Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ujenzi Unaomletea Yehova Sifa

Ujenzi Unaomletea Yehova Sifa

Ujenzi Unaomletea Yehova Sifa

“Siamini macho yangu. Sikuwahi kamwe kufikiri kwamba tungekuwa na mahali maridadi sana kama hapa pa kukutania na kumtukuza Yehova. Huwezi kamwe kununua shangwe ninayohisi!”—MARIA, MEXICO.

MASHAHIDI WA YEHOVA wanapenda kukutana ili kujifunza Neno la Mungu, Biblia. (Zaburi 27:4; Waebrania 10:23-25) Na wanafurahia hasa kufanya hivyo wanapoweza kukutania mahali penye kuheshimika pa ibada. Katika miaka ya karibuni, katika nchi nyingi ulimwenguni wamejenga maelfu ya majengo mapya ya ibada yanayoitwa Majumba ya Ufalme.

Kwa nini majengo hayo yote yanajengwa? Ni nani wanaofanya kazi hiyo? Na kazi hiyo ya ujenzi ina uvutano gani juu ya watu wanaoifanya? Ili kupata majibu ya maswali hayo, fikiria yale ambayo yamekuwa yakifanyika huko Mexico na Belize.

Maelfu ya Majumba Mapya ya Ufalme Yanahitajiwa!

Katika miaka ya nyuma, Mashahidi wa Yehova huko Mexico walikusanyika kwa ajili ya ibada mahali popote pale—nyuma ya nyumba, katika nyumba za Mashahidi, mabohari, mabanda ya kuegeshea magari, au majumba ya kukodi. Wakati huo, mara nyingi Mashahidi hao washikamanifu waliona ingefaa sana wajenge Majumba yao wenyewe ya Ufalme.

Kufikia 1994, kulikuwa na Mashahidi 388,000 huko Mexico. Uchunguzi uliofanywa mwaka huo ulionyesha kwamba ili Mashahidi wote wawe na mahali pao wenyewe pa ibada, wangehitaji kujenga Majumba ya Ufalme 3,300. Hiyo ingekuwa kazi kubwa kama nini!

Wakati huo, makutaniko fulani yaliyokuwa na uwezo yalikuwa yakijijengea yenyewe Majumba ya Ufalme. Lakini katika miaka mitano iliyofuata, ilikuwa wazi kwamba ili kutimiza uhitaji wa Majumba ya Ufalme tunapaswa kujenga majumba zaidi—na kuyajenga haraka zaidi. Uhitaji huo unatimizwa jinsi gani?

Vikundi Vinavyosafiri vya Wafanyakazi wa Kujitolea Wenye Ustadi

Katika mwaka wa 1999 mpango mpya wa ujenzi ulianzishwa. Vikundi vya Ujenzi wa Majumba ya Ufalme vilianza kuundwa kotekote nchini Mexico. Mashahidi wa Yehova kutoka sehemu zote nchini, wengi wao wakiwa na ustadi wa ujenzi, walijitolea kushiriki katika mpango huo wenye kusisimua. Wakati huu, Mexico ina vikundi 35 kama hivyo, na kikundi kimoja kimeundwa huko Belize.

Kwa kawaida, kila Kikundi cha Ujenzi wa Majumba ya Ufalme kina wafanyakazi wanane hivi, wanaume na wanawake ambao ni wafanyakazi wa wakati wote wasiolipwa. Vikundi hivyo vyenye furaha vya wajitoleaji vinahama kutoka eneo moja hadi lingine nchini kote ili kuongoza katika miradi ya ujenzi. Kila mjitoleaji anafanya kazi kwa muda wa saa nane kila siku kuanzia Jumatatu (Siku ya 1) mpaka Ijumaa (Siku ya 5) na pia Jumamosi kadhaa (Siku ya Posho). Siku inaanza saa moja asubuhi kwa mazungumzo ya andiko la Biblia, na baadaye kunakuwa na kiamsha-kinywa. Wote wako tayari kufanya kwa bidii kazi yoyote wanayopewa. Kwa mfano, wanawake wanafanya kazi ileile pamoja na wanaume, kazi kama vile kupiga lipu au plasta, kuezeka, na kupaka rangi.

Makutaniko yanasaidia kwa kuandaa mahali pa kulala, kufua nguo, na kupika chakula kwa ajili ya wajitoleaji hao wanaosafiri. Zaidi ya kufanya kazi pamoja katika ujenzi wa jumba, wajitoleaji hao na Mashahidi wenyeji wanafurahia kushirikiana katika mikutano ya Kikristo na kuhubiri nyumba kwa nyumba.

Baraka za Kuwa Mfanyakazi wa Kujitolea

Wajitoleaji hao wana maoni gani kuhusu kazi wanayofanya? “Ni kweli kwamba tunafanya kazi katika hali ya joto na baridi, tunakula chakula ambacho hatukuzoea, tunahama mara nyingi, tunaishi mbali na familia zetu, na mara nyingi hatuna vitu vya kisasa,” anasema Daniel, ambaye amefanya kazi ya kujitolea kwa zaidi ya miaka mitatu. Anaongezea hivi: “Lakini matatizo hayo si kitu yakilinganishwa na baraka ambazo tunapata.”

Wanapata baraka gani? Wafanyakazi wengi wa kujitolea wanajifunza ustadi mpya wa ujenzi. Lakini mfanyakazi mmoja anayeitwa Carlos, anayesimamia mojawapo ya vikundi vikubwa zaidi, anasema yale anayoona kuwa yenye faida kubwa zaidi. Anasema hivi: “Tumekuwa kama familia ya watu 20. Tunakula pamoja, tunafanya kazi pamoja, tunajifunza pamoja, tunasali pamoja. Tumekuwa na uhusiano wa karibu sana.”

Pia, vikundi vya ujenzi vinajenga uhusiano wa karibu sana pamoja na makutaniko ambayo vinasaidia. José, ambaye ameshiriki katika miradi zaidi ya 100 ya ujenzi, anasema: “Inapendeza sana kuona machozi ya shangwe na tabasamu za uthamini za Mashahidi wenyeji wanapoona ndoto zao za kuwa na Jumba jipya la Ufalme zikitimia.” Anaongeza: “Tunafurahi kujua kwamba imani ya wengine inatiwa nguvu hata tunapotimiza sehemu ndogo katika kufanikisha ujenzi wa nyumba nyingine ya ibada safi.”

Kazi ya Ajabu Imetimizwa!

Majengo hayo ya ibada si ya kifahari. Badala yake, Majumba ya Ufalme ni majengo ya kawaida tu, na hivyo inawezekana kuyajenga haraka na kwa gharama ndogo. Inapowezekana majengo hayo yanajengwa kwa vifaa na ufundi unaotumiwa katika eneo linalohusika. Kwa hivyo, jumba linaweza kujengwa hata kwa muda wa majuma sita tu!

Kufikia mwaka wa 2007, makutaniko yote huko Belize yalikuwa na Jumba jipya la Ufalme. Kwa ujumla, majumba 17 yalijengwa. Huko Mexico, zaidi ya majumba 1,400 yamejengwa tangu mwaka wa 1999!

Ingawa kazi nyingi nzuri imetimizwa, bado kuna mengi ya kufanya. (Mathayo 9:37) Hesabu ya Mashahidi huko Mexico imeongezeka kufikia zaidi ya 600,000, na wote hao wanakutanika mara tatu kwa juma ili kufundishwa Neno la Mungu. Kwa hiyo, majumba mapya karibu 2,000 bado yanahitajiwa. Ikiwa kazi hiyo ya kujitolea kujenga ingetegemea tu jitihada za wanadamu, ingekuwa vigumu kutimiza mradi huo. Lakini kama matokeo yanavyoonyesha, kwa msaada wa Yehova Mungu, “mambo yote yanawezekana.”—Mathayo 19:26.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22]

“Wanatimiza Kile Wanachosema”

Kazi ya ujenzi wa Jumba la Ufalme haina uvutano tu juu ya maisha ya washiriki wa kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Kwa mfano, wakati wa ujenzi wa Jumba la Ufalme huko Belize, mwanamume mmoja ambaye mke wake ni mshiriki wa dini ya Pentekoste alimwambia mke wake kwamba Mashahidi wa Yehova wakimaliza kujenga “kanisa” lao, angetaka kuhudhuria mikutano yao. Ni nini kilichomfanya atake kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme? Alisema hivi: “Ninaona kwamba Mungu yuko pamoja nao. Hawapigani wanapofanya kazi pamoja. Na wanatimiza kile wanachosema.”

[Picha]

Jumba la Ufalme huko Orange Walk, Belize

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

Jitihada za Ulimwenguni Pote

Vikundi vya Ujenzi wa Majumba ya Ufalme vimeanzishwa katika nchi 120. Ni nchi chache tu zilizoonyeshwa hapa chini ambako wafanyakazi wa kujitolea wanashiriki kwa furaha katika kazi hiyo:

Angola, Bolivia, Ethiopia, Fiji, Ghana, Hong Kong, India, Jamaika, Jamhuri ya Dominika, Kazakhstan, Kroatia, Liberia, Moldova, Nigeria, Papua New Guinea, Rwanda, Tuvalu, Ukrainia, Venezuela, Zambia.

[Picha]

Jumba la Ufalme huko Tlaxcala, Mexico

Washiriki wa Kikundi cha Ujenzi wa Majumba ya Ufalme huko Mexico

[Picha katika ukurasa wa 23]

Jumba la Ufalme huko Acapulco, Mexico