Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kukabiliana na Ukosefu wa Haki!

Unaweza Kukabiliana na Ukosefu wa Haki!

Unaweza Kukabiliana na Ukosefu wa Haki!

NI NANI hajawahi kutendewa isivyo haki katika maisha yake yote? Ingawa huenda ukosefu mbalimbali wa haki ukawa wa kuwaziwa tu, ukosefu mwingine wa haki unatukia kihalisi.

Wakati wowote tunapotendewa isivyo haki, tunasikia uchungu moyoni na tunaweza kuruhusu uchungu huo uharibu hali yetu ya kiroho. Huenda tukatamani sana kurekebisha hali hiyo. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba Muumba wetu, Yehova Mungu, “ambaye hana ukosefu wowote wa haki,” aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya kuona haki ikifuatwa. (Kumbukumbu la Torati 32:4; Mwanzo 1:26) Hata hivyo, huenda tukakabili hali fulani ambazo zinafanya tuhisi kwamba haki haikufuatwa. Mtu mmoja mwenye hekima alisema hivi wakati fulani: “Nikarudi nipate kuona matendo yote ya uonevu yanayofanywa chini ya jua, na, tazama! machozi ya wale wanaokandamizwa, lakini hawakuwa na mtu wa kuwafariji; nao wakandamizaji walikuwa na nguvu, hivi kwamba hawakuwa na mtu wa kuwafariji.” (Mhubiri 4:1) Basi tunaweza kukabiliana jinsi gani na ukosefu wa haki?

Ukosefu wa Haki Ni Nini Hasa?

Ukosefu wa haki ni hali au zoea la kuvunja viwango vya haki. Ni nini kiwango cha haki kwa ajili ya wanadamu? Kwa wazi, Muumba wetu mwadilifu na asiyebadilika ana haki ya kuweka kiwango cha yaliyo haki na yasiyo haki. Kwa maoni yake, kutembea “katika sheria za uzima” kunatia ndani “kutotenda ukosefu wa haki.” (Ezekieli 33:15) Hivyo, Yehova alipomuumba mtu wa kwanza, alimpa dhamiri, yaani, sauti ya ndani ambayo ingeweza kumsaidia kutofautisha yaliyo sawa na yasiyo sawa. (Waroma 2:14, 15) Kwa kuongezea, Yehova anaeleza katika Neno lake, Biblia, mambo yaliyo ya haki na yale yasiyo ya haki.

Namna gani ikiwa tunahisi kwamba tulitendewa isivyo haki? Tunapaswa kuchunguza jambo hilo vizuri ili kuona ikiwa kwa kweli tulitendewa isivyo haki. Kwa mfano, fikiria hali ambayo nabii Mwebrania Yona alikabili. Yehova alimtuma awaambie Waninawi kuhusu msiba ambao ulikuwa ukija. Mwanzoni, Yona alikimbia badala ya kutimiza mgawo wake. Hata hivyo, mwishowe alienda Ninawi na kuwaonya wakaaji wake kuhusu msiba huo. Walipoitikia kwa njia nzuri, Yehova aliamua kutoliharibu jiji hilo na kuwaokoa wakaaji wake. Yona alihisi namna gani? “Jambo hilo halikumpendeza Yona hata kidogo, naye akawaka hasira.” (Yona 4:1) Alihisi kwamba Yehova hakutenda kabisa kwa njia ya haki.

Bila shaka, Yehova, ambaye anaweza kusoma mioyo na ambaye “anapenda uadilifu na haki,” hakuwa amekosea. (Zaburi 33:5) Yona alihitaji tu kujifunza kwamba uamuzi wa Yehova ulipatana na haki kamilifu. Tunapohisi kwamba tumetendewa isivyo haki, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, inawezekana kwamba Yehova angeona jambo hili kwa njia tofauti?’

Kukabiliana na Ukosefu wa Haki

Biblia inaripoti visa vingi vya watu ambao walitendewa isivyo haki. Tunaweza kujifunza mengi kwa kuchunguza jinsi walivyokabiliana na matatizo yao magumu. Mfikirie Yosefu, ambaye aliuzwa utumwani huko Misri na ndugu zake wenye wivu. Huko Misri, mke wa bwana wake alijaribu kumtongoza Yosefu, na alipokataa, mke huyo alimshtaki kwa uwongo kwamba alitaka kulala naye. Kwa sababu hiyo, Yosefu alitiwa gerezani. Hata hivyo, imani yake ilikuwa na nguvu kuliko pingu za chuma ambazo alifungwa. Hakuruhusu ukosefu huo wa haki uharibu hali yake ya kiroho au udhoofishe tumaini lake katika Yehova.—Mwanzo 37:18-28; 39:4-20; Zaburi 105:17-19.

Mtu mwingine aliyetendewa isivyo haki ni Nabothi. Yezebeli, mke wa Mfalme Ahabu wa Israeli alipanga njama ya hila juu yake. Mfalme alitamani shamba la urithi la Nabothi ambalo lilikuwa kando ya jumba la mfalme. Mwisraeli hakupaswa kumpa mtu mwingine shamba lake la urithi, hivyo Nabothi alikataa kumuuzia mfalme shamba hilo. (Mambo ya Walawi 25:23) Basi, mke mwovu wa Ahabu alipanga mashahidi wa uwongo wamshtaki Nabothi kwa kudai kwamba amemkufuru Mungu na kumlaani mfalme. Kwa sababu hiyo, Nabothi na wanawe waliuawa. Hebu wazia jinsi Nabothi alivyohisi watu walipokuwa wakiokota mawe ili wamuue!—1 Wafalme 21:1-14; 2 Wafalme 9:26.

Hata hivyo, matukio hayo hayawezi kamwe kulinganishwa na ukosefu wa haki ambao Kristo Yesu alitendewa. Alihukumiwa kifo kwa mashtaka ya uwongo na kesi isiyo halali. Gavana Mroma aliyekuwa akimhukumu hakuwa imara kutetea mambo aliyoona kuwa sawa. (Yohana 18:38-40) Ndiyo, Shetani alimtendea Kristo Yesu matendo makubwa zaidi yasiyo ya haki kuliko yale ambayo mtu mwingine yeyote amewahi kutendewa!

Je, visa hivyo vinaonyesha kwamba Yehova anapuuza ukosefu wa haki? Hapana! Yehova hakuona visa hivyo kama wanadamu wanavyoviona. (Isaya 55:8, 9) Kwa kuwa Yosefu aliuzwa utumwani, aliweza kuokoa familia yake. Alikuja kuwa msimamizi wa chakula nchini Misri kabla ya njaa kubwa ambayo iliikumba familia yake. Hebu fikiria, ikiwa Yehova angezuia Yosefu asitendewe isivyo haki, Yosefu hangekuwa gerezani. Aliweza kutafsiri ndoto za wale wafungwa wawili humo gerezani, na ni mfungwa mmoja kati yao ndiye aliyemwambia Farao baadaye kumhusu Yosefu, na hivyo Yosefu akawekwa kuwa msimamizi wa chakula.—Mwanzo 40:1; 41:9-14; 45:4-8.

Namna gani Nabothi? Jaribu tena kuona jambo hilo kama Yehova alivyoliona. Machoni pa Yehova, ambaye anaweza kuwafufua wafu, ni kana kwamba Nabothi alikuwa hai ingawa alikuwa maiti. (1 Wafalme 21:19; Luka 20:37, 38) Nabothi hana budi kungoja mpaka wakati ambapo Yehova atamfufua, lakini muda huo ni mfupi tu, kwa kuwa wafu hawajui lolote kamwe. (Mhubiri 9:5) Zaidi ya hilo, Yehova alimlipizia kisasi Nabothi kwa kumhukumu Ahabu na watu wa nyumba yake.—2 Wafalme 9:21, 24, 26, 35, 36; 10:1-11; Yohana 5:28, 29.

Yesu alikufa. Hata hivyo, Mungu alimfufua na kumpa cheo cha juu “zaidi kuliko kila serikali na mamlaka na nguvu na utawala na kila jina linalotajwa.” (Waefeso 1:20, 21) Ukosefu wa haki ambao Shetani alimtendea Kristo Yesu haungeweza kumzuia Yehova asimthawabishe Mwana wake. Yesu alikuwa na hakika kwamba Yehova angeweza kuzuia mara moja hatua isiyo ya haki ya kumkamata kinyume cha sheria, kama yangekuwa mapenzi ya Yehova kufanya hivyo. Lakini, Kristo alijua pia kwamba Yehova ana wakati wa kutimiza Maandiko na kuondoa ukosefu wowote wa haki.

Ni kweli kwamba Shetani na watumishi wake waliwatendea isivyo haki watu waadilifu, lakini mwishowe Yehova alirekebisha mambo na kukomesha kabisa ukosefu huo wa haki au atauondoa wakati ujao. Kwa hiyo, ni lazima tumngojee Mungu ili arekebishe ukosefu wa haki.—Kumbukumbu la Torati 25:16; Waroma 12:17-19.

Kwa Nini Yehova Anaweza Kuachilia Ukosefu wa Haki

Huenda Yehova akawa na sababu za kutorekebisha hali fulani. Anaweza kuacha tutendewe isivyo haki kama sehemu ya mazoezi yetu ya Kikristo. Bila shaka, ‘Mungu hamjaribu yeyote na mambo maovu.’ (Yakobo 1:13) Hata hivyo, anaweza kuacha hali fulani iendelee, naye anaweza kuwatia nguvu wale wanaofaidika na mazoezi hayo. “Mkiisha kuteseka kitambo kidogo,” Biblia inatuhakikishia, “Mungu wa fadhili zote zisizostahiliwa . . . yeye mwenyewe atamaliza mazoezi yenu, atawafanya ninyi kuwa imara, atawafanya ninyi kuwa wenye nguvu.”—1 Petro 5:10.

Zaidi ya hayo, kwa kuachilia ukosefu fulani wa haki, Yehova anaweza kuwapa wakosaji wakati wa kutubu. Majuma machache tu baada ya Yesu kuuawa, Wayahudi fulani ambao walisikiliza shauri la Petro “walichomwa moyoni.” Walikubali neno la Mungu kwa ukunjufu wa moyo nao wakabatizwa.—Matendo 2:36-42.

Kwa kweli, si watu wote wanaowatendea wengine isivyo haki watatubu. Huenda wengine hata wakapata ujasiri wa kutenda matendo mabaya zaidi ya ukosefu wa haki. Hata hivyo, Methali 29:1 inasema: “Mtu anayekaripiwa tena na tena lakini anayeifanya shingo yake kuwa ngumu atavunjika ghafula, na hivyo pasipo kuponywa.” Kwa hakika, mwishowe Yehova atachukua hatua na kuwaharibu kabisa wale wanaoendelea kutenda mambo yasiyofaa.—Mhubiri 8:11-13.

Hata tukiteseka kwa muda mrefu kadiri gani kwa sababu ya ukosefu wa haki, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anajua jinsi ya kutusaidia. Na bila shaka ataondoa ukosefu wowote wa haki ambao huenda tumekabili katika mfumo huu mwovu wa mambo. Zaidi ya hayo, ameahidi kutupa thawabu mwishowe, thawabu ya uzima wa milele katika ulimwengu mpya ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Nabothi alihisi namna gani alipotendewa isivyo haki?