Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usitenganishe Kile Ambacho Mungu Ameunganisha

Usitenganishe Kile Ambacho Mungu Ameunganisha

Usitenganishe Kile Ambacho Mungu Ameunganisha

“Wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—MATHAYO 19:6.

1, 2. Kwa nini kutazamia kwamba wenzi wa ndoa watapata matatizo mara kwa mara ni jambo linalopatana na Maandiko na la hakika?

WAZIA kwamba uko tayari kufunga safari ndefu kwa gari. Je, utapata matatizo njiani? Lingekuwa jambo la upumbavu kufikiri kwamba hutapata matatizo yoyote! Kwa mfano, huenda ukakumbana na matatizo ya hali ya hewa na kulazimika kupunguza mwendo wako na kuendesha gari kwa uangalifu zaidi. Pia, gari linaweza kuharibika na usiweze kulirekebisha wewe mwenyewe na hivyo ikakubidi kulisukuma kando ya barabara na kuomba msaada wa watu wengine. Je, matatizo hayo yanapaswa kukufanya ukate kauli kwamba ulikosea kufunga safari hiyo na kwamba unapaswa kulitupilia mbali gari hilo? Hapana. Unapofunga safari ndefu, unatazamia kwamba utapata matatizo fulani na kwa hekima unatafuta njia za kuyatatua.

2 Ndivyo ilivyo kuhusu ndoa. Matatizo hayaepukiki, na ni jambo la kipumbavu kwa wale wanaotarajia kufunga ndoa kufikiri kwamba wataishi raha mustarehe. Kwenye 1 Wakorintho 7:28, Biblia inasema waziwazi kwamba waume na wake watakuwa na “dhiki katika mwili wao.” Kwa nini iwe hivyo? Kwa ufupi, ni kwa sababu waume na wake si wakamilifu, nasi tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1; Waroma 3:23) Hivyo, hata wenzi wa ndoa wanaopatana na wanaofuata maoni ya Mungu watapata matatizo mara kwa mara.

3. (a) Watu wengi katika ulimwengu wana maoni gani kuhusu ndoa? (b) Kwa nini Wakristo wanajitahidi kudumisha ndoa zao?

3 Katika ulimwengu wa leo, wenzi fulani wa ndoa wanapopata matatizo, jambo la kwanza wanalofikiria ni kuvunja ndoa yao. Katika nchi nyingi, idadi ya talaka inazidi kuongezeka. Hata hivyo, Wakristo wa kweli wanashughulikia matatizo badala ya kuyakimbia. Kwa nini? Kwa sababu wanaiona ndoa kuwa zawadi takatifu kutoka kwa Yehova. Yesu alisema hivi kuhusu wenzi wa ndoa: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mathayo 19:6) Ni kweli kwamba si rahisi sikuzote kuishi kulingana na kiwango hicho. Kwa mfano, mara nyingi watu wa ukoo na watu wengine, kutia ndani washauri fulani wa ndoa, ambao hawakubali kanuni za Biblia, wanawahimiza wenzi wa ndoa watengane au watalikiane kwa sababu zisizo za kimaandiko. * Lakini Wakristo wanajua kwamba ni afadhali zaidi kutatua matatizo na kudumisha ndoa kuliko kuivunja haraka-haraka. Kwa kweli, ni muhimu kwamba tangu mwanzo tuazimie kufanya mambo kulingana na njia ya Yehova wala si kupatana na mashauri ya watu wengine.—Methali 14:12.

Kushinda Matatizo

4, 5. (a) Lazima ndoa ipambane na matatizo gani? (b) Kwa nini kanuni zilizo katika Neno la Mungu zinafanikiwa hata matatizo yanapotokea katika ndoa?

4 Ukweli ni kwamba katika kila ndoa matatizo yanahitaji kusuluhishwa mara kwa mara. Katika visa vingi, hilo litahusisha kutatua matatizo madogo. Hata hivyo, katika ndoa nyingi, huenda kukawa na matatizo mazito yanayotishia msingi wa uhusiano wa ndoa. Nyakati nyingine, huenda ukahitaji kuomba msaada wa mzee Mkristo mwenye uzoefu ambaye ameoa. Lakini, hali hizo hazionyeshi kwamba ndoa yako haijafanikiwa. Badala yake, inakazia tu umuhimu wa kufuata kabisa kanuni za Biblia katika kusuluhisha matatizo.

5 Akiwa Muumba wa wanadamu na Mwanzilishi wa mpango wa ndoa, Yehova anajua vema zaidi kuliko mtu mwingine yeyote kile tunachohitaji ili ndoa zetu zifanikiwe. Swali ni, Je, tutasikiliza na kutii mashauri yaliyo katika Neno lake? Bila shaka, tutafaidika tukifanya hivyo. Yehova aliwaambia hivi watu wake wa kale: “Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.” (Isaya 48:18) Kufuata mwongozo wa Biblia kunaweza kufanya ndoa ifanikiwe. Acheni kwanza tuzungumzie mashauri ambayo Biblia inawapa waume.

“Endeleeni Kuwapenda Wake Zenu”

6. Maandiko yanawapa waume shauri gani?

6 Barua ya mtume Paulo kwa Waefeso inatoa mwongozo ulio wazi kwa ajili ya waume. Paulo aliandika hivi: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake. Vivyo hivyo waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Yeye anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza kwa upendo, kama vile Kristo pia anavyolitendea kutaniko. Hata hivyo, pia, kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake.”—Waefeso 5:25, 28, 29, 33.

7. (a) Ni nini kinachopaswa kuwa sehemu ya msingi wa ndoa ya Kikristo? (b) Waume wanaendelea jinsi gani kuwapenda wake zao?

7 Paulo hazungumzii kila tatizo linaloweza kutokea kati ya mume na mke. Badala yake, anazungumzia suluhisho lenyewe la matatizo ya ndoa anapotaja ule unaopaswa kuwa sehemu kuu ya msingi wa kila ndoa ya Kikristo, yaani, upendo. Kwa hakika, upendo unatajwa mara sita katika mistari iliyo hapo juu. Ona pia kwamba Paulo anawaambia waume: “Endeleeni kuwapenda wake zenu.” Bila shaka, Paulo alitambua kwamba ni rahisi kuvutiwa kimapenzi na mtu kuliko kuendelea kumpenda. Hivyo ndivyo ilivyo hasa katika hizi “siku za mwisho,” wakati ambapo wengi wamekuwa “wenye kujipenda wenyewe” na “wasiotaka makubaliano yoyote.” (2 Timotheo 3:1-3) Sifa mbaya kama hizo zinaharibu ndoa nyingi leo, lakini mume mwenye upendo hataruhusu mwelekeo wa ubinafsi wa ulimwengu huu uongoze mawazo na matendo yake.—Waroma 12:2.

Unaweza Kutimiza Mahitaji ya Mke Wako Jinsi Gani?

8, 9. Mume Mkristo anatimiza mahitaji ya mke wake kwa njia gani?

8 Ikiwa wewe ni mume Mkristo, unaweza kuepuka jinsi gani mwelekeo wa ubinafsi na hivyo kumpenda kikweli mke wako? Katika maneno yaliyotajwa mapema ambayo Paulo aliwaandikia Waefeso, alionyesha mambo mawili unayohitaji kufanya, yaani, kumtimizia mahitaji yake na kumtunza kama unavyotunza mwili wako mwenyewe. Unaweza kutimiza kwa njia gani mahitaji ya mke wako? Njia moja ni kutimiza mahitaji ya kimwili ya mke wako. Paulo alimwandikia hivi Timotheo: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.”—1 Timotheo 5:8.

9 Hata hivyo, zaidi ya kuandaa tu chakula, mavazi, na makao, mambo mengine mengi yanahusika. Kwa nini? Kwa sababu mume anaweza kutimiza vizuri mahitaji ya kimwili ya mke wake lakini ashindwe kutimiza mahitaji ya kihisia na ya kiroho ya mke wake. Ni jambo la lazima kumtimizia mahitaji yake ya kihisia na ya kiroho. Ni kweli kwamba wanaume wengi Wakristo wana shughuli nyingi za kutaniko. Lakini kuwa na madaraka mazito ya kutaniko hakumpi mume sababu ya kutotimiza wajibu aliopewa na Mungu wa kuwa kichwa cha familia. (1 Timotheo 3:5, 12) Likizungumzia jambo hilo, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilisema hivi miaka fulani iliyopita: “Kulingana na matakwa ya Kibiblia, inaweza kusemwa kwamba ‘uchungaji huanzia nyumbani.’ Mzee asipoangalia jamaa yake, angeweza kuhatarisha kuwekwa kwake rasmi.” * Kwa wazi, ni muhimu umtimizie mke wako mahitaji yake ya kimwili, ya kihisia, na ya kiroho ambayo ndiyo ya maana zaidi kuliko yote.

Inamaanisha Nini Kumtunza Mke Wako?

10. Mume anaweza kuonyesha jinsi gani kwamba anamthamini mke wake?

10 Ikiwa unamthamini mke wako, utamtunza sana kwa sababu unampenda. Unaweza kufanya hivyo kwa njia mbalimbali. Kwanza, tumia wakati wa kutosha pamoja na mwenzi wako. Ukimpuuza mke wako kuhusiana na jambo hilo, upendo wake kwako unaweza kupoa. Pia, fikiria hili, inapohusu wakati na uangalifu huenda kile ambacho unadhani mke wako anahitaji kisiwe kile anachohitaji. Haitoshi tu kusema kwamba unamthamini mwenzi wako. Ni lazima mke wako ahisi kwamba anathaminiwa. Paulo aliandika hivi: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.” (1 Wakorintho 10:24) Ukiwa mume mwenye upendo, unapaswa kujitahidi kuelewa mahitaji kamili ya mke wako.—Wafilipi 2:4.

11. Jinsi mume anavyomtendea mke wake kunaweza kuwa na matokeo gani juu ya uhusiano wake pamoja na Mungu na kutaniko?

11 Njia nyingine ya kuonyesha kwamba unamthamini mke wako ni kumtendea kwa wororo, kwa maneno na kwa matendo. (Methali 12:18) Paulo aliwaandikia hivi Wakolosai: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.” (Wakolosai 3:19) Kulingana na kitabu kimoja, sehemu ya mwisho ya maneno ya Paulo inaweza kutafsiriwa hivi “usimtendee mke kama mfanyakazi wa nyumbani” au “usimfanye mke kuwa mtumwa.” Bila shaka, mume ambaye ni mkatili, iwe hadharani au faraghani, anaonyesha kwa kweli kwamba hamthamini mke wake. Mume anayemtendea mke wake kwa ukali, anaweza kuharibu uhusiano wake pamoja na Mungu. Mtume Petro aliwaandikia waume hivi: “Enyi waume, endeleeni kukaa nao [wake zenu] vivyo hivyo kulingana na ujuzi, mkiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi, yaani, mwanamke, kwa kuwa ninyi pia ni warithi pamoja nao wa pendeleo lisilostahiliwa la uzima, kusudi sala zenu zisizuiwe.” *1 Petro 3:7.

12. Mume Mkristo anaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyolitendea kutaniko la Kikristo?

12 Usipuuze upendo wa mke wako. Mhakikishie kwamba bado unaendelea kumpenda. Yesu aliwawekea waume Wakristo mfano kupitia jinsi alivyolitendea kutaniko la Kikristo. Alikuwa mwororo, mwenye fadhili, na mwenye kusamehe, hata wafuasi wake waliporudia-rudia kuonyesha sifa zisizopendeza. Hivyo, Yesu angeweza kuwaambia wengine hivi: “Njooni kwangu, . . . kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.” (Mathayo 11:28, 29) Mume Mkristo anayemwiga Yesu anamtendea mke wake kama Yesu alivyolitendea kutaniko. Mwanamume ambaye kwa kweli anamthamini mke wake, na kuonyesha hivyo kwa maneno na matendo, atakuwa chanzo cha burudisho la kweli kwa mke wake.

Wake Wanaoishi Kulingana na Kanuni za Biblia

13. Biblia ina kanuni gani zinazoweza kuwasaidia wake?

13 Biblia ina kanuni zinazoweza kuwasaidia wake pia. Andiko la Waefeso 5:22-24, 33 linasema hivi: “Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko, yeye akiwa mwokozi wa mwili huu. Kwa kweli, kama kutaniko linavyojitiisha kwa Kristo, vivyo hivyo wanawake pia na wajitiishe kwa waume zao katika mambo yote. . . . Mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”

14. Kwa nini kanuni ya Kimaandiko kuhusu kujitiisha haiwavunjii wanawake heshima?

14 Ona jinsi Paulo alivyokazia sana ujitiisho na heshima. Mke anakumbushwa ajitiishe kwa mume wake. Hilo linapatana na mpango wa Mungu. Kila kiumbe kilicho hai mbinguni na duniani kiko chini ya mtu fulani. Hata Yesu yuko chini ya Yehova Mungu. (1 Wakorintho 11:3) Bila shaka, mume anayetumia ukichwa wake kwa njia inayofaa atafanya iwe rahisi kwa mke wake kuendelea kujitiisha kwake.

15. Taja mashauri fulani yanayopatikana katika Biblia kuhusu wake.

15 Paulo alisema pia kwamba mke “anapaswa kumheshimu sana mume wake.” Mke Mkristo anapaswa kuonyesha “roho ya utulivu na ya upole,” wala hapaswi kupinga mamlaka ya mume wake kwa kiburi au kujiamulia mambo kivyake. (1 Petro 3:4) Mke anayemwogopa Mungu anafanya kazi kwa bidii kwa faida ya nyumba yake na analetea kichwa chake heshima. (Tito 2:4, 5) Atajitahidi kusema mambo mazuri kumhusu mume wake na kuepuka kufanya chochote kinachoweza kumvunjia heshima. Pia, atajitahidi sana kufanikisha maamuzi ya mume wake.—Methali 14:1.

16. Wake Wakristo wanaweza kujifunza nini kutokana na Sara na Rebeka?

16 Kuwa na roho ya utulivu na upole hakumaanishi kwamba mwanamke Mkristo hana maoni yake mwenyewe au kwamba mawazo yake hayafai. Wanawake wa zamani waliomwogopa Mungu kama vile Sara na Rebeka, walichukua hatua ya kueleza mahangaiko yao kuhusu mambo, na masimulizi ya Biblia yanaonyesha kwamba Yehova aliunga mkono hatua walizochukua. (Mwanzo 21:8-12; 27:46–28:4) Wake Wakristo pia wanaweza kueleza hisia zao. Hata hivyo, wanapaswa kufanya hivyo kwa ufikirio wala si kwa madharau. Inaelekea kwamba mazungumzo ya aina hiyo yatakuwa yenye kupendeza na yenye matokeo zaidi.

Jinsi Wajibu Unavyohusika

17, 18. Waume na wake wanaweza kupinga kwa njia gani jitihada za Shetani za kuharibu ndoa yao?

17 Ndoa ni wajibu wa maisha yote. Kwa hiyo, mume na mke wanapaswa kutamani sana kufanikisha ndoa yao. Kukosa kuzungumza waziwazi kunaweza kufanya matatizo yawe mazito na yazidi kumkasirisha mtu. Mara nyingi, wenzi wa ndoa wanaacha kuzungumza matatizo yanapotokea, na hivyo wanakuwa na kinyongo moyoni. Wenzi fulani hata wanajaribu kutafuta njia za kuvunja ndoa, labda kwa kuanzisha uhusiano wa kimapenzi nje ya ndoa. Yesu alionya hivi: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.”—Mathayo 5:28.

18 Mtume Paulo aliwashauri hivi Wakristo wote, kutia ndani Wakristo waliofunga ndoa: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.” (Waefeso 4:26, 27) Adui yetu mkuu, Shetani, anajaribu kutumia kutoelewana kokote ambako huenda kukatokea kati ya Wakristo. Msimwache afanikiwe! Matatizo yakitokea, fanyeni utafiti kuhusu yale ambayo Biblia inasema juu ya maoni ya Yehova kuhusu tatizo hilo, mkitumia vichapo vinavyotegemea Biblia. Zungumzieni matatizo kwa utulivu na unyoofu. Tendeni kulingana na mambo ambayo mmejifunza kuhusu viwango vya Yehova. (Yakobo 1:22-25) Inapohusu ndoa yenu, mwazimie kutembea pamoja na Mungu mkiwa mume na mke, na msiruhusu kitu chochote wala mtu yeyote atenganishe kile ambacho Mungu ameunganisha!—Mika 6:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Ona sanduku “Talaka na Kutengana” katika gazeti la Amkeni! la Februari 8, 2002 (8/2/2002), ukurasa wa 10, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 9 Ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1989 (15/5/1989), ukurasa wa 12.

^ fu. 11 Ili astahili kupata mapendeleo katika kutaniko la Kikristo, mwanamume hapaswi kuwa “mwenye kupiga watu,” yaani, kuwapiga kihalisi au kwa maneno. Hivyo, gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1990 (1/9/1990), linasema hivi katika ukurasa wa 25: “Ikiwa amefunga ndoa, mwanamume hastahili ikiwa atenda kwa njia ya kimungu mahali penginepo lakini ni mbabe nyumbani.”—1 Timotheo 3:2-5, 12.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini hata ndoa za Wakristo zinaweza kuwa na matatizo?

• Mume anaweza kutimiza mahitaji ya mke wake jinsi gani na kuonyesha kwamba anamthamini?

• Mke anaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba anamheshimu sana mume wake?

• Mume na mke wanaweza kuimarisha wajibu wao kwa njia gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mume anapaswa kutimiza vizuri mahitaji ya mke wake ya kimwili na pia ya kiroho

[Picha katika ukurasa wa 21]

Mwanamume anayemtunza mke wake ni chanzo cha burudisho kwa mke wake

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wake Wakristo wanaeleza hisia zao kwa njia ya heshima