji. Ili kuwe na kiwango hicho cha joto, ni lazima sayari hiyo iwe umbali unaofaa kabisa kutoka kwenye jua lake. Masimulizi ya Mwanzo yanataja tena na tena jua na jinsi linavyoisaidia dunia.

Ili sayari ikaliwe na watu, inapaswa kuwa na angahewa iliyo na mchanganyiko hususa wa gesi mbalimbali. Hali hiyo muhimu inatajwa katika Mwanzo 1:6-8. Kukua kwa mimea inayotajwa katika Mwanzo 1:11, 12, kunasaidia kutokeza kiasi kikubwa cha oksijeni. Sayari ambamo wanyama wa aina mbalimbali wanaweza kuishi inapaswa kuwa na mabara ya nchi kavu inayozaa kama ile inayotajwa katika Mwanzo 1:9-12. Mwishowe, ili kuwe na hali ya hewa inayofaa, lazima sayari iiname kwenye pembe inayofaa kabisa na ibaki papo hapo. Dunia imekaa hivyo kwa sababu ya nguvu za uvutano za mwezi wetu. Hali hiyo na baadhi ya faida zake zinatajwa katika Mwanzo 1:14, 16.

Musa, mwandikaji wa zamani, ambaye hakuwa na elimu ya kisasa ya sayansi angeweza kujua mambo hayo namna gani? Je, alikuwa na uwezo usio wa kawaida wa kuelewa umuhimu wa mambo hayo, uwezo ambao watu wa siku zake hawakuwa nao? Alieleza mambo hayo kwa sababu aliongozwa na roho ya Muumba wa mbingu na dunia. Hilo ni jambo muhimu hasa tunapofikiria usahihi wa masimulizi ya Mwanzo.

Biblia inaonyesha waziwazi kwamba maajabu ya ulimwengu unaotuzunguka yana kusudi fulani. “Mbingu ni mbingu za Yehova,” inasema Zaburi 115:16, “Bali dunia amewapa wana wa binadamu.” Zaburi nyingine inasema: “Ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Ikiwa ulimwengu na dunia yetu maridadi ilibuniwa na kutokezwa na Muumba, bila shaka si vigumu kuamini kwamba yeye ana uwezo wa kutegemeza ulimwengu na dunia. Hilo linamaanisha kwamba unaweza kutarajia kwa uhakika kutimizwa kwa ahadi hii nzuri sana: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Kwa kweli, Mungu “hakuiumba [dunia] tu bila sababu” lakini “aliiumba ili ikaliwe” milele na wanadamu wanaothamini na kuheshimu kazi zake.—Isaya 45:18.

Kulingana na Maandiko, Yesu alikuja duniani ili kutufundisha kumhusu Mungu na kusudi Lake la kuwapa wanadamu watiifu uzima wa milele. (Yohana 3:16) Tunahakikishiwa kwamba hivi karibuni Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia,’ nao watu wanaopenda amani kutoka mataifa yote na ambao wanakubali maandalizi yake ya wokovu wataokoka. (Ufunuo 7:9, 14; 11:18) Maisha yatakuwa yenye kufurahisha kama nini kadiri wanadamu watakavyoendelea milele kugundua na kupendezwa na maajabu ya uumbaji wa Mungu!—Mhubiri 3:11; Waroma 8:21.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]

NASA photo