Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafundishe Watoto Wako Kumpenda Yehova

Wafundishe Watoto Wako Kumpenda Yehova

Wafundishe Watoto Wako Kumpenda Yehova

“Kama mishale mkononi mwa mwanamume mwenye nguvu, ndivyo walivyo wana wa ujanani.”—ZABURI 127:4.

1, 2. Watoto ni kama “mishale mkononi mwa mwanamume mwenye nguvu” jinsi gani?

MPIGA-MISHALE anajitayarisha kupiga shabaha. Anautia mshale kwa uangalifu kwenye upinde, kisha anavuta upinde kwa nguvu. Ingawa anatumia nguvu, anachukua wakati kulenga mshale. Kisha anauachilia mshale huo! Je, utapiga shabaha? Jibu linategemea mambo fulani, kama vile ustadi wa yule mpiga-mishale, msukumo wa upepo, na hali ya mshale.

2 Mfalme Sulemani aliwalinganisha watoto na “mishale mkononi mwa mwanamume mwenye nguvu.” (Zaburi 127:4) Fikiria jinsi mfano huo unavyoweza kutumiwa. Mpiga-mishale anatia mshale kwenye upinde kwa muda mfupi tu. Ili upige shabaha, ni lazima auachilie haraka. Vivyo hivyo, wazazi wana muda mfupi tu wa kuwasaidia watoto wao kumpenda Yehova kutoka moyoni. Baada ya miaka michache tu, watoto wanakua na kuondoka nyumbani. (Mathayo 19:5) Je, watoto watafikia shabaha, yaani, wataendelea kumpenda na kumtumikia Mungu baada ya kuondoka nyumbani? Matokeo yanategemea mambo mengi. Mambo matatu kati ya hayo ni ustadi wa mzazi, mazingira ambamo mtoto analelewa, na jinsi ‘mshale,’ au mtoto anavyofuata mazoezi ambayo anapokea. Acheni tuchunguze kila moja ya mambo hayo kwa undani zaidi. Kwanza, tutazungumzia sifa fulani za mzazi mwenye ustadi.

Wazazi Wenye Ustadi Wanaweka Mfano Mzuri

3. Kwa nini ni lazima maneno ya mzazi yaambatane na matendo?

3 Yesu aliwawekea wazazi mfano kwa sababu alitenda kupatana na mambo aliyohubiri. (Yohana 13:15) Kwa upande mwingine, aliwashutumu Mafarisayo ambao walikuwa ‘wakisema’ lakini ‘hawakutenda.’ (Mathayo 23:3) Ili kuwachochea watoto wao wampende Yehova, ni lazima maneno ya wazazi yaambatane na matendo. Maneno bila matendo ni bure tu kama upinde bila kamba ya upinde.—1 Yohana 3:18.

4. Wazazi wanapaswa kujiuliza maswali gani, na kwa nini?

4 Kwa nini mfano wa wazazi ni wa maana sana? Kama vile tu watu wazima wanavyoweza kujifunza kumpenda Mungu kwa kutazama mfano wa Yesu, ndivyo watoto wanavyoweza kujifunza kumpenda Yehova kwa kufuata mfano mzuri wa wazazi wao. Mashirika ya mtoto yanaweza kumsaidia au ‘kuharibu tabia yake nzuri.’ (1 Wakorintho 15:33) Watu ambao mtoto anashirikiana nao kwa ukaribu zaidi kwa miaka mingi, na hasa miaka muhimu sana ya maisha yake, ni wazazi wake. Wanakuwa na uvutano mkubwa kwa mtoto. Kwa hiyo, wazazi wanapaswa kujiuliza: ‘Mimi ni mshirika wa aina gani? Je, mfano wangu unamtia moyo mtoto wangu asitawishe tabia nzuri? Ninaweka mfano wa aina gani katika mambo ya maana kama vile sala na funzo la Biblia?’

Wazazi Wenye Ustadi Wanasali Pamoja na Watoto Wao

5. Watoto wanaweza kujifunza nini kutokana na sala za mzazi?

5 Watoto wako wanaweza kujifunza mengi kumhusu Yehova kwa kusikiliza sala zako. Wakikusikia ukimshukuru Mungu wakati wa chakula na kusali wakati wa funzo la Biblia, wanaweza kukata kauli gani? Inaelekea kuwa watajifunza kwamba Yehova anatutimizia mahitaji yetu ya kimwili, na hivyo tunapaswa kumshukuru, na watajifunza pia kwamba anatufundisha kweli za kiroho. Hayo ni masomo ya maana sana.—Yakobo 1:17.

6. Wazazi wanaweza kuwasaidia jinsi gani watoto waone kwamba Yehova anapendezwa kibinafsi na kila mmoja wao?

6 Hata hivyo, ukisali pamoja na familia yako katika pindi nyingine si tu wakati wa chakula na wa funzo la Biblia la familia, na ukizungumzia mambo hususa ambayo yanakusumbua wewe na watoto wako, utakuwa na matokeo zaidi. Utawasaidia watoto wako wahisi kwamba Yehova ni sehemu ya familia yenu, na kwamba anakujali wewe sana kibinafsi. (Waefeso 6:18; 1 Petro 5:6, 7) Baba mmoja anasema: “Tangu binti yetu alipozaliwa, tulisali pamoja naye. Alipoendelea kukua, tulisali kuhusu mahusiano na mambo mengine ambayo yalimhusu. Hatukukosa kamwe kusali pamoja naye hata siku moja, mpaka alipoolewa na kuondoka nyumbani.” Je, unaweza pia kusali pamoja na watoto wako kila siku? Je, unaweza kuwasaidia wamwone Yehova kuwa Rafiki ambaye anatimiza mahitaji yao ya kimwili na ya kiroho na vilevile anayejali mahitaji yao ya kihisia?—Wafilipi 4:6, 7.

7. Wazazi wanahitaji kujua nini ili kutoa sala hususa?

7 Bila shaka, ili utoe sala hususa, unahitaji kujua mambo ambayo yanampata mtoto wako maishani. Ona maelezo ya baba mmoja ambaye alilea watoto wawili: “Mwishoni mwa kila juma, nilikuwa nikijiuliza maswali mawili: ‘Watoto wangu walihangaishwa na mambo gani juma hili? Na ni mambo gani mazuri yaliyotukia katika maisha yao ya kila siku?’” Wazazi, je, mnaweza kujiuliza maswali kama hayo na kisha mtaje baadhi ya mambo hayo katika sala mnazotoa pamoja na watoto wenu? Mkifanya hivyo, hamtakuwa tu mkiwafundisha kusali kwa Yehova, yule Msikiaji wa sala, bali pia mtakuwa mkiwafundisha kumpenda.—Zaburi 65:2.

Wazazi Wenye Ustadi Wanawasaidia Watoto Kusitawisha Mazoea Mazuri ya Kujifunza

8. Kwa nini ni lazima wazazi wawasaidie watoto wao kusitawisha mazoea ya kujifunza Neno la Mungu?

8 Mtazamo wa mzazi kuhusu funzo la Biblia unaweza kuwa na matokeo gani katika uhusiano wa mtoto pamoja na Mungu? Ili mtu awe na uhusiano wowote ule na kuudumisha, hapaswi tu kuzungumza bali pia kumsikiliza mwenzake akizungumza. Njia moja ya kumsikiliza Yehova ni kujifunza Biblia kwa kutumia vichapo vinavyotayarishwa na “mtumwa mwaminifu.” (Mathayo 24:45-47; Methali 4:1, 2) Kwa hiyo, ili kuwasaidia watoto wao wasitawishe uhusiano wa kudumu na wenye upendo pamoja na Yehova, wazazi wanapaswa kuwatia moyo watoto wawe na mazoea ya kujifunza Neno la Mungu.

9. Watoto wanaweza kusaidiwa jinsi gani wasitawishe mazoea mazuri ya kujifunza?

9 Watoto wanaweza kusaidiwa jinsi gani kusitawisha mazoea mazuri ya kujifunza? Katika jambo hili pia, njia bora ambayo mzazi anaweza kutumia ni kuwawekea mfano. Je, watoto wako wanakuona kwa ukawaida ukisoma au ukijifunza Biblia kibinafsi? Ni kweli kwamba huenda unajishughulisha sana kuwatunza watoto wako, na labda unajiuliza utapata wapi wakati wa kusoma na kujifunza. Lakini jiulize, ‘Je, kwa kawaida watoto wangu wananiona nikitazama televisheni?’ Ikiwa ndivyo ilivyo, je, unaweza kutumia sehemu fulani ya wakati huo kuwawekea mfano mzuri kuhusu funzo la kibinafsi?

10, 11. Kwa nini wazazi wanapaswa kuwa na mazungumzo ya Biblia ya kawaida ya familia?

10 Njia nyingine nzuri ambayo mzazi anaweza kuwafundisha watoto kumsikiliza Yehova ni kwa kuwa na mazungumzo ya Biblia ya familia kwa ukawaida. (Isaya 30:21) Hata hivyo, huenda watu wengine wakauliza, ‘Kwa nini watoto wanahitaji funzo la familia ikiwa wazazi wao wanaenda nao kwa ukawaida kwenye mikutano ya kutaniko?’ Kuna sababu fulani nzuri. Yehova anawapa wazazi daraka mkubwa zaidi wa kuwafundisha watoto wao. (Methali 1:8; Waefeso 6:4) Kuwa na funzo la Biblia la familia kunawafundisha watoto kwamba ibada si jambo la kidesturi tu linalofanywa mbele ya watu, lakini ni sehemu ya maisha ya faraghani ya familia.—Kumbukumbu la Torati 6:6-9.

11 Kwa kuongezea, funzo la familia linaloongozwa vizuri linaweza kuwasaidia wazazi kuelewa jinsi watoto wanavyoona mambo ya kiroho na ya kimaadili. Kwa mfano, watoto wanapokuwa wachanga, wazazi wanaweza kutumia vitabu kama vile Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. * Katika karibu kila fungu la kitabu hicho cha kujifunzia Biblia, watoto wanaombwa watoe maoni yao kuhusu jambo linalozungumziwa. Wazazi wakijadiliana na watoto wakitumia maandiko yaliyotajwa katika kitabu hicho, wanaweza kuwasaidia kusitawisha nguvu zao za ufahamu ili “kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.”—Waebrania 5:14.

12. Wazazi wanaweza kubadili jinsi gani funzo la familia kupatana na mahitaji ya mtoto, na ni njia gani ambayo umeona kuwa ina matokeo?

12 Kadiri watoto wanavyokua, badili funzo kulingana na mahitaji yao. Ona jinsi wenzi fulani walivyowasaidia wasichana wao matineja kufikiria ombi la kwenda katika dansi fulani shuleni. Baba anasema hivi: “Tuliwaambia watoto wetu kwamba wakati wa funzo letu la familia linalofuata, mimi na mke wangu tutaigiza sehemu ya watoto, na wao watakuwa wazazi. Mmoja wao atakuwa Baba na mwingine Mama, lakini walipaswa kufanya utafiti kuhusu dansi za shule na kuonyesha mwongozo kuhusu jambo hilo.” Matokeo yalikuwa nini? Baba anaendelea kusema: “Tulishangaa jinsi mabinti wetu walivyokuwa wakomavu (wakiwa kama wazazi) walipokuwa wakitueleza (tukiwa kama watoto) sababu zao zinazotegemea Biblia kuonyesha kwa nini halingekuwa jambo la hekima kwenda katika dansi hiyo. Tulivutiwa sana pia tuliposikia mapendekezo yao kuhusu mambo mazuri ya kufanya badala ya dansi hiyo. Walitusaidia kuelewa mambo wanayofikiri na yale wanayotamani.” Ni kweli kwamba wazazi wanahitaji kujitahidi daima na kufikiria sana ili funzo la familia liwe la kawaida na linalofaa mahitaji ya familia, lakini wakifanya hivyo watabarikiwa sana.—Methali 23:15.

Sitawisha Mazingira Yenye Amani

13, 14. (a) Wazazi wanaweza kufanya nini ili mazingira ya nyumbani yawe yenye amani? (b) Kuna faida gani ya mzazi kukubali kwamba amekosea?

13 Inaelekea kwamba mshale utapiga shabaha ikiwa mpiga-mishale anaulenga na kuuachilia katika hali zenye utulivu. Vivyo hivyo, inaelekea kwamba watoto watajifunza kumpenda Yehova ikiwa wazazi watafanya mazingira ya nyumbani yawe yenye amani. “Mbegu ya tunda la uadilifu hupandwa chini ya hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani,” akaandika Yakobo. (Yakobo 3:18) Wazazi wanaweza jinsi gani kufanya mazingira ya nyumbani yawe yenye amani? Wenzi wa ndoa wanahitaji kudumisha kifungo cha ndoa chenye nguvu. Mume na mke ambao wanapendana na kuheshimiana wana nafasi nzuri ya kuwafundisha watoto wao kuwapenda na kuwaheshimu wengine, kutia ndani Yehova. (Wagalatia 6:7; Waefeso 5:33) Upendo na heshima zinaendeleza amani. Na wenzi wa ndoa ambao wana amani kati yao wanaweza kutatua migogoro ambayo inaweza kutokea katika familia.

14 Bila shaka hakuna ndoa kamilifu, vivyo hivyo hakuna familia kamilifu duniani leo. Huenda nyakati nyingine wazazi wakakosa kuonyesha matunda ya roho wanaposhughulika na watoto wao. (Wagalatia 5:22, 23) Wazazi wanapaswa kufanya nini hali inapokuwa hivyo? Je, wakikubali kwamba wamekosea, watapunguza heshima ya mtoto kuwaelekea? Fikiria mfano wa mtume Paulo. Alikuwa kama baba wa kiroho kwa watu wengi. (1 Wakorintho 4:15) Lakini, alikubali waziwazi kwamba alikosea. (Waroma 7:21-25) Hata hivyo, badala ya kupunguza heshima yetu kumwelekea, unyenyekevu na unyoofu wake unatufanya tumheshimu zaidi. Ingawa alikuwa na kasoro, Paulo aliliandikia hivi kutaniko la Korintho akiwa na uhakika: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.” (1 Wakorintho 11:1) Wewe pia ukikubali makosa yako, inaelekea kwamba watoto wako hawatakazia fikira kasoro zako.

15, 16. Kwa nini wazazi wanapaswa kuwazoeza watoto wao kuwapenda ndugu na dada zao Wakristo, na wanaweza kufanya hivyo jinsi gani?

15 Wazazi wanaweza kufanya jambo gani lingine ili kusitawisha mazingira ambayo yatawasaidia watoto wao wampende Yehova zaidi? Mtume Yohana aliandika hivi: “Yeyote akisema: ‘Mimi nampenda Mungu,’ na bado anamchukia ndugu yake, yeye ni mwongo. Kwa maana yeye ambaye hampendi ndugu yake, ambaye amemwona, hawezi kuwa anampenda Mungu, ambaye hajamwona.” (1 Yohana 4:20, 21) Hivyo, unapowazoeza watoto wako kuwapenda ndugu na dada zao Wakristo, unawafundisha kumpenda Mungu. Wazazi wanapaswa kujiuliza, ‘Je, kila mara ninazungumza mambo yenye kutia moyo kuhusu kutaniko au ninalichambua?’ Unaweza kujua hilo jinsi gani? Sikiliza kwa makini jinsi watoto wako wanavyozungumza kuhusu mikutano na washiriki wa kutaniko. Inaelekea kwamba utasikia wakirudia mawazo yako katika mazungumzo yao.

16 Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao wawapende ndugu zao wa kiroho? Peter, ambaye ni baba mwenye wavulana wawili matineja, anasema hivi: “Tangu wavulana wetu walipokuwa wachanga, tumekuwa tukiwaalika kwa ukawaida watu waliokomaa kiroho ili wale chakula pamoja nasi na kututembelea nyumbani mwetu, nasi tumefurahia sana kufanya hivyo. Wavulana wetu wamekua huku wakishirikiana na watu wanaompenda Yehova, na sasa wanaona kwamba kumtumikia Mungu ni njia bora ya maisha.” Dennis, ambaye ni baba mwenye wasichana watano, anasema hivi: “Tuliwatia moyo wasichana wetu wasitawishe urafiki na mapainia wenye umri mkubwa kutanikoni, na ilipowezekana tuliwakaribisha waangalizi wanaosafiri na wake zao.” Je, unaweza pia kuchukua hatua ya kuwasaidia watoto wako kuliona kutaniko kuwa sehemu ya familia yenu?—Marko 10:29, 30.

Wajibu wa Mtoto

17. Mwishowe ni lazima watoto wafanye uamuzi gani?

17 Fikiria tena ule mfano wa mpiga-mishale. Ingawa huenda akawa stadi, inaelekea kwamba hatapiga shabaha ikiwa mshale anaolenga umekunjika au kupindika. Bila shaka, kwa njia ya mfano, wazazi watajaribu sana kuunyoosha mshale uliokunjika kwa kujitahidi kurekebisha mawazo yasiyofaa ya mtoto. Lakini mwishowe ni lazima watoto wajiamulie wenyewe ikiwa wataruhusu ulimwengu huu uwakunje kupatana na mapenzi yake au ikiwa watamruhusu Yehova ‘anyooshe mapito’ yao.—Methali 3:5, 6; Waroma 12:2.

18. Uamuzi wa mtoto unaweza kuwa na matokeo gani kwa wengine?

18 Ingawa wazazi wana daraka zito la kuwalea watoto katika “nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova,” mtoto mwenyewe ndiye atakayeamua atakuwa mtu mzima wa aina gani. (Waefeso 6:4) Kwa hiyo, watoto, jiulizeni hivi: ‘Je, nitakubali mazoezi yenye upendo yanayotolewa na wazazi wangu?’ Ukifanya hivyo, utakuwa ukichagua njia bora zaidi ya maisha. Utawafurahisha sana wazazi wako. Na jambo la maana zaidi ni kwamba utaufanya moyo wa Yehova ushangilie.—Methali 27:11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Wazazi wanaweza jinsi gani kuweka mfano mzuri katika kusali na kujifunza Biblia?

• Wazazi wanaweza kufanya nini ili mazingira ya nyumbani yawe yenye amani?

• Watoto wanapaswa kufanya uamuzi gani, na uamuzi wao utakuwa na matokeo gani kwa wengine?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Je, unamwekea mtoto wako mfano mzuri katika kujifunza kibinafsi?

[Picha katika ukurasa wa 29]

Mazingira yenye amani katika familia yanachangia furaha