Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana—fuatieni Miradi Inayomletea Mungu Heshima

Vijana—fuatieni Miradi Inayomletea Mungu Heshima

Vijana—fuatieni Miradi Inayomletea Mungu Heshima

“Uwe ukijizoeza ujitoaji-kimungu ukiwa ni shabaha yako.”—1 TIMOTHEO 4:7.

1, 2. (a) Kwa nini Paulo alimpongeza Timotheo? (b) Leo vijana ‘wanajizoeza ujitoaji-kimungu ukiwa ni shabaha yao’ kwa njia gani?

“SINA mtu mwingine yeyote aliye na mwelekeo kama wake atakayejali kwa unyoofu mambo yenu. . . . Kama mtoto na baba yake yeye alitumika pamoja nami katika kuendeleza habari njema.” (Wafilipi 2:20, 22) Mtume Paulo alitoa pongezi hiyo changamfu katika barua aliyowaandikia Wakristo wa karne ya kwanza huko Filipi. Alikuwa akimpongeza nani? Alikuwa akimpongeza Timotheo, kijana aliyeambatana naye katika safari zake. Wazia jinsi uhakikisho huo wa upendo na uhakika wa Paulo ulivyomchangamsha moyo Timotheo!

2 Nyakati zote, vijana wanaopenda mambo ya kiroho kama Timotheo wamekuwa msaada mkubwa kati ya watu wa Yehova. (Zaburi 110:3) Leo, tengenezo la Mungu lina vijana wengi wanaotumika wakiwa mapainia, wamishonari, wajenzi wa kujitolea, na Wanabetheli. Wengine ambao wanastahili kupongezwa sana ni wale wanaoshiriki kwa bidii katika shughuli za kutaniko huku wakitimiza madaraka mengine. Vijana kama hao wanapata uradhi wa kweli unaotokana na kufuatia miradi inayomletea heshima Baba yetu wa kimbingu, Yehova. Kwa kweli, ‘wanajizoeza ujitoaji-kimungu ukiwa ni shabaha yao.’—1 Timotheo 4:7, 8.

3. Ni maswali gani yatakayojibiwa katika habari hii?

3 Ukiwa kijana, je, unajitahidi kufikia miradi hususa ya kiroho? Ni wapi unapoweza kupata msaada na kitia-moyo ili ufikie miradi hiyo? Unaweza kupinga jinsi gani uvutano wa ulimwengu huu unaopenda vitu vya kimwili? Unaweza kutazamia kupata baraka gani ukifuatia miradi inayomletea Mungu heshima? Acheni tuchunguze maisha na kazi ya Timotheo ili tupate majibu ya maswali hayo.

Malezi ya Timotheo

4. Eleza kwa ufupi maisha ya Timotheo akiwa Mkristo.

Timotheo alilelewa huko Listra, mji mdogo katika jimbo la Roma lililoitwa Galatia. Inaelekea kwamba alipata habari kuhusu Ukristo akiwa tineja, Paulo alipohubiri huko Listra karibu mwaka wa 47 W.K. Muda si muda, Timotheo alisifiwa vyema na akina ndugu Wakristo wa eneo hilo. Paulo aliporudi Listra miaka miwili baadaye, alipata habari kuhusu maendeleo ya Timotheo na akamchukua ili asafiri pamoja naye katika safari zake za umishonari. (Matendo 14:5-20; 16:1-3) Timotheo alipoendelea kukomaa, alipewa madaraka mazito hata zaidi, kutia ndani migawo muhimu ya kuwatia nguvu akina ndugu. Mwaka wa 65 W.K. hivi, Paulo akiwa gerezani huko Roma, alimwandikia Timotheo barua. Wakati huo Timotheo alikuwa mzee Mkristo huko Efeso.

5. Kulingana na 2 Timotheo 3:14, 15, ni mambo gani mawili yaliyomsaidia Timotheo afanye uamuzi wa kufuatia miradi ya kiroho?

5 Ni wazi kwamba Timotheo aliamua kufuatia miradi ya kiroho. Lakini kwa nini alifanya uamuzi huo? Katika barua yake ya pili kwa Timotheo, Paulo alitaja mambo mawili yaliyomsaidia Timotheo. “Endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini,” akaandika, “ukijua ni kutoka kwa watu gani ulijifunza hayo na kwamba tangu utoto mchanga umeyajua maandishi matakatifu.” (2 Timotheo 3:14, 15) Acheni kwanza tuchunguze jinsi Wakristo wengine walivyomsaidia Timotheo kufanya maamuzi mazuri.

Faida ya Uvutano Mzuri

6. Timotheo alipata mazoezi gani, naye aliitikia jinsi gani?

Timotheo alilelewa katika familia iliyogawanyika kidini. Baba yake alikuwa Mgiriki, mama yake, Eunike, na nyanya yake Loisi walikuwa Wayahudi. (Matendo 16:1) Eunike na Loisi walimfundisha Timotheo tangu utotoni kweli kutoka katika Maandiko ya Kiebrania. Baada ya kuwa Wakristo, bila shaka walisaidia kumshawishi aamini mafundisho ya Kikristo. Kwa wazi, Timotheo alijitahidi kufaidika kabisa na mazoezi hayo bora. Paulo alisema hivi: “Naikumbuka imani iliyo ndani yako isiyo na unafiki wowote, na ambayo ilikaa kwanza katika nyanya yako Loisi na mama yako Eunike, lakini ambayo mimi nina hakika imo ndani yako pia.”—2 Timotheo 1:5.

7. Vijana wengi wanapata baraka gani, na baraka hizo zinaweza kuwafaidi jinsi gani?

7 Leo, vijana wengi wamebarikiwa kuwa na wazazi, babu, na nyanya wanaomwogopa Mungu, ambao kama Loisi na Eunike, wanatambua umuhimu wa miradi ya kiroho. Kwa mfano, Samira angali anakumbuka mazungumzo marefu ambayo alikuwa nayo na wazazi wake alipokuwa tineja. “Mama na Baba walinifundisha kuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu mambo na kutanguliza kazi ya kuhubiri katika maisha yangu,” anasema. “Sikuzote walinichochea nifuatie utumishi wa wakati wote.” Samira aliitikia kitia-moyo cha wazazi wake na sasa ana pendeleo la kutumika akiwa Mwanabetheli katika nchi yao. Ikiwa wazazi wako wanakutia moyo ukazie fikira miradi ya kiroho, fikiria mashauri yao kwa uzito. Wanataka ufanikiwe maishani.—Methali 1:5.

8. Timotheo alifaidika jinsi gani na ushirika wenye kujenga wa Wakristo?

8 Pia, ni jambo la maana kwako kutafuta marafiki wenye kujenga katika undugu wa Kikristo. Timotheo alijulikana sana na wazee Wakristo katika kutaniko lao na pia wale wa kutaniko la Ikoniamu, ambalo lilikuwa umbali wa kilomita 30 hivi kutoka kwao. (Matendo 16:1, 2) Alijenga uhusiano wa karibu sana na Paulo, ambaye alikuwa na bidii nyingi. (Wafilipi 3:14) Barua za Paulo zinaonyesha kwamba Timotheo alikubali mashauri na kwamba alikuwa tayari kufuata vielelezo vya imani. (1 Wakorintho 4:17; 1 Timotheo 4:6, 12-16) Paulo aliandika hivi: “Umefuata kwa ukaribu fundisho langu, mwendo wangu wa maisha, kusudi langu, imani yangu, ustahimilivu wangu, upendo wangu, uvumilivu wangu.” (2 Timotheo 3:10) Ndiyo, Timotheo alifuata kwa ukaribu sana mfano wa Paulo. Vivyo hivyo, ukisitawisha uhusiano wa karibu pamoja na watu wenye nguvu kiroho katika kutaniko, watakusaidia kufuatia miradi mizuri ya kiroho.—2 Timotheo 2:20–22.

Jifunze “Maandishi Matakatifu”

9. Zaidi ya kuwa na mashirika mazuri, unapaswa kufanya ili ‘kujizoeza ujitoaji-kimungu ukiwa shabaha yako’?

9 Je, utafikia miradi ya kiroho kwa sababu tu ya kuwa na mashirika mazuri? Hapana. Kama Timotheo, unahitaji kuchunguza kwa makini “maandishi matakatifu.” Labda hupendi sana kujifunza, lakini kumbuka kwamba Timotheo alipaswa ‘kujizoeza ujitoaji-kimungu ukiwa ni shabaha yake.’ Mara nyingi, wakimbiaji wanajizoeza kwa bidii sana na kwa miezi mingi ili wafikie mradi wao. Vivyo hivyo, ili kufikia miradi ya kiroho tunahitaji kujidhabihu na kujitahidi kabisa. (1 Timotheo 4:7, 8, 10) Lakini huenda ukauliza, ‘Kujifunza Biblia kunaweza kunisaidia kwa njia gani kufikia miradi yangu?’ Acha tuzungumzie njia tatu.

10, 11. Kwa nini Maandiko yatakuchochea ufikie miradi ya kiroho? Toa mfano.

10 Kwanza, Maandiko yatakupa kichocheo kinachofaa. Yanafunua utu wenye kuvutia wa Baba yetu wa mbinguni, tendo lake kuu la upendo kutuelekea, na baraka za milele ambazo atawapa watumishi wake waaminifu. (Amosi 3:7; Yohana 3:16; Waroma 15:4) Kadiri ujuzi wako kumhusu Yehova unavyoongezeka, ndivyo upendo wako kumwelekea na tamaa yako ya kujiweka wakfu kwake itakavyoongezeka.

11 Vijana wengi Wakristo wanasema kwamba kujifunza Biblia kibinafsi kwa ukawaida kumewasaidia sana kuifanya kweli iwe mali yao. Kwa mfano, Adele alilelewa katika familia ya Kikristo lakini hakujiwekea miradi yoyote ya kiroho. Anasema hivi: “Wazazi wangu walinipeleka kwenye Jumba la Ufalme, lakini sikujifunza kibinafsi au kusikiliza mikutanoni.” Baada ya dada yake kubatizwa, Adele alianza kuchukua kweli kwa uzito. “Nilijiwekea mradi wa kusoma Biblia nzima. Nilikuwa nikisoma sehemu ndogo na kisha kuandika maelezo fulani kuhusiana na sehemu niliyosoma. Bado nina maandishi yangu yote. Niliisoma Biblia nzima kwa mwaka mmoja.” Hilo lilimchochea Adele aweke maisha yake wakfu kwa Yehova. Ingawa amelemaa vibaya sana, kwa sasa yeye ni painia, au mweneza-injili wa wakati wote.

12, 13. (a) Kujifunza Biblia kutamsaidia kijana afanye mabadiliko gani, na jinsi gani? (b) Toa mifano ya hekima inayotumika iliyo katika Neno la Mungu.

12 Pili, Biblia itakusaidia ufanye mabadiliko yanayohitajiwa katika utu wako. Paulo alimwambia Timotheo kwamba “maandishi matakatifu” ni ‘yenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa kutafakari kwa ukawaida mambo yanayohusiana na Neno la Mungu na kutumia kanuni za Biblia, utaruhusu roho ya Mungu iboreshe utu wako. Itakuza ndani yako sifa muhimu, kama vile unyenyekevu, uvumilivu, bidii, na upendo wa kweli kwa Wakristo wenzako. (1 Timotheo 4:15) Timotheo alikuwa na sifa hizo, nazo zilimfanya awe msaada mkubwa kwa Paulo na kwa makutaniko aliyotumikia.—Wafilipi 2:20-22.

13 Tatu, Neno la Mungu ni hazina ya hekima inayotumika. (Zaburi 1:1-3; 19:7; 2 Timotheo 2:7; 3:15) Litakusaidia uchague marafiki kwa hekima, uchague burudani zinazofaa, na kukabiliana na matatizo mengine mengi. (Mwanzo 34:1, 2; Zaburi 119:37; 1 Wakorintho 7:36) Kufanya maamuzi yenye hekima sasa kutakusaidia kufikia miradi yako ya kiroho.

“Pigana Pigano Zuri”

14. Kwa nini kufuatia miradi ya kiroho si jambo rahisi?

14 Kutanguliza miradi ambayo inamletea Yehova heshima ndilo jambo lenye hekima zaidi, lakini bila shaka si jambo rahisi. Kwa mfano, inapohusu kuchagua kazi, huenda ukasukumwa sana na watu wa ukoo, wanashule wenzako, na walimu wenye nia nzuri ambao wanaamini kwamba elimu ya juu na kazi nzuri ndiyo siri ya kupata furaha na mafanikio ya kweli. (Waroma 12:2) Kama Timotheo, utahitaji ‘kupigana pigano zuri la imani’ ili “ushike imara ule uzima wa milele” ambao Yehova anakuahidi.—1 Timotheo 6:12; 2 Timotheo 3:12.

15. Labda Timotheo alikabiliana na upinzani gani?

15 Wakati washiriki wa familia ambao si waamini wanapopinga maamuzi yako, hilo linaweza kuwa jaribu kali zaidi. Labda, Timotheo alilazimika kushinda upinzani kama huo. Kitabu kimoja kinasema kwamba labda familia ya Timotheo “ilikuwa yenye elimu na yenye utajiri.” Huenda baba yake alimtazamia Timotheo apate elimu ya juu na kuendeleza biashara ya familia. * Wazia jinsi ambavyo huenda baba ya Timotheo alihisi alipogundua kwamba Timotheo alipendelea kazi hatari na isiyo na pesa ya kufanya umishonari pamoja na Paulo!

16. Kijana mmoja alipambana jinsi gani na upinzani kutoka kwa mzazi wake?

16 Leo vijana Wakristo wanakabili matatizo kama hayo. Matthew, ambaye anafanya kazi katika moja ya ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova, anakumbuka hivi: “Nilipoanza utumishi wa upainia, baba yangu alihuzunika sana. Alihisi kwamba nilikuwa ‘nimepoteza’ elimu yangu kwa kufanya kazi ya kusafisha ofisi ili nipate mahitaji yangu na kuendelea na huduma. Alikuwa akinidhihaki na kunikumbusha kwamba ningepata pesa nyingi ikiwa ningefanya kazi ya wakati wote.” Matthew alipambana jinsi gani na upinzani huo? “Nilifuata kabisa programu yangu ya kusoma Biblia na nilisali kwa ukawaida, hasa nilipokabili mambo ambayo yangeweza kunikasirisha kwa urahisi.” Matthew amepata thawabu kwa sababu ya azimio lake. Baada ya muda, uhusiano wake pamoja na baba yake ukawa mzuri zaidi. Pia, Matthew amekuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova. Matthew anasema hivi: “Nimeona Yehova akitosheleza mahitaji yangu, akinitia moyo, na kunilinda nisifanye maamuzi mabaya. Singefurahia mambo hayo yote ikiwa singefikia miradi yangu ya kiroho.”

Kazia Fikira Miradi ya Kiroho

17. Watu fulani wanaweza kimakosa kuwavunja moyo jinsi gani wale wanaopanga kuanza utumishi wa wakati wote? (Mathayo 16:22)

17 Huenda hata waamini wenzako wakakuvunja moyo kimakosa usifuatie miradi yako ya kiroho. Huenda wengine wakauliza, ‘Kwa nini uwe painia? Unaweza kuishi maisha ya kawaida na bado ushiriki katika kazi ya kuhubiri. Tafuta kazi nzuri ili uwe na usalama wa kifedha.’ Hayo yanaweza kuonekana kuwa mashauri mazuri, lakini ukiyafuata mashauri hayo, je, kweli utakuwa ukijizoeza ujitoaji-kimungu ukiwa ni shabaha yako?

18, 19. (a) Unaweza kukazia fikira miradi ya kiroho jinsi gani? (b) Eleza jinsi unavyojidhabihu ukiwa kijana kwa ajili ya Ufalme.

18 Inaelekea kwamba Wakristo fulani katika siku za Timotheo walikuwa na maoni kama hayo. (1 Timotheo 6:17) Ili kumsaidia Timotheo akazie macho yake miradi ya kiroho, Paulo alimtia moyo kwa kusema hivi: “Mtu anayetumikia akiwa askari-jeshi hajihusishi katika shughuli za kibiashara za maisha, ili apate kibali cha yule aliyemwandika kuwa askari-jeshi.” (2 Timotheo 2:4) Askari-jeshi aliye katika shughuli za kijeshi hawezi kuruhusu shughuli za kawaida za raia zimkengeushe fikira. Uhai wake na uhai wa wengine unategemea yeye kuwa tayari sikuzote kutekeleza amri za amiri-jeshi wake. Ukiwa askari-jeshi chini ya uongozi wa Kristo unapaswa pia kuazimia kukazia fikira jambo moja na kuepuka kunaswa na shughuli za kufuatia mambo ya kimwili yasiyo ya lazima ambayo yanaweza kukuzuia usitimize kikamili huduma yako inayookoa uhai.—Mathayo 6:24; 1 Timotheo 4:16; 2 Timotheo 4:2, 5.

19 Badala ya kuweka mradi wa kuishi maisha ya starehe, kuza roho ya kujidhabihu. “Uwe tayari kuishi bila starehe za maisha, kama mmoja wa askari-jeshi wa Kristo Yesu.” (2 Timotheo 2:3, The English Bible in Basic English) Aliposhirikiana na Paulo, Timotheo alijifunza siri ya kuridhika hata alipokabili hali ngumu zaidi. (Wafilipi 4:11, 12; 1 Timotheo 6:6-8) Unaweza kufanya vivyo hivyo. Je, uko tayari kujidhabihu kwa ajili ya Ufalme?

Baraka za Sasa na za Wakati Ujao

20, 21. (a) Eleza baraka fulani ambazo utapata ukifuatia miradi ya kiroho. (b) Unaazimia kufanya nini?

20 Timotheo alishikamana kabisa na Paulo kwa miaka 15 hivi. Timotheo aliona makutaniko mapya yakianzishwa kadiri habari njema ilivyoenea karibu sehemu zote za kaskazini ya Mediterania. Maisha yake yalikuwa yenye kusisimua na kuridhisha kuliko yale angekuwa nayo kama angechagua kuishi maisha “ya kawaida.” Ukifuatia miradi ya kiroho, wewe pia utapata baraka za kiroho zenye thamani sana. Utakuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova na utapendwa na kuheshimiwa na Wakristo wenzako. Badala ya uchungu na kukatishwa tamaa kunakosababishwa na kufuatia mali za kimwili, utapata furaha ya kweli inayotokana na kujidhabihu bila uchoyo. Jambo la maana zaidi ni kwamba ‘utaushika imara uzima ulio wa kweli,’ yaani, uzima wa milele katika paradiso duniani.—1 Timotheo 6:9, 10, 17-19; Matendo 20:35.

21 Kwa hiyo, tunakuhimiza kwa uchangamfu uanze sasa kujizoeza ujitoaji-kimungu ukiwa shabaha yako ikiwa bado hujafanya hivyo. Wakaribie zaidi washiriki wa kutaniko ambao wanaweza kukusaidia kufikia miradi ya kiroho, na utafute mwongozo wao. Tanguliza funzo la kibinafsi la kawaida la Neno la Mungu katika maisha yako. Azimia kuipinga roho ya ulimwengu huu ya kufuatia vitu vya kimwili. Na kumbuka sikuzote kwamba Mungu “ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie” anakuahidi baraka nyingi sasa na wakati ujao ikiwa utachagua miradi ambayo inamletea heshima.—1 Timotheo 6:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Wagiriki walithamini sana elimu. Plutarch, aliyeishi wakati mmoja na Timotheo, aliandika hivi: “Kupata elimu inayofaa ni chanzo cha mambo yote mazuri. . . . Ninasema, ni elimu inayomsaidia mtu kuwa na maadili bora na furaha. . . . Mambo mengine yote ni ya kibinadamu, ni madogo na ni ya hali ya chini sana, na hayastahili kuhangaikiwa sana.”—Moralia, I, “The Education of Children.”

Je, Unakumbuka?

• Vijana wanaweza kupata wapi msaada wa kufikia miradi ya kiroho?

• Kwa nini ni muhimu sana kujifunza Biblia kwa makini?

• Vijana wanaweza jinsi gani kupinga uvutano wa ulimwengu huu wa kufuatia vitu vya kimwili?

• Kufuatia miradi ya kiroho kunaleta baraka gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24]

Timotheo alifuatia miradi mizuri

[Picha katika ukurasa wa 25]

Ni uvutano gani mzuri uliomsaidia Timotheo?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Je, unajitahidi kufikia miradi ya kiroho?