Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yale Anayotabiri Yehova Yanatimia

Yale Anayotabiri Yehova Yanatimia

Yale Anayotabiri Yehova Yanatimia

“MIMI ni Mungu wala hakuna Mungu mwingine, wala yeyote kama mimi; Yeye anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.” (Isaya 46:9, 10) Hivyo ndivyo anavyosema Yehova, yule anayeweza kutabiri wakati ujao bila kukosea.

Inajulikana kwamba mwanadamu hana uwezo wa kutabiri wakati ujao kwa usahihi. Uhakika wa kwamba Biblia ni kitabu cha unabii unapaswa kuwachochea wote wanaotafuta kweli wachunguze madai yake ya kwamba ilitungwa na Mungu. Acheni basi tuchunguze unabii mbalimbali ambao tayari umetimia.

Mataifa ya Kale

Mungu alitabiri kwamba Babiloni lingeharibiwa milele na kwamba mataifa ya Edomu, Moabu, na Amoni pia yangeharibiwa milele. (Yeremia 48:42; 49:17, 18; 51:24-26; Obadia 8, 18; Sefania 2:8, 9) Kutoweka kwa mataifa hayo kunathibitisha usahihi wa Neno la Mungu la kinabii.

Bila shaka, huenda mtu akabisha kwamba mtu yeyote anaweza kutabiri kuwa taifa fulani, hata likiwa na nguvu kadiri gani, litatoweka. Lakini hoja hiyo inapuuza uhakika ulio muhimu kwamba Biblia ilitoa habari zaidi. Kwa mfano, ilitoa habari zaidi kuhusu namna jiji la Babiloni lingeangushwa. Biblia ilitabiri kwamba jiji hilo lingeharibiwa na Wamedi, kwamba askari-jeshi wavamizi wangekuwa chini ya uongozi wa Koreshi, na kwamba mito iliyozunguka jiji hilo na kulipa ulinzi ingekauka.—Isaya 13:17-19; 44:27–45:1.

Biblia haikutabiri kwamba watu au mataifa yote yaliyoshindwa yangetoweka milele. Kinyume na hilo, akitabiri kuhusu kuharibiwa kwa Yerusalemu na Wababiloni, Mungu alisema kwamba wakaaji wa jiji hilo wangerudishwa, ingawa Wababiloni hawakuwa na zoea la kuwaachilia huru mateka wao. (Yeremia 24:4-7; 29:10; 30:18, 19) Hilo lilitimia, na wazao wa Wayahudi wanaendelea kuishi wakiwa taifa mpaka leo.

Zaidi ya hayo, Yehova alitabiri kwamba Misri ambayo ilikuwa serikali kuu ya ulimwengu ingepinduliwa lakini ‘baadaye watu wangekaa ndani yake kama katika siku za zamani za kale.’ Baada ya muda, serikali hiyo ya kale ‘ingekuwa ufalme wa hali ya chini.’ (Yeremia 46:25, 26; Ezekieli 29:14, 15) Hilo pia lilitimia. Zaidi ya hilo, Yehova alitabiri kwamba serikali ya Ugiriki ambayo pia ilikuwa serikali kuu ya ulimwengu ingepinduliwa, lakini hakusema kamwe kwamba taifa hilo lingetoweka. Tunajifunza nini kuhusu kutoweka kwa mataifa ambayo Yehova alitabiri kwamba yangetoweka na kuendelea kuwapo kwa mataifa ambayo hakutabiri kuwa yangetoweka? Kwamba Neno la Mungu lina unabii wa kweli na wenye kutegemeka.

Mambo Yenye Kushangaza

Kama ilivyotajwa hapo juu, Yehova alitoa habari nyingi kuhusu namna Babiloni lingeangushwa. Vivyo hivyo, kilipotabiri kuhusu kuanguka kwa Tiro, kitabu cha Ezekieli kilisema kwamba mawe, mbao, na mavumbi yake yangewekwa “katikati ya maji.” (Ezekieli 26:4, 5, 12) Unabii huo ulitimia mwaka wa 332 K.W.K. Aleksanda Mkuu alipoamuru majeshi yake yatumie vifusi kutoka katika magofu ya jiji la Tiro lililokuwa barani na kutengeneza njia hadi kwenye jiji la Tiro lililokuwa kisiwani na kuliharibu jiji hilo pia.

Pia, unabii wa Danieli 8:5-8, 21, 22 na 11:3, 4 unatoa habari zenye kustaajabisha kuhusu “mfalme wa Ugiriki” aliyekuwa mkuu isivyo kawaida. Mfalme huyo angeuawa akiwa katika upeo wa mamlaka yake, na ufalme wake ungegawanywa mara nne lakini si kati ya wazao wake. Zaidi ya miaka 200 baada ya unabii huo kuandikwa, Aleksanda Mkuu alithibitika kuwa mfalme huyo mwenye nguvu. Historia ya ulimwengu inatueleza kwamba alikufa kifo cha mapema na kwamba milki yake iligawanywa kati ya majenerali wake wanne, wala si kati ya wazao wake.

Wachambuzi wamedai kwamba unabii huo uliandikwa baada ya tukio hilo. Hata hivyo, chunguza tena masimulizi ya kitabu cha Danieli yaliyotajwa hapo juu. Yanapoonwa kuwa unabii, mambo yanayotajwa humo ni yenye kushangaza. Lakini yanapoonwa kuwa historia inayodaiwa kuwa unabii, je, huoni kwamba masimulizi hayo hayana habari nyingi muhimu? Ikiwa mdanganyifu fulani aliyeishi baada ya Aleksanda alikuwa akijaribu kuwavutia wasomaji kwa masimulizi yanayodaiwa kuwa unabii, kwa nini hakueleza kwamba punde tu baada ya kifo cha Aleksanda, wawili kati ya wana wake wangejaribu kusimamisha ufalme wao lakini wangeuawa? Kwa nini hakutaja kwamba miaka mingi ingepita kabla ya majenerali wote wanne kuimarisha mamlaka yao katika maeneo mbalimbali ya milki ya Aleksanda? Kwa kweli, kwa nini hakutaja majina ya mfalme mkuu na ya majenerali wake wanne?

Madai ya kwamba unabii wa Biblia uliandikwa baada ya matukio ni madai ambayo yameshikiliwa kwa muda mrefu lakini hayajathibitishwa. Madai hayo yametolewa na wale ambao kabla ya kuchunguza uthibitisho wamekata kauli kwamba haiwezekani kutabiri matukio ya wakati ujao. Kwa sababu wanakataa kukubali Biblia kuwa Neno la Mungu, wanalazimika kueleza mambo yote kulingana tu na maoni ya kibinadamu. Hata hivyo, Mungu alitoa kwa hekima habari za kutosha za unabii ili kuthibitisha kwamba yeye ndiye mtungaji wa Biblia. *

Unabii wa Biblia unaweza kuitia nguvu imani yako ikiwa unatumia wakati kutafakari kuhusu unabii mbalimbali hususa na jinsi ulivyotimia. Kwa nini usichunguze unabii wa Biblia? Chati kwenye ukurasa wa 343 mpaka 346 wa kitabu “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa” zinaweza kukusaidia. * Ukifuata dokezo hilo, chunguza unabii ukiwa na kusudi la kuijenga imani yako. Usisome haraka-haraka ili tu kumaliza habari unayosoma. Badala yake, tafakari kuhusu uhakika wa kwamba jambo lolote ambalo Yehova anatabiri linatimia bila kukosea.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Kwa habari zaidi zinazokanusha madai ya kwamba unabii wa Biblia uliandikwa baada ya matukio, ona ukurasa wa 106-111 wa kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 14 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]

KANUNI ZINAZOFAA MAISHANI

Ona jambo lingine la kutafakari. Mungu ambaye alitabiri kwa usahihi kutokea na kuanguka kwa serikali kuu za ulimwengu, ndiye Aliyetoa kanuni za Biblia zinazofaa maishani. Baadhi ya kanuni hizo ni:

Unavuna kile unachopanda.Wagalatia 6:7.

Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.Matendo 20:35.

Furaha inategemea kutosheleza mahitaji ya kiroho.Mathayo 5:3.

Ukitumia kanuni hizo maishani, unaweza kuwa na hakika kwamba zitakuletea furaha na mafanikio.

[Picha katika ukurasa wa 22, 23]

Neno la Mungu lilitabiri kutoweka kabisa kwa mataifa haya . . .

EDOMU

BABILONI

. . . lakini si kutoweka kwa

UGIRIKI

MISRI

[Hisani]

Pictorial Archive (Near Eastern History) Est.

WHO photo by Edouard Boubat

[Picha katika ukurasa wa 23]

Aleksanda Mkuu