Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazazi—Wazoezeni Watoto Wenu Kwa Upendo

Wazazi—Wazoezeni Watoto Wenu Kwa Upendo

Wazazi—Wazoezeni Watoto Wenu Kwa Upendo

“Mambo yenu yote na yatendeke kwa upendo.”—1 WAKORINTHO 16:14.

1. Wazazi wanahisi namna gani wanapomzaa mtoto?

WAZAZI wengi wanakubali kwamba kumzaa mtoto kunaweza kuwa moja ya mambo yenye kufurahisha sana maishani. Mama mmoja anayeitwa Aleah anasema hivi: “Nilifurahi sana nilipomtazama kwa mara ya kwanza binti yangu mchanga. Sijawahi kamwe kuona mtoto mrembo kama huyo.” Hata hivyo, jambo kama hilo lenye kufurahisha linaweza pia kuwaletea wazazi mahangaiko. Mume wa Aleah anasema: “Jambo ambalo lilinihangaisha ni ikiwa ningeweza kumzoeza inavyofaa binti yangu ili apambane kwa mafanikio na matatizo ya maisha.” Wazazi wengi wana mahangaiko kama hayo na wanatambua uhitaji wa kuwazoeza watoto wao kwa upendo. Lakini, wazazi Wakristo ambao wanatamani kuwazoeza watoto wao kwa upendo wanakabili magumu. Magumu gani?

2. Wazazi wanakabili magumu gani?

Sasa tunaishi siku za mwisho kabisa za mfumo huu. Kama ilivyotabiriwa, watu wengi ulimwenguni hawaonyeshi upendo. Hata katika familia, watu ‘hawana upendo wa asili,’ na wamekuwa “wasio na shukrani, wasio washikamanifu, . . . wasiojizuia, wakali.” (2 Timotheo 3:1-5) Kushughulika kila siku na watu wenye sifa hizo mbaya kunaweza kuwa na matokeo mabaya juu ya namna washiriki wa familia za Kikristo wanavyotendeana. Kwa kuongezea, wazazi wanapambana na mielekeo waliyorithi ya kutojizuia, kusema mambo bila kufikiri, na kufanya maamuzi yasiyo ya busara katika mambo mengine.—Waroma 3:23; Yakobo 3:2, 8, 9.

3. Wazazi wanaweza jinsi gani kulea watoto wenye furaha?

3 Hata ingawa kuna magumu hayo, wazazi wanaweza kulea watoto wenye furaha ambao wanampenda Mungu. Jinsi gani? Kwa kufuata shauri hili la Biblia: “Mambo yenu yote na yatendeke kwa upendo.” (1 Wakorintho 16:14) Kwa kweli, upendo ni “kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Na tuchunguze sifa tatu za upendo ambazo zinaelezwa na mtume Paulo katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho na tuzungumzie njia fulani hususa ambazo wazazi wanaweza kuonyesha sifa hizo wanapowazoeza watoto wao.—1 Wakorintho 13:4-8.

Uhitaji wa Ustahimilivu

4. Kwa nini wazazi wanahitaji kuwa wastahimilivu?

4 Paulo aliandika hivi: “Upendo ni wenye ustahimilivu.” (1 Wakorintho 13:4) Neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “ustahimilivu” linamaanisha kuwa na subira na kutokasirika haraka. Kwa nini wazazi wanahitaji kuwa wastahimilivu? Bila shaka, wazazi wengi wanaweza kufikiria sababu nyingi za kuwa wastahimilivu. Fikiria sababu chache tu. Kwa kawaida, watoto wanaomba tena na tena kitu fulani wanachotaka. Hata ikiwa mzazi anakataa kwa uthabiti, huenda mtoto akaendelea kuomba tena na tena akitumaini kwamba mzazi atakubali. Huenda vijana wakabishana kwa muda mrefu na wazazi ili waruhusiwe kufanya jambo fulani ambalo wazazi wanajua ni la ujinga. (Methali 22:15) Na kama sisi sote, watoto wana mwelekeo wa kurudia-rudia makosa fulani.—Zaburi 130:3.

5. Ni nini kinachoweza kuwasaidia wazazi kuwa wastahimilivu?

5 Ni nini kinachoweza kuwasaidia wazazi wawe wastahimilivu na wenye subira kwa watoto wao? Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake.” (Methali 19:11) Wazazi wanaweza kuelewa tabia za watoto wao wakikumbuka kwamba wakati fulani wao pia ‘walikuwa wakisema kama watoto, wakifikiri kama watoto, wakiwaza kama watoto.’ (1 Wakorintho 13:11) Wazazi, je, mnaweza kukumbuka jinsi mlivyowasumbua mama au baba zenu ili wakubali ombi lenu la kitoto? Mkiwa vijana, je, mlifikiri kwamba wazazi wenu hawakuelewa kamwe matatizo yenu au jinsi mlivyohisi? Ikiwa ndivyo, inaelekea kwamba mnaelewa kwa nini watoto wenu wanajiendesha kwa njia hiyo na kwa nini mnahitaji kuendelea kuwakumbusha maamuzi yenu kwa subira. (Wakolosai 4:6) Ni vizuri kukumbuka kwamba Yehova aliwaambia wazazi Waisraeli ‘wakazie’ sheria zake katika mioyo ya watoto wao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘kazia’ linamaanisha “kurudia” “kusema tena na tena,” “kusisitiza.” Hilo linamaanisha kwamba huenda wazazi wakahitaji kurudia-rudia jambo lilelile mara nyingi kabla mtoto hajajifunza kufuata sheria za Mungu. Mara nyingi wanahitaji kurudia-rudia ili kuwafundisha watoto mambo mengine maishani.

6. Kwa nini mzazi mstahimilivu si mzazi anayewaachilia watoto wafanye wanavyotaka?

6 Hata hivyo, mzazi mstahimilivu si mzazi anayewaachilia watoto wafanye wanavyotaka. Neno la Mungu linaonya hivi: “Mvulana aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.” Ili kuepuka matokeo kama hayo, methali hiyohiyo inasema hivi: “Fimbo na karipio ndivyo hutia hekima.” (Methali 29:15) Nyakati nyingine, huenda watoto wakafikiri kwamba wazazi hawana haki ya kuwakaripia. Lakini familia za Kikristo hazifuati mfumo wa demokrasia, kana kwamba watoto ndio wanaoamua ikiwa wazazi wana haki ya kuwawekea sheria. Badala yake, Yehova, akiwa Kichwa juu ya familia, anawapa wazazi mamlaka ya kuwazoeza na kuwatia nidhamu watoto wao kwa upendo. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 3:15; 6:1-4) Kwa kweli, nidhamu inahusiana sana na sifa ya pili ya upendo ambayo inatajwa na Paulo.

Jinsi ya Kutia Nidhamu kwa Upendo

7. Kwa nini wazazi wenye fadhili wanawatia nidhamu watoto wao, na nidhamu hiyo inatia ndani nini?

7 Paulo aliandika kwamba “upendo ni . . . wenye fadhili.” (1 Wakorintho 13:4) Wazazi ambao kwa kweli ni wenye fadhili watawatia watoto wao nidhamu kila mara inapohitajiwa. Wanapofanya hivyo, wanamwiga Yehova. Paulo aliandika hivi: “Yeye ambaye Yehova anampenda, humtia nidhamu.” Tafadhali ona kwamba nidhamu inayotajwa katika Biblia haimaanishi kutoa adhabu tu. Inamaanisha kuzoeza na kuelimisha. Nidhamu hiyo inatolewa kwa kusudi gani? Paulo anasema: “Kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo huzaa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” (Waebrania 12:6, 11) Wazazi wanapowaelimisha kwa fadhili watoto wao kupatana na mapenzi ya Mungu, wanawasaidia kuwa watu wazima wanyoofu na wenye kufanya amani. Watoto wakikubali “nidhamu ya Yehova,” wanapata hekima, ujuzi, na utambuzi, sifa zenye thamani sana kuliko fedha au dhahabu.—Methali 3:11-18.

8. Kwa kawaida matokeo yanakuwa nini wazazi wanapokosa kuwatia nidhamu watoto wao?

8 Kwa upande mwingine, wazazi hawaonyeshi fadhili wanapokosa kuwatia nidhamu watoto wao. Yehova alimwongoza Sulemani kwa roho kuandika hivi: “Anayezuia fimbo yake anamchukia mwana wake, lakini anayempenda ni yule anayemwangalia kwa nidhamu.” (Methali 13:24) Inaelekea kwamba watoto wanaolelewa bila kutiwa nidhamu ipasavyo watakuwa wachoyo na hawatakuwa na furaha. Kwa upande mwingine, watoto ambao wana wazazi wenye huruma lakini wanaoshikilia kwa uthabiti mipaka waliyoweka wanafanya vizuri shuleni, wanashirikiana vizuri na wengine, na kwa ujumla wanakuwa wenye furaha. Bila shaka, wazazi wanaowatia nidhamu watoto wao wanawatendea kwa fadhili.

9. Wazazi Wakristo wanawafundisha watoto wao nini, na matakwa hayo yanapaswa kuonwa jinsi gani?

9 Kuwatia nidhamu watoto kwa fadhili na upendo kunatia ndani nini? Wazazi wanahitaji kuzungumza pamoja na watoto wao mambo hususa wanayotaka wafanye. Kwa mfano, wazazi Wakristo wanawafundisha watoto wao tangu wakiwa wachanga kanuni za msingi za Biblia na vilevile uhitaji wa kushiriki katika utendaji mbalimbali wa ibada ya kweli. (Kutoka 20:12-17; Mathayo 22:37-40; 28:19; Waebrania 10:24, 25) Watoto wanahitaji kujua kwamba matakwa hayo hayabadiliki kamwe.

10, 11. Kwa nini wazazi wanaweza kutilia maanani mapendezi ya watoto wao wanapoweka sheria za nyumbani?

10 Hata hivyo, nyakati nyingine huenda wazazi wakataka kuzungumza na watoto wao wanapoweka sheria za nyumbani. Ikiwa vijana wanaweza kushiriki katika mazungumzo ya kuweka sheria hizo, inaelekea sana kwamba watazitii. Kwa mfano, wazazi wakiamua kuweka wakati wa kurudi nyumbani, wanaweza kuchagua saa fulani hususa ambayo watoto wanapaswa kuwa nyumbani. Au badala yake, wanaweza kuwaruhusu watoto wao wapendekeze saa ya kurudi nyumbani na waeleze sababu za uchaguzi wao. Kisha wazazi wanaweza kutaja saa ambayo wanapendelea na kueleza kwa nini wanaona kwamba inafaa. Ikiwa maoni yao yanatofautiana na ya watoto, na inaelekea yatatofautiana, watafanya nini? Nyakati nyingine, wazazi wanaweza kuamua kukubali maoni ya watoto wao ikiwa hayavunji kanuni za Biblia. Je, hilo linamaanisha kwamba wazazi wanawaachia watoto madaraka yao au kuyapuuza?

11 Ili kujibu swali hilo, fikiria jinsi Yehova alivyotumia mamlaka yake kwa upendo aliposhughulika na Loti na familia yake. Baada ya kumsindikiza Loti, mke wake, na mabinti wake kutoka Sodoma, malaika hao walimwambia: “Kimbilia eneo lenye milima usije ukafagiliwa mbali!” Hata hivyo, Loti alijibu hivi: “Sivyo, tafadhali, Yehova!” Kisha Loti akapendekeza jambo tofauti: “Tafadhali, sasa, jiji hili liko karibu kuweza kukimbiliwa nalo ni dogo. Tafadhali, acha nikimbilie huko.” Yehova alimwambia nini? “Haya, nakujali kwa kadiri hii pia,” akasema. (Mwanzo 19:17-22) Je, Yehova aliachilia mamlaka yake? Bila shaka hapana! Hata hivyo, alitilia maanani ombi la Loti na kuamua kumwonyesha fadhili ya pekee kuhusiana na jambo hilo. Ikiwa wewe ni mzazi, je, kuna nyakati fulani ambapo unaweza kutilia maanani mapendezi ya watoto wako unapoweka sheria za familia?

12. Ni nini kinachoweza kumfanya mtoto ajihisi akiwa salama?

12 Bila shaka, watoto hawapaswi kujua tu sheria hizo bali pia adhabu ya kuzivunja. Baada ya kuzungumzia na kuelewa adhabu itakayotolewa, sheria hizo zinapaswa kutekelezwa. Wazazi hawaonyeshi fadhili wanapowaonya kila mara watoto wao kwamba watawaadhibu lakini wanakosa kuwaadhibu. Biblia inasema: “Kwa maana hukumu juu ya kazi mbaya haikutekelezwa upesi, ndiyo sababu moyo wa wana wa binadamu umeazimia kabisa ndani yao kutenda yaliyo mabaya.” (Mhubiri 8:11) Ni kweli kwamba mzazi anaweza kuamua kutomwadhibu mtoto mbele ya watu au mbele ya watoto wenzake, ili asimwaibishe. Lakini watoto wanahisi wakiwa salama zaidi na wanawaheshimu na kuwapenda zaidi wazazi wao wanapojua kwamba wazazi wao wanaposema “Ndiyo” wanamaanisha ndiyo na wanaposema “Siyo” wanamaanisha siyo, hata ikiwa inamaanisha kutiwa nidhamu.—Mathayo 5:37.

13, 14. Wazazi wanaweza kumwiga Yehova jinsi gani wanapowazoeza watoto wao?

13 Ili adhabu iwe yenye fadhili, ni lazima adhabu yenyewe na njia ya kuitoa ilingane na mahitaji ya mtoto. Pam anakumbuka hivi: “Watoto wetu wawili walihitaji kutiwa nidhamu kwa njia tofauti. Nidhamu iliyokuwa na matokeo kwa mtoto mmoja haikuwa na matokeo kwa yule mwingine.” Larry, mume wake anaeleza: “Binti yetu mkubwa alikuwa mgumu na alibadilika tu tulipomwadhibu kwa ukali. Lakini, binti yetu mdogo alibadilika haraka tuliposema kwa uthabiti na hata kwa kumtazama kwa ukali.” Kwa kweli, wazazi wenye fadhili wanajitahidi kutambua aina ya nidhamu ambayo inamfaa zaidi kila mmoja wa watoto wao.

14 Yehova anawawekea wazazi mfano kwa sababu anajua sifa nzuri na udhaifu wa kila mmoja wa watumishi wake. (Waebrania 4:13) Kwa kuongezea, anapowaadhibu, Yehova si mkali kupita kiasi wala hawaendekezi watumishi wake kupita kiasi. Badala yake, sikuzote anawatia nidhamu watu wake “kwa kiwango kinachofaa.” (Yeremia 30:11) Wazazi, je, mnajua sifa nzuri na udhaifu wa watoto wenu? Je, mnaweza kutumia ujuzi huo kwa njia inayofaa ili kuwazoeza kwa fadhili? Ikiwa ndivyo, mnathibitisha kwamba mnawapenda watoto wenu.

Watie Moyo Wazungumze kwa Unyoofu

15, 16. Wazazi wanaweza jinsi gani kuwatia moyo watoto wazungumze kwa unyoofu, na wazazi fulani Wakristo wamefanikiwa kwa kutumia njia gani?

15 Pia, upendo “haushangilii juu ya ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli.” (1 Wakorintho 13:6) Wazazi wanaweza kuwazoeza jinsi gani watoto wao ili wapende yaliyo sawa na yaliyo kweli? Hatua muhimu ni kuwatia moyo watoto waeleze maoni yao kwa unyoofu, hata ikiwa ni vigumu kwa wazazi kuyakubali. Kwa kweli, wazazi wanafurahi wakati watoto wanapoeleza mawazo na hisia zao kupatana na viwango vya uadilifu. Lakini nyakati nyingine mtoto anaweza kusema kutoka moyoni mambo ambayo yanaonyesha mwelekeo wa kutofuatia uadilifu. (Mwanzo 8:21) Wazazi wanapaswa kufanya nini? Huenda wakakimbilia kuwatia nidhamu watoto wao kwa sababu ya kusema mambo hayo. Wazazi wakifanya hivyo, baada ya muda watoto wanaweza kuanza kusema tu mambo ambayo wanafikiri wazazi wanataka kusikia. Bila shaka, wazazi wanapaswa kuwarekebisha upesi ikiwa wanazungumza bila heshima, lakini kuna tofauti kati ya kuwafundisha watoto jinsi ya kuongea kwa upole na kuwaambia mambo ambayo wanapaswa kusema.

16 Wazazi wanaweza jinsi gani kusitawisha mawasiliano mazuri? Aleah, ambaye alitajwa mapema, anasema hivi: “Tunajizuia kukasirika wakati watoto wetu wanapotuambia mambo ambayo yanaudhi na hivyo tunawasiliana kwa unyoofu.” Baba mmoja ambaye anaitwa Tom anasema: “Tulimtia moyo binti yetu kutuambia maoni yake, hata wakati ambapo hakukubaliana na maoni yetu. Tuliona kwamba sikuzote tukimzuia kuongea na kumlazimisha kufuata maoni yetu, angevunjika moyo na angeamua kutosema mambo yaliyo moyoni mwake. Kwa upande mwingine, kumsikiliza kulimtia moyo atusikilize.” Bila shaka, watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao. (Methali 6:20) Lakini mawasiliano ya wazi yanawapa wazazi nafasi ya kuwasaidia watoto wao kukuza uwezo wa kufikiri. Vincent, ambaye ni baba mwenye watoto wanne, anasema hivi: “Kwa kawaida, tulizungumza sana kuhusu faida na hasara za jambo fulani ili watoto wetu waweze kujionea wenyewe matokeo ambayo ni bora. Kufanya hivyo kuliwasaidia kukuza uwezo wa kufikiri.”—Methali 1:1-4.

17. Wazazi wanaweza kuwa na uhakika gani?

17 Bila shaka, hakuna mzazi ambaye anaweza kutumia kikamilifu mashauri ya Biblia kuhusu kuwalea watoto. Hata hivyo, unaweza kuwa na hakika kwamba watoto wako watathamini sana bidii yako ya kuwazoeza kwa ustahimilivu, kwa fadhili, na kwa upendo. Bila shaka, Yehova atabariki jitihada zako za kufanya hivyo. (Methali 3:33) Kwa kweli, wazazi wote Wakristo wanataka watoto wao wajifunze kumpenda Yehova kama wao wanavyompenda. Wazazi wanaweza kutimiza jinsi gani mradi huo mzuri? Habari inayofuata itazungumzia njia fulani hususa.

Je, Unakumbuka?

• Busara inaweza kumsaidia namna gani mzazi awe mstahimilivu?

• Kuna uhusiano gani kati ya fadhili na nidhamu?

• Kwa nini mawasiliano ya unyoofu kati ya wazazi na watoto ni ya maana?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wazazi, je, mnakumbuka mlivyokuwa mlipokuwa watoto?

[Picha katika ukurasa wa 24]

Je, unawatia moyo watoto wako wazungumze nawe kwa unyoofu na waziwazi?