Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Mpenda-haki

Yehova Ni Mpenda-haki

Yehova Ni Mpenda-haki

“Mimi, Yehova, napenda haki.”—ISAYA 61:8.

1, 2. (a) Maneno “haki” na “ukosefu wa haki” yanamaanisha nini? (b) Biblia inasema nini kumhusu Yehova na sifa yake ya haki?

HAKI inafafanuliwa kuwa ‘sifa ya kutokuwa na ubaguzi, kutopendelea, kutenda kupatana na yaliyo manyoofu na mazuri kiadili.’ Ukosefu wa haki unamaanisha kupendelea, kuwa mwenye ubaguzi, kuwa mbaya, na mwenye kuwaumiza wengine.

2 Karibu miaka 3,500 iliyopita, Musa aliandika hivi kumhusu Mwenye Enzi Kuu, Yehova: “Njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Zaidi ya karne saba baadaye, Mungu alimwongoza Isaya kwa roho takatifu kuandika maneno yafuatayo: “Mimi, Yehova, napenda haki.” (Isaya 61:8) Kisha katika karne ya kwanza, Paulo alisema hivi: “Je, Mungu ana ukosefu wa haki? Isiwe hivyo kamwe!” (Waroma 9:14) Na katika karne hiyohiyo, Petro alisema: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Ndiyo, “Yehova ni mpenda-haki.”—Zaburi 37:28; Malaki 3:6.

Ukosefu wa Haki Unaenea

3. Ukosefu wa haki ulianza duniani jinsi gani?

3 Leo sifa ya haki imetoweka. Tunaweza kutendewa isivyo haki katika kila sehemu ya maisha, yaani, kazini, shuleni, tunaposhughulika na wenye mamlaka, katika njia nyinginezo, na hata katika familia. Bila shaka, ukosefu wa haki kama huo si jambo geni. Ukosefu wa haki ulianza katika jamii ya wanadamu wakati wazazi wetu wa kwanza walipoasi na kuwa waasi-sheria, wakichochewa na kiumbe wa roho aliyeasi na kuwa Shetani Ibilisi. Bila shaka, Adamu, Hawa, na Shetani, walitenda isivyo haki kwa kutumia vibaya zawadi bora ya uhuru wa kuchagua ambayo walipewa na Yehova. Matendo yao mabaya yalitokeza mateso makubwa na kifo kwa jamii nzima ya wanadamu.—Mwanzo 3:1-6; Waroma 5:12; Waebrania 2:14.

4. Ukosefu wa haki umekuwa sehemu ya historia ya wanadamu kwa muda gani?

4 Kwa miaka 6,000 hivi tangu uasi utokee katika Edeni, ukosefu wa haki umekuwa sehemu ya maisha ya jamii ya wanadamu. Bila shaka, hilo lingetarajiwa kwa sababu Shetani ndiye mungu wa ulimwengu huu. (2 Wakorintho 4:4) Yeye ni mwongo na baba ya uwongo, mchongezi, na mpinzani wa Yehova. (Yohana 8:44) Sikuzote amesababisha matendo mabaya sana ya ukosefu wa haki. Kwa mfano, kwa sababu ya uvutano mwovu wa Shetani kabla ya Gharika ya siku za Noa, Mungu aliona kwamba “ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila mwelekeo wa fikira za moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote.” (Mwanzo 6:5) Hali hiyo bado ilikuwepo hata katika siku za Yesu. Alisema hivi: “Unatosha kila siku ubaya wake,” akimaanisha matatizo yenye kufadhaisha ya siku hiyo, kama vile ukosefu wa haki. (Mathayo 6:34) Biblia inasema hivi kwa usahihi: “Uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja mpaka sasa.”—Waroma 8:22.

5. Kwa nini kuna ukosefu mwingi wa haki leo kuliko wakati mwingine wowote?

5 Hivyo, mambo mabaya yanayosababisha ukosefu mkubwa sana wa haki yametukia katika historia yote ya wanadamu. Leo hali ni mbaya hata zaidi. Kwa nini? Kwa sababu mfumo huu wa mambo usiomwogopa Mungu umekuwa katika ‘siku zake za mwisho’ kwa miaka mingi, nao umekumbwa na “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo” huku ukikaribia mwisho wake. Biblia ilitabiri kwamba katika kipindi hiki cha historia, watu wangekuwa wenye “kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, . . . wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi.” (2 Timotheo 3:1-5) Sifa mbaya kama hizo zinaongoza kwenye ukosefu wa haki wa kila aina.

6, 7. Ni matendo gani ya ukosefu mkubwa wa haki ambayo yameiumiza jamii ya wanadamu katika nyakati za kisasa?

6 Katika muda wa miaka mia moja iliyopita, kumekuwa na ukosefu mwingi wa haki ambao haujawahi kamwe kutukia. Sababu moja ni kwamba miaka hiyo imekuwa yenye vita vingi zaidi. Kwa mfano, wanahistoria fulani wanakadiria kwamba katika Vita vya Pili vya Ulimwengu tu, jumla ya watu waliouawa ilikuwa kutoka milioni 50 mpaka milioni 60 hivi, na wengi wao walikuwa raia; wanaume, wanawake, na watoto wasio na hatia. Tangu vita hivyo viishe, mamilioni ya watu wameuawa katika vita mbalimbali, wengi wao wakiwa raia. Shetani anasababisha ukosefu huo mwingi wa haki kwa sababu ana ghadhabu, akijua kwamba hivi karibuni Yehova atamshinda kabisa. Unabii wa Biblia unasema hivi: “Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:12.

Sasa gharama za kijeshi ulimwenguni pote ni dola trilioni moja hivi kila mwaka. Mamia ya mamilioni ya watu hawawezi kutimiza mahitaji yao ya lazima ya maisha. Hivyo, fikiria faida ambayo ingepatikana ikiwa pesa hizo zote zingetumiwa kwa mambo yenye kuchangia amani. Karibu watu bilioni moja hawana chakula cha kutosha, lakini wengine wana chakula kingi zaidi. Kulingana na chanzo kimoja cha Umoja wa Mataifa, watoto milioni tano hivi wanakufa kila mwaka kwa sababu ya matokeo ya njaa. Ni ukosefu mkubwa wa haki kama nini! Halafu, fikiria pia watoto wengi wasio na hatia ambao wanauawa kwa utoaji wa mimba. Inakadiriwa kwamba kila mwaka, kati ya watoto milioni 40 na milioni 60 hivi wanauawa ulimwenguni pote. Ni ukosefu wa haki wenye kuhuzunisha kama nini!

8. Haki ya kweli kwa wanadamu inaweza kupatikana kwa njia gani tu?

8 Wanadamu wanaotawala hawapati suluhisho kwa matatizo mengi yanayowakumba wanadamu leo; wala jitihada za wanadamu haziwezi kuboresha hali. Neno la Mungu lilitabiri kwamba katika wakati wetu “watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi, wakipotosha na kupotoshwa.” (2 Timotheo 3:13) Ukosefu wa haki umeenea sana katika maisha yetu ya kila siku hivi kwamba wanadamu hawawezi kuuondoa. Mungu wa haki tu ndiye anayeweza kuuondoa. Ni yeye tu anayeweza kumwondoa Shetani, roho waovu, na wanadamu waovu.—Yeremia 10:23, 24.

Kuna Sababu Nzuri ya Kuwa na Hangaiko

9, 10. Kwa nini Asafu alishuka moyo?

9 Zamani, hata waandikaji fulani wa Biblia walijiuliza kwa nini Mungu hakuwa ameingilia kati mambo ya wanadamu na hivyo kuleta haki ya kweli na uadilifu. Fikiria mfano wa mwanamume mmoja katika nyakati za Biblia. Maandishi ya utangulizi ya Zaburi ya 73 yanaonyesha jina Asafu, yakirejelea Mlawi mmoja ambaye alikuwa mwanamuziki mashuhuri wakati wa utawala wa Mfalme Daudi au wanamuziki wa nyumba ambayo Asafu alikuwa ndiye baba wa ukoo. Asafu na wazao wake waliandika nyimbo nyingi ambazo zilitumiwa katika ibada ya watu wote. Hata hivyo, wakati fulani katika maisha yake, mwandikaji wa zaburi hiyo alishuka moyo kiroho. Aliona utajiri wa kimwili wa watu waovu, na mara nyingi walionekana kuwa wenye kutosheka maishani, na kwamba hawakupata matokeo yoyote mabaya.

10 Tunasoma hivi: “Niliwaonea wivu wenye kujisifu, nilipokuwa nikiiona amani ya watu waovu. Kwa maana hawana maumivu ya kifo; na kitambi chao ni kinono. Wala hawamo katika taabu ya mwanadamu anayeweza kufa, wala hawapati mapigo kama wanadamu wengine.” (Zaburi 73:2-8) Lakini baadaye mwandikaji huyo wa Biblia alitambua kwamba maoni kama hayo yalikuwa yenye makosa. (Zaburi 73:15, 16) Mtunga-zaburi huyo alijaribu kurekebisha njia yake ya kufikiri, lakini hangeweza kuelewa kabisa kwa nini waovu walionekana wanaepuka adhabu huku watu wanyoofu wakiteseka mara nyingi.

11. Mtunga-zaburi Asafu alipata kuelewa nini?

11 Mwishowe, mwanamume huyo mwaminifu wa kale alipata kuelewa yale ambayo yangewapata waovu na kwamba mwishowe Yehova angerekebisha mambo. (Zaburi 73:17-19) Daudi aliandika hivi: “Mtumaini Yehova na kuishika njia yake, naye atakuinua uimiliki dunia. Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.”—Zaburi 37:9, 11, 34.

12. (a) Kusudi la Yehova ni nini kuhusiana na uovu na ukosefu wa haki? (b) Wewe unahisi jinsi gani kuhusu suluhisho hilo la tatizo la ukosefu wa haki?

12 Kwa hakika, Yehova anakusudia kwa wakati wake kuondoa duniani pote uovu na ukosefu mwingi wa haki unaotokana nao. Hilo ni jambo ambalo hata Wakristo washikamanifu wanapaswa kujikumbusha kwa ukawaida. Yehova atawaondoa wale wanaopinga mapenzi yake, naye atawathawabisha wale wanaoishi kulingana nayo. “Macho yake yanaangalia, macho yake yanayong’aa yanawachunguza wana wa binadamu. Yehova humchunguza mwadilifu na pia mwovu, na mtu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake hakika inamchukia. Yeye atawanyeshea waovu mitego, moto na kiberiti na upepo wenye kuunguza . . . Kwa maana Yehova ni mwadilifu; yeye huyapenda matendo ya uadilifu.”—Zaburi 11:4-7.

Ulimwengu Mpya wa Haki

13, 14. Kwa nini kutakuwa na uadilifu na haki katika ulimwengu mpya?

13 Yehova atakapoharibu mfumo huu wa mambo usio na haki ambao unaongozwa na Shetani, Yeye ataanzisha ulimwengu mpya wenye utukufu. Utatawaliwa na Ufalme wa kimbingu wa Mungu, ambao Yesu aliwafundisha wafuasi wake kusali kuuhusu. Kutakuwa na uadilifu na haki badala ya uovu na ukosefu wa haki, kwa kuwa wakati huo sala hii itajibiwa katika maana kamili: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:10.

14 Biblia inatuambia ni aina gani ya utawala tunaoweza kutazamia, utawala ambao sasa watu wote wanyoofu wanatazamia sana. Kisha, Zaburi 145:16 itatimia katika maana kamili: “Unaufumbua [Yehova Mungu] mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” Zaidi ya hayo, andiko la Isaya 32:1 linasema hivi: “Tazama! Mfalme [Kristo Yesu akiwa mbinguni] atatawala kwa ajili ya uadilifu; nao wakuu [wawakilishi wa Kristo duniani] watatawala wakiwa wakuu kwa ajili ya haki.” Kuhusu Mfalme Yesu Kristo, andiko la Isaya 9:7 linatabiri hivi: “Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani, juu ya kiti cha ufalme cha Daudi na juu ya ufalme wake ili kuufanya imara na kuutegemeza kwa njia ya haki na kwa njia ya uadilifu, kuanzia sasa na kuendelea mpaka wakati usio na kipimo. Bidii ya Yehova wa majeshi itafanya hayo.” Je, unaweza kujiona mwenyewe ukiishi chini ya utawala huo wa haki?

15. Yehova atawafanyia wanadamu nini katika ulimwengu mpya?

15 Katika ulimwengu mpya wa Mungu, hatutakuwa tena na sababu ya kusema maneno yaliyo katika Mhubiri 4:1: “Nikarudi nipate kuona matendo yote ya uonevu yanayofanywa chini ya jua, na, tazama! machozi ya wale wanaokandamizwa, lakini hawakuwa na mtu wa kuwafariji; nao wakandamizaji walikuwa na nguvu, hivi kwamba hawakuwa na mtu wa kuwafariji.” Ni kweli kwamba kwa sababu ya akili zetu zisizo kamilifu, ni vigumu kuwazia hasa jinsi ulimwengu huo mpya wenye uadilifu utakavyokuwa mzuri ajabu. Mabaya hayatakuwepo tena; badala yake kila siku itajawa na mambo mazuri. Ndiyo, Yehova atarekebisha kila kitu ambacho si sawa, naye atafanya hivyo kwa njia inayopita kabisa matazamio yetu. Inafaa kama nini kwamba Yehova Mungu alimwongoza kwa roho mtume Petro kuandika hivi: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa”!—2 Petro 3:13.

16. “Mbingu mpya” zimesimamishwa jinsi gani, na ni katika maana gani “dunia mpya” inatayarishwa leo?

16 Kwa kweli, hizo “mbingu mpya,” yaani, serikali ya kimbingu ya Mungu mikononi mwa Kristo, tayari imesimamishwa. Wale ambao watakuwa msingi wa “dunia mpya,” ambayo ni jamii mpya ya kidunia ya wanadamu wenye mwelekeo unaofaa, wanakusanywa katika siku hizi za mwisho. Tayari idadi yao inakaribia milioni saba, katika nchi 235 hivi na katika makutaniko 100,000 hivi. Mamilioni hao wamekuwa wakijifunza njia za uadilifu na za haki za Yehova, na kwa sababu hiyo, wana umoja unaotegemea upendo wa Kikristo ulimwenguni pote. Umoja wao unaonekana zaidi na ni wenye kudumu katika historia ya ulimwengu. Unazidi chochote kile ambacho watu wa Shetani wamepata kufanya. Upendo na umoja kama huo unaonyesha kimbele wakati ujao ulio mzuri ajabu katika ulimwengu mpya wa Mungu ambao utaongozwa kwa uadilifu na haki.—Isaya 2:2-4; Yohana 13:34, 35; Wakolosai 3:14.

Shambulio la Shetani Halitafanikiwa

17. Kwa nini ni hakika kwamba shambulio la mwisho la Shetani juu ya watu wa Yehova halitafanikiwa?

17 Hivi karibuni Shetani na wafuasi wake watawashambulia waabudu wa Yehova na kujaribu kuwaharibu. (Ezekieli 38:14-23) Hiyo itakuwa sehemu ya kile ambacho Yesu aliita “dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.” (Mathayo 24:21) Je, shambulio la Shetani litafanikiwa? Hapana. Neno la Mungu linatuhakikishia hivi: “Yehova ni mpenda-haki, naye hatawaacha washikamanifu wake. Hakika watalindwa mpaka wakati usio na kipimo; lakini wazao wa waovu, hakika watakatiliwa mbali. Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:28, 29.

18. (a) Mungu atachukua hatua gani Shetani atakapowashambulia watu Wake? (b) Umefaidika kwa njia gani kwa kuchunguza tena habari hii inayotegemea Biblia kuhusu ushindi wa haki?

18 Shambulio hilo la Shetani na jeshi lake juu ya watu wa Yehova litakuwa ndilo tendo lao la mwisho lenye kuchukiza. Yehova alitabiri hivi kupitia Zekaria: “Yeye anayewagusa ninyi anaigusa mboni ya jicho langu.” (Zekaria 2:8) Ni kana kwamba mtu fulani anadunga mboni ya jicho la Yehova kwa kidole. Yehova atachukua hatua haraka na kuwaondoa kabisa wakosaji hao. Watumishi wa Yehova ni watu wenye upendo, umoja, amani, na wenye kutii sheria zaidi duniani. Kwa hiyo, shambulio hilo juu yao litakuwa lisilostahiliwa na lisilo la haki. “Mpenda-haki” mkuu hatavumilia jambo hilo. Hatua ambayo Mungu atachukua kwa ajili ya watu wake itakuwa na matokeo yafuatayo: Kuharibiwa milele kwa maadui wao, ushindi wa haki, na wokovu wa wale wanaomwabudu Mungu wa pekee wa kweli. Matukio hayo yaliyo mbele yetu ni yenye kustaajabisha na kusisimua kama nini!—Methali 2:21, 22.

Ungetoa Jibu Gani?

• Kwa nini ukosefu wa haki umeenea?

• Yehova atatatua tatizo la ukosefu wa haki duniani jinsi gani?

• Ni nini kimekuvutia katika funzo hili kuhusu ushindi wa haki?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Ubaya ulikuwa mwingi kabla ya Gharika, na ni mwingi pia katika ‘siku hizi za mwisho’

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Katika ulimwengu mpya wa Mungu, kutakuwa na haki na uadilifu badala ya uovu