Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alitetea Ibada Safi

Alitetea Ibada Safi

Igeni Imani Yao

Alitetea Ibada Safi

ELIYA aliutazama umati ulipokuwa ukipanda polepole Mlima Karmeli. Ijapokuwa ilikuwa asubuhi na mapema, na hakukuwa na mwangaza wa kutosha, umaskini na uhitaji wa watu ulionekana waziwazi. Hali yao ilizorota sana kwa sababu ya miaka mitatu na nusu ya ukame.

Kati yao manabii 450 wa Baali walitembea kwa majivuno, wakiwa wamejaa kiburi na wakiwa na chuki kali kumwelekea Eliya, nabii wa Yehova. Malkia Yezebeli alikuwa amewaua watumishi wengi wa Yehova, hata hivyo, mwanamume huyo bado alikuwa akipinga ibada ya Baali kwa uthabiti. Lakini angeendelea kufanya hivyo kwa muda gani? Huenda makuhani hao walifikiri kwamba mtu mmoja hangeweza kamwe kuwashinda. (1 Wafalme 18:3, 19, 20) Mfalme Ahabu pia alikuwa amekuja kwa gari lake la kifalme. Yeye pia hakumpenda Eliya.

Siku hiyo ingekuwa ya pekee sana maishani mwa nabii huyo aliyekuwa peke yake. Eliya alitazama mambo yalipokuwa yakipangwa kwa ajili ya mapambano yenye kustaajabisha zaidi kati ya wema na uovu, mapambano ambayo hayajawahi kamwe kuonekana ulimwenguni. Eliya alihisi namna gani siku ilipozidi kupambazuka? Alikuwa na woga kwa kuwa alikuwa “mtu mwenye hisia kama zetu.” (Yakobo 5:17) Tunaweza kuwa na hakika kuhusu angalau jambo moja: Akiwa amezungukwa na watu wasio na imani, mfalme wao aliyeasi imani, na makuhani wauaji, Eliya alijihisi akiwa peke yake kabisa.—1 Wafalme 18:22.

Hata hivyo, ni nini kilichowaingiza Waisraeli katika hali hiyo hatari? Na simulizi hili linakuhusu namna gani leo? Biblia inatuhimiza tuwaangalie sana watumishi waliojitoa kwa Mungu na ‘kuiga imani yao.’ (Waebrania 13:7) Sasa fikiria mfano wa Eliya.

Mapambano ya Muda Mrefu Yanafikia Upeo

Kwa muda mrefu, Eliya alitazama jambo bora zaidi katika taifa lake na nchi yao likipuuzwa na kukanyagwa-kanyagwa, naye hakuwa na uwezo wa kuchukua hatua. Waisraeli walikuwa katika mapambano ya muda mrefu, vita kati ya ibada safi na ibada ya uwongo, kati ya ibada ya Yehova Mungu na ibada ya sanamu za mataifa yaliyowazunguka. Katika siku za Eliya, mapambano hayo yalikuwa makali zaidi.

Mfalme Ahabu alikuwa amemwoa Yezebeli, binti ya mfalme wa Sidoni. Yezebeli aliazimia kueneza ibada ya Baali katika nchi ya Israeli na kuifagilia mbali ibada ya Yehova. Ahabu alikubali haraka uvutano wa Yezebeli. Alijenga hekalu na madhabahu kwa Baali naye akaongoza katika kumwinamia mungu huyo wa kipagani. Alimchukiza sana Yehova.—1 Wafalme 16:30-33. *

Kwa nini ibada ya Baali ilichukiza sana? Ni kwa sababu iliwashawishi Waisraeli na kuwageuzia wengi mbali na Mungu wa kweli. Pia, ilikuwa dini yenye upotovu na ukatili. Ilihusisha makahaba wa kiume na wa kike wa hekaluni, sherehe za ngono, na hata kuwatoa dhabihu watoto. Yehova alichukua hatua kwa kumtuma Eliya akamwambie Ahabu kwamba kutakuwa na ukame hadi nabii wa Mungu atakapotangaza mwisho wa ukame. (1 Wafalme 17:1) Miaka kadhaa ilipita kabla Eliya hajajitokeza mbele ya Ahabu na kumwambia awakusanye watu pamoja na manabii wa Baali kwenye Mlima Karmeli.

Lakini, mapambano hayo yana maana gani kwetu leo? Kwa kuwa hatuzungukwi na mahekalu na madhabahu ya Baali, huenda watu fulani wakafikiri kwamba hadithi kuhusu ibada ya Baali haituhusu leo. Lakini simulizi hili si historia ya zamani tu. (Waroma 15:4) Neno “Baali” linamaanisha “mmiliki” au “bwana.” Yehova aliwaambia watu wake kwamba wanapaswa kumchagua kuwa “baali” wao, au mume wao. (Isaya 54:5) Je, hukubali kwamba bado watu wanatumikia mabwana mbalimbali badala ya Mungu Mweza-Yote? Iwe watu wanatumia maisha yao kufuatia pesa, kazi, burudani, raha ya ngono, au kutumikia yoyote kati ya miungu mingi sana inayoabudiwa leo badala ya Yehova, kwa kweli wanamchagua bwana fulani. (Mathayo 6:24; Waroma 6:16) Hivyo, kwa njia fulani, sehemu muhimu zaidi za ibada ya kale ya Baali zinasitawi leo. Mapambano hayo ya zamani kati ya Yehova na Baali yanaweza kutusaidia kuchagua kwa hekima yule tutakayemtumikia.

‘Kuyumba-Yumba’—Jinsi Gani?

Mtu akiwa kwenye kilele chenye upepo mkali cha Mlima Karmeli, anaweza kuona vizuri sana eneo la Israeli—kuanzia bonde la Mto la Kishoni kushuka kwenye Bahari Kuu (Bahari ya Mediterania) iliyo karibu, mpaka milima ya Lebanoni upande wa mbali wa kaskazini. * Lakini jua lilipoinuka siku hiyo ya pekee, nchi ilikuwa katika hali mbaya sana. Nchi yenye rutuba ambayo Yehova alikuwa amewapa wazao wa Abrahamu ilikuwa imezorota. Sasa nchi hiyo ilikuwa imepigwa na jua kali na kuharibika kwa sababu ya upumbavu wa watu wa Mungu! Watu hao walipokusanyika, Eliya aliwakaribia na kusema: “Mtayumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti mpaka wakati gani? Ikiwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, mfuateni yeye; lakini ikiwa ni Baali, mfuateni yeye.”—1 Wafalme 18:21.

Eliya alimaanisha nini aliposema kuhusu ‘kuyumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti’? Watu hao hawakutambua kwamba wanapaswa kuchagua kati ya ibada ya Yehova na ibada ya Baali. Walifikiri wangeweza kushiriki ibada zote mbili, yaani, kumfurahisha Baali kwa desturi zao zenye kuchukiza na bado waombe baraka kutoka kwa Yehova Mungu. Huenda walifikiri kwamba Baali angebariki mimea na mifugo yao, huku “Yehova wa majeshi” akiwalinda vitani. (1 Samweli 17:45) Walikuwa wamesahau kweli fulani ya msingi—kweli ambayo wengi leo hawatambui—kwamba Yehova hakubali ibada yake ichanganywe na ibada ya miungu mingine. Anataka na anastahili ujitoaji kamili. Kuchanganya ibada yake na ya miungu mingine ni jambo lisilokubalika machoni pake na hata linamchukiza!—Kutoka 20:5.

Hivyo, Waisraeli hao walikuwa ‘wakiyumba-yumba’ kama mtu anayejaribu kufuata barabara mbili tofauti wakati uleule. Leo watu wengi wanafanya kosa hilohilo, wakiruhusu “mabaali” wengine wawe sehemu ya maisha yao, na kuweka kando ibada ya Mungu wa kweli! Mwito wa Eliya ulio wazi kuhusu kuacha kuyumba-yumba unaweza kutusaidia kuchunguza tena mambo tunayotanguliza maishani mwetu na ibada yetu.

Jaribu la Kukata Maneno

Kisha Eliya akapendekeza wafanye jaribu fulani. Lilikuwa jaribu rahisi sana. Makuhani wa Baali walipaswa kujenga madhabahu na kuweka dhabihu juu yake; kisha wamwombe mungu wao aiteketeze dhabihu hiyo kwa moto. Eliya angefanya vivyo hivyo pia. Alisema hivi: “Yule Mungu wa kweli atakayejibu kupitia moto, huyo ndiye Mungu wa kweli.” Eliya alijua vema ni nani aliyekuwa Mungu wa kweli. Alikuwa na imani yenye nguvu sana hivi kwamba hakusita kuwaruhusu manabii hao wa Baali wawe wa kwanza katika jaribu hilo. Aliwaruhusu wapinzani wake wafanye chochote walichotaka, wajichagulie ng’ombe-dume kwa ajili ya dhabihu, na wawe wa kwanza kumwomba Baali. *1 Wafalme 18:24, 25.

Leo hakuna miujiza. Hata hivyo, Yehova hajabadilika. Na tuwe na uhakika katika Yehova kama Eliya alivyokuwa. Kwa mfano, wengine wakipinga yale ambayo Biblia inafundisha, hatupaswi kuogopa kuwaacha wajieleze. Kama Eliya, tunaweza kumtegemea Mungu wa kweli ashughulikie hali hiyo. Hatufanyi hivyo kwa kujitegemea wenyewe, bali kwa kutegemea Neno lake lililoongozwa kwa roho, ambalo limekusudiwa “kunyoosha mambo.”—2 Timotheo 3:16.

Manabii wa Baali walitayarisha dhabihu yao na kumwita mungu wao. Walirudia-rudia kupaaza sauti hivi: “Ee Baali, tupe jibu!” Walizidi kufanya hivyo kadiri wakati ulivyosonga. “Lakini hapakuwa na sauti yoyote, wala hakuna yeyote aliyetoa jibu,” Biblia inasema. Ilipofika katikati ya mchana, Eliya akaanza kuwadhihaki na kuwatania kwamba hapana shaka Baali ana shughuli nyingi asiweze kuwajibu, ameenda chooni, au amelala na hivyo anapaswa kuamshwa. “Iteni kwa sauti kubwa,” Eliya anawahimiza wadanganyifu hao. Ni wazi kwamba aliiona ibada ya Baali kuwa ya udanganyifu na inayostahili kudhihakiwa, naye alitaka watu wa Mungu waone udanganyifu huo.—1 Wafalme 18:26, 27.

Kwa sababu hiyo, makuhani wa Baali wakawa na wazimu hata zaidi, “wakaanza kuita kwa sauti yao yote, wakijikatakata kwa visu na mikuki kulingana na desturi yao, mpaka walipojitiririsha damu.” Lakini jitihada zao hazikufanikiwa! “Hapakuwa na sauti yoyote, wala hapakuwa na yeyote aliyejibu, wala aliyewasikiliza.” (1 Wafalme 18:28, 29) Kwa kweli, Baali hakuwepo. Wazo la Baali lilianzishwa na Shetani ili kuwageuzia watu mbali na Yehova. Leo, kama zamani, mtu akimchagua bwana mwingine badala ya Yehova atavunjika moyo na hata kuaibika.—Zaburi 25:3; 115:4-8.

Jibu Lapatikana

Baadaye jioni ilipofika, zamu ya Eliya ikafika. Alirekebisha madhabahu ya Yehova ambayo hapana shaka ilikuwa imebomolewa na maadui wa ibada safi. Huenda alitumia mawe 12 ili kuwakumbusha wengi katika taifa la Israeli lenye makabila 10 kwamba bado walipaswa kutii ile Sheria ambayo makabila yote 12 yalipewa. Kisha, akaweka dhabihu yake kwenye madhabahu na kulowesha kabisa dhabihu na madhabahu hiyo kwa maji, ambayo labda yaliyotolewa katika Bahari ya Mediterania iliyokuwa karibu. Hata alichimba mtaro kuzunguka madhabahu hiyo na kuujaza maji. Alirahisisha mambo sana kwa manabii wa Baali, lakini akafanya jaribu la Yehova liwe gumu iwezekanavyo—alimtumaini sana Mungu wake.—1 Wafalme 18:30-35.

Mambo yote yalipokuwa tayari Eliya alitoa sala. Ilikuwa sala fupi yenye ufasaha, nayo ilionyesha wazi mambo ambayo Eliya alitanguliza. Kwanza kabisa, alitaka watu wajue kwamba Yehova ndiye “Mungu katika Israeli” wala si Baali. Pili, alitaka kila mtu ajue kwamba yeye ni mtumishi wa Yehova; sifa na utukufu wote ni wa Mungu. Na mwisho, alionyesha kwamba bado anawajali watu wake, kwa sababu alitamani sana kumwona Yehova akigeuza “moyo wao urudi.” (1 Wafalme 18:36, 37) Eliya aliwapenda hata ingawa walikuwa wamejiletea taabu kubwa kwa kukosa kuwa waaminifu. Tunapotoa sala, je, sisi pia tunaweza kuhangaikia jina la Mungu, kuwa wanyenyekevu, na kuwahurumia wengine?

Kabla Eliya hajaomba, huenda umati ulijiuliza ikiwa Yehova angethibitika kuwa mdanganyifu kama Baali alivyokuwa. Hata hivyo, jibu lilipatikana mara tu baada ya sala hiyo. Simulizi hilo linasema hivi: “Ndipo moto wa Yehova ukashuka, ukala lile toleo la kuteketezwa na zile kuni na mawe na mavumbi, nao ukaramba maji yaliyokuwa katika mtaro.” (1 Wafalme 18:38) Hilo lilikuwa jibu la ajabu kama nini! Nao watu waliitikia namna gani?

“Yehova ndiye Mungu wa kweli! Yehova ndiye Mungu wa kweli!” wote wakapaaza sauti. (1 Wafalme 18:39) Mwishowe walijua ukweli. Hata hivyo, hawakuwa wameonyesha imani yao. Kwa kweli, kukubali Yehova ndiye Mungu wa kweli baada ya kuona akijibu sala hiyo kwa kushusha moto kutoka mbinguni hakukuthibitisha waziwazi kwamba wana imani. Hivyo, Eliya aliwataka waonyeshe imani yao kwa kufanya jambo fulani. Aliwaambia wafanye jambo ambalo walipaswa kufanya miaka mingi mapema—kutii Sheria ya Yehova. Sheria ya Mungu ilisema kwamba manabii wa uwongo na waabudu-sanamu walipaswa kuuawa. (Kumbukumbu la Torati 13:5-9) Makuhani hao wa Baali walikuwa maadui sugu wa Yehova Mungu na walipinga makusudi yake kimakusudi. Je, walistahili kuonyeshwa rehema? Jiulize, je, watoto wasio na hatia ambao waliteketezwa wakiwa hai na kutolewa dhabihu kwa Baali walionyeshwa rehema yoyote? (Methali 21:13; Yeremia 19:5) Kwa kweli, makuhani hao hawakustahili kuonyeshwa rehema hata kidogo. Hivyo, Eliya aliagiza wauawe, na kwa kweli wakauawa.—1 Wafalme 18:40.

Wachambuzi fulani leo wanapinga hatua hiyo ya mwisho ambayo Eliya alichukua katika Mlima Karmeli. Wengine wanaogopa kwamba wanadini wenye msimamo mkali wanaweza kutumia kisa hicho kutetea matendo ya kikatili yanayosababishwa na chuki ya kidini. Na inasikitisha kwamba kuna wanadini wengi wajeuri wenye msimamo mkali. Hata hivyo, Eliya hakuwa mtu mwenye msimamo mkali. Alitenda kupatana na agizo la Yehova la kutekeleza hukumu ya haki. Zaidi ya hilo, Wakristo wa kweli wanajua hawawezi kufuata mfano wa Eliya na kuwaua watu waovu. Tangu Masihi alipotokea, wanafunzi wote wa Yesu wanapaswa kufuata kiwango kinachopatikana katika maneno ambayo Kristo alimwambia Petro: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52) Wakati ujao, Yehova atamtumia Mwana wake kutekeleza haki ya kimungu.

Wajibu wa Mkristo wa kweli ni kuishi kupatana na imani. (Yohana 3:16) Njia moja ya kufanya hivyo ni kuwaiga wanaume waaminifu kama Eliya. Eliya alimwabudu Yehova kikamili na akawahimiza wengine wafanye vivyo hivyo. Alifunua kwa ujasiri udanganyifu wa dini ambayo Shetani alitumia kuwageuzia watu mbali na Yehova. Na badala ya kufanya alivyotaka na kutegemea uwezo wake mwenyewe, Eliya alimtegemea Yehova ashughulikie mambo. Bila shaka, Eliya aliitetea ibada safi. Kila mmoja wetu na aige imani ya Eliya!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Kwa habari zaidi kuhusu shughuli za mapema kati ya Eliya na Ahabu, ona makala “Je! Wewe Una Imani Kama Ile ya Eliya?” katika Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1992 (1/4/1992).

^ fu. 13 Kwa kawaida Mlima Karmeli huwa na mimea mingi ya kijani, kwa sababu pepo zenye mvuke kutoka baharini zinapanda juu ya mabonde yake na hivyo kutokeza mvua na umande kwa ukawaida. Kwa kuwa Baali alionwa kuwa ndiye anayeleta mvua, mlima huo ulikuwa kituo muhimu cha ibada ya Baali. Mlima Karmeli ambao ulikuwa umekauka kwa sababu ya ukame ulikuwa mahali panapofaa zaidi pa kufunua ibada ya Baali kuwa ya udanganyifu.

^ fu. 17 Inapendeza kwamba Eliya aliwaambia: “Msiwashe moto” ili kuteketeza dhabihu. Wasomi fulani wanasema kwamba nyakati nyingine waabudu hao wa sanamu walitumia madhabahu yaliyokuwa na mwanya uliofichika chini ya madhabahu ili ionekane kana kwamba moto uliwashwa kimuujiza.

[Blabu katika ukurasa wa 20]

Mtu akimchagua bwana mwingine badala ya Yehova atavunjika moyo

[Picha katika ukurasa wa 21]

“Yehova ndiye Mungu wa kweli!”