Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ujenzi wa Kiroho Katika “Nyumba ya Mawe”

Ujenzi wa Kiroho Katika “Nyumba ya Mawe”

Ujenzi wa Kiroho Katika “Nyumba ya Mawe”

Jina la nchi hii ya Afrika linamaanisha “Nyumba ya Mawe.” Ni nchi inayojulikana sana kwa sababu ya Maporomoko ya Viktoria na kwa sababu ina wanyama mbalimbali wa porini. Hata hivyo, ina majengo makubwa zaidi na ya zamani zaidi kuwahi kujengwa na mwanadamu kusini mwa Sahara. Sehemu ya kati ya nchi hiyo ina uwanda wa juu wenye mawe ya matale. Kwa sababu ya hali nzuri ya hewa, uwanda huo una udongo wenye rutuba na mimea mingi. Nchi hiyo ni Zimbabwe, nchi yenye wakaaji milioni 12 hivi.

KWA nini iliitwa Nyumba ya Mawe? Mnamo 1867, Adam Renders, ambaye alikuwa mwindaji na mvumbuzi, aliona magofu makubwa ya mawe katika eneo lenye ukubwa wa ekari 1,800. Alikuwa akisafiri kwenye mbuga za Afrika ambako kwa kawaida nyumba zilijengwa kwa udongo, miti, na kuezekwa nyasi. Kisha, akafika kwenye magofu ya mawe ya jiji kubwa, ambalo sasa linaitwa Great Zimbabwe.

Magofu hayo yako kusini mwa eneo ambalo sasa linaitwa Masvingo. Kuta nyingine zina kimo cha mita 9, na mawe ya matale yamepangwa moja juu ya lingine bila kushikanishwa na sementi. Katika magofu hayo, kuna mnara wa pekee wenye umbo la pia unaofikia mita 11 hivi kutoka kwenye jukwaa la mviringo lenye kipenyo cha mita 6. Kusudi la jengo hilo bado halijulikani. Magofu yake ni ya karne ya nane W.K., lakini kuna uthibitisho wa kwamba eneo hilo lilikaliwa mamia ya miaka kabla ya wakati huo.

Mnamo 1980 nchi hiyo ambayo ilikuwa ikiitwa Rhodesia, ilipata uhuru kutoka kwa Uingereza na ikapewa jina Zimbabwe. Wakaaji wa nchi hiyo wanatoka katika makabila mawili makubwa, yaani, Washona, ambao ni wengi zaidi, na Wandebele. Watu hao ni wakarimu, na mara nyingi Mashahidi wa Yehova wametambua jambo hilo wanapofanya kazi yao ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Nyakati nyingine, hata kabla mgeni hajajitambulisha, mara tu anapobisha mlango, anakaribishwa kwa kuambiwa “Ingia ndani” na “Tafadhali keti.” Wazimbabwe wengi wanaheshimu sana Biblia na mara nyingi wanasisitiza kwamba watoto wao waketi na kusikiliza wakati wa mazungumzo ya Biblia.

Kutoa Ujumbe wa Faraja Wenye Kujenga

“UKIMWI” na “ukame” ni maneno yanayotumiwa sana na vyombo vya habari nchi ya Zimbabwe inapozungumziwa. Kuenea kwa UKIMWI kumeathiri sana idadi ya watu na uchumi wa nchi za Afrika zilizo kusini ya jangwa la Sahara. Mara nyingi watu wanaolazwa hospitalini nchini humo wana virusi vya UKIMWI. Ugonjwa huo umeharibu maisha ya familia nyingi.

Ili kuwasaidia watu wa Zimbabwe, Mashahidi wa Yehova wanatangaza kwa bidii kwamba njia bora ya maisha ni ile inayoongozwa na viwango vya Mungu vilivyo katika Biblia. Kwa mfano, Neno la Mungu linafundisha kwamba ngono ni zawadi kutoka kwa Mungu na inapaswa kufurahiwa katika ndoa tu, na kwamba ngono ya watu wa jinsia moja haikubaliwi na Mungu, na kwamba sheria ya Yehova inakataza kutiwa damu mishipani na kutumia dawa za kulevya ili kujifurahisha. (Matendo 15:28, 29; Waroma 1:24-27; 1 Wakorintho 7:2-5; 2 Wakorintho 7:1) Pia, Mashahidi wanaeneza ujumbe unaotoa tumaini hakika, unaokazia kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa magonjwa yote.—Isaya 33:24.

Kutoa Misaada

Ukame umeathiri sana nchi ya Zimbabwe katika miaka 10 iliyopita. Wanyama wa porini wamekufa kutokana na njaa na ukosefu wa maji. Mamia ya maelfu ya ng’ombe wamekufa. Misitu mikubwa imeteketezwa. Watoto na wazee wengi wamekufa kwa sababu ya utapiamlo. Hata maji ya Mto Zambezi ulio mkubwa sana yalipungua na kuathiri vituo vinavyotumia maji kuzalisha umeme.

Kwa sababu ya hali hiyo mbaya sana, Mashahidi wa Yehova walianzisha halmashauri nane za kutoa misaada katika sehemu mbalimbali za nchi. Waangalizi wanaosafiri walitembelea makutaniko ili kuchanganua mahitaji hususa. Kisha, halmashauri ya misaada inayohusika ikapewa habari kuhusu mahitaji hayo. Mwangalizi mmoja anayesafiri alisema hivi: “Katika miaka mitano iliyopita, tumegawa zaidi ya tani 1,000 za mahindi, tani 10 za samaki waliokaushwa, na kiasi kama hicho cha maharagwe. Ndugu zetu wa kiroho walitayarisha tani mbili za mufushwa [mboga zilizokaushwa]. Pia, tuligawa kiasi kikubwa sana cha nguo zilizotolewa kama mchango na pesa zilizohitajiwa.” Mwangalizi mwingine anayesafiri alisema hivi: “Ninapofikiria matatizo ambayo tumekabili ili kupata vibali vinavyohitajiwa na serikali ya Zimbabwe na ya Afrika Kusini ili kuleta misaada na pia upungufu wa daima wa petroli inayohitajiwa ili kusafirisha misaada hiyo inayohitajiwa sana, ninaweza kusema tu kwamba mafanikio yetu yanathibitisha zaidi uhakikisho wa Yesu kwamba Baba yetu wa mbinguni anajua tunahitaji vitu hivi vyote.”—Mathayo 6:32.

Waangalizi wanaosafiri wanakabiliana jinsi gani na hali hizo wanapotumika katika maeneo yenye ukame? Wengine wanabeba chakula chao na cha familia ambazo wataishi nazo. Mmoja wao alisema kwamba dada fulani Wakristo walikuwa wakijadiliana ikiwa ingefaa waache kuhubiri siku hiyo ili wapange msururu wa kungoja msaada kutoka kwa serikali. Waliamua kumtumaini Yehova na kukazia fikira kazi ya kuhubiri huku wakingoja waone jinsi mambo yatakavyokuwa. Siku hiyo msaada wa serikali haukuletwa.

Mkutano wa Kikristo ulipangiwa siku iliyofuata, na dada hao walihitaji kufanya uamuzi tena. Je, wangehudhuria mkutano, au wangeenda kungoja msaada ufike? Waliamua kutanguliza mambo yanayofaa na kuhudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme. (Mathayo 6:33) Walipokuwa wakiimba wimbo wa mwisho, walisikia gari kubwa likija. Msaada ulifika kwenye Jumba la Ufalme. Uliletwa na ndugu zao wa kiroho wa halmashauri ya kutoa misaada! Mashahidi waaminifu waliohudhuria mkutano huo walijawa na shangwe nyingi nao wakashukuru sana.

Upendo Unajenga

Matendo ya fadhili kuelekea wale walio nje ya kutaniko la Kikristo yametoa nafasi ya kutoa ushahidi mzuri. Mwangalizi mmoja anayesafiri katika eneo la Masvingo, pamoja na Mashahidi kadhaa wenyeji, walikuwa wakihubiri. Walimwona msichana aliyelala kando ya barabara. Mashahidi hao walitambua kwamba alikuwa mgonjwa sana kwa kuwa hangeweza kuzungumza vizuri na sauti yake ilikuwa ikitetemeka. Msichana huyo aliitwa Hamunyari, jina la Kishona linalomaanisha “Je, Hamwoni Aibu?” Ndugu hao walipata habari kwamba msichana huyo alikuwa ameachwa na washiriki wa kanisa lao ambao walienda kuabudu milimani. Mashahidi hao walimsaidia kwa upendo na kumpeleka katika kijiji kilichokuwa karibu.

Katika kijiji hicho, watu fulani walimjua Hamunyari, kwa hiyo wakawaita watu wake wa ukoo waje kumchukua. Wanakijiji walisema hivi kuhusu Mashahidi: “Hii ndiyo dini ya kweli. Huu ndio upendo ambao Wakristo wanapaswa kuonyesha.” (Yohana 13:35) Kabla ya kuondoka, ndugu walimpa Hamunyari trakti Je, Ungependa Kujua Mengi Zaidi Kuhusu Biblia? *

Juma lililofuata mwangalizi huyo anayesafiri alitembelea kutaniko la eneo anakoishi Hamunyari. Alitaka kujua ikiwa Hamunyari alifika salama nyumbani. Familia nzima ilifurahi sana kumwona mwangalizi huyo na ndugu wa eneo hilo. Wazazi wa Hamunyari walisema hivi: “Ninyi watu, dini yenu ni ya kweli. Mlimwokoa binti yetu aliyeachwa afie njiani.” Walikuwa wamewauliza hivi washiriki wa kanisa la Hamunyari: “Je, hamkuona aibu, kama jina la Hamunyari linavyomaanisha, kumwacha afe?” Mashahidi hao walianzisha mazungumzo ya Biblia na kuiachia familia ya Hamunyari vichapo vya Biblia. Waliwaomba ndugu warudi na kujifunza nao Biblia. Watu fulani wa familia hiyo ambao walikuwa wanawapinga Mashahidi walibadili maoni yao. Mmoja wao, ndugu-mkwe wa Hamunyari ambaye alikuwa kiongozi wa kanisa moja katika eneo hilo, alikubali kujifunza Biblia.

Kujenga Nyumba za Ibada

Mtungaji wa mashairi aliyeongozwa na roho aliandika hivi: “Ee Mungu, . . . nafsi yangu ina kiu kwa ajili yako. . . . Katika nchi iliyokauka na kuchoka, ambapo hakuna maji.” (Zaburi 63:1) Maneno hayo yamethibitika kuwa ya kweli kwa watu wengi nchini Zimbabwe! Kimwili wanavumilia ukame, lakini kiroho wana kiu kwa ajili ya Mungu na wema wake. Unaweza kuona hilo kupitia matokeo ya huduma ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova. Zimbabwe ilipopata uhuru mwaka wa 1980, Mashahidi 10,000 hivi walikuwa wakitumika katika makutaniko 476. Sasa, miaka 27 baadaye, idadi ya Mashahidi wanaotenda ni mara tatu zaidi na idadi ya makutaniko ni karibu mara mbili.

Ni makutaniko machache yaliyokuwa na mahali pa ibada. Mnamo Januari (Mwezi wa 1) 2001, ni makutaniko 98 tu kati ya makutaniko 800 nchini Zimbabwe yalikuwa na nyumba ya ibada, yaani, Jumba la Ufalme la kufanyia mikutano. Makutaniko mengi yalifanyia mikutano chini ya miti au katika vibanda vya miti, vyenye kuta za udongo na paa za nyasi.

Kwa sababu ya michango ya ukarimu na kazi ya bidii ya kujitolea ya ndugu zao Wakristo wa ulimwenguni pote, Mashahidi nchini Zimbabwe wameanza programu ambayo inayawezesha makutaniko mengi zaidi kupata Majumba ya Ufalme yanayofaa na yenye kuheshimika. Mashahidi wengi kutoka nchi za ng’ambo ambao wana ustadi wa ujenzi walifanya mipango ya kwenda Zimbabwe na kufanya kazi pamoja na wafanyakazi wa kujitolea wa nchi hiyo. Shahidi mmoja wa Zimbabwe aliandika hivi: “Tunawashukuru kutoka moyoni ndugu na dada wote wa nchi nyingi ambao wamekuja Zimbabwe ili kutusaidia kujenga Majumba maridadi ya Ufalme. Na pia tunawashukuru wengine wote kwa sababu ya michango mnayotoa kwa ajili ya Hazina ya Majumba ya Ufalme ambayo inafanikisha kazi hii.”

Katika sehemu ya mashariki ya nchi hiyo, akina ndugu walikutanika chini ya mti mkubwa wa mbuyu kwa muda wa miaka 50. Wazee Wakristo walipoambiwa kwamba nyumba halisi ya ibada ingejengwa, mzee mmoja kati yao alitokwa na machozi. Katika kutaniko moja la karibu, mzee mmoja mwenye umri wa miaka 91 alisema hivi: “Nimekuwa nikimlilia Yehova kwa miaka mingi sana ili jambo kama hili litukie!”

Watu wengi wameeleza jinsi majengo hayo yenye kuvutia yanavyojengwa kwa haraka. Mtu mmoja alisema hivi: “Ninyi watu mnajenga wakati wa mchana, lakini lazima Mungu awe anajenga usiku!” Umoja na furaha ya wafanyakazi inaonekana pia. Kufikia sasa, Majumba mapya ya Ufalme zaidi ya 350 yamekamilishwa nchini kote. Hivyo, makutaniko 534 yanakutana katika Majumba ya Ufalme yaliyo imara ambayo yamejengwa kwa matofali.

Ujenzi muhimu wa kiroho unaendelea huko Zimbabwe. Tunapofikiria yale ambayo yametimizwa, tunachochewa kumsifu Yehova ambaye ndiye chanzo cha baraka kama hizo. Ndiyo, “Yehova mwenyewe asipoijenga nyumba, ni bure kwamba wajenzi wake wameifanyia kazi ngumu.”—Zaburi 127:1.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Ramani katika ukurasa wa 9]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

ZIMBABWE

HARARE

Masvingo

Great Zimbabwe

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mnara wenye umbo la pia

[Picha katika ukurasa wa 12]

Jumba jipya la Ufalme, Kutaniko la Concession

[Picha katika ukurasa wa 12]

Washiriki wa Kutaniko la Lyndale nje ya Jumba lao Jipya la Ufalme

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 9]

Ruins with steps: ©Chris van der Merwe/AAI Fotostock/age fotostock; tower inset: ©Ingrid van den Berg/AAI Fotostock/age fotostock