Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vigae vya Kale Vinaunga Mkono Masimulizi ya Biblia

Vigae vya Kale Vinaunga Mkono Masimulizi ya Biblia

Vigae vya Kale Vinaunga Mkono Masimulizi ya Biblia

BIBLIA ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (2 Timotheo 3:16) Yale ambayo inasema kuhusu watu, maeneo, na hali za kidini na za kisiasa za nyakati za kale ni sahihi. Kutumainika kwa Biblia hakutegemei hata kidogo vitu vya kale vilivyochimbuliwa. Hata hivyo, vitu hivyo vinaunga mkono au kutusaidia kuelewa zaidi masimulizi ya Biblia.

Vigae, yaani, vipande vya vyombo vya udongo, ndivyo vitu vingi zaidi kati ya vitu vya kale vilivyochimbuliwa katika maeneo ya kale. Vipande hivyo vya vyombo vya udongo vilitumiwa kama vitu vya kuandikia vya gharama ya chini katika maeneo mengi huko Mashariki ya Kati, kutia ndani Misri na Mesopotamia. Vigae vilitumiwa kuandikia mikataba, hesabu, mauzo, na kadhalika, kama vile karatasi zinavyotumiwa leo. Kwa kawaida, watu walitumia wino kuandika habari kwenye vigae, na habari iliyoandikwa ingeweza kuwa neno moja tu au mistari mingi ya maneno.

Vigae vingi vya nyakati za Biblia vimechimbuliwa huko Israel. Vikundi vitatu vya vigae vya kuanzia karne ya saba na ya nane K.W.K., vinatupendeza sana kwa sababu vinaunga mkono mambo fulani katika masimulizi ya kihistoria ya Biblia. Hivyo ni vigae vya Samaria, vigae vya Aradi, na vigae vya Lakishi. Acheni tuchunguze zaidi vikundi hivyo vitatu vya vigae.

Vigae vya Samaria

Jiji la Samaria lilikuwa mji mkuu wa ufalme wa kaskazini wa makabila kumi ya Israeli hadi jiji hilo lilipopinduliwa na Waashuru mwaka wa 740 K.W.K. Andiko la 1 Wafalme 16:23, 24 linasema hivi kuhusu mwanzo wa jiji la Samaria: “Katika mwaka wa 31 wa Asa mfalme wa Yuda [947 K.W.K.], Omri akawa mfalme juu ya Israeli . . . Naye akanunua mlima wa Samaria kutoka kwa Shemeri kwa talanta mbili za fedha, naye akaanza kujenga juu ya huo mlima na kuita jina la jiji alilolijenga Samaria.” Jiji hilo lilikuwapo hata wakati wa enzi ya Roma, jina lake lilipobadilishwa na kuwa Sebaste. Mwishowe lilitoweka katika karne ya sita W.K.

Eneo la Samaria la kale lilipochimbuliwa mwaka wa 1910, wataalamu wa vitu vya kale vilivyochimbuliwa walipata vigae ambavyo walisema ni vya kuanzia karne ya nane K.W.K. Vigae hivyo vilikuwa na maandishi kuhusu shehena za mafuta na divai iliyoingizwa Samaria kutoka maeneo ya karibu. Kikizungumzia ugunduzi huo, kitabu kimoja (Ancient Inscriptions—Voices From the Biblical World) kinasema: ‘Vigae 63 vilivyopatikana mnamo 1910 vinaonwa ifaavyo kuwa kikundi muhimu zaidi cha maandishi yaliyopo ya Israeli la kale. Umuhimu huo hautegemei vigae vya Samaria vyenyewe bali unategemea orodha yake ndefu ya majina ya kibinafsi ya Waisraeli, majina ya ukoo, na ya maeneo.’ Majina hayo yanaunga mkono jinsi gani masimulizi ya Biblia?

Waisraeli walipoitwaa Nchi ya Ahadi na kuigawanya kati ya makabila yao, Samaria lilikuwa katika eneo la kabila la Manase. Kulingana na Yoshua 17:1-6, vikundi kumi vya ukoo wa Manase, kupitia mjukuu wake Gileadi, vilipewa mashamba katika eneo hilo. Vikundi hivyo vilikuwa ukoo wa Abiezeri, wa Heleki, wa Asrieli, wa Shekemu, na wa Shemida. Mwanamume wa sita, Heferi, hakuwa na wajukuu wa kiume lakini alikuwa na wajukuu watano wa kike—Mala, Noa, Hogla, Milka, na Tirsa—na kila mmoja wao alipewa shamba.—Hesabu 27:1-7.

Vigae vya Samaria vilikuwa na majina saba kati ya majina hayo ya ukoo—majina yote matano ya wana wa Gileadi na majina mawili ya binti za Heferi, yaani, Hogla na Noa. Biblia moja (NIV Archaeological Study Bible) inasema kwamba “mbali na Biblia, majina hayo ya ukoo kwenye vigae vya Samaria yanahusianisha vikundi vya ukoo wa Manase na maeneo ambayo Biblia inasema walimiliki.” Hivyo, masimulizi ya historia ya mapema ya makabila ya Israeli yaliyo katika Biblia yanaungwa mkono na vigae hivyo.

Pia, inaonekana kwamba vigae vya Samaria vinaunga mkono masimulizi kuhusu hali ya kidini ya Waisraeli kama inavyoelezwa katika Biblia. Vigae hivyo vya Samaria vilipokuwa vikiandikwa, Waisraeli walikuwa wakichanganya ibada ya Yehova na ile ya mungu wa Wakanaani aliyeitwa Baali. Unabii wa Hosea, ambao uliandikwa katika karne ya nane K.W.K., ulitabiri wakati ambapo Waisraeli waliotubu wangemwita Yehova “Mume wangu,” wala hawangemwita tena “Baali wangu,” au “Mmiliki wangu.” (Hosea 2:16, 17) Baadhi ya majina ya kibinafsi kwenye vigae vya Samaria yalimaanisha “Baali ni baba yangu,” “Baali anaimba,” “Baali ni mwenye nguvu,” “Baali anakumbuka,” na kadhalika. Kati ya kila majina  11 yaliyo na sehemu ya jina Yehova, kuna majina saba yaliyo na sehemu ya jina “Baali.”

Vigae vya Aradi

Aradi lilikuwa jiji la kale lililokuwa katika eneo kame lililoitwa Negebu, kusini mwa Yerusalemu. Eneo la Aradi lilipochimbuliwa kulipatikana ngome sita za Waisraeli zilizofuatana tangu wakati wa ufalme wa Sulemani (1037-998 K.W.K.) mpaka Yerusalemu lilipoharibiwa na Wababiloni katika 607 K.W.K. Huko Aradi, wachimbuaji walipata vigae vingi zaidi vya tangu nyakati za Biblia. Vigae hivyo vinatia ndani vipande zaidi ya 200 vyenye maandishi ya Kiebrania, ya Kiaramu, na ya lugha nyinginezo.

Baadhi ya vigae vya Aradi vinaunga mkono masimulizi ya Biblia kuhusu familia za kikuhani. Kwa mfano, kigae kimoja kinawataja “wana wa Kora” wanaotajwa katika Kutoka 6: 24 na Hesabu 26:11. Utangulizi wa Zaburi 42, 44-49, 84, 85, 87, na 88 unasema waziwazi kuwa zaburi hizo zilitungwa na “wana wa Kora.” Familia nyingine za kikuhani zinazotajwa na vigae vya Aradi ni zile za Pashuri na Meremothi.—1 Mambo ya Nyakati 9:12; Ezra 8:33.

Fikiria mfano mwingine. Katika magofu ya ngome inayosemwa kuwa ya kipindi kilichotangulia tu kuharibiwa kwa Yerusalemu na Wababiloni, wachimbuaji walipata kigae alichoandikiwa kamanda wa ngome. Kichapo fulani (The Context of Scripture) kinasema hivi kwa sehemu: “Kwa bwana wangu Elyashib. Yahweh [Yehova] na ahangaikie hali njema yako. . . . Kuhusu mambo uliyoniagiza: kila jambo liko sawa sasa: anakaa katika nyumba ya Yahweh.” Wasomi wengi wanaamini kwamba hekalu linalozungumziwa ni hekalu la Yerusalemu, ambalo lilijengwa kwanza katika siku za Sulemani.

Vigae vya Lakishi

Lakishi, jiji la kale lenye ngome, lilikuwa kilomita 43 kusini-magharibi ya Yerusalemu. Katika shughuli za uchimbuaji za mwaka wa 1930, vigae kadhaa vilipatikana, na vigae 12 kati ya hivyo vinasemwa kuwa barua “muhimu sana . . . katika kuelezea hali ya kisiasa na msukosuko uliokuwepo Yuda lilipokuwa likijitayarisha kwa shambulizi lisiloepukika la Nebukadneza [Mfalme wa Babiloni].”

Barua zilizo muhimu zaidi ni zile ambazo ofisa fulani wa cheo cha chini na Yaoshi waliandikiana. Inaelekea kwamba Yaoshi alikuwa mmoja wa wakuu wa jeshi huko Lakishi. Lugha inayotumiwa katika barua hizo inafanana na ile ya nabii Yeremia ambaye aliishi katika kipindi hichohicho. Chunguza jinsi barua mbili kati ya hizo zinavyounga mkono masimulizi ya Biblia kuhusu kipindi hicho muhimu.

Katika Yeremia 34:7, nabii huyo anaeleza kuhusu “majeshi ya mfalme wa Babiloni yalipokuwa yakipiga vita juu ya Yerusalemu na juu ya majiji yote ya Yuda ambayo yalikuwa yamebaki, juu ya Lakishi na juu ya Azeka; kwa maana hayo, majiji yenye ngome, ndiyo yaliyobaki kati ya majiji ya Yuda.” Inaonekana kwamba mwandishi wa mojawapo ya Barua za Lakishi anazungumzia matukio hayohayo. Anaandika hivi: “Tunatazama ishara za [moto] za Lakishi . . . , kwa kuwa hatuwezi kuona Azeqah.” Wasomi wengi wanaamini kwamba hilo linaonyesha kwamba Azeqah, au Azeka, lilikuwa limeshindwa na Wababiloni na kwamba Lakishi lingefuata. Maneno “ishara za moto” katika barua hiyo yanapendeza. Yeremia 6:1 linataja pia kwamba ishara ya moto ilitumiwa kama njia ya mawasiliano.

Inaaminika kwamba Barua nyingine ya Lakishi inaunga mkono yale ambayo nabii Yeremia na Ezekieli wanasema kuhusu jitihada za mfalme wa Yuda za kutafuta utegemezo wa Misri katika uasi dhidi ya Babiloni. (Yeremia 37:5-8; 46:25, 26; Ezekieli 17:15-17) Barua hiyo ya Lakishi inasema hivi: “Sasa mtumishi wako amepata habari ifuatayo: Jemadari Konyahu mwana wa Elnatan amesonga kusini ili kuingia Misri.” Wasomi wengi wanakubaliana kwamba hatua hiyo ilikuwa jitihada ya kutafuta msaada wa kijeshi kutoka Misri.

Vigae vya Lakishi vinataja pia majina kadhaa yanayopatikana katika kitabu cha Yeremia. Majina hayo ni Neria, Yaazania, Gemaria, Elnathani, na Hoshaya. (Yeremia 32:12; 35:3; 36:10, 12; 42:1) Ni vigumu kuwa na uhakika ikiwa majina hayo yanarejelea watu walewale. Lakini kwa kuwa Yeremia aliishi katika kipindi hichohicho kuna ufanani mkubwa.

Ufanani Kati ya Vigae Hivyo Vyote

Vigae vya Samaria, vya Aradi, na vya Lakishi, vinaunga mkono mambo fulani yanayosimuliwa katika Biblia. Mambo hayo yanatia ndani majina ya familia, majina ya maeneo, na pia mambo yanayohusu hali ya kidini na ya kisiasa ya nyakati hizo. Hata hivyo, kuna ufanani fulani kati ya vigae hivyo vyote.

Barua zilizopatikana huko Aradi na Lakishi zina maneno kama vile “Yehova na akuombee amani.” Katika jumbe saba za Lakishi, jina la Mungu linatajwa mara 11. Zaidi ya hilo, majina mengi ya Kiebrania ya watu binafsi yaliyo katika vigae hivyo vyote yana sehemu za jina Yehova. Kwa hiyo, vigae hivyo vinathibitisha kwamba katika nyakati hizo, Waisraeli walitumia jina la Mungu kwa ukawaida.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kigae kutoka katika magofu ya Aradi ambacho mtu anayeitwa Elyashib aliandikiwa

[Hisani]

Photograph © Israel Museum, Jerusalem; courtesy of Israel Antiquities Authority

[Picha katika ukurasa wa 14]

Barua ya Lakishi iliyo na jina la Mungu

[Hisani]

Photograph taken by courtesy of the British Museum