Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waandishi wa Zamani na Neno la Mungu

Waandishi wa Zamani na Neno la Mungu

Waandishi wa Zamani na Neno la Mungu

KUANDIKWA kwa Maandiko ya Kiebrania kulikamilishwa kufikia mwishoni mwa karne ya tano K.W.K. Katika karne zilizofuata, wasomi Wayahudi, hasa Wasoferi na baadaye Wamasora, walijitahidi sana kuhakikisha kwamba usahihi wa maandishi ya Kiebrania unadumishwa. Hata hivyo, vitabu vya kale zaidi vya Biblia viliandikwa katika siku za Musa na Yoshua, miaka elfu moja kabla ya Wasoferi kutokea. Vitabu hivyo viliandikwa kwenye hati ambazo ziliharibika haraka; kwa hivyo, ni lazima iwe vitabu hivyo vya kukunjwa vilinakiliwa mara nyingi. Tunajua nini kuhusu kazi ya uandishi iliyofanywa siku hizo za zamani? Je, kulikuwa na waandishi stadi katika Israeli la kale?

Hati za kale zaidi zilizopo leo za Biblia ni visehemu vya vitabu vya kukunjwa vya Bahari ya Chumvi. Baadhi ya hati hizo zilinakiliwa katika karne ya pili na ya tatu K.W.K. “Nakala za mapema zaidi za kitabu chochote cha Biblia hazipatikani,” anaeleza Profesa Alan R. Millard, msomi wa lugha na akiolojia ya Mashariki ya Karibu. Anaongeza hivi: “Tamaduni za jamii jirani zinaweza kuonyesha jinsi waandishi wa zamani walivyofanya kazi yao, na ujuzi huo unaweza kusaidia katika kuchanganua maandishi ya Kiebrania na historia yake.”

Kazi ya Uandishi Zamani

Maandishi ya kihistoria, kidini, kisheria, kisanaa, na ya wasomi, yalikuwa yakitokezwa huko Mesopotamia miaka elfu nne iliyopita. Shule za waandishi zilisitawi, na moja ya mambo ambayo yalifundishwa ni kunakili kwa uaminifu maandishi yaliyokuwapo. Wasomi wa siku hizi wamegundua mabadiliko madogo katika maandishi ya Kibabiloni yaliyonakiliwa tena na tena kwa miaka elfu moja au zaidi.

Kulikuwa na waandishi katika maeneo mengine mbali na Mesopotamia. Kitabu kimoja (The Oxford Encyclopedia of Archaeology in the Near East) kinasema: “Mwandishi Mbabiloni aliyeishi katika miaka ya 1500 KWK, angeelewa vizuri mbinu zilizotumiwa katika vituo vingi vya uandishi katika Mesopotamia, Siria, Kanaani, na hata Misri.” *

Katika siku za Musa kazi ya uandishi ilikuwa ya pekee sana huko Misri. Waandishi walinakili daima maandishi ya sanaa. Mambo waliyonakili yanaweza kuonekana katika mapambo ya makaburi huko Misri ambayo ni ya zaidi ya miaka elfu nne iliyopita. Kitabu kilichotajwa mapema kinasema hivi kuhusu waandishi wa kale katika kipindi hicho cha mapema: “Kufikia milenia ya pili KWK, walikuwa wamenakili na kukusanya maandishi mengi ya sanaa yaliyohusu ustaarabu maarufu wa Mesopotamia na Misri nao walitunga mfumo wa miongozo na sheria kwa ajili ya kazi ya uandishi.”

“Mfumo” huo ulionyesha matumizi ya maandishi yaliyoongezwa mwishoni mwa sehemu kuu ya maandishi. Maandishi hayo yaliyoongezwa yalikuwa na majina ya wanakili na mmiliki wa jiwe au bamba la udongo, tarehe, chanzo cha maandishi ya awali, idadi ya mistari, na kadhalika. Mara nyingi waandishi waliongeza maneno haya: “Maandishi haya yalinakiliwa kutoka kwenye nakala ya awali na kulinganishwa nayo.” Maneno hayo yanaonyesha kwamba watu waliofanya kazi ya kunakili zamani waliona umuhimu wa kunakili maandishi kwa usahihi.

Profesa Millard, aliyetajwa mapema, anasema: “Tunaweza kuona kwamba waandishi walikuwa na utaratibu wa kunakili uliotia ndani kukagua na kurekebisha, utaratibu ambao ulikuwa na njia za kuzuia makosa yasiingizwe. Baadhi ya njia hizo, hasa kuhesabu mistari na maneno, zilianza tena kutumiwa na Wamasora mwanzoni mwa Enzi za Kati.” Hivyo, katika siku za Musa na Yoshua, mtazamo uliowachochea waandishi kunakili kwa uangalifu na kwa usahihi tayari ulikuwako katika Mashariki ya Kati.

Je, Waisraeli pia walikuwa na watu waliokuwa na ustadi wa kunakili? Maandishi ya Biblia yanaonyesha nini?

Waandishi Katika Israeli la Kale

Musa alilelewa katika nyumba ya Farao. (Kutoka 2:10; Matendo 7:21, 22) Kulingana na mtaalamu mmoja wa mambo ya kale ya Misri, huenda elimu ya Musa ilitia ndani kujifunza kusoma na kuandika maandishi ya Kimisri na angalau ustadi fulani-fulani wa uandishi. Katika kitabu chake (Israel in Egypt), Profesa James K. Hoffmeier anasema: “Kuna msingi wa kuamini wazo la kibiblia kwamba Musa alikuwa na uwezo wa kuandika matukio, kukusanya habari kuhusu safari, na kufanya kazi nyinginezo za uandishi.” *

Biblia inawataja watu fulani waliokuwa na ustadi wa uandishi katika Israeli la kale. Kulingana na kichapo kimoja (The Cambridge History of the Bible), Musa “aliweka rasmi maofisa waliojua kusoma na kuandika . . . ili waandike habari kuhusu maamuzi na orodha za watu waliopangwa katika vikundi mbalimbali.” Kauli hiyo inategemea Kumbukumbu la Torati 1:15, linalosema: “Basi [mimi Musa] nikawachukua vichwa vya makabila yenu . . . na kuwaweka kuwa vichwa juu yenu, wakuu wa maelfu na wakuu wa mamia na wakuu wa 50 na wakuu wa makumi na maofisa wa makabila yenu.” Maofisa hao walikuwa nani?

Neno “ofisa” katika Kiebrania linapatikana mara kadhaa katika maandishi ya Biblia yanayozungumza kuhusu siku za Musa na Yoshua. Wasomi mbalimbali wameeleza kwamba neno hilo linamaanisha “mwandishi wa habari,” “yule ‘anayeandika’ au ‘kurekodi,’” na “ofisa aliyemsaidia mwamuzi kuandika habari.” Kwa kuwa neno hilo la Kiebrania limerudiwa-rudiwa, ni wazi kwamba kulikuwa na waandishi wengi kama hao katika Israeli na kwamba walikuwa na wajibu mkubwa katika usimamizi wa mapema wa taifa hilo.

Mfano wa tatu unahusu makuhani wa Israeli. Kitabu kimoja (Encyclopaedia Judaica) kinasema kwamba “walipaswa kujua kusoma na kuandika kwa sababu ya wajibu wao wa kidini na wa kiserikali.” Kwa mfano, Musa aliwaamuru hivi wana wa Lawi: “Mwishoni mwa kila miaka saba, . . . mtasoma sheria hii mbele ya Israeli wote.” Makuhani wakawa watunzaji wa nakala rasmi ya Sheria. Waliidhinisha na kusimamia kazi ya kunakili sheria.—Kumbukumbu la Torati 17:18, 19; 31:10, 11.

Fikiria jinsi nakala ya kwanza ya Sheria ilivyotengenezwa. Katika mwezi wa mwisho wa maisha yake, Musa aliwaambia hivi Waisraeli: ‘Utakapovuka Yordani kuingia katika nchi ambayo Yehova Mungu wako anakupa wewe, utajiwekea pia mawe makubwa na kuyapaka chokaa. Nawe utaandika juu yake maneno yote ya sheria hii.’ (Kumbukumbu la Torati 27:1-4) Baada ya uharibifu wa Yeriko na Ai, Waisraeli walikusanyika kwenye Mlima Ebali, uliokuwa katikati ya Nchi ya Ahadi. Kwa hakika, wakiwa kwenye mlima huo, Yoshua aliandika juu ya mawe ya madhabahu “nakala ya maandishi ya sheria ya Musa.” (Yoshua 8:30-32) Waandishi na wasomaji walihitajiwa ili kunakili maandishi kama hayo. Hilo linaonyesha kwamba Waisraeli wa kale walikuwa na ustadi uliohitajiwa ili kuhifadhi kwa usahihi maandishi yao matakatifu.

Usahihi wa Maandiko

Baada ya siku za Musa na Yoshua, vitabu vingine vya kukunjwa vya Kiebrania viliandikwa, na nakala za mkono za vitabu hivyo zikanakiliwa. Nakala hizo zilihitaji kunakiliwa upya kadiri zilivyozeeka au kuharibiwa na unyevunyevu au kuvu. Kazi hiyo ya kunakili iliendelea kwa karne nyingi.

Ingawa watu walionakili Biblia walikuwa waangalifu sana, kasoro fulani ziliingia kimakosa. Lakini je, kasoro hizo zilibadili sana maandishi ya Biblia? Hapana. Kwa ujumla, kasoro hizo ni ndogo na hazifanyi maandishi ya Biblia yasiwe sahihi, kama inavyothibitishwa wakati maandishi hayo yanapolinganishwa kwa makini na hati za zamani.

Maoni ya Yesu Kristo kuhusu vitabu vya mapema vya Biblia yanawathibitishia Wakristo kwamba maandishi ya Maandiko Matakatifu ni sahihi. Maneno kama vile “Je, hamkusoma katika kitabu cha Musa?” na “Musa aliwapa ninyi Sheria, sivyo?” yanaonyesha kwamba Yesu aliona nakala zilizonakiliwa kwa mkono ambazo zilikuwako alipokuwa duniani ni zenye kutegemeka. (Marko 12:26; Yohana 7:19) Zaidi ya hilo, Yesu alithibitisha usahihi wa Maandiko yote ya Kiebrania aliposema: “Mambo yote yaliyoandikwa katika sheria ya Musa na katika Manabii na Zaburi juu yangu lazima yatimizwe.”—Luka 24:44.

Hivyo, tuna sababu nzuri ya kuwa na uhakika kwamba Maandiko Matakatifu yamenakiliwa kwa usahihi kutoka katika maandishi ya awali. Ni kama vile nabii Isaya aliyeongozwa na roho alivyosema: “Majani mabichi yamekauka, ua limenyauka; lakini kwa habari ya neno la Mungu wetu, litadumu mpaka wakati usio na kipimo.”—Isaya 40:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Yoshua, aliyeishi katika miaka ya 1500 K.W.K., anataja jiji la Wakanaani lililoitwa Kiriath-seferi, jina ambalo linamaanisha “Mji wa Vitabu” au “Mji wa Waandishi.”—Yoshua 15:15, 16.

^ fu. 12 Mambo ya kisheria ambayo Musa aliandika yanapatikana katika Kutoka 24:4, 7; 34:27, 28; na Kumbukumbu la Torati 31:24-26. Wimbo alioandika unapatikana katika Kumbukumbu la Torati 31:22, na habari alizokusanya kuhusu safari ya nyikani zimo katika Hesabu 33:2.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mwandishi Mmisri akifanya kazi

[Picha katika ukurasa wa 19]

Vitabu vya zamani zaidi vya Biblia viliandikwa katika siku za Musa