Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kuwa na Maisha Yenye Kusudi!

Unaweza Kuwa na Maisha Yenye Kusudi!

Unaweza Kuwa na Maisha Yenye Kusudi!

WATU wengi wanaishi tu wakiwa na kusudi la kupata pesa na kununua vitu. Kusudi kuu katika maisha ya watu fulani ni kujitafutia umashuhuri ulimwenguni. Wengine wanaishi wakiwa na kusudi la kuwa wasanii bora kabisa. Pia, kuna wale ambao wanatumia maisha yao kuwasaidia wengine. Lakini wengi hawajui kwa nini wanaishi au kusudi la maisha ni nini.

Namna gani wewe? Je, umefikiria kwa uzito kuhusu kwa nini unaishi? Mbona usichunguze mambo fulani ambayo wanadamu wanafuatia ili uone kama kweli yanaleta uradhi na kusudi maishani? Ni nini kinachofanya maisha yawe yenye kusudi?

Raha na Pesa Zina Mahali Pake

Biblia inasema hivi katika Mhubiri 7:12: “Hekima ni ulinzi, kama vile pesa ni ulinzi; lakini faida ya ujuzi ni kwamba hekima huwahifadhi hai waliyo nayo.” Ndiyo, pesa zina faida. Unahitaji pesa ili uishi, hasa ikiwa una daraka la kuiandalia mahitaji familia yako.—1 Timotheo 5:8.

Maisha yangekuwa namna gani ikiwa hatungekuwa na starehe inayotokana na pesa? Ingawa Yesu Kristo, Mwanzilishi wa Ukristo, alikiri kwamba hakuwa na mahali pa kulaza kichwa chake, mara kwa mara alifurahia chakula kizuri na divai. Kwa kuongezea, alivaa vazi la bei ghali.—Mathayo 8:20; Yohana 2:1-11; 19:23, 24.

Hata hivyo, kusudi kuu katika maisha ya Yesu halikuwa kuponda raha. Alitanguliza miradi inayofaa. Yesu alisema: “Hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” Kisha akasimulia mfano wa mtu fulani tajiri ambaye alikusanya mazao mengi na kujiambia hivi: “Nitafanya nini, sasa kwa kuwa sina mahali popote pa kukusanya mazao yangu? . . . Nitabomoa maghala yangu na kujenga yaliyo makubwa zaidi, na humo nitakusanya nafaka yangu yote na vitu vyangu vyema vyote; nami nitaiambia nafsi yangu: ‘Nafsi yangu, una vitu vyema vingi vilivyokusanywa kwa miaka mingi; starehe, ule, unywe, na kujifurahisha.’” Kufikiri kwa mtu huyo kulikuwa na kasoro gani? Mfano huo unaendelea hivi: “Mungu akamwambia, ‘Wewe usiye na akili, usiku huu wanadai nafsi yako kutoka kwako. Basi, vitu ulivyoviweka akiba vitakuwa vya nani?’” Hata ikiwa mtu huyo alikuwa amehifadhi mazao yake, ikiwa angekufa hangeweza kufurahia utajiri ambao alikuwa amekusanya. Yesu alimalizia kwa kuwapa wasikilizaji wake somo hili: “Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.”—Luka 12:13-21.

Ndiyo, tunahitaji kiasi fulani cha pesa na starehe maishani. Hata hivyo, jambo la maana zaidi maishani si pesa wala raha. Kuwa tajiri kwa Mungu, yaani, kuishi kwa njia inayompendeza Mungu, ndilo jambo la maana zaidi la kufuatia.

Je, Kuwa Mashuhuri Ni Jambo la Maana?

Watu wengi wanajitafutia umashuhuri. Hakuna ubaya kutamani kuwa mashuhuri na kutaka kukumbukwa na wengine. Biblia inasema: “Jina ni bora kuliko mafuta mazuri, na siku ya kufa kuliko siku ya kuzaliwa kwa mtu.”—Mhubiri 7:1.

Ni kana kwamba rekodi ya maisha ya mtu inakuwa tayari imeandikwa siku ya kufa. Ikiwa amefanya mambo mazuri, siku yake ya kufa inakuwa nzuri kuliko siku yake ya kuzaliwa kwa kuwa anapozaliwa bado haijulikani ataishi maisha ya aina gani.

Mfalme Sulemani ndiye aliyeandika kitabu cha Biblia cha Mhubiri. Absalomu, ndugu mkubwa wa kambo wa Sulemani alitaka kujifanyia jina. Hata hivyo, watoto wake watatu wa kiume ambao wangetokeza vizazi vyake vya baadaye, walikufa wangali wachanga. Basi, Absalomu alifanya nini? Maandiko yanasema hivi: ‘Absalomu alikuwa amejisimamishia nguzo, ambayo ipo katika Nchi Tambarare ya Chini ya Mfalme, kwa maana alisema: “Sina mwana ili kuweka jina langu katika kumbukumbu.” Basi akaiita nguzo hiyo kwa jina lake mwenyewe.’ (2 Samweli 14:27; 18:18) Mabaki ya nguzo hiyo hayajapatikana. Wanafunzi wa Biblia wanajua kwamba Absalomu alijulikana kuwa mwasi ambaye alipanga njama ya kukinyakua kwa hila kiti cha ufalme cha Daudi, baba yake.

Watu wengi leo wanataka wakumbukwe kwa sababu ya mambo ambayo wametimiza. Wanataka watukuzwe na wanadamu wenye mapendezi yanayobadilika-badilika. Hata hivyo, ni nini kinachotukia kwa umashuhuri wa aina hiyo? Katika kitabu kimoja (The Culture of Narcissism), Christopher Lasch anaandika hivi: “Katika siku zetu, wakati ambapo mafanikio yanategemea kuonekana ukiwa kijana mwenye kuvutia, na kuwa tofauti na wengine, umashuhuri haudumu hata kidogo, na wale ambao wanasifiwa na watu wanaogopa daima kupoteza umashuhuri wao.” Ndiyo sababu watu wengi mashuhuri wanatumia dawa za kulevya na vileo, na mara nyingi wanakufa mapema. Kwa kweli, kutafuta umashuhuri ni jambo la ubatili.

Basi, tunapaswa kujitahidi kuwa na sifa nzuri machoni pa nani? Akizungumza kuhusu watu fulani ambao walishika Sheria yake, Yehova alisema hivi kupitia nabii wake Isaya: “Nitawapa ukumbusho na jina katika nyumba yangu na katika kuta zangu . . . Nitawapa jina mpaka wakati usio na kipimo, ambalo halitakatiliwa mbali.” (Isaya 56:4, 5) Kwa sababu ya kumtii Mungu, wale ambao wana kibali chake watakuwa na “ukumbusho na jina.” Mungu atakumbuka jina lao “mpaka wakati usio na kipimo” na hivyo hawatakatiliwa mbali. Biblia inatuhimiza tujifanyie jina kama hilo, sifa nzuri machoni pa Yehova, Muumba wetu.

Isaya alikuwa akitabiri kuhusu wakati ambapo watu waaminifu watapokea uzima wa milele katika Paradiso duniani. “Uzima wa milele” katika Paradiso hiyo ndio “uzima ulio wa kweli,” aina ya uzima ambao Mungu alikusudia wanadamu wawe nao alipowaumba. (1 Timotheo 6:12, 19) Badala ya kuishi maisha mafupi tu na yasiyoridhisha, je, hatupaswi kujitahidi kuufikia uzima wa milele?

Kufuatia Sanaa au Kutoa Misaada Hakuridhishi

Wasanii wengi wanatamani kuboresha ustadi wao ili wawe wasanii bora sana. Hawawezi kufikia lengo hilo katika maisha haya mafupi sana. Hideo, mchoraji aliyetajwa mwanzoni mwa habari iliyotangulia, alipokuwa na umri wa miaka 90 hivi, alijitahidi kuboresha ustadi wake wa kuchora. Hata wakati msanii anaporidhika na kazi yake, huenda asiweze tena kufanya kazi kama alivyofanya alipokuwa na umri mdogo na afya nzuri zaidi. Lakini namna gani kama angeishi milele? Wazia nafasi zote ambazo angekuwa nazo za kuboresha ustadi wake!

Tunaweza kusema nini kuhusu jitihada za kutoa misaada? Mtu anayewajali maskini na kutumia mali yake kuwasaidia wenye uhitaji anastahili kupongezwa. Biblia inasema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Kwa kweli, kuhangaikia mahitaji ya wengine kunaweza kuleta uradhi. Hata hivyo, mtu mmoja anaweza kutimiza nini, hata akitumia maisha yake yote katika kazi hiyo? Mambo ambayo tunaweza kufanya ili kupunguza mateso ya wengine yana mipaka. Hakuna kitu chochote cha kimwili kinachoweza kutosheleza uhitaji wa msingi ambao unapuuzwa na watu wengi na ambao hautoshelezwi kamwe katika maisha yao. Ni uhitaji gani huo?

Ni Lazima Uhitaji Fulani wa Asili Utoshelezwe

Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alitaja uhitaji wa msingi tuliozaliwa nao aliposema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mathayo 5:3) Basi, kulingana na Biblia, furaha ya kweli haitegemei utajiri, umashuhuri, kufuatia sanaa, au kuwasaidia maskini. Badala yake, inategemea kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho, uhitaji wa kumwabudu Mungu.

Mtume Paulo aliwahimiza wale ambao hawakumjua Muumba wamtafute. Paulo alisema hivi: “[Mungu] alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso wa dunia nzima, naye aliamuru nyakati na mipaka ya makao ya watu, ili wao wamtafute Mungu, ikiwa wangeweza kupapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate, ijapokuwa, kweli, hayuko mbali sana na kila mmoja wetu. Kwa maana kupitia kwake tuna uhai na tunaenda na kuwako.”—Matendo 17:26-28.

Siri ya kupata furaha ya kweli maishani ni kutosheleza uhitaji wa kumwabudu Mungu wa kweli. Kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho pia kunatupa tumaini la kupata “uzima ulio wa kweli.” Fikiria mfano wa Teresa. Alisifiwa sana katika televisheni nchini mwao kwa sababu ya kuwa mwigizaji wa kwanza Mmarekani mwenye asili ya Kiafrika kuigiza sehemu kubwa katika kipindi chake mwenyewe cha mfululizo cha saa moja. Hata hivyo, muda si muda, aliacha mambo hayo yote. Kwa nini? Alisema hivi: “Ninasadiki kwamba kutii mashauri ya Neno la Mungu ndiyo njia bora ya maisha.” Teresa hakutaka kuharibu uhusiano wake pamoja na Mungu kwa kushiriki katika kipindi cha mfululizo cha televisheni ambacho kilitukuza ngono na jeuri. Hakuonekana tena kwenye televisheni lakini alianza kuishi maisha yenye kuridhisha kikweli, kwa kuwa alitumika akiwa mhubiri wa wakati wote wa habari njema ya Ufalme wa Mungu, akijaribu kuwasaidia wengine kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu.

Kuhusu uamuzi wa Teresa wa kuacha kuigiza, mtu mmoja ambaye alishirikiana naye alinukuliwa akisema hivi: “Nilivunjika moyo kwa sababu nilichukizwa kumwona akitupilia mbali kazi yake yenye mafanikio. Lakini bila shaka alipata kitu kingine cha maana zaidi na bora zaidi.” Baadaye Teresa alikufa. Hata hivyo, baada ya kifo chake, mtu yuleyule aliyekuwa akishirikiana naye zamani alisema hivi: “Alikuwa na furaha, na hakuna jambo lingine tunalotaka maishani linalopita hilo. Ni wangapi kati yetu wanaokubaliana na maneno hayo?” Kwa wale ambao wanatanguliza uhusiano wao pamoja na Mungu maishani mwao lakini wanakufa, kuna tumaini zuri ajabu la ufufuo chini ya utawala wa Ufalme.—Yohana 5:28, 29.

Muumba ana kusudi kwa ajili ya dunia na wanadamu. Anataka uelewe kusudi hilo na ufurahie uzima wa milele katika Paradiso duniani. (Zaburi 37:10, 11, 29) Huu ndio wakati wa kujifunza mengi kumhusu Yehova, Muumba wa mbingu na dunia, na kujifunza kuhusu kusudi lake kwa ajili yako. Mashahidi wa Yehova wa eneo lenu watafurahi kukusaidia kupata ujuzi huo. Tafadhali wasiliana nao, au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kufikiri kwa yule mtu tajiri katika mfano wa Yesu kulikuwa na kasoro gani?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, ungependa kufurahia uzima wa milele katika Paradiso duniani?