Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Bahari ya kuyeyushwa katika hekalu la Sulemani ilikuwa na ukubwa gani?

Simulizi la 1 Wafalme 7:26 linasema kwamba bahari hiyo ilichukua “vipimo elfu mbili vya bathi” vya maji ambayo yalitumiwa na makuhani, huku simulizi linalofanana na hilo katika 2 Mambo ya Nyakati 4:5 likisema kwamba ilichukua “vipimo elfu tatu vya bathi.” Hilo limefanya watu fulani wadai kwamba simulizi la Mambo ya Nyakati lina kasoro iliyosababishwa na waandishi.

Hata hivyo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatusaidia kuelewa jinsi tunavyoweza kupatanisha masimulizi hayo mawili. Tunasoma hivi katika Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 7:26: “Ingeweza kuchukua vipimo elfu mbili vya bathi.” Ona kwamba 2 Mambo ya Nyakati 4:5 linasema: “Ikiwa kitu cha kuhifadhia, ingeweza kuchukua vipimo elfu tatu vya bathi.” Hivyo, 2 Mambo ya Nyakati 4:5 linazungumzia kiasi kamili cha maji ambacho kingeweza kuhifadhiwa humo, huku 1 Wafalme 7:26 likitaja kiasi cha maji ambayo kwa kawaida yalitiwa katika beseni la hekalu. Kwa maneno mengine, bahari hiyo haikujazwa kabisa. Inaonekana kwamba kwa kawaida walijaza theluthi mbili, yaani, sehemu mbili za tatu za bahari hiyo.

Kwa nini Yesu na Petro walilipa kodi ya hekalu wakitumia sarafu moja tu?

Katika siku za Yesu, kila mwanamume Myahudi aliyekuwa na umri wa miaka zaidi ya 20 alipaswa kulipa drakma mbili kama kodi ya kila mwaka ya hekalu. Kiasi hicho kililingana na mshahara wa siku mbili hivi. Swali lilipozushwa kuhusu kulipa kodi hiyo, Yesu alimwagiza Petro hivi: “Nenda baharini, utupe ndoano, na kuchukua samaki wa kwanza atakayetokea, ukifungue kinywa chake, nawe utapata sarafu ya stateri. Ichukue na uwape kwa ajili yangu na kwa ajili yako.”—Mathayo 17:24-27.

Wasomi wengi wanaamini kwamba kwa kweli sarafu ya stateri inayotajwa hapo ilikuwa tetradrakma. Sarafu hiyo ilikuwa na thamani ya drakma nne, au ililingana na malipo ya kodi ya hekalu ya watu wawili. Tetradrakma hiyo ilikuwa ya kawaida sana na ilipatikana kwa urahisi kuliko didrakma. Hivyo, kamusi fulani (The New Bible Dictionary) inasema hivi: “Inaelekea kwamba kwa kawaida Wayahudi wawili-wawili waliungana na kulipa kodi ya Hekalu pamoja.”

Zaidi ya hilo, mtu yeyote ambaye angetaka kulipa kodi ya mtu mmoja tu angetozwa malipo ya kubadilisha pesa yaliyoitwa agio. Malipo hayo yangefikia hata asilimia 8. Hata hivyo, watu wawili ambao wangelipa kodi hiyo pamoja hawangetozwa malipo hayo. Hivyo, hata katika jambo hilo dogo, simulizi la Mathayo linapatana na mambo yanayojulikana kuhusu mazoea ya watu katika siku za Yesu.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Picha kubwa ya tetradrakma