Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yoeli na cha Amosi

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yoeli na cha Amosi

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yoeli na cha Amosi

“YOELI mwana wa Pethueli,” hayo ndiyo mambo yote anayosema kujihusu. (Yoeli 1:1) Katika kitabu kinachoitwa kwa jina lake, Yoeli hasemi mengi kuhusu mambo mengine ila ujumbe wake. Hivyo tunaweza tu kukadiria wakati aliotoa unabii wake kuwa karibu mwaka wa 820 K.W.K., miaka tisa baada ya Uzia kuwa mfalme wa Yuda. Kwa nini Yoeli hasemi mengi kujihusu? Inaelekea ni kwa sababu anataka kukazia ujumbe badala ya mjumbe.

Pia katika siku za Uzia, Amosi, mkaaji wa Yuda ambaye alikuwa “mchungaji na mminyaji wa tini za mikuyu,” anapewa utume wa kuwa nabii. (Amosi 7:14) Tofauti na Yoeli, ambaye anatoa unabii huko Yuda, Amosi anatumwa kaskazini kwenye ufalme wa makabila kumi ya Israeli. Kitabu cha Amosi ambacho kilikamilika karibu mwaka wa 804 K.W.K. baada ya nabii huyo kurudi Yuda, kimeandikwa kwa lugha rahisi lakini yenye kuvutia.

“OLE WAKE SIKU ILE”—KWA NINI?

(Yoeli 1:1–3:21)

Shambulio la viwavi, nzige, na mende, ndilo jambo ambalo Yoeli anaona katika maono. Washambulizi hao wanasemwa kuwa kama “kundi la watu wengi sana na wenye nguvu” na kama “wanaume wenye nguvu.” (Yoeli 1:4; 2:2-7) “Ole wake siku ile,” anasema Yoeli kwa kuugua, “kwa sababu siku ya Yehova iko karibu, nayo itakuja kama mporaji kutoka kwa Mweza-Yote!” (Yoeli 1:15) Yehova anawashauri hivi wakaaji wa Sayuni: “Rudini kwangu kwa mioyo yenu yote.” Wakifanya hivyo, Yehova “atawaonea huruma watu wake” na atamweka mbali “mkaaji wa kaskazini”—shambulio la wadudu. Hata hivyo, kabla siku yake kuu haijaja, Yehova ‘ataimimina roho yake juu ya kila namna ya mwili’ naye ‘atatoa maajabu mbinguni na duniani.’—Yoeli 2:12, 18-20, 28-31.

Mataifa yanaalikwa kwenye vita: “Fueni majembe yenu yawe panga na miundu yenu iwe mikuki” na kujitayarisha kwa ajili ya vita. Yanaamriwa “yaje kwenye bonde la Yehoshafati,” mahali ambapo yatahukumiwa na kupondwa. “Bali Yuda, itakaliwa sikuzote, na Yerusalemu kizazi baada ya kizazi.”—Yoeli 3:10, 12, 20.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:15; 2:1, 11, 31; 3:14—“Siku ya Yehova” ni nini? Siku ya Yehova ni wakati wa kutekelezwa kwa hukumu ya Yehova juu ya maadui wake, matokeo yakiwa kuharibiwa kwa waovu na kuokolewa kwa waabudu wa kweli. Kwa mfano, siku ya Yehova ilikuja juu ya Babiloni la kale mnamo 539 K.W.K. jiji hilo liliposhindwa na Wamedi na Waajemi. (Isaya 13:1, 6) ‘Siku nyingine ya Yehova’ inakaribia, wakati ambapo atatekeleza hukumu yake juu ya “Babiloni Mkubwa”—milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo.—Ufunuo 18:1-4, 21.

2:1-10, 28—Unabii kuhusu shambulio la wadudu umetimizwa kwa njia gani? Katika Biblia hakuna masimulizi kuhusu shambulio kubwa la wadudu katika nchi ya Kanaani kama lile linalotajwa katika kitabu cha Yoeli. Hivyo, inaelekea kwamba shambulio linalotajwa na Yoeli ni la kinabii nalo linahusu mwaka wa 33 W.K. Yehova alipomimina roho yake juu ya wafuasi wa mapema wa Kristo nao wakaanza kuhubiri ujumbe uliowatesa viongozi wa dini za uwongo. (Matendo 2:1, 14-21; 5:27-33) Tuna pendeleo la kufanya kazi kama hiyo leo.

2:32—Inamaanisha nini ‘kuliitia jina la Yehova’? Kuliitia jina la Mungu kunamaanisha kulijua jina hilo, kuliheshimu sana, na kumtegemea na kumtumaini mwenye jina hilo.—Waroma 10:13, 14.

3:14—“Bonde la uamuzi” ni nini? Ni mahali pa mfano ambapo hukumu ya Mungu inatekelezwa. Wakati wa utawala wa Mfalme Yehoshafati wa Yudea, ambaye jina lake linamaanisha “Yehova Ni Mwamuzi,” Mungu alivuruga majeshi ya mataifa yaliyozunguka Yuda na hivyo kukomboa Yuda. Kwa hiyo, mahali hapo panaitwa pia “bonde la Yehoshafati.” (Yoeli 3:2, 12) Katika siku yetu, bonde hilo linafananisha mahali pa mfano ambapo mataifa yatapondwa-pondwa kama zabibu ndani ya shinikizo la divai.—Ufunuo 19:15.

Mambo Tunayojifunza:

1:13, 14. Toba ya kweli na kumtambua Yehova kuwa Mungu wa kweli ni muhimu kwa ajili ya wokovu.

2:12, 13. Toba ya kweli inatoka moyoni. Ni hatua ya ndani inayohusisha ‘kurarua mioyo yetu,’ wala si hatua ya nje tu, kama vile ‘kurarua mavazi yetu.’

2:28-32. Yule tu ‘anayeliitia jina la Yehova ndiye atakayeokoka’ “ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha.” Tunashukuru kama nini kwamba Yehova anamimina roho yake juu ya kila namna ya mwili na anawatumia vijana kwa wazee, wanaume na wanawake, katika kazi ya kutoa unabii, yaani, kutangaza “mambo makuu ya Mungu”! (Matendo 2:11) Siku ya Yehova inapozidi kukaribia, je, hatupaswi kujaa “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu”?—2 Petro 3:10-12.

3:4-8, 19. Yoeli alitabiri kwamba mataifa yaliyozunguka Yuda yangetozwa hesabu kwa sababu ya kuwatendea vibaya watu wa Mungu waliochaguliwa. Kupatana na maneno hayo ya kinabii, jiji la Tiro lililokuwa katika nchi kavu liliharibiwa na Mfalme Nebukadneza wa Babiloni. Baadaye, wakati jiji la kisiwani liliposhindwa na Aleksanda Mkuu, maelfu ya askari-jeshi na watu mashuhuri wa jiji hilo waliuawa, na wakaaji 30,000 wa jiji hilo wakauzwa utumwani. Wafilisti walitendewa vivyo hivyo na Aleksanda na wafalme wengine waliotawala baada yake. Kufikia karne ya nne K.W.K., Edomu lilikuwa ukiwa. (Malaki 1:3) Unabii huo mbalimbali ambao umetimizwa unaimarisha imani yetu katika Yehova akiwa Mtimizaji wa ahadi zake. Pia, unaonyesha jinsi Yehova atakavyoyatendea mataifa ambayo yanawatesa waabudu wake leo.

3:16-21. “Mbingu na dunia zitatikisika,” nayo mataifa yatahukumiwa vikali na Yehova. “Bali Yehova atakuwa kimbilio kwa watu wake,” naye atawapa uzima katika hali za kiparadiso. Je, hatupaswi kuazimia kabisa kukaa karibu na Yehova kadiri siku yake ya kutekeleza hukumu juu ya ulimwengu mbovu inavyozidi kukaribia?

“JITAYARISHE KUKUTANA NA MUNGU WAKO”

(Amosi 1:1–9:15)

Amosi ana ujumbe kwa mataifa adui yanayozunguka Israeli na pia ujumbe kwa Yuda na Israeli. Mataifa ya Siria, Ufilisti, Tiro, Edomu, na Moabu yataangamizwa kwa sababu ya kuwatendea watu wa Mungu kwa ukatili. Wakaaji wa Yuda wataangamizwa “kwa sababu wamekataa sheria ya Yehova.” (Amosi 2:4) Namna gani ufalme wa Israeli wa makabila kumi? Dhambi zake zinatia ndani kuwakandamiza maskini kwa pupa, mwenendo mpotovu kiadili, na kuwatendea kwa dharau manabii wa Yehova. Amosi anaonya kwamba Yehova ‘atatoza hesabu madhabahu za Betheli’ na ‘kuiangusha nyumba ya wakati wa majira ya baridi kali pamoja na nyumba ya wakati wa kiangazi.’—Amosi 3:14, 15.

Ingawa tayari wameadhibiwa kwa njia mbalimbali, Waisraeli wanaoabudu sanamu wanaendelea kuwa na shingo ngumu. Amosi anawaambia hivi: “Jitayarishe kukutana na Mungu wako.” (Amosi 4:12) Kwa Waisraeli, siku ya Yehova itamaanisha kupelekwa “uhamishoni ng’ambo ya Damasko,” yaani, Ashuru. (Amosi 5:27) Amosi anakabili upinzani kutoka kwa kuhani wa Betheli lakini haogopeshwi kamwe. “Mwisho umewafikia watu wangu Israeli,” Yehova anamwambia Amosi. “Sitawasamehe zaidi tena.” (Amosi 8:2) Wala Kaburi wala milima iliyoinuka haiwezi kuwazuia wasipate hukumu za Mungu. (Amosi 9:2, 3) Lakini kuna ahadi ya kurudishwa. “Nitakusanya na kurudisha mateka wa watu wangu Israeli, nao watajenga majiji yaliyofanywa ukiwa na kukaa ndani yake, watapanda mashamba ya mizabibu na kunywa divai yake, watafanyiza bustani na kula matunda yake.”—Amosi 9:14.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

4:1—Ni nani wanaofananishwa na “ng’ombe za Bashani”? Nyanda za juu za Bashani, eneo lililo mashariki ya Bahari ya Galilaya, zilijulikana kwa sababu ya wanyama bora wa eneo hilo kutia ndani ng’ombe. Wanyama hao walikuwa na afya nzuri kwa sababu ya malisho mazuri sana ya eneo hilo. Amosi aliwalinganisha wanawake wa Samaria waliopenda starehe na ng’ombe za Bashani. Bila shaka, wanawake hao waliwasukuma ‘mabwana wao,’ au waume wao, wawapunje maskini ili wajipatie utajiri.

4:6—Maneno “usafi wa meno” yanamaanisha nini? Yanapotumiwa pamoja na maneno “upungufu wa mkate,” maneno hayo yanaweza kumaanisha kipindi cha njaa kali wakati ambapo meno yanabaki yakiwa safi kwa sababu ya kukosa chakula.

5:5—Waisraeli hawakupaswa ‘kuitafuta tena Betheli’ katika njia gani? Yeroboamu alikuwa ameanzisha ibada ya ndama huko Betheli. Tangu wakati huo, jiji hilo likawa kitovu cha ibada ya uwongo. Hapana shaka kwamba Gilgali na Beer-sheba pia yalikuwa vitovu vya ibada ya uasi-imani. Ili kuepuka msiba uliotabiriwa, Waisraeli walipaswa kuacha kutembelea maeneo hayo kwa makusudi ya kidini na kuanza kumtafuta Yehova.

7:1—“Majani yaliyofyekwa ya mfalme” yanarejelea nini? Inaelekea majani hayo yanarejelea kodi ambayo mfalme alitoza ili kutunza wapanda-farasi wake na wanyama wake. Kodi hiyo ilipaswa kulipwa “mwanzoni mwa kuota kwa mimea iliyopandwa baadaye.” Baada ya hapo, watu wangevuna mazao yao. Hata hivyo, kabla tu hawajavuna, kundi la nzige lilikuja na kula kabisa mimea yao pamoja na mimea mingine.

8:1, 2—“Kikapu cha matunda ya wakati wa kiangazi” kilimaanisha nini? Kilimaanisha kwamba siku ya Yehova ilikuwa karibu. Matunda ya wakati wa kiangazi yalikusanywa mwishoni mwa kipindi cha mavuno, yaani, mwishoni mwa mwaka wa kilimo. Yehova alipomfanya Amosi aone “kikapu cha matunda ya wakati wa kiangazi,” ilimaanisha kwamba mwisho wa Israeli ulikuwa umekaribia. Hivyo, Mungu alimwambia Amosi: “Mwisho umewafikia watu wangu Israeli. Nami sitawasamehe zaidi tena.”

Mambo Tunayojifunza:

1:3, 6, 9, 11, 13; 2:1, 4, 6Yehova anasema hivi kuhusu hasira yake kuelekea Israeli, Yuda, na mataifa mengine sita yaliyowazunguka: “Sitaizuia.” Hukumu za Yehova haziepukiki.—Amosi 9:2-5.

2:12. Hatupaswi kuwavunja moyo mapainia, waangalizi wanaosafiri, wamishonari, au washiriki wa familia ya Betheli ambao wanafanya kazi kwa bidii kwa kuwahimiza waache utumishi wa wakati wote ili waishi maisha yanayoitwa eti maisha ya kawaida. Badala yake, tunapaswa kuwatia moyo waendelee kufanya kazi yao nzuri.

3:8. Kama vile mtu anavyoogopa anaposikia simba akinguruma, ndivyo Amosi alilazimika kuhubiri alipomsikia Yehova akisema: “Nenda, watolee unabii watu wangu.” (Amosi 7:15) Woga wa kimungu unapaswa kutuchochea tuwe wahubiri wenye bidii wa ujumbe wa Ufalme.

3:13-15; 5:11. Kwa msaada wa Yehova, Amosi mchungaji maskini alifaulu ‘kuwatolea ushahidi’ watu waliokuwa matajiri na wasiojali. Yehova anaweza kutusaidia sisi pia kutangaza ujumbe wa Ufalme hata eneo likiwa gumu kadiri gani.

4:6-11; 5:4, 6, 14. Ingawa Waisraeli walishindwa tena na tena ‘kumrudia’ Yehova, walihimizwa ‘wamtafute Yehova ili waendelee kuishi.’ Kwa muda wote ambao Yehova ataendelea kwa subira kuruhusu mfumo huu mbovu uwepo, tunapaswa kuwahimiza wale waliomo wamgeukie Mungu.

5:18, 19. ‘Kuitamani siku ya Yehova’ bila kuwa tayari kwa ajili yake ni jambo la upumbavu. Mtu anayefanya hivyo ni kama mtu anayemkimbia simba lakini anakutana na dubu, kisha anamkimbia dubu huyo halafu anaumwa na nyoka. Tunatenda kwa hekima ‘tunapoendelea kukesha’ kiroho na kuwa tayari.—Luka 21:36.

7:12-17. Tunapaswa kutangaza ujumbe wa Mungu bila woga na kwa ujasiri.

9:7-10. Kuwa wazao wa wazee wa ukoo waliokuwa waaminifu na pia wazao wa wale waliokombolewa kutoka Misri wakiwa watu wa Mungu waliochaguliwa, hakukuwazuia Waisraeli wasio waaminifu wasiwe na msimamo mbaya mbele za Mungu kama Wakushi walivyokuwa. Kuwa na msimamo unaokubalika machoni pa Mungu asiye na upendeleo hakutegemei ukoo wa mtu bali kunategemea ‘kumwogopa Mungu na kutenda uadilifu.’—Matendo 10:34, 35.

Jambo Tunalopaswa Kufanya

Siku ya kutekeleza hukumu ya Mungu juu ya ulimwengu wa Shetani iko karibu. Mungu ameimimina roho yake juu ya waabudu wake, akiwawezesha kuwaonya wanadamu kuhusu siku yake inayokaribia. Je, hatupaswi kushiriki kabisa kuwasaidia wengine kumjua Yehova na ‘kuliitia jina lake’?—Yoeli 2:31, 32.

“Chukieni yaliyo mabaya,” anahimiza Amosi, “pendeni yaliyo mema, na mwipatie haki nafasi langoni.” (Amosi 5:15) Kadiri siku ya Yehova inavyokaribia, ni jambo la hekima kumkaribia Mungu na kujitenga na ulimwengu mbovu na ushirika wake wenye kupotosha. Vitabu vya Biblia vya Yoeli na Amosi vina masomo yanayoweza kutusaidia sana kufanya hivyo!—Waebrania 4:12.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Yoeli alitabiri hivi: “Siku ya Yehova iko karibu!”

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kama Amosi, tunapaswa kutangaza ujumbe wa Mungu bila woga na kwa ujasiri