Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Bado “Agano la Kale” Linafaa?

Je, Bado “Agano la Kale” Linafaa?

Je, Bado “Agano la Kale” Linafaa?

MWAKA wa 1786, daktari mmoja Mfaransa alichapisha kitabu kinachoitwa Mazungumzo Kuhusu Viungo na Fisiolojia (Traité d’anatomie et de physiologie). Wakati huo kitabu hicho kilionwa kuwa kitabu sahihi zaidi kuhusu neva, na hivi majuzi nakala moja kati ya nakala chache zilizopo za kitabu hicho iliuzwa kwa zaidi ya dola 27,000! Hata hivyo, wagonjwa wengi hawawezi kumtumaini daktari anayetegemea utafiti wa kitiba uliofanywa karne zilizopita ulio katika kitabu hicho. Ingawa ni chenye thamani ya kihistoria na ya kimaandishi, kitabu hicho hakiwezi kumsaidia mgonjwa leo.

Wengi wanahisi vivyo hivyo kuhusu kitabu kinachoitwa Agano la Kale. Wanathamini masimulizi yake ya historia ya Waisraeli na wanavutiwa na mashairi yake mazuri. Hata hivyo, hawaoni kuwa ni jambo la hekima kufuata mwongozo uliotolewa miaka zaidi ya 2,400 iliyopita. Ujuzi wa kisayansi, biashara, na hata maisha ya familia leo yanatofautiana sana na jinsi ilivyokuwa wakati Biblia ilipoandikwa. Philip Yancey, aliyekuwa msimamizi wa maandishi wa gazeti moja (Christianity Today), aliandika hivi katika kitabu chake (The Bible Jesus Read): “Kitabu hicho hakipatani na akili kila mara, na kinapopatana na akili kinawaudhi watu wa leo. Kwa sababu hiyo na nyinginezo, mara nyingi watu hawasomi Agano la Kale ambalo ni robo tatu ya Biblia.” Maoni hayo si mapya.

Miaka isiyozidi 50 baada ya kifo cha mtume Yohana kilichotokea mwaka wa 100 W.K., kijana tajiri aliyeitwa Marcion alidai waziwazi kwamba Wakristo wanapaswa kukataa Agano la Kale. Kulingana na mwanahistoria Mwingereza, Robin Lane Fox, Marcion alisema kwamba “‘Mungu’ katika Agano la Kale alikuwa ‘mkatili kabisa’ naye aliwapendelea waporaji na magaidi kama vile Mfalme Daudi wa Israeli. Kinyume naye, Kristo alifunua Mungu mpya aliyekuwa tofauti na bora zaidi.” Fox anaandika kwamba maoni hayo “yakawa ‘Imani ya Marcioni,’ nayo iliendelea kuwavutia watu mpaka kufikia karne ya nne, hasa katika maeneo ya Mashariki ambako watu walizungumza Kisiria.” Watu fulani bado wanafuata imani hiyo. Kwa sababu hiyo, miaka zaidi ya 1,600 baadaye, anaandika Philip Yancey, “ujuzi wa Agano la Kale unadidimia haraka kati ya Wakristo nao unaelekea kutoweka kabisa katika jamii ya leo.”

Je, agano lingine limechukua mahali pa Agano la Kale? Tunaweza kupatanisha jinsi gani ujuzi wetu kuhusu “Yehova wa majeshi” katika Agano la Kale na “Mungu wa upendo na amani” katika Agano Jipya? (Isaya 13:13; 2 Wakorintho 13:11) Je, Agano la Kale linaweza kukufaidi leo?