Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Kusudi la Maisha?

Ni Nini Kusudi la Maisha?

Ni Nini Kusudi la Maisha?

KWA NINI JIBU LA SWALI HILO NI LA MAANA? Ni mambo machache sana yanayomhangaisha mwanadamu kama wazo la kwamba maisha hayana maana wala kusudi. Kwa upande mwingine, mtu ambaye ana kusudi halisi maishani anavumilia matatizo mengi. Viktor E. Frankl, mtaalamu wa mishipa ambaye aliokoka Maangamizi Makubwa, aliandika hivi: “Hakuna kitu chochote ulimwenguni ambacho ninaweza kusema kinaweza kumsaidia sana mtu kuokoka hata hali mbaya zaidi, kama kujua kwamba maisha yake yana kusudi.”

Lakini kuna maoni mengi yanayopingana kuhusu jambo hilo. Wengi wanahisi kwamba mtu mwenyewe ndiye anayepaswa kujiamulia kusudi la maisha yake. Kinyume chake, wengine wanaoamini mageuzi wanafundisha kwamba maisha hayana kusudi lolote.

Hata hivyo, kwa kweli njia nzuri zaidi ya kujua kusudi la maisha ni kujifunza kutoka kwa Yehova Mungu ambaye ni Mpaji-Uhai. Fikiria yale ambayo Neno lake linasema kuhusu jambo hilo.

Yale Ambayo Biblia Inasema

Biblia inafundisha kwamba Yehova Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke ili watimize kusudi fulani. Yehova aliwapa wazazi wetu wa kwanza amri ifuatayo.

Mwanzo 1:28. “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.”

Mungu alikusudia Adamu na Hawa na watoto wao waifanye dunia yote kuwa paradiso. Hakukusudia wanadamu wazeeke na kufa; wala hakutaka wanadamu wayaharibu mazingira. Hata hivyo, tumerithi dhambi na kifo kwa sababu ya maamuzi mabaya ambayo wazazi wetu wa kwanza walifanya. (Mwanzo 3:2-6; Waroma 5:12) Lakini, kusudi la Yehova halijabadilika. Hivi karibuni dunia itakuwa paradiso.—Isaya 55:10, 11.

Yehova alituumba tukiwa na uwezo wa kimwili na kiakili wa kutimiza kusudi lake. Hakutuumba ili tuishi bila kumtegemea. Ona jinsi kusudi la Mungu kwa ajili yetu linavyoelezwa na maandiko yafuatayo ya Biblia.

Mhubiri 12:13. “Huu ndio mwisho wa mambo, kila jambo limekwisha sikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”

Mika 6:8. “Yehova anataka ni kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?”

Mathayo 22:37-39. “‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza. Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’”

Jinsi Jibu la Biblia Linavyoleta Amani ya Kweli ya Akili

Ili mashini yoyote ya hali ya juu ifanye kazi vizuri, ni lazima itumiwe kwa kusudi na kwa njia ambayo mtengenezaji alikusudia. Vivyo hivyo, ili tuepuke kujiumiza wenyewe kiroho, kiakili, kihisia, au kimwili, tunahitaji kutumia maisha yetu kwa njia ambayo Mtengenezaji wetu alikusudia. Fikiria jinsi kujua kusudi la Mungu kunavyoweza kutuletea amani ya akili katika mambo yafuatayo maishani.

Wanapochagua mambo ya kutanguliza, watu wengi leo wanatumia maisha yao kukusanya mali. Hata hivyo, Biblia inaonya hivi: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru.”—1 Timotheo 6:9, 10.

Kwa upande mwingine, wale wanaojifunza kumpenda Mungu badala ya pesa wanagundua siri ya kutosheka. (1 Timotheo 6:7, 8) Wanaelewa umuhimu wa kufanya kazi kwa bidii na wanajua kwamba wana wajibu wa kutosheleza mahitaji yao ya kimwili. (Waefeso 4:28) Lakini pia wanachukua kwa uzito onyo hili la Yesu: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda yule mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau yule mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.”—Mathayo 6:24.

Kwa hiyo, badala ya kutanguliza kazi ya kimwili au utafutaji wa mali maishani, wale wanaompenda Mungu wanaona kufanya mapenzi yake kuwa jambo kuu zaidi maishani mwao. Wanajua kwamba wakitanguliza mapenzi ya Mungu maishani, Yehova Mungu atawatunza. Kwa kweli, Yehova anaona kwamba ana wajibu wa kuwatunza.—Mathayo 6:25-33.

Wanaposhughulika na wengine, watu wengi wanajitanguliza. Leo, ulimwengu hauna amani, hasa kwa sababu watu wengi sana wamekuwa “wenye kujipenda wenyewe, . . .  wasio na upendo wa asili.”  (2  Timotheo 3:2,  3) Mtu fulani anapowaudhi au kukataa maoni yao, wanamwaga “hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano.” (Waefeso 4:31) Kutojizuia kama huko “huchochea ugomvi” tu badala ya kuleta amani ya akili.— Methali  15:18.

Kinyume chake, wale wanaotii amri ya Mungu ya kumpenda jirani yao kama wanavyojipenda ni ‘wenye fadhili wao kwa wao, wenye huruma nyororo, wanasameheana kwa hiari.’ (Waefeso 4:32; Wakolosai 3:13) Hata wengine wanapowatendea kwa njia isiyo ya fadhili, wanajitahidi kumwiga Yesu, ambaye alipokuwa akitukanwa “hakujibu kwa matukano.” (1 Petro 2:23) Kama Yesu, wanaelewa kwamba kuwatumikia wengine kunaleta uradhi, hata kuwatumikia wale ambao hawathamini mambo wanayofanyiwa. (Mathayo 20:25-28; Yohana 13:14, 15; Matendo 20:35) Yehova Mungu anawapa roho yake wale wanaomwiga Mwana wake, na roho hiyo inatokeza amani ya kweli katika maisha yao.—Wagalatia 5:22.

Hata hivyo, maoni yako kuhusu wakati ujao yanaweza kuwa na matokeo gani kwa amani yako ya akili?

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Mtu anahitaji kuwa na kusudi la wazi maishani

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu anatufundisha jinsi ya kupata amani ya akili