Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Obadia, cha Yona, na cha Mika

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Obadia, cha Yona, na cha Mika

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Obadia, cha Yona, na cha Mika

“MAONO ya Obadia.” (Obadia 1) Huo ndio utangulizi wa kitabu cha Biblia cha Obadia. Katika kitabu alichoandika mwaka wa 607 K.W.K., nabii huyo hasemi lolote kuhusu maisha yake isipokuwa tu jina lake. Katika kitabu kilichokamilishwa zaidi ya karne mbili mapema, nabii Yona anaeleza waziwazi mambo yaliyompata kuhusiana na mgawo wake wa umishonari. Mika alitoa unabii katika kipindi cha miaka 60 kati ya siku za Obadia na Yona, kuanzia mwaka wa 777 K.W.K. hadi mwaka wa 717 K.W.K. Mika anasema tu kwamba yeye ni “wa [kijiji cha] Moreshethi” na kwamba neno la Yehova lilimjia “katika siku za Yothamu, Ahazi, Hezekia, wafalme wa Yuda.” (Mika 1:1) Mifano ambayo nabii huyo anatumia ili kukazia ujumbe wake inaonyesha wazi kwamba alijua vizuri maisha ya mashambani.

EDOMU ‘LITAKATILIWA MBALI MPAKA WAKATI USIO NA KIPIMO’

(Obadia 1-21)

Kuhusu Edomu, Obadia anasema: “Kwa sababu ya jeuri uliyomtendea ndugu yako Yakobo, aibu itakufunika, nawe utakatiliwa mbali mpaka wakati usio na kipimo.” Nabii huyo anakumbuka vizuri matendo ya karibuni ya jeuri ambayo Waedomu waliwatendea wana wa Yakobo, yaani, Waisraeli. Mwaka wa 607 K.W.K., Wababiloni walipoliharibu jiji la Yerusalemu, Waedomu ‘walisimama kando’ na kujiunga na “wageni” waliowavamia Waisraeli.—Obadia 10, 11.

Tofauti na hilo, nyumba ya Yakobo inangoja kurudishwa. Unabii wa Obadia unasema hivi: “Katika Mlima Sayuni ndipo watakapokuwa wale wanaoponyoka, nao utakuwa kitu kitakatifu.”—Obadia 17.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

5-8—Kulinganisha uharibifu wa Edomu na kuja kwa waporaji usiku na wakusanya-zabibu kunamaanisha nini? Ikiwa wezi wangeingia Edomu, wangechukua tu kile walichotaka. Ikiwa wavunaji wangekuja kwake, wangeacha mbegu fulani kwa ajili ya wale wanaookota masalio. Hata hivyo, Edomu linapoanguka, hazina zake zitatafutwa kwa makini na zitaporwa kabisa na ‘watu walewale walio katika agano pamoja naye,’ yaani, Wababiloni ambao ni washiriki wake.—Yeremia 49:9, 10.

10—Edomu ‘lilikatiliwa mbali mpaka wakati usio na kipimo’ jinsi gani? Kama ilivyotabiriwa, taifa la Edomu, ambalo lilikuwa taifa halisi lililokuwa na serikali na watu wanaoishi katika eneo hususa duniani, lilitoweka. Mfalme Nabonido wa Babiloni alishinda Edomu katikati ya karne ya 6 K.W.K. hivi. Kuanzia karne ya nne K.W.K., eneo la Edomu lilikaliwa na Wanabataea, na Waedomu walilazimika kubaki katika sehemu ya kusini ya Yudea, eneo la Negebu ambalo baadaye liliitwa Idumea. Baada ya Waroma kuliharibu jiji la Yerusalemu mwaka wa 70 W.K., Waedomu walitoweka kabisa.

Mambo Tunayojifunza:

3, 4Kwa kuwa waliishi katika eneo lenye milima mirefu na mabonde yenye kina ambayo yalizuia uwezo wa adui wa kupigana vita, huenda kwa kiburi Waedomu walijidanganya kwa kufikiri kwamba walikuwa salama. Lakini hukumu za Yehova haziepukiki.

8, 9, 15. Hekima na uwezo wa wanadamu hauwezi kuwalinda katika “siku ya Yehova.”—Yeremia 49:7, 22.

12-14. Waedomu ni mfano wenye kuonya kwa wale wanaoshangilia wakati watumishi wa Mungu wanapopatwa na matatizo. Yehova anaona kutendewa vibaya kwa watu wake kuwa jambo zito.

17-20. Unabii huo kuhusu kurudishwa kwa wana wa Yakobo ulianza kutimizwa wakati mabaki walipoanza kurudi Yerusalemu kutoka Babiloni mwaka wa 537 K.W.K. Sikuzote neno la Yehova linatimia. Tunaweza kuwa na hakika kabisa katika ahadi zake.

“NINAWI LITAANGAMIZWA”

(Yona 1:1–4:11)

Badala ya kutii amri ya Mungu ya ‘kwenda Ninawi lile jiji kubwa na kulitangazia’ ujumbe wa hukumu, Yona anakimbilia upande mwingine. Kwa kutokeza “upepo mkubwa baharini” na kwa kutumia “samaki mkubwa,” Yehova anamrudisha Yona na kumtuma kwa mara ya pili kwenye mji mkuu wa Waashuru.—Yona 1:2, 4, 17; 3:1, 2.

Yona anaingia Ninawi na kuanza kutangaza ujumbe huu ulio wazi: “Bado siku 40 tu, na Ninawi litaangamizwa.” (Yona 3:4) Matokeo yasiyotazamiwa ya kazi yake ya kuhubiri yanamfanya Yona ‘awake hasira.’ Yehova anatumia mmea wa “mtango” ili kumfundisha Yona kuwa mwenye rehema.—Yona 4:1, 6.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

3:3—Je, ni kweli kwamba ukubwa wa Ninawi ulikuwa kama “mwendo wa kutembea wa siku tatu”? Ndiyo. Katika nyakati za zamani, inaelekea kwamba Ninawi lilitia ndani maeneo mengine kuanzia Khorsabad huko kaskazini mpaka Nimrud upande wa kusini. Maeneo yote yaliyohusianishwa na Ninawi yalikuwa umbali wa kilomita 100 kuzunguka jiji hilo.

3:4—Je, Yona alihitaji kujifunza lugha ya Waashuru ili kuwahubiria Waninawi? Huenda Yona alikuwa tayari anaijua lugha ya Waashuru, au pengine alipokea kimuujiza uwezo wa kuizungumza. Inawezekana pia kwamba alitoa ujumbe wake moja kwa moja katika Kiebrania, halafu mtu fulani akautafsiri. Ikiwa mtu fulani aliutafsiri, maneno yake yangefanya watu wapendezwe na ujumbe wake.

Mambo Tunayojifunza:

1:1-3. Kupanga kimakusudi utendaji mwingine ili kuepuka kushiriki kikamilifu katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi ni ishara ya nia mbaya. Mtu anayefanya hivyo ni kana kwamba anakimbia mgawo aliopewa na Mungu.

1:12; 3:10. Yehova haonyeshi rehema zake kwa taifa au jamii moja tu au kwa kikundi fulani cha pekee. “Yehova ni mwema kwa wote, na rehema zake ziko juu ya kazi zake zote.”—Zaburi 145:9.

1:17; 2:10. Kipindi cha siku tatu mchana na usiku ambacho Yona alikaa ndani ya samaki mkubwa kinaonyesha kinabii kifo na ufufuo wa Yesu.—Mathayo 12:39, 40; 16:21.

1:17; 2:10; 4:6. Yehova alimwokoa Yona kutoka katika bahari iliyochafuka. Pia, Mungu ‘aliweka mtango, kwamba uje juu ya Yona, uwe kivuli juu ya kichwa chake, ili kumwokoa kutoka katika hali yake ya taabu.’ Leo, watumishi wa Yehova wanaweza kumtumaini Mungu wao na kutumaini fadhili zake zenye upendo, ili walindwe na kuokolewa.—Zaburi 13:5; 40:11.

2:1, 2, 9, 10. Yehova anasikiliza sala na maombi ya watumishi wake.—Zaburi 120:1; 130:1, 2.

3:8, 10. Mungu wa kweli ‘alijuta,’ au alibadili maoni yake kuhusu msiba ambao alikuwa amekusudia, naye “hakuuleta.” Kwa nini? Kwa sababu Waninawi “walikuwa wamegeuka kutoka katika njia yao mbaya.” Vivyo hivyo leo, Mungu anaweza kugeuza hukumu kali aliyokuwa amekusudia ikiwa mtenda-dhambi anaonyesha toba ya kweli.

4:1-4. Hakuna mwanadamu anayeweza kumzuia Mungu asionyeshe rehema Zake. Tunapaswa kuwa waangalifu ili tusichambue-chambue njia za Yehova za rehema.

4:11. Yehova anaongoza kwa subira kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme duniani pote kwa sababu, kama alivyowasikitikia watu 120,000 huko Ninawi, ndivyo anavyowasikitikia wale “wasiojua hata kidogo tofauti kati ya mkono wao wa kuume na wa kushoto.” Je, hatupaswi kuwasikitikia watu katika eneo letu na hivyo kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi?—2 Petro 3:9.

‘UPARA WAO UTAPANULIWA’

(Mika 1:1–7:20)

Mika anaonyesha wazi dhambi za Israeli na Yuda, anatabiri uharibifu wa miji yao mikuu, na anaahidi kwamba watarudishwa katika nchi zao. Samaria litakuwa “rundo la mabomoko ya shambani.” Kwa sababu ya ibada yao ya sanamu, nchi za Israeli na Yuda zinastahili “upara,” au aibu. Kwa kupelekwa utekwani, upara wao ungepanuliwa “kama ule wa tai.” Inaelekea tai huyo ni aina fulani ya ndege anayewinda ambaye ana nywele chache laini kwenye kichwa chake. Yehova anaahidi hivi: “Hakika nitamkusanya Yakobo.” (Mika 1:6, 16; 2:12) Kwa sababu ya viongozi wapotovu na manabii wa uwongo, jiji la Yerusalemu pia “litakuwa marundo ya mabomoko.” Lakini Yehova ‘atawakusanya watu wake pamoja.’ Na kutoka “Bethlehemu Efratha” kutatokea “yeye atakayekuwa mtawala katika Israeli.”—Mika 3:12; 4:12; 5:2.

Je, Yehova ametendea Israeli isivyo haki? Je, matakwa yake ni makali mno? Hapana. Yehova anawaomba tu waabudu wake ‘watende haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi’ katika kutembea pamoja na Mungu wao. (Mika 6:8) Hata hivyo, watu wanaoishi katika siku za Mika ni waovu hivi kwamba “mtu aliye bora zaidi kwao ni kama mchongoma, aliye mnyoofu zaidi kwao ni mbaya kuliko ukuta wa miiba,” akiumiza na kumtia uchungu mtu yeyote anayemkaribia. Lakini nabii anauliza hivi: “Ni nani aliye Mungu kama [Yehova]?” Mungu ataonyesha tena rehema kwa watu wake na ‘atazitupa dhambi zao zote katika vilindi vya bahari.’—Mika 7:4, 18, 19.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:12—Unabii kuhusu ‘kuwakusanya pamoja waliobaki wa Israeli’ ulitimia wakati gani? Ulitimia kwa mara ya kwanza mwaka wa 537 K.W.K. wakati mabaki ya Wayahudi waliporudi katika nchi yao kutoka uhamishoni huko Babiloni. Katika siku za kisasa, unabii huo unatimia kwa “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16) Tangu mwaka wa 1919, Wakristo watiwa-mafuta wamekusanywa pamoja “kama kundi zizini.” Wakiungwa mkono na “umati mkubwa” wa “kondoo wengine,” hasa tangu 1935, Wakristo watiwa-mafuta wamekuwa “na kelele za wanadamu.” (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Wote pamoja, wanaendeleza ibada ya kweli kwa bidii.

4:1-4 —“Katika siku za mwisho,” Yehova “atafanya hukumu kati ya vikundi vingi vya watu, na kunyoosha mambo kuhusu mataifa yenye nguvu” jinsi gani? Maneno “vikundi vingi vya watu” na “mataifa yenye nguvu” hayarejelei vikundi vya kitaifa au serikali za kisiasa. Badala yake, maneno hayo yanahusu watu mmoja-mmoja kutoka katika mataifa, ambao wamekuwa waabudu wa Yehova. Kwa njia ya kiroho, Yehova anahukumu na kunyoosha mambo kuwahusu.

Mambo Tunayojifunza:

1:6, 9; 3:12; 5:2. Samaria liliharibiwa na Waashuru mwaka wa 740 K.W.K., yaani, katika siku za Mika. (2 Wafalme 17:5, 6) Waashuru walikuja mpaka Yerusalemu wakati wa utawala wa Hezekia. (2 Wafalme 18:13) Jiji la Yerusalemu liliharibiwa na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K. (2 Mambo ya Nyakati 36:19) Kama ilivyotabiriwa, Masihi alizaliwa “Bethlehemu Efratha.” (Mathayo 2:3-6) Neno la Yehova la kinabii halikosi kamwe kutimia.

2:1, 2Ni hatari kama nini kudai kwamba tunamtumikia Mungu huku tukitafuta kwanza utajiri badala ya kuutafuta kwanza “ufalme na uadilifu wake.”—Mathayo 6:33; 1 Timotheo 6:9, 10.

3:1-3, 5Yehova anatazamia wale wanaoongoza miongoni mwa watu wake watende kwa haki.

3:4. Tukitaka Yehova ajibu sala zetu, hatupaswi kutenda dhambi au kuishi maisha maradufu.

3:8. Kazi yetu ya kuhubiri habari njema, ambayo inatia ndani ujumbe mbalimbali wa hukumu, inaweza kutimizwa ikiwa tu tunatiwa nguvu na roho takatifu ya Yehova.

5:5. Unabii huo wa Kimasihi unatuhakikishia kwamba watu wa Mungu wanaposhambuliwa na maadui wao, “wachungaji saba,” idadi inayowakilisha ukamili, na “watawala wadogo wanane,” idadi inayowakilisha kikundi cha wanaume wenye uwezo, wanatokezwa ili kuwaongoza watu wa Yehova.

5:7, 8Kwa watu wengi, Wakristo watiwa-mafuta leo ni “kama umande kutoka kwa Yehova,” baraka kutoka kwa Mungu. Inakuwa hivyo kwa sababu Mungu anatumia watiwa-mafuta ili kutangaza ujumbe wa Ufalme. “Kondoo wengine” wanasaidia kuwaburudisha watu kiroho kwa kuwaunga mkono kwa bidii watiwa-mafuta katika kazi ya kuhubiri. (Yohana 10:16) Ni pendeleo kama nini kushiriki katika kazi hiyo ambayo inawaburudisha wengine kikweli.

6:3, 4Tunapaswa kumwiga Yehova Mungu na kuwa wenye fadhili na huruma hata kuwaelekea wale ambao ni wagumu kushughulika nao au walio dhaifu kiroho.

7:7. Tunapopambana na matatizo mwishoni mwa mfumo huu mbovu wa mambo, hatupaswi kukata tamaa. Badala yake, kama Mika, tunahitaji ‘kuonyesha mtazamo wa kumngojea Mungu wetu.’

7:18, 19. Kwa kuwa Yehova yuko tayari kutusamehe makosa yetu, tunapaswa pia kuwa tayari kuwasamehe wale wanaotutendea dhambi.

Endelea ‘Kutembea Katika Jina la Yehova’

Wale wanaopigana na Mungu na watu wake ‘watakatiliwa mbali mpaka wakati usio na kipimo.’ (Obadia 10) Hata hivyo, Yehova anaweza kuigeuza hasira yake tukitii onyo lake na ‘kugeuka kutoka katika njia mbaya.’ (Yona 3:10) “Katika siku za mwisho,” yaani, ‘siku hizi za mwisho,’ ibada ya kweli imeinuliwa juu ya dini zote za uwongo na watu watiifu wanaelekezwa kwenye ibada ya kweli. (Mika 4:1; 2 Timotheo 3:1) Hivyo basi, na tuazimie ‘kutembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.’—Mika 4:5.

Vitabu vya Obadia, Yona, na Mika vinatufundisha masomo yenye thamani kama nini! Ingawa viliandikwa zaidi ya miaka 2,500 iliyopita, ujumbe wa vitabu hivyo ‘uko hai nao una nguvu,’ hata leo.—Waebrania 4:12.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Obadia alitabiri: ‘Edomu litakatiliwa mbali mpaka wakati usio na kipimo’

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mika ‘alionyesha mtazamo wa kumngojea Yehova,’ wewe pia unaweza kufanya vivyo hivyo

[Picha katika ukurasa wa 16]

Kazi ya kuhubiri ni pendeleo linalopaswa kuthaminiwa sana