Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafundishe Watoto Wako

Mark Did Not Give Up

Mark Did Not Give Up

MARKO aliandika kimoja cha vitabu vinne vya Biblia vinavyohusu maisha ya Yesu. Ndicho kitabu kifupi zaidi na rahisi zaidi kusoma. Marko alikuwa nani? Je, unafikiri alimfahamu Yesu?— * Acheni tuone majaribu makali ambayo Marko alikabiliana nayo na tujifunze kwa nini Marko hakukata tamaa na kuacha kuwa Mkristo.

Marko anatajwa mara ya kwanza katika Biblia baada ya Mfalme Herode Agripa kumtupa mtume Petro gerezani. Usiku mmoja malaika alimweka huru Petro, na papo hapo Petro akaenda nyumbani kwa Maria, mama ya Marko, ambaye alikuwa akiishi Yerusalemu. Petro aliachiliwa huru kutoka gerezani miaka kumi hivi baada ya Yesu kuuawa wakati wa Pasaka ya 33 W.K.—Matendo 12:1-5, 11-17.

Je, unajua ni kwa nini Petro alienda nyumbani kwa Maria?—Inaelekea ni kwa sababu alijua familia ya Maria na alijua kwamba wanafunzi wa Yesu walikuwa wakifanya mikutano nyumbani kwa Maria. Barnaba, binamu ya Marko, alikuwa mwanafunzi kwa miaka mingi, angalau tangu Sherehe ya Pentekoste ya 33 W.K. Ukarimu ambao aliwaonyesha wanafunzi wapya wakati huo unatajwa katika Biblia. Hivyo, huenda Yesu alimfahamu Barnaba, na pia shangazi yake Maria na mwana wake Marko.—Matendo 4:36, 37; Wakolosai 4:10.

Katika Injili yake, Marko aliandika kwamba usiku ambao Yesu alikamatwa, kijana fulani aliyekuwa amevaa vazi fulani “juu ya mwili wake ulio uchi” alikuwepo. Marko aliandika kwamba maadui walipomshika Yesu, kijana huyo alikimbia. Unafikiri kijana huyo alikuwa nani?—Ndiyo, huenda alikuwa Marko! Hivyo, Yesu na mitume wake walipotoka usiku sana, inaelekea Marko alivaa haraka vazi fulani na kuwafuata.—Marko 14:51, 52.

Huenda kijana huyu ni nani? Anapatwa na nini, na kwa nini?

Kwa kweli, Marko alipata malezi mazuri sana ya kiroho. Inaelekea alikuwepo roho takatifu ilipomiminwa Pentekoste ya  33 W.K., na alikuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na watumishi waaminifu wa Mungu, kama vile Petro. Lakini aliandamana na binamu yake Barnaba, ambaye alimsaidia Sauli kwa kumjulisha kwa Petro miaka mitatu hivi baada ya Yesu kumtokea Sauli katika maono. Miaka kadhaa baadaye, Barnaba alienda Tarso kumtafuta Sauli.—Matendo 9:1-15, 27; 11:22-26; 12:25; Wagalatia 1:18, 19.

Mwaka wa 47 W.K., Barnaba na Sauli walichaguliwa wafanye kazi ya umishonari. Walimchukua Marko kwenda pamoja nao, lakini kwa sababu fulani zisizoelezwa, baadaye Marko aliwaacha na kurudi nyumbani, Yerusalemu. Sauli, aliyejulikana baadaye kwa jina lake la Kiroma Paulo, alikasirika. Na hakupuuza ule ambao aliona kuwa udhaifu mkubwa wa Marko.—Matendo 13:1-3, 9, 13.

Waliporudi kutoka safari yao ya umishonari, Paulo na Barnaba walieleza mafanikio mazuri sana ambayo walipata. (Matendo 14:24-28) Miezi mingi baadaye, wanaume hao wawili walipanga kurudi na kuwatembelea wanafunzi wapya katika maeneo ambako walikuwa wamehubiri. Barnaba alitaka waende pamoja na Marko, lakini je, unajua Paulo alikuwa na maoni gani?— “Hakuona kwamba inafaa” kwa sababu mapema Marko aliwaacha na kurudi nyumbani. Bila shaka, yale yaliyotukia baadaye yalimhuzunisha sana Marko!

Hasira zilipanda, na baada ya ‘hasira kali kutokea,’ Paulo na Barnaba wakatengana. Barnaba akamchukua Marko kwenda kuhubiri naye huko Kipro, naye Paulo akamchagua Sila na kwenda kuwatembelea tena wanafunzi wapya, kama ilivyopangwa hapo awali. Ni wazi kwamba Marko aliumizwa sana moyoni kwa kusababisha mvurugo kati ya Paulo na Barnaba!—Matendo 15:36-41.

Hatujui kwa nini Marko alikuwa amewaacha na kurudi nyumbani. Inaelekea alihisi kwamba alikuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. Kwa vyovyote vile, Barnaba alikuwa na uhakika kwamba jambo kama hilo halingetokea tena. Na ilikuwa hivyo. Marko hakukata tamaa! Baadaye, alifanya kazi ya umishonari pamoja na Petro huko Babiloni, mbali na nyumbani. Wakiwa Babiloni, Petro alituma salamu, na akaongeza hivi: “Na vilevile Marko mwanangu.”1 Petro 5:13.

Petro na Marko walikuwa na uhusiano wa karibu sana wa kiroho. Pia, jambo hilo linaonekana wazi tunaposoma Injili ya Marko. Katika Injili hiyo, Marko anazungumza kuhusu mambo ambayo Petro alijionea mwenyewe. Kwa mfano, linganisha masimulizi kuhusu dhoruba kwenye Bahari ya Galilaya. Marko anaongeza mambo kuhusu mahali ambapo Yesu alikuwa amelala ndani ya mashua na kitu alichokuwa amelalia, mambo ambayo mvuvi kama Petro angeweza kutambua. Kwa nini tusichunguze wenyewe mambo hayo kwa kusoma pamoja na kulinganisha masimulizi hayo ya Biblia katika Mathayo 8:24; Marko 4:37, 38; na Luka 8:23?

Baadaye, Paulo alipokuwa gerezani huko Roma, alimpongeza Marko kwa kumsaidia kwa ushikamanifu. (Wakolosai 4:10, 11) Na Paulo alipokuwa tena gerezani huko Roma, alimwandikia Timotheo na kumwomba amlete Marko, na akaeleza hivi: “Yeye ni mwenye faida kwangu kwa ajili ya huduma.” (2 Timotheo 4:11) Kwa kweli, Marko alipata mapendeleo makubwa kama nini ya utumishi kwa sababu hakukata tamaa!

Marko alipata baraka gani kwa kutokata tamaa?

^ fu. 3 Ikiwa unasoma pamoja na mtoto, kistari kirefu kinakukumbusha kwamba unapaswa kutua na kumtia mtoto moyo ajieleze.