Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumhusu Mungu wa Kweli

Kumhusu Mungu wa Kweli

Tunayojifunza Kutoka Kwa Yesu

Kumhusu Mungu wa Kweli

Je, Mungu ana jina?

Yesu alifundisha kwamba Mungu ana jina. Yesu alisema hivi: “Basi, ninyi msali hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.’” (Mathayo 6:9) Biblia inafunua kwamba jina la Mungu ni Yehova. (Zaburi 83:18) Akizungumza kuhusu wanafunzi wake, Yesu alimwambia Baba yake hivi katika sala: “Nimewajulisha jina lako.”—Yohana 17:26.

Yehova ni nani?

Yesu alimwita Yehova “Mungu wa pekee wa kweli” kwa sababu Yehova ndiye Muumba. (Yohana 17:3) Yesu alisema: “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke?” (Mathayo 19:4) Yesu alisema hivi pia: “Mungu ni roho.” (Yohana 4:24) Hivyo, hatuwezi kumwona Mungu.—Kutoka 33:17-20.

Mungu anataka tufanye nini?

Mtu fulani alipomuuliza Yesu ni amri gani iliyo kuu zaidi, alijibu hivi: “Ya kwanza ni hii, ‘Sikia, Ee Israeli, Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja, nawe lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote. Ya pili ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’”—Marko 12:28-31.

Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunampenda Mungu?

Yesu alisema: “Ninampenda Baba.” Alionyesha upendo wake kwa njia gani? “Kama vile Baba amenipa amri kufanya,” akasema, “ndivyo ninavyofanya.” (Yohana 14:31) Pia alisema hivi: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.” (Yohana 8:29) Tunaweza kumpendeza Mungu kwa kujifunza kumhusu. Akisali kwa ajili ya wanafunzi wake, Yesu alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli.”—Yohana 17:3; 1 Timotheo 2:4.

Tunaweza kujifunza kumhusu Mungu kwa njia gani?

Njia moja ya kujifunza kumhusu Mungu ni kuchunguza vitu alivyoumba. Kwa mfano, Yesu alisema: “Waangalieni kwa makini ndege wa mbinguni, kwa sababu hawapandi mbegu au kuvuna au kukusanya ghalani; na bado Baba yenu wa mbinguni huwalisha wao. Je, ninyi si bora kuliko wao?” Yesu alimaanisha nini? Alimaanisha kwamba hatupaswi kuruhusu mahangaiko kuhusu mahitaji yetu ya kimwili yatuzuie kumtumikia Mungu.—Mathayo 6:26-33.

Njia bora zaidi ya kumjua Yehova ni kujifunza Neno lake, Biblia. Yesu aliyaita Maandiko “neno la Mungu.” (Luka 8:21) Yesu alimwambia Mungu hivi: “Neno lako ni kweli.”—Yohana 17:17; 2 Petro 1:20, 21.

Yesu aliwasaidia watu kujifunza kweli kumhusu Yehova. Mmoja wa wanafunzi wa Yesu alisema hivi kumhusu: “Je, mioyo yetu haikuwa ikiwaka alipokuwa akisema nasi barabarani, alipokuwa akitufungulia Maandiko?” (Luka 24:32) Ili kujifunza kumhusu Mungu, ni lazima tuwe wanyenyekevu na tukubali kufundishwa. Yesu alisema: “Msipogeuka na kuwa kama watoto wachanga, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.”—Mathayo 18:3.

Kwa nini ujuzi juu ya Mungu unaleta furaha?

Mungu anatosheleza uhitaji wetu wa kujifunza kuhusu kusudi la maisha. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Yehova anatufundisha njia bora ya maisha. “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!” akasema Yesu.—Luka 11:28; Isaya 11:9.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 1 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 16]

“Nimewajulisha jina lako.”—Yohana 17:26

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Tunaweza kujifunza kumhusu Yehova kupitia uumbaji na Biblia