Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yesu alimaanisha nini aliposema kwamba mtumwa wake mwaminifu angekuwa “mwenye busara”?

Yesu aliuliza hivi: “Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, awape chakula chao kwa wakati unaofaa?” (Mathayo 24:45) “Mtumwa” anayeandaa “chakula” cha kiroho ni kutaniko la Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho. Kwa nini Yesu aliwaita wenye busara? *

Mafundisho ya Yesu yanaweza kutusaidia kuelewa vizuri kile alichomaanisha aliposema “mwenye busara.” Kwa mfano, alipozungumza kuhusu “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” Yesu alitoa mfano wa mabikira kumi ambao walikuwa wakimngoja bwana-arusi afike. Mabikira hao wanatukumbusha kuhusu Wakristo watiwa-mafuta walioishi kabla ya mwaka wa 1914 ambao walikuwa wakingoja kwa hamu kufika kwa Bwana-arusi mkuu, Yesu Kristo. Mabikira watano kati ya wale kumi, hawakuwa na mafuta ya kutosha wakati bwana-arusi alipofika, na kwa sababu hiyo walikosa kuhudhuria karamu ya arusi. Wale wengine watano walikuwa wenye busara. Walikuwa wamebeba mafuta ya kutosha na hivyo taa zao ziliendelea kuwaka wakati bwana-arusi alipofika, nao wakaruhusiwa kuingia katika karamu hiyo.—Mathayo 25:10-12.

Yesu alipokuja katika mamlaka yake ya Ufalme mwaka wa 1914, wengi kati ya Wakristo watiwa-mafuta walikuwa wakitazamia kujiunga naye mara moja huko mbinguni. Hata hivyo, walikuwa na kazi zaidi ya kufanya duniani, na wengine wao hawakuwa tayari kwa ajili ya kazi hiyo. Kama wale mabikira wasio na busara, Wakristo hao hawakuwa wamejitia nguvu mapema kiroho, na hivyo hawakuwa tayari kuendelea kuangaza nuru. Hata hivyo, Wakristo wengi walikuwa wametenda kwa busara, yaani, kwa hekima na utambuzi, nao walikuwa na nguvu kiroho. Waliposikia kwamba walikuwa na kazi zaidi ya kufanya, walianza kuitimiza kwa shangwe. Kwa hiyo, wakathibitika kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”

Fikiria pia jinsi Yesu alivyotumia maneno “mwenye busara” katika Mathayo 7:24. Yesu alisema hivi: “Kila mtu anayesikia maneno yangu haya na kuyatenda atafananishwa na mtu mwenye busara, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba.” Mtu mwenye busara anajenga nyumba imara akifikiria hatari ya dhoruba. Kwa upande mwingine, mtu mpumbavu anajenga juu ya mchanga na nyumba yake inaporomoka. Hivyo, mfuasi mwenye busara wa Yesu ni yule anayeona mapema matokeo mabaya ya kufuata hekima ya wanadamu. Utambuzi na busara yake inamchochea kuhakikisha kwamba imani, matendo, na mafundisho yake yanategemea kabisa mafundisho ya Yesu. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anatenda vivyo hivyo.

Pia, ona jinsi neno linalotafsiriwa “mwenye busara” linavyotumiwa katika tafsiri nyingi za Maandiko ya Kiebrania. Kwa mfano, Farao alimweka Yosefu asimamie hazina zote za chakula za Misri. Hatua hiyo ilikuwa sehemu ya mpango wa Yehova wa kuwaandalia watu wake chakula. Kwa nini Yosefu alichaguliwa? Farao alisema hivi kumhusu: “Hakuna mtu mwenye busara na mwenye hekima kama wewe.” (Mwanzo 41:33-39; 45:5) Vivyo hivyo, Biblia inasema kwamba Abigaili alikuwa “mwenye busara njema.” Alimpa chakula mtiwa-mafuta wa Yehova, yaani, Daudi pamoja na wanaume wake. (1 Samweli 25:3, 11, 18) Yosefu na Abigaili waliitwa wenye busara kwa sababu walitambua mapenzi ya Mungu na kutenda kwa busara na hekima.

Kwa hivyo, Yesu aliposema kwamba mtumwa mwaminifu ni mwenye busara, alimaanisha kwamba wale wanaowakilishwa na mtumwa huyo wangeonyesha utambuzi, hekima, na ufahamu kwa sababu imani, matendo, na mafundisho yao yanategemea Neno la Mungu la kweli.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Usemi “mwenye busara” umetafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki phroʹni·mos. Kitabu kimoja (Word Studies in the New Testament) cha M. R. Vincent, kinasema kwamba kwa kawaida neno hilo linamaanisha hekima na busara inayotumika.