Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunaweza Jinsi Gani Kutenda Kwa Rehema?

Tunaweza Jinsi Gani Kutenda Kwa Rehema?

Tunaweza Jinsi Gani Kutenda Kwa Rehema?

“Tuwatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.”—WAGALATIA 6:10.

1, 2. Mfano wa Msamaria mwema unatufundisha nini kuhusu rehema?

ALIPOKUWA akizungumza na Yesu, mtu mmoja mwenye ujuzi mwingi wa Sheria alimuuliza hivi: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Yesu alimjibu kwa kusimulia mfano unaofuata: “Mtu fulani alikuwa akishuka kutoka Yerusalemu kwenda Yeriko akaanguka katikati ya wanyang’anyi, ambao walimvua nguo na pia kumpiga, kisha wakaenda zao, wakamwacha karibu kufa. Sasa, ikatukia kwamba, kuhani fulani alikuwa akishuka katika barabara hiyo, lakini, alipomwona, akapita upande ule mwingine. Vivyo hivyo, Mlawi pia, alipofika chini katika mahali hapo na kumwona, akapita kando upande wa pili. Lakini Msamaria fulani aliyekuwa akisafiri katika barabara ile alikuja, akamkuta na, alipomwona, akamsikitikia. Kwa hiyo akamkaribia akayafunga majeraha yake, na kumwaga mafuta na divai juu yake. Kisha akampandisha juu ya mnyama wake mwenyewe akamleta kwenye nyumba ya wageni na kumtunza. Na siku iliyofuata akatoa dinari mbili, akampa hizo mtu aliyekuwa akitunza nyumba hiyo ya wageni, na kusema, ‘Mtunze, na chochote utakachotumia mbali na hiki, mimi nitakulipa nitakaporudi hapa.’” Kisha, Yesu akamuuliza hivi msikilizaji wake: “Ni nani kati ya watu hao watatu anayeonekana kwako kuwa alijifanya kuwa jirani kwa mtu aliyeanguka katikati ya wanyang’anyi?” Mtu huyo akajibu: “Ni yule aliyemtendea kwa rehema.”—Luka 10:25, 29-37a.

2 Tendo la Msamaria huyo la kumtunza mtu aliyeumizwa linaonyesha waziwazi maana ya rehema ya kweli. Akichochewa na sikitiko, au huruma, Msamaria huyo alitenda kwa njia ambayo ilimtuliza mtu huyo aliyeumizwa. Zaidi ya hayo, Msamaria huyo hakumjua mtu huyo aliyekuwa na uhitaji. Rehema haizuiwi na mipaka ya kitaifa, kidini, au kitamaduni. Baada ya kutoa mfano huo wa Msamaria mwema, Yesu alimshauri msikilizaji wake hivi: “Nenda, na uwe ukifanya vivyo hivyo.” (Luka 10:37b) Tunaweza kutii himizo hilo na kujitahidi kuwa wenye rehema kwa wengine. Lakini jinsi gani? Tunaweza kutenda kwa rehema katika maisha yetu ya kila siku katika njia gani?

“Ikiwa Ndugu . . . Yuko Uchi”

3, 4. Kwa nini tuhangaikie kutenda kwa rehema hasa katika kutaniko la Kikristo?

3 Mtume Paulo alisema hivi: “Tukiwa na wakati unaofaa kwa ajili ya hilo, tuwatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Basi, acheni kwanza tuchunguze jinsi tunavyoweza kuwatendea kwa rehema nyingi wale ambao katika imani ni jamaa zetu.

4 Akiwahimiza Wakristo wa kweli wawe wenye rehema kuelekea mmoja na mwenzake, mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Yeye asiye na mazoea ya kuonyesha rehema atapata hukumu yake bila rehema.” (Yakobo 2:13) Mistari inayozunguka maneno hayo yaliyoongozwa na roho inatuonyesha njia fulani tunazoweza kutenda kwa rehema. Kwa mfano, tunasoma hivi kwenye Yakobo 1:27: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kuwatunza mayatima na wajane katika dhiki yao, na kuendelea kujitunza bila doa kutokana na ulimwengu.” Andiko la Yakobo 2:15, 16 linasema hivi: “Ikiwa ndugu au dada yuko uchi naye hana chakula cha kutosha kwa ajili ya siku, na mmoja wenu amwambie: ‘Nenda kwa amani, jipashe moto na kula vizuri,’ lakini ninyi mkose kumpa mahitaji ya mwili wake, ina faida gani?”

5, 6. Tunaweza jinsi gani kutenda matendo mengi ya rehema tunaposhirikiana na kutaniko la kwetu?

5 Kuwajali wengine na kuwasaidia wale walio katika uhitaji ni jambo linaloitambulisha dini ya kweli. Ibada yetu haituruhusu kuwahangaikia wengine kwa maneno matupu tu ya kuwatakia mema. Badala yake, hisia nyororo za huruma zinatuchochea kuwasaidia wale walio na uhitaji mkubwa. (1 Yohana 3:17, 18) Ndiyo, kumpikia mgonjwa, kumsaidia kazi za nyumbani mtu aliyezeeka, kumpeleka kwenye mikutano ya Kikristo inapohitajika, na kutokuwa mchoyo kuelekea wale wanaostahili msaada ni kati ya matendo mengi ya rehema ambayo tunapaswa kutenda.—Kumbukumbu la Torati 15:7-10.

6 Ingawa ni jambo la maana kuwasaidia kimwili washiriki wa kutaniko la Kikristo linalopanuka, ni jambo la maana hata zaidi kuwasaidia kiroho. Tunahimizwa ‘tuseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika, na kutegemeza walio dhaifu.’ (1 Wathesalonike 5:14) “Wanawake wenye umri mkubwa” wanatiwa moyo kuwa “walimu wa yaliyo mema.” (Tito 2:3) Kuhusu waangalizi Wakristo, Biblia inasema hivi: “Kila mmoja atakuwa kama mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua.”—Isaya 32:2.

7. Tunajifunza nini kuhusu kuonyesha rehema kutokana na wanafunzi huko Siria ya Antiokia?

7 Zaidi ya kuwajali wajane, mayatima, na wale waliohitaji kusaidiwa na kutiwa moyo katika maeneo ya kwao, nyakati nyingine makutaniko ya karne ya kwanza yalituma misaada kwa waamini wenzao wa maeneo mengine. Kwa mfano, nabii Agabo alipotabiri kwamba “njaa kali ilikuwa karibu kuja juu ya dunia nzima inayokaliwa,” wanafunzi huko Siria ya Antiokia ‘waliamua, kila mmoja kwa kadiri ambayo yeyote angeweza kutoa, wafanye huduma ya kupeleka misaada kwa akina ndugu waliokuwa wakikaa Yudea.’ Misaada hiyo ilitumwa kwa wazee wa huko “kwa mkono wa Barnaba na Sauli.” (Matendo 11:28-30) Namna gani leo? “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” amepanga kuwe na halmashauri za kutoa misaada ili ziwatunze ndugu zetu ambao huenda wamepatwa na misiba ya asili, kama vile vimbunga, matetemeko ya nchi, au mawimbi ya tsunami. (Mathayo 24:45) Kujitolea kutumia wakati, nguvu, na mali zetu kuhusiana na mpango huo ni njia moja nzuri ya kuonyesha rehema.

“Mkiendelea Kuonyesha Upendeleo”

8. Upendeleo unatuzuia jinsi gani tusionyeshe rehema?

8 Akionya kuhusu tabia inayotuzuia kuonyesha rehema na kufuata “sheria ya kifalme” ya upendo, Yakobo aliandika hivi: “Mkiendelea kuonyesha upendeleo, mnafanya dhambi, kwa maana sheria inawakaripia ninyi kuwa ni wakosaji.” (Yakobo 2:8, 9) Kumwonyesha upendeleo mtu aliye tajiri kimwili au wale walio mashuhuri kunaweza kutufanya tusisikie “kilio cha kulalamika cha mtu wa hali ya chini.” (Methali 21:13) Upendeleo unazuia roho ya rehema. Tunaonyesha rehema kwa kuwatendea wengine bila ubaguzi.

9. Kwa nini si vibaya kuwaonyesha ufikirio wa pekee wale wanaostahili?

9 Je, kutokuwa na ubaguzi kunamaanisha kwamba hatuwezi kumwonyesha mtu fulani ufikirio wa pekee? Bila shaka hapana. Kuhusu mfanyakazi mwenzake Epafrodito, mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wa Filipi hivi: “Mwendelee kuwaheshimu sana watu wa namna hiyo.” Kwa nini? “Kwa sababu alikaribia sana kufa kwa ajili ya kazi ya Bwana, akiihatarisha nafsi yake, ili ajazie kikamilifu kutokuwapo kwenu hapa ili kunitolea mimi utumishi wa kibinafsi.” (Wafilipi 2:25, 29, 30) Utumishi wa uaminifu uliofanywa na Epafrodito ulistahili kuthaminiwa. Zaidi ya hayo, kwenye andiko la 1 Timotheo 5:17, tunasoma hivi: “Wanaume wazee wanaosimamia kwa njia nzuri wahesabiwe kustahili heshima mara mbili, hasa wale wanaofanya kazi kwa bidii katika kusema na kufundisha.” Sifa nzuri za kiroho zinastahili pia kuthaminiwa. Kuonyesha ufikirio kama huo si kuonyesha upendeleo.

‘Hekima Inayotoka Juu Ni Yenye Kujaa Rehema’

10. Kwa nini tunapaswa kuuzuia ulimi wetu?

10 Kuhusu ulimi, Yakobo alisema hivi: “Huo ni kitu kitundu chenye kudhuru, umejaa sumu yenye kuua. Kwa huo sisi humbariki Yehova, naam, Baba, na bado kwa huo sisi huwalaani wanadamu ambao wamekuja kuwako ‘kwa mfano wa Mungu.’ Kubariki na kulaani hutoka katika kinywa kilekile.” Kuhusiana na hilo, Yakobo aliongeza hivi: “Ikiwa mna wivu mkali na ugomvi katika mioyo yenu, msiwe mkijigamba na kusema uwongo juu ya ile kweli. Hii siyo hekima inayoshuka kutoka juu, bali ni ya kidunia, ya kinyama, ya roho waovu. Kwa maana mahali ambapo pana wivu na ugomvi, hapo pana machafuko na kila jambo baya. Lakini hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, haifanyi tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki.”—Yakobo 3:8-10a, 14-17.

11. Tunaweza kuwa wenye rehema jinsi gani katika kutumia ulimi wetu?

11 Hivyo, jinsi tunavyotumia ulimi wetu inaweza kuonyesha ikiwa tuna hekima yenye “kujaa rehema.” Namna gani ikiwa kwa sababu ya wivu au ugomvi tunajigamba, kusema uwongo, au kueneza porojo zenye kuumiza? Andiko la Zaburi 94:4 linasema: “Wote wanaofanya mambo yenye kuumiza wanaendelea kujivuna wenyewe.” Porojo zenye kuumiza zinaweza kuharibu haraka sifa nzuri ya mtu asiye na hatia! (Zaburi 64:2-4) Zaidi ya hayo, fikiria madhara ambayo “shahidi wa uwongo [ambaye] husema uwongo mtupu” anaweza kusababisha. (Methali 14:5; 1 Wafalme 21:7-13) Baada ya kuzungumza kuhusu kutumia vibaya ulimi, Yakobo anasema hivi: “Haifai, ndugu zangu, mambo haya kuendelea kutendeka kwa njia hiyo.” (Yakobo 3:10b) Tukiwa na rehema ya kweli tutatumia ulimi wetu kwa njia iliyo safi, yenye amani, na usawaziko. Yesu alisema: “Ninawaambia ninyi kwamba kila neno lisilofaa ambalo watu husema, watatoa hesabu juu yake katika Siku ya Hukumu.” (Mathayo 12:36) Ni jambo la maana kama nini kwamba tuwe wenye rehema katika kutumia ulimi wetu!

‘Mwasamehe Watu Makosa Yao’

12, 13. (a) Tunajifunza nini kuhusu rehema kutokana na mfano wa mtumwa aliyekuwa na deni kubwa la pesa la bwana wake? (b) Inamaanisha nini kumsamehe ndugu yetu “mpaka mara 77”?

12 Mfano wa Yesu wa mtumwa aliyedaiwa deni la dinari 60,000,000 na bwana wake, mfalme, unaonyesha njia nyingine ya kuwa wenye rehema. Kwa kuwa hakuwa na mali ya kulipa deni hilo, mtumwa huyo alisihi aonyeshwe rehema. “Akisikitishwa na hayo,” bwana wa mtumwa huyo alimsamehe deni lake. Lakini mtumwa huyo alitoka na kumkuta mtumwa mwenzake aliyekuwa na deni lake la dinari mia moja tu na bila rehema akamtupa gerezani. Mfalme aliposikia yale yaliyotukia, alimwita yule mtumwa aliyesamehewa na kumwambia: “Mtumwa mwovu, nilifuta lile deni lote kwa ajili yako, uliponisihi. Haikukupasa wewe, nawe, kuwa na rehema juu ya mtumwa mwenzako, kama mimi pia nilivyokuwa na rehema juu yako?” Kwa hiyo, bwana akaamuru mtumwa huyo apelekwe kwa walinzi wa jela. Yesu alimalizia mfano huo hivi: “Vivyo hivyo Baba yangu wa mbinguni atashughulika nanyi pia ikiwa kila mmoja wenu hatamsamehe ndugu yake kutoka moyoni mwake.”—Mathayo 18:23-35.

13 Mfano huo unaonyesha waziwazi kama nini kwamba rehema inatia ndani kuwa tayari kusamehe! Yehova ametusamehe deni kubwa la dhambi. Je, sisi pia hatupaswi ‘kuwasamehe watu makosa yao’? (Mathayo 6:14, 15) Kabla ya Yesu kusimulia mfano huo kuhusu mtumwa asiye na rehema, Petro alimuuliza hivi: “Bwana, ndugu yangu atanitendea dhambi mara ngapi nami nimsamehe? Mpaka mara 7?” Yesu akamjibu: “Ninakuambia, si, Mpaka mara 7, bali, Mpaka mara 77.” (Mathayo 18:21, 22) Ndiyo, mtu mwenye rehema yuko tayari kusamehe “mpaka mara 77,” yaani, kuendelea kusamehe.

14. Kulingana na Mathayo 7:1-4, tunaweza kutenda kwa rehema kila siku jinsi gani?

14 Akitaja njia nyingine ya kuonyesha rehema, Yesu alisema hivi katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe; kwa maana kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa . . . Basi, kwa nini unautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako, lakini hulifikirii boriti lililo katika jicho lako mwenyewe? Au unawezaje kumwambia ndugu yako, ‘Niruhusu niutoe unyasi ulio katika jicho lako’; wakati, tazama! boriti limo katika jicho lako mwenyewe?” (Mathayo 7:1-4) Kwa hiyo, kila siku tunaweza kutenda kwa rehema kwa kuvumilia kasoro za wengine bila kuwahukumu au kuwachambua-chambua sana.

“Tuwatendee Wote Mema”

15. Kwa nini hatupaswi kuwatendea kwa rehema waamini wenzetu tu?

15 Ingawa kitabu cha Biblia cha Yakobo kinakazia kuwatendea waamini wenzetu kwa rehema, hilo halimaanishi kwamba tunapaswa kuwatendea kwa rehema wale walio tu katika kutaniko la Kikristo. Andiko la Zaburi 145:9 linasema hivi: “Yehova ni mwema kwa wote, na rehema zake ziko juu ya kazi zake zote.” Tunahimizwa tuwe “waigaji wa Mungu” na “tuwatendee wote mema.” (Waefeso 5:1; Wagalatia 6:10) Ijapokuwa hatuupendi “ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu,” hatuyapuuzi mahitaji ya wale walio katika ulimwengu.—1 Yohana 2:15.

16. Ni mambo gani yanayopaswa kuamua jinsi tunavyoweza kuwaonyesha wengine rehema?

16 Tukiwa Wakristo, tuko tayari sikuzote kuwasaidia kwa njia yoyote tunayoweza wale wanaopatwa na “tukio lisilotazamiwa” au wale walio katika hali mbaya sana. (Mhubiri 9:11) Bila shaka, hali zetu zitaamua yale tunayoweza kufanya na kadiri tunavyoweza kufanya. (Methali 3:27) Tunapowasaidia wengine kimwili, tunapaswa kuwa waangalifu ili matendo yetu mazuri yasifanye wengine wawe wavivu. (Methali 20:1, 4; 2 Wathesalonike 3:10-12) Hivyo, mtu anayeonyesha rehema ya kweli anatenda kwa hisia nyororo za huruma na pia kupatana na akili.

17. Ni njia gani bora ya kuwaonyesha rehema wale walio nje ya kutaniko la Kikristo?

17 Njia bora ya kuwaonyesha rehema wale walio nje ya kutaniko la Kikristo ni kuwahubiria kweli za Biblia. Kwa nini? Kwa sababu wanadamu wengi leo wanapapasa-papasa katika giza la kiroho. Kwa kuwa hawajui jinsi ya kukabiliana na matatizo yao wala hawana tumaini lolote la wakati ujao, watu wengi “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Ujumbe wa Neno la Mungu unaweza kuwa ‘taa kwa mguu wao,’ na hivyo kuwasaidia kukabiliana na matatizo ya maisha. Pia, unaweza kuwa ‘nuru kwa barabara yao’ katika maana ya kwamba Biblia inatabiri kusudi la Mungu la wakati ujao, na hivyo kuwapa msingi wa kuwa na tumaini zuri. (Zaburi 119:105) Ni pendeleo kama nini kuwapelekea ujumbe mzuri ajabu wa kweli wale ambao wanauhitaji sana! Kwa kuwa “dhiki kuu” inakaribia sana, huu ndio wakati wa kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:3-8, 21, 22, 36-41; 28:19, 20) Hakuna tendo lingine la rehema lililo la maana kuliko hilo.

Toeni “Vitu Vilivyo Ndani”

18, 19. Kwa nini tunapaswa kuonyesha rehema zaidi katika maisha yetu?

18 Yesu alisema hivi: “Vitoeni viwe kama zawadi za rehema vitu vilivyo ndani.” (Luka 11:41) Ili tendo zuri la wema liwe tendo la rehema ya kweli, linapaswa kutoka ndani, yaani, katika moyo wenye upendo na ulio tayari kusaidia. (2 Wakorintho 9:7) Rehema kama hiyo inaburudisha kama nini katika ulimwengu huu wenye ukatili, uchoyo, ambamo watu wengi hawajali mateso na matatizo ya wengine!

19 Basi, acheni tujitahidi kuonyesha rehema zaidi katika maisha yetu. Kadiri tunavyokuwa wenye rehema, ndivyo tunavyomwiga Mungu. Hilo linatusaidia kuishi maisha yenye kusudi na yenye kuridhisha.—Mathayo 5:7.

Umejifunza Nini?

• Kwa nini ni jambo la maana kuwaonyesha rehema hasa waamini wenzetu?

• Tunaweza namna gani kutenda kwa rehema katika kutaniko la Kikristo?

• Tunaweza jinsi gani kuwatendea mema wale walio nje ya kutaniko?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Msamaria alitenda kwa rehema

[Picha katika ukurasa wa 27]

Wakristo wanatenda matendo mengi ya rehema

[Picha katika ukurasa wa 30]

Njia bora ya kuwaonyesha rehema wale walio nje ya kutaniko ni kuwahubiria kweli ya Biblia