Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukombolewa Kutoka Katika Mitego ya Mwindaji wa Ndege

Kukombolewa Kutoka Katika Mitego ya Mwindaji wa Ndege

Kukombolewa Kutoka Katika Mitego ya Mwindaji wa Ndege

“[Yehova] mwenyewe atakukomboa kutoka katika mtego wa mwindaji wa ndege.”—ZABURI 91:3.

1. “Mwindaji wa ndege” ni nani, na kwa nini yeye ni hatari?

WAKRISTO wote wa kweli wanawindwa na adui fulani mwenye ujanja na akili zinazopita za wanadamu. Katika Zaburi 91:3 anaitwa “mwindaji wa ndege.” Adui huyo ni nani? Kuanzia toleo la Juni 1, 1883 (1/6/1883), gazeti la Mnara wa Mlinzi limemtambulisha adui huyo kuwa Shetani Ibilisi. Adui huyo mwenye nguvu nyingi sana anajaribu kwa ujanja kuwapotosha na kuwanasa watu wa Yehova kama vile mwindaji wa ndege anavyojaribu kumnasa ndege.

2. Kwa nini Shetani analinganishwa na mwindaji wa ndege?

2 Katika nyakati za zamani, ndege walikamatwa kwa ajili ya nyimbo zao tamu, manyoya yao maridadi, chakula, na pia kwa ajili ya dhabihu. Hata hivyo, kwa asili ndege ni viumbe wanaojihadhari sana, wanaotambua hatari haraka, na wasionaswa kwa urahisi katika mtego. Kwa hiyo, mwindaji wa ndege katika nyakati za Biblia alichunguza kwanza kwa uangalifu tabia na mazoea ya ndege ambao alitaka kunasa. Kisha, alitafuta njia za ujanja za kuwanasa. Biblia inapomlinganisha Shetani na mwindaji wa ndege, inatusaidia kuelewa njia anazotumia. Ibilisi anamchunguza kila mmoja wetu. Anaona tabia na sifa zetu naye anaweka mitego iliyofichwa ili ajaribu kutushika tukiwa hai. (2 Timotheo 2:26) Shetani akitushika, uhusiano wetu pamoja na Mungu utaharibika na mwishowe tutakabili hatari ya kuharibiwa. Kwa hiyo, ili tujilinde tunahitaji kutambua mbinu mbalimbali za ‘mwindaji huyo wa ndege.’

3, 4. Ni wakati gani Shetani anatumia mbinu kama za simba? za swila?

3 Akitumia mifano iliyo wazi, mtunga-zaburi analinganisha pia mbinu za Shetani na za mwana-simba au za swila. (Zaburi 91:13) Kama simba, nyakati nyingine Shetani anawashambulia watu wa Yehova kwa njia ya moja kwa moja kupitia mateso au kupitia hatua za kisheria. (Zaburi 94:20) Mashambulizi hayo yaliyo kama ya simba yanaweza kuwafanya watu wachache wamwache Yehova. Hata hivyo, mara nyingi mashambulizi hayo ya waziwazi hayafanikiwi, badala yake yanawaunganisha watu wa Mungu. Lakini namna gani mashambulizi yenye hila zaidi ya Shetani yaliyo kama ya swila?

4 Ibilisi anatumia akili yake inayopita ya wanadamu ili kuwashambulia kwa hila na kwa njia iliyo hatari sana kama nyoka mwenye sumu aliyejificha. Kwa kutumia njia hiyo, amefanikiwa kutia sumu akili ya watu fulani wa Mungu, amewadanganya ili wafanye mapenzi yake badala ya kufanya mapenzi ya Yehova, na matokeo yamekuwa mabaya sana. Inafurahisha kwamba hatukosi kuzijua mbinu za Shetani. (2 Wakorintho 2:11) Acheni sasa tuchunguze mitego minne kati ya mitego hatari ambayo inatumiwa na ‘mwindaji huyo wa ndege.’

Kuwaogopa Wanadamu

5. Kwa nini mtego wa “kutetemeshwa na wanadamu” una matokeo sana?

5 “Mwindaji wa ndege” anaelewa tamaa ya kawaida ya wanadamu ya kukubaliwa na kupendwa na wengine. Wakristo wanajali hisia na maoni ya wengine kuwaelekea. Ibilisi anajua hivyo naye angependa kuwanasa kwa kutumia mahangaiko yao kuhusu maoni ya watu. Kwa mfano, anawanasa baadhi ya watu wa Mungu kwa kutumia mtego wa “kutetemeshwa na wanadamu.” (Methali 29:25) Ikiwa kwa sababu ya kuwaogopa wanadamu, watumishi wa Mungu wanajiunga na wengine kufanya mambo ambayo Yehova anakataza au wanakosa kufanya yale ambayo Neno la Mungu linawaamuru wafanye, basi wamenaswa na “mwindaji wa ndege.”—Ezekieli 33:8; Yakobo 4:17.

6. Ni mfano gani unaoonyesha jinsi kijana anavyoweza kunaswa na “mwindaji wa ndege”?

6 Kwa mfano, kijana anaweza kushindwa akibanwa na wanashule wenzake na hivyo kuvuta sigara. Alipoenda shuleni siku hiyo huenda hakufikiri kamwe kwamba atavuta sigara. Hata hivyo, muda si muda anajikuta akifanya jambo lisilompendeza Mungu na linaloharibu afya yake. (2 Wakorintho 7:1) Alishawishiwa kwa njia gani? Labda alishirikiana na marafiki wabaya na akaogopa kwamba watamdhihaki. Enyi vijana, msimruhusu “mwindaji wa ndege” awashawishi na kuwanasa! Ili kuepuka kushikwa mkiwa hai, jilindeni ili msilegeze msimamo wenu hata katika mambo madogo. Mtii onyo la Biblia la kuepuka mashirika mabaya.—1 Wakorintho 15:33.

7. Shetani anaweza jinsi gani kuwafanya wazazi fulani wapoteze usawaziko wao wa kiroho?

7 Wazazi Wakristo wenye bidii wanachukua kwa uzito daraka lao la Kimaandiko la kutimizia familia zao mahitaji ya kimwili. (1 Timotheo 5:8) Hata hivyo, kusudi la Shetani ni kuwafanya Wakristo wapoteze usawaziko wao katika jambo hilo. Huenda wanakosa mikutano kwa ukawaida kwa sababu wanasukumwa na wafanyakazi wenzao wafanye kazi ya ziada. Labda wanaogopa kuomba ruhusa kazini ili wahudhurie kusanyiko lote la wilaya na kumwabudu Yehova pamoja na ndugu zao. ‘Kumtegemea Yehova’ kutatulinda kutokana na mtego huo. (Methali 3:5, 6) Kwa kuongezea, kukumbuka kwamba sote ni watu wa nyumba ya Yehova na kwamba amejitwika wajibu wa kututunza kutatusaidia kudumisha usawaziko wetu. Wazazi, je, mna imani kwamba kwa njia moja au nyingine Yehova atawatunza pamoja na familia zenu mnapofanya mapenzi yake? Au, Ibilisi atawashika mkiwa hai na kuwashawishi mfanye mapenzi yake kwa sababu ya kuwaogopa wanadamu? Tunawasihi msali na kufikiria maswali hayo.

Mtego wa Kupenda Vitu vya Kimwili

8. Shetani anatumia jinsi gani tamaa ya vitu vya kimwili?

8 Shetani anatumia pia tamaa ya vitu vya kimwili ili kutunasa. Mara nyingi mfumo wa biashara wa ulimwengu huu unawahimiza watu wafuatie mipango ya kutajirika haraka ambayo inaweza hata kuwadanganya baadhi ya watu wa Mungu. Nyakati nyingine, watu wanaweza kutiwa moyo hivi: “Fanya kazi kwa bidii. Ukipata pesa nyingi, unaweza kustarehe na kufurahia maisha. Hata unaweza kufanya upainia.” Huenda watu fulani ambao wanajifaidi kifedha kutokana na washiriki wenzao wa kutaniko la Kikristo wakawa na mawazo hayo yasiyo na usawaziko. Fikiria kwa uangalifu kitia-moyo hicho. Je, hakilingani na mawazo ya yule mtu tajiri ambaye ‘hakuwa na akili’ katika mfano wa Yesu?—Luka 12:16-21.

9. Kwa nini Wakristo fulani wanaweza kunaswa na tamaa ya vitu?

9 Shetani anaendesha mfumo wake mbovu katika njia ambayo inawachochea watu kutamani vitu. Mwishowe, tamaa hiyo inaweza kuharibu maisha ya Mkristo, kulisonga neno na kulifanya ‘likose kuzaa matunda.’ (Marko 4:19) Biblia inatutia moyo turidhike na chakula na kitu cha kujifunika. (1 Timotheo 6:8) Hata hivyo, wengi wananaswa na “mwindaji wa ndege” kwa sababu hawafuati shauri hilo. Je, huenda kiburi kinawafanya waone kwamba ni lazima wawe na mtindo fulani wa maisha? Namna gani sisi binafsi? Je, tamaa yetu ya kuwa na vitu vya kimwili inatufanya tuone ibada ya kweli si ya maana? (Hagai 1:2-8) Inahuzunisha kwamba Wakristo fulani wanapokabili matatizo ya kiuchumi wanapuuza hali yao ya kiroho ili wadumishe kiwango cha maisha ambacho walizoea. Mtazamo kama huo wa kimwili unampendeza “mwindaji wa ndege”!

Mtego wa Burudani Zisizofaa

10. Kila Mkristo anapaswa kujichunguza kwa njia gani?

10 Mbinu nyingine ambayo ‘mwindaji huyo wa ndege’ anatumia ni kudhoofisha hisia za asili za watu kuelekea mema na mabaya. Burudani nyingi leo zinakazia mtazamo kama ule uliokuwa Sodoma na Gomora. Hata habari za televisheni na magazeti zimejaa jeuri na zinawachochea watu kutosheleza tamaa zao zilizopotoka sana za ngono. Burudani nyingi katika vyombo vya habari zinaharibu uwezo wa watu wa “kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Hata hivyo, kumbuka maneno haya ambayo Yehova alisema kupitia nabii Isaya: “Ole wao wanaosema kwamba wema ni ubaya na ubaya ni wema!” (Isaya 5:20) Je, yule “mwindaji wa ndege” amepotosha kwa ujanja fikira zako kupitia burudani kama hizo zisizofaa? Ni jambo la maana sana kujichunguza.—2 Wakorintho 13:5.

11. Gazeti Mnara wa Mlinzi lilitoa onyo gani kuhusu vipindi vya mfululizo vya televisheni?

11 Miaka 25 hivi iliyopita, gazeti la Mnara wa Mlinzi liliwaonya kwa upendo waabudu wa kweli wa Mungu kuhusu vipindi vya mfululizo katika televisheni. * Lilisema hivi kuhusu madhara yaliyojificha ya vipindi vya mfululizo ambavyo vinapendwa sana: “Jitihada za kutafuta mapenzi zinatumiwa kutetea mwenendo wowote ule. Kwa mfano, msichana mmoja mja-mzito ambaye hana mume anamwambia hivi rafiki yake: ‘Lakini ninampenda Victor. Mimi sijali. . . . Jambo la maana sana kwangu ni kuzaa mtoto wake!’ Muziki unaoimba kwa sauti ya chini unafanya iwe vigumu kwa watu kutambua kwamba mwenendo wake ni mpotovu sana. Wewe pia unampenda Victor. Unamhurumia msichana huyo. Unakubaliana na mwenendo wake. Mtazamaji mmoja ambaye alirudiwa na ufahamu baadaye alisema hivi: ‘Inashangaza jinsi unavyoweza kutetea maoni yako. Tunajua kwamba mwenendo mpotovu wa ngono ni mbaya. . . . Lakini nilitambua kwamba nilikuwa nikishiriki mwenendo huo katika akili yangu.’”

12. Ni mambo gani ya hakika yanayoonyesha kwamba onyo kuhusu vipindi fulani vya televisheni linafaa leo?

12 Tangu habari hiyo ilipochapishwa, vipindi hivyo vinavyochafua moyo vimeongezeka. Katika sehemu nyingi, vipindi hivyo vinaonyeshwa muda wa saa 24 kwa siku. Wanaume, wanawake, na vijana wengi wanalisha akili na mioyo yao kwa ukawaida na burudani kama hizo. Hata hivyo, hatupaswi kujidanganya wenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli. Ni kosa kusema kwamba burudani zilizopotoka ni sawa tu na mambo halisi yanayotukia ulimwenguni. Je, kwa kweli Mkristo anaweza kujitetea kwa kuchagua kuburudishwa na watu ambao hangeweza kamwe kuwaalika nyumbani mwake?

13, 14. Watu fulani walisema walifaidika jinsi gani kwa kutii maonyo kuhusu televisheni?

13 Wengi walifaidika walipotii onyo hilo ambalo lilitolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Baada ya kusoma shauri hilo la moja kwa moja linalotegemea Biblia, watu fulani walituma barua na kusema jinsi habari hizo zilivyowasaidia sana. * Mwanamke mmoja alikiri hivi: “Kwa miaka 13 nilizoea kutazama vipindi vya mfululizo vya televisheni. Nilifikiri kwamba nilikuwa salama kwa kuhudhuria tu mikutano ya Kikristo na kushiriki katika utumishi wa shambani mara kwa mara. Lakini nilifuata mtazamo wa kilimwengu ulioonyeshwa katika vipindi vya mfululizo, mtazamo wa kwamba mume wako akikutendea vibaya au ukihisi kwamba hupendwi, unaruhusiwa kufanya uzinzi, yeye ndiye wa kulaumiwa. Kwa hiyo, nilipoona kwamba nina ‘sababu’ nilifanya uzinzi na kumtendea dhambi Yehova na mume wangu pia.” Mwanamke huyo alitengwa na ushirika. Baadaye, alirudiwa na ufahamu, akatubu, na kurudishwa kutanikoni. Makala kuhusu vipindi vya mfululizo vya televisheni zilimtia nguvu aepuke burudani ambazo Yehova anachukia.—Amosi 5:14, 15.

14 Msomaji mwingine ambaye alichochewa kubadili maisha yake alisema hivi: “Nililia niliposoma habari hizo, kwa kuwa nilitambua kwamba moyo wangu haukuwa kamili tena kumwelekea Yehova. Nilimwahidi Mungu wangu kwamba singekuwa mtumwa tena wa vipindi hivyo.” Baada ya kushukuru kwa ajili ya habari hizo, mwanamke mmoja Mkristo alikubali kwamba alikuwa na zoea la kutazama vipindi hivyo naye akaandika hivi: “Nilijiuliza . . . ikiwa uhusiano wangu pamoja na Yehova ungeweza kuharibiwa. Ningeweza jinsi gani kuwa rafiki ya ‘waigizaji hao’ na pia kuwa rafiki ya Yehova?” Ikiwa vipindi hivyo vya televisheni vilichafua mioyo ya watu miaka 25 iliyopita, vina matokeo gani leo? (2 Timotheo 3:13) Tunapaswa kuwa macho kutambua mtego wa Shetani wa burudani zisizofaa za kila aina, iwe ni vipindi vya mfululizo vya televisheni, michezo ya video yenye jeuri, au video za muziki zenye maadili mapotovu.

Mtego wa Tofauti za Kibinafsi

15. Wengine wanashikwa wakiwa hai na Ibilisi kwa njia gani?

15 Shetani anatumia tofauti za kibinafsi kama mtego ili kusababisha migawanyiko kati ya watu wa Yehova. Hata tuwe na mapendeleo gani ya utumishi, tunaweza kunaswa na mtego huo. Wengine wanashikwa wakiwa hai na Ibilisi kwa sababu wanaruhusu tofauti za kibinafsi zivuruge amani, umoja na ufanisi wa kiroho wenye kuvutia sana ambao Yehova ametokeza.—Zaburi 133:1-3.

16. Shetani amekuwa akijaribu kwa hila kuvuruga umoja wetu jinsi gani?

16 Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Shetani alijaribu kuharibu sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova kupitia mashambulizi ya moja kwa moja, lakini akashindwa. (Ufunuo 11:7-13) Tangu wakati huo, amekuwa akijaribu kwa hila kuvuruga umoja wetu. Tunaporuhusu kutoelewana kati yetu kusababishe migawanyiko, tunampa yule “mwindaji wa ndege” nafasi ya kutushambulia. Kwa kufanya hivyo tunaweza kuizuia roho takatifu isitende kazi kwa uhuru katika maisha yetu na pia kutanikoni. Ikiwa hilo litatukia, Shetani atafurahi kwa sababu amani na umoja wa kutaniko ukivurugika kwa njia yoyote ile, kazi ya kuhubiri inavurugika pia.—Waefeso 4:27, 30-32.

17. Wale walio na tofauti za kibinafsi wanapaswa kutatua tofauti hizo jinsi gani?

17 Unaweza kufanya nini ikiwa una tofauti za kibinafsi na Mkristo mwenzako? Ni kweli kwamba kila hali ni tofauti. Hata hivyo, ingawa huenda kukawa na mambo mengi yanayosababisha matatizo, hakuna sababu yoyote ya kukosa kutatua tofauti za kibinafsi. (Mathayo 5:23, 24; 18:15-17) Mashauri ya Neno la Mungu yameandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu nayo ni makamilifu. Kanuni za Biblia zinapofuatwa, hazishindwi kamwe. Sikuzote kufuata kanuni hizo kunakuwa na matokeo mazuri!

18. Kwa nini kumwiga Yehova kutatusaidia kutatua tofauti za kibinafsi?

18 Yehova ‘yuko tayari kusamehe,’ naye anatoa “msamaha wa kweli.” (Zaburi 86:5; 130:4) Tunaonyesha kwamba sisi ni watoto wapendwa wa Yehova tunapomwiga. (Waefeso 5:1) Sisi sote ni watenda-dhambi na tunahitaji sana msamaha wa Yehova. Hivyo, ni lazima tuwe waangalifu ikiwa tuna mwelekeo wa kutowasamehe wengine. Tunaweza kuwa kama yule mtumwa katika mfano wa Yesu ambaye alikataa kumsamehe mtumwa mwenzake deni dogo sana likilinganishwa na deni ambalo alikuwa tayari amesamehewa na bwana wake. Bwana huyo alipojulishwa habari hizo, aliagiza mtumwa ambaye hakusamehe atupwe gerezani. Yesu alimalizia mfano huo hivi: “Vivyo hivyo Baba yangu wa mbinguni atashughulika nanyi pia ikiwa kila mmoja wenu hatamsamehe ndugu yake kutoka moyoni mwake.” (Mathayo 18:21-35) Bila shaka, kutafakari kuhusu mfano huo na kufikiria ni mara ngapi Yehova ametusamehe kwa kupenda kutatusaidia tunapojitahidi kutatua tofauti za kibinafsi kati yetu na ndugu zetu!—Zaburi 19:14.

Kukaa kwa Usalama Katika “Mahali pa Siri pa Aliye Juu”

19, 20. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuelekea “mahali pa siri” pa Yehova na “kivuli” chake katika nyakati hizi za hatari?

19 Tunaishi katika nyakati za hatari. Bila shaka, Shetani angetuangamiza sote ikiwa Yehova hangekuwa akitulinda kwa upendo. Kwa hiyo, ili kuepuka kunaswa na huyo “mwindaji wa ndege,” ni lazima tuendelee kukaa katika mahali pa ulinzi pa mfano, ‘mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi,’ na kujipatia “makao katika kivuli cha Mweza-Yote.”—Zaburi 91:1.

20 Acheni sikuzote tuone vikumbusho na mielekezo ya Yehova kuwa ulinzi wala si vizuizi. Sisi sote tunawindwa na mwindaji mwenye akili inayopita ya wanadamu. Bila msaada wenye upendo wa Yehova, hakuna atakayefanikiwa kuepuka kunaswa. (Zaburi 124:7, 8) Kwa hiyo, acheni tusali ili Yehova atukomboe kutoka katika mitego ya “mwindaji wa ndege”!—Mathayo 6:13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Desemba 1, 1982 (1/12/1982), ukurasa wa 3-7.

^ fu. 13 Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Desemba 1, 1983, ukurasa wa 23.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini “kutetemeshwa na wanadamu” ni mtego hatari?

• Ibilisi anatumia jinsi gani tamaa ya vitu vya kimwili?

• Shetani amewanasa namna gani watu fulani akitumia mtego wa burudani zisizofaa?

• Ibilisi anatumia mtego gani kuvuruga umoja wetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 27]

Watu fulani wamenaswa na mtego wa “kutetemeshwa na wanadamu”

[Picha katika ukurasa wa 28]

Je, unafurahia mambo ambayo Yehova anachukia?

[Picha katika ukurasa wa 29]

Unaweza kufanya nini ukiwa na tofauti za kibinafsi na Mkristo mwenzako?