Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tuepuke Mtazamo wa Kupita Kiasi?

Kwa Nini Tuepuke Mtazamo wa Kupita Kiasi?

Kwa Nini Tuepuke Mtazamo wa Kupita Kiasi?

YEHOVA ndiye mfano bora zaidi wa usawaziko. “Kazi zake ni kamilifu,” naye hatekelezi kamwe haki kwa ukali kwa kuwa sifa yake ya haki inaonyeshwa kwa rehema. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Sikuzote upendo wake unategemea kanuni kwa kuwa anatenda kupatana na sheria kamilifu. (Zaburi 89:14; 103:13, 14) Wazazi wetu wa kwanza waliumbwa wakiwa na usawaziko katika kila jambo. Hawakuwa na mwelekeo wa kupita kiasi katika jambo lolote. Hata hivyo, dhambi iliingia na kuleta “kasoro,” yaani, kutokamilika ambako kumesababisha ukosefu wa usawaziko.—Kumbukumbu la Torati 32:5.

Kwa mfano: Je, umewahi kusafiri kwa gari au baiskeli iliyo na gurudumu ambalo lina sehemu iliyovimba sana? Hapana shaka kwamba kasoro hiyo ilifanya safari isiwe yenye kustarehesha na pia iwe hatari. Gurudumu kama hilo linahitaji kurekebishwa kabla halijaharibika zaidi au kupasuka. Vivyo hivyo, hali yetu ya kutokamilika inatufanya tusiwe na usawaziko. Tukiacha sehemu hizo “zilizovimba” zizidi kuwa kubwa, safari yetu maishani itakuwa ngumu na hata hatari zaidi.

Nyakati nyingine, sifa zetu nzuri au uwezo wetu unaweza kuonyeshwa kupita kiasi. Kwa mfano, ingawa Sheria ya Musa iliwataka Waisraeli wavae nguo zenye upindo wenye nyuzinyuzi, Mafarisayo wa siku za Yesu, ambao walitaka kuwa tofauti na watu wengine, waliongeza kupita kiasi “ukubwa wa pindo zenye nyuzinyuzi za mavazi yao.” Walifanya hivyo ili waonekane kuwa watakatifu kuliko wanadamu wenzao.—Mathayo 23:5; Hesabu 15:38-40.

Leo, watu fulani wanajaribu kuwavutia wengine kwa njia yoyote ile, hata kwa kufanya mambo yanayowashtua wengine. Huenda hicho kikawa kilio cha kusema: “Nitambueni! Mimi pia ni mtu!” Lakini kupita kiasi katika mavazi, mitazamo, na matendo hakuwezi kutosheleza mahitaji ya kweli ya Mkristo.

Mtazamo Uliosawazika Kuhusu Kazi

Kazi nzuri ni mojawapo ya mambo yanayofanya maisha yetu yawe na kusudi haidhuru sisi ni nani au tunaishi wapi. Tuliumbwa ili tupate uradhi kwa kufanya kazi kama hizo. (Mwanzo 2:15) Kwa sababu hiyo, Biblia inashutumu uvivu. Mtume Paulo alisema hivi waziwazi: “Ikiwa yeyote hataki kufanya kazi, basi na asile chakula.” (2 Wathesalonike 3:10) Kwa kweli, kuwa mvivu kuelekea kazi kunaweza kumfanya mtu awe maskini, akose uradhi, na hata akose kibali cha Mungu.

Kwa upande mwingine, watu fulani wanakosa usawaziko kwa kujitoa kabisa kwa kazi zao, na hivyo wanajifanya kuwa watumwa wa kazi. Wanaondoka nyumbani asubuhi na mapema na kurudi usiku, na huenda wakadai kwamba wanafanya kazi kwa faida ya familia zao. Lakini, kwa kweli huenda familia zao zinaumia kwa sababu wanajitoa sana kwa kazi. Mke mmoja wa nyumbani, ambaye mara nyingi mume wake anafanya kazi kwa saa za ziada, anasema hivi: “Ni afadhali nikose vitu vyote vyenye thamani katika nyumba hii ya fahari lakini nipate nafasi ya kuwa hapa pamoja na mume wangu na watoto wetu.” Wale wanaochagua kufanya kazi kupita kiasi wanapaswa kufikiria kwa uzito kisa cha Mfalme Sulemani mwenyewe: “Mimi, naam, mimi nikageuka kuelekea kazi zangu zote ambazo mikono yangu ilikuwa imefanya na kuelekea kazi ngumu niliyokuwa nimejitahidi kuitimiza, na, tazama! kila kitu kilikuwa ubatili na kufuatilia upepo.”—Mhubiri 2:11.

Ndiyo, tunapaswa kuepuka kuwa wavivu au kufanya kazi kupita kiasi. Tunaweza kuwa wafanyakazi wenye bidii, huku tukikumbuka kwamba tukiwa watumwa wa kazi tutakosa furaha na labda kupata hasara nyingine nyingi.—Mhubiri 4:5, 6.

Epuka Maoni Yenye Kupita Kiasi Kuhusu Raha

Biblia ilitabiri hivi kuhusu nyakati zetu: “Watu watakuwa . . . wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:2, 4) Mbinu moja ambayo Shetani ametumia kwa mafanikio ili kuwafanya watu wamwache Mungu ni kupenda raha. Watu wengi zaidi na zaidi wanapenda tafrija na burudani, kama vile michezo hatari inayomfanya mtu asisimke sana. Michezo ya aina hiyo inazidi kuongezeka na ndivyo na idadi ya watu wanaoicheza. Kwa nini watu wengi wanaipenda? Kwa kuwa watu wengi hawaridhiki na maisha yao ya kila siku, wanatafuta mambo yanayoweza kuwasisimua zaidi. Ili wasisimke hata zaidi, wanahitaji kucheza michezo hatari zaidi na zaidi. Wakristo wanafuata dhamiri zao na kuepuka michezo hatari kwa sababu wanaheshimu zawadi ya uhai na Yule aliyeitoa.—Zaburi 36:9.

Mungu alipowaumba wanadamu wa kwanza, aliwaweka wapi? Katika bustani ya Edeni, neno ambalo katika lugha ya awali linamaanisha “Raha,” au “Furaha.” (Mwanzo 2:8) Hapana shaka kwamba kusudi la Yehova kwa wanadamu lilitia ndani kuwa na maisha ya raha na yenye kupendeza.

Yesu alituwekea kielelezo kikamilifu cha kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu raha. Alijitoa kabisa kutimiza mapenzi ya Yehova, naye hakuacha kamwe kuishi kupatana na sheria na kanuni za Mungu. Alishughulikia watu wenye uhitaji, hata alipokuwa amechoka. (Mathayo 14:13, 14) Ndiyo, Yesu alikubali alipoalikwa kula chakula naye alitenga wakati wa kupumzika na kuburudika. Bila shaka, alijua kwamba maadui fulani walikuwa wakimchambua kwa sababu ya kufanya hivyo. Walisema hivi kumhusu: “Tazama! Mtu mlafi na mwenye mazoea ya kunywa divai.” (Luka 7:34; 10:38; 11:37) Lakini Yesu hakuamini kwamba kujitoa kikweli kunamaanisha kujinyima kabisa raha.

Kwa wazi, inapohusu tafrija, ni jambo la hekima kuepuka kupita kiasi kwa njia yoyote ile. Kufanya raha na tafrija kuwa mambo muhimu zaidi maishani mwetu hakuwezi kutuletea furaha ya kweli. Kunaweza kutufanya tupuuze mambo yaliyo ya maana zaidi, kutia ndani uhusiano wetu pamoja na Mungu. Hata hivyo, hatupaswi kujinyima kabisa raha au kuwachambua wale wanaojifurahisha kwa usawaziko.—Mhubiri 2:24; 3:1-4.

Pata Furaha kwa Kuwa na Usawaziko Maishani

Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yakobo 3:2) Tunaweza kujikuta katika hali kama hiyo tunapojitahidi kuepuka kuwa wenye kupita kiasi. Ni nini kinachoweza kutusaidia kudumisha usawaziko wetu? Tunahitaji kutambua uwezo na udhaifu wetu. Si rahisi kufanya hivyo. Huenda bila kujua, tumeanza kupoteza usawaziko. Hivyo, ni jambo la hekima tushirikiane kwa ukaribu na Wakristo wengine wakomavu na kusikiliza mashauri yao yenye usawaziko. (Wagalatia 6:1) Tunaweza kumwomba rafiki tunayemtumaini au mzee wa kutaniko mwenye uzoefu atupe mashauri. Maandiko pamoja na mashauri hayo yanayotegemea Biblia yanaweza kuwa kama “kioo” ambacho tunaweza kutumia ili kujichunguza jinsi tulivyo machoni pa Yehova.—Yakobo 1:22-25.

Ni vizuri kujua kwamba hatuhitaji kuwa wenye kupita kiasi maishani. Tukijitahidi kabisa na tukimtegemea Yehova, tunaweza kuwa wenye usawaziko na hivyo kuwa na furaha. Tukifanya hivyo, uhusiano wetu pamoja na ndugu na dada zetu Wakristo utakuwa mzuri zaidi, na tunaweza kuwa mifano bora zaidi kwa watu tunaohubiria. Zaidi ya yote, tutamwiga hata zaidi Yehova, Mungu wetu mwenye usawaziko na upendo.—Waefeso 5:1.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 28]

©Greg Epperson/age fotostock