Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Kitakachotokea Wakati Ujao?

Ni Nini Kitakachotokea Wakati Ujao?

Ni Nini Kitakachotokea Wakati Ujao?

KWA NINI JIBU LA SWALI HILO NI LA MAANA? Matarajio ya mtu ya wakati ujao yanaweza kuongoza jinsi anavyotenda leo. Kwa mfano, wale ambao hawana tumaini la wakati ujao wanaweza kuwa na mtazamo huu: “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:32) Mara nyingi mtazamo kama huo hauleti amani ya kweli ya akili, badala yake unawafanya watu wawe walafi, wanywe kupindukia, na wahangaike.

Kwa kweli, ikiwa wanadamu wangeachiwa kabisa daraka la kujiamulia kuhusu wakati ujao, hatungekuwa na tumaini lolote. Hewa, maji, na udongo wa dunia unachafuliwa kuliko wakati mwingine wowote. Tishio la vita vya nyuklia na mashambulizi ya kigaidi yanaongezeka. Mabilioni ya watu ulimwenguni pote ni wagonjwa na maskini. Hata hivyo, tuna sababu nzuri za kuwa na tumaini.

Ingawa wanadamu hawawezi kutabiri kwa usahihi wakati ujao, Yehova Mungu anasema yeye ndiye “anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.” (Isaya 46:10) Yehova anasema nini kuhusu kitakachotukia wakati ujao?

Yale Ambayo Biblia Inasema

Yehova hataruhusu dunia iharibiwe kabisa au uhai uliomo uangamizwe. Kwa kweli, Biblia inaahidi kwamba Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Kupitia Ufalme wake, au serikali yake ya kimbingu, Yehova ataondoa kabisa uovu duniani na hali ziwe kama alivyokusudia mwanzoni. (Mwanzo 1:26-31; 2:8, 9; Mathayo 6:9, 10) Mistari inayofuata ya Biblia inatusaidia kuelewa wakati ujao. Inaeleza matukio ambayo hivi karibuni yatamgusa kila mtu duniani.

Zaburi 46:8, 9. “Njooni, tazameni matendo ya Yehova, jinsi ambavyo ameweka matukio ya kushangaza duniani. Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mkuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza motoni.”

Isaya 35:5, 6. “Wakati huo macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Wakati huo kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha. Kwa maana maji yatakuwa yamebubujika katika nyika, na mito katika nchi tambarare ya jangwani.”

Isaya 65:21, 22. “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale.”

Danieli 2:44. “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”

Yohana 5:28, 29. “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka.”

Ufunuo 21:3, 4. “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”

Jinsi Jibu la Biblia Linavyoleta Amani ya Kweli ya Akili

Mwanzoni, huenda mtu akafikiri kwamba hali zinazoelezwa katika maandiko hayo ni ndoto tu. Lakini Mungu ndiye anayetoa ahadi hizo, si wanadamu. Na Yehova Mungu ‘hawezi kusema uwongo.’—Tito 1:2.

Ukijifunza kutegemea ahadi za Mungu na kuishi kupatana na sheria zake, utakuwa na amani ya akili hata ukikabili hali ngumu zaidi. Vita, umaskini, magonjwa, kifo, na hata matatizo ya uzee hayawezi kukunyang’anya kabisa amani yako. Kwa nini? Kwa sababu una hakika kwamba Ufalme wa Mungu utaondoa kabisa madhara ya matatizo hayo yote.

Unaweza jinsi gani kuwa na tumaini kama hilo la wakati ujao? Ni lazima ‘ufanye upya akili yako’ na kujihakikishia mwenyewe “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Waroma 12:2) Inaelekea kwamba utahitaji uthibitisho zaidi wa kwamba ahadi za Biblia zinategemeka. Utafaidika ukijitahidi kuchunguza uthibitisho huo. Ni mambo machache sana maishani ambayo yanaweza kukuletea amani nyingi ya akili kuliko jambo hilo.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Neno la Mungu linasema nini kuhusu wakati ujao?

Isaya 35:5

Isaya 35:6

Yohana 5:28, 29