Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwafariji Watu Wenye Ugonjwa Usioweza Kupona

Kuwafariji Watu Wenye Ugonjwa Usioweza Kupona

Kuwafariji Watu Wenye Ugonjwa Usioweza Kupona

“Sikuamini nilipogundua kwamba Mama ana ugonjwa usioweza kupona. Nilifadhaika sana, kwa kuwa singeweza kukubali kwamba mama yangu mpendwa angekufa.”—Grace, Kanada.

INAPOGUNDULIWA kwamba mpendwa ana ugonjwa usioweza kupona, watu wa familia na marafiki wanafadhaika sana na huenda wasijue la kufanya. Huenda wengine wakajiuliza ikiwa wanapaswa kumwambia mgonjwa ukweli kuhusu hali yake. Wengine wanaona kwamba hawataweza kuvumilia kumwona mpendwa wao akiteseka na labda kupoteza heshima yake kwa sababu ya madhara ya ugonjwa. Watu wengi wanakuwa na wasiwasi kwamba hawatajua la kusema au la kufanya wakati wa dakika za mwisho za mgonjwa.

Ni mambo gani unayopaswa kujua kuhusu jinsi ya kutenda unapopata habari hizo mbaya? Na unaweza kufanya nini ili uwe “rafiki wa kweli” na kutoa faraja na msaada wakati huo wa taabu?—Methali 17:17.

Hisia ya Kawaida

Ni kawaida kufadhaika mpendwa anapopatwa na ugonjwa hatari. Hata ingawa kwa kawaida madaktari wanashughulika na watu wanaokufa, mara nyingi wanafadhaika na hata wanajihisi hoi wanapojaribu kutosheleza mahitaji ya kimwili na ya kihisia ya wale wenye ugonjwa usioweza kupona.

Huenda hata wewe ukashindwa kuzuia hisia zako unapomwona mpendwa akiteseka. Hosa, mwanamke anayeishi Brazili ambaye dada yake alikuwa na ugonjwa usioweza kupona, anasema, “Inaumiza sana kuona mtu unayempenda sana akiendelea kupatwa na maumivu.” Yule mwanamume mwaminifu Musa alipomwona dada yake akiwa amepigwa na ukoma, alipaaza sauti na kusema: “Ee Mungu, tafadhali! Mponye, tafadhali!”—Hesabu 12:12, 13.

Tunafadhaishwa na hali ya wapendwa wetu wagonjwa kwa sababu tumeumbwa kwa mfano wa Mungu wetu mwenye huruma, Yehova. (Mwanzo 1:27; Isaya 63:9) Yehova anahisi jinsi gani anapoona wanadamu wakiteseka? Fikiria jinsi Yesu alivyohisi. Aliiga utu wa Baba yake kikamili. (Yohana 14:9) Yesu alipoona watu wakiteseka kwa sababu ya ugonjwa, ‘aliwasikitikia.’ (Mathayo 20:29-34; Marko 1:40, 41) Kama makala iliyotangulia katika gazeti hili ilivyosema, wakati rafiki yake Lazaro alipokufa, Yesu aliona jinsi watu wa familia na marafiki walivyoteseka hivi kwamba alitaabika sana na ‘kutokwa na machozi.’ (Yohana 11:32-35) Kwa kweli, Biblia inataja kifo kuwa adui na inaahidi kwamba hivi karibuni kifo na magonjwa hayatakuwapo tena.—1 Wakorintho 15:26; Ufunuo 21:3, 4.

Ni jambo linaloeleweka wakati unapohisi kwamba unataka kumlaumu mtu fulani—mtu yeyote—unapopata habari zenye kuhuzunisha kwamba mpendwa wako ana ugonjwa usioweza kupona. Hata hivyo, Dakt. Marta Ortiz, ambaye aliandika ripoti kuhusu kuwashughulikia watu wenye ugonjwa usioweza kupona, anatoa shauri hili: “Epuka kuwalaumu wengine—wafanyakazi katika hospitali au usijilaumu mwenyewe—kwa sababu ya hali ya mgonjwa. Hilo linaweza kuleta mkazo zaidi katika mahusiano yenu na kuwakengeusha msishughulikie jambo kuu, yaani, mahitaji ya yule mwenye ugonjwa usioweza kupona.” Ni hatua gani unazoweza kuchukua kumsaidia mpendwa wako kuvumilia ugonjwa wake na kuelewa kwamba huenda akafa?

Kazia Fikira Mgonjwa, Si Ugonjwa

Hatua ya kwanza ni kumkazia fikira mgonjwa badala ya kukazia fikira madhara ya ugonjwa. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Sarah, ambaye ni muuguzi, anasema hivi: “Ninatumia wakati kutazama picha za mgonjwa wakati alipokuwa na nguvu nyingi. Ninasikiliza kwa makini anaponieleza mambo aliyofanya zamani. Hilo linanisaidia kukumbuka maisha na historia ya mgonjwa huyo badala ya kukazia fikira hali yake ya wakati huu.”

Anne-Catherine, ambaye pia ni muuguzi, anaeleza jinsi anavyoepuka kukazia tu fikira ugonjwa wa mgonjwa. Anasema: “Ninamtazama mgonjwa mwenyewe uso kwa uso na kukazia fikira mambo ambayo ninaweza kufanya ili kuboresha hali yake.” Kitabu kimoja (The Needs of the Dying—A Guide for Bringing Hope, Comfort, and Love to Life’s Final Chapter) kinasema: “Ni jambo la kawaida kufadhaika sana unapoona mpendwa akidhoofika kutokana na ugonjwa au aksidenti. Hatua bora ya kuchukua ni kumtazama mpendwa huyo uso kwa uso na kuona kwamba utu wake haujabadilika hata ingawa ni mgonjwa.”

Ni kweli kwamba unahitaji kujizuia na kuazimia kufanya hivyo. Georges, mwangalizi Mkristo ambaye anawatembelea kwa ukawaida wagonjwa wasioweza kupona, anasema hivi: “Upendo wetu kwa rafiki zetu unapaswa kuwa wenye nguvu kuliko ugonjwa.” Ukikazia fikira mgonjwa badala ya ugonjwa, wewe mwenyewe na mpendwa wako mnafaidika. Yvonne, ambaye amewatunza watoto wanaougua kansa, anasema hivi: “Kutambua kwamba unaweza kuwasaidia wagonjwa kuendelea kujiheshimu kunakusaidia kukabiliana na hali yao ya kudhoofika kimwili.”

Uwe Tayari Kusikiliza

Huenda watu wakasita kuwasiliana na mtu ambaye anakaribia kufa hata ingawa wanampenda sana. Kwa nini? Wanaogopa kwamba hawatajua la kusema. Hata hivyo, Anne-Catherine, ambaye hivi karibuni alimtunza rafiki yake mwenye ugonjwa usioweza kupona, anasema kwamba kuna wakati wa kunyamaza. Anasema hivi: “Tunawafariji wengine, si kwa maneno yetu tu, bali pia kwa mtazamo wetu. Tunaweza kuonyesha kwamba tunamjali mgonjwa tunapoketi pamoja naye, tunapomkaribia na kumgusa, na kutozuia machozi yetu anapotuambia jinsi anavyohisi.”

Huenda mpendwa wako anataka kueleza hisia zake—kujieleza kwa unyoofu na waziwazi. Lakini, mara nyingi, wagonjwa wanaepuka kuzungumzia matatizo mazito ya kibinafsi wanapoona kwamba wapendwa wao wana wasiwasi. Pia, huenda marafiki na watu wa familia wenye nia nzuri wakaepuka kuzungumzia mambo yanayomhusu mgonjwa, na hata kutomweleza mambo muhimu kuhusu afya yake. Kuficha habari kunaweza kuwa na matokeo gani? Daktari mmoja anayeshughulikia watu wenye ugonjwa usioweza kupona anasema kwamba jitihada za kuficha ukweli “zinawakengeusha watu kutoka kwa mambo muhimu kama vile kuzungumzia na kushughulikia ugonjwa.” Hivyo, ikiwa mgonjwa anataka, anapaswa kuruhusiwa kuongea waziwazi kuhusu hali yake au uwezekano wa kwamba atakufa.

Walipokabili kifo, watumishi wa zamani wa Mungu hawakusita kumweleza Yehova Mungu mahangaiko yao. Kwa mfano, alipojua kwamba atakufa, Mfalme Hezekia ambaye alikuwa na umri wa miaka 39 alieleza jinsi alivyofadhaika. (Isaya 38:9-12, 18-20) Vivyo hivyo, watu wenye ugonjwa usioweza kupona wanapaswa kuruhusiwa kueleza jinsi wanavyohuzunika kwa sababu maisha yao ni mafupi. Labda wanafadhaika kwa sababu hawawezi kutimiza miradi yao ya kibinafsi, kama vile kusafiri, kupata familia, kuona wajukuu wakikua, au kumtumikia Mungu kwa ukamili. Labda wanaogopa kwamba marafiki na watu wa familia watajitenga nao kwa sababu hawajui la kufanya. (Ayubu 19:16-18) Kuogopa kuteseka, kupoteza uwezo wa kimwili, au kuogopa kifo kunaweza pia kuwalemea.

Anne-Catherine anasema hivi: “Ni jambo la maana kumruhusu rafiki yako ajieleze, bila kumkatiza au kumhukumu au kupuuza mahangaiko yake. Hiyo ndiyo njia bora ya kujua jinsi anavyohisi na kuelewa mapendezi, mahangaiko, na matarajio yake.”

Elewa Mahitaji ya Msingi

Hali ngumu ya rafiki yako, ambayo huenda inazidishwa na matibabu yenye kuumiza na madhara yake, inaweza kukusumbua sana hata usahau uhitaji fulani wa msingi wa mgonjwa huyo. Mgonjwa anahitaji kujifanyia maamuzi ya kibinafsi.

Katika maeneo fulani, familia inaweza kujaribu kumlinda mgonjwa kwa kumficha ukweli kuhusu hali yake, na hata kutomhusisha katika maamuzi yanayohusu matibabu. Katika maeneo mengine, huenda tatizo lingine likatokea. Kwa mfano, Jerry, ambaye ni muuguzi, anasema hivi: “Nyakati nyingine wageni wanapenda kuzungumza kuhusu mgonjwa wakiwa wamesimama kando ya kitanda chake, kana kwamba hayupo.” Katika visa vyote viwili, wale wanaofanya hivyo hawamheshimu mgonjwa.

Kuwa na tumaini ni uhitaji mwingine wa msingi. Katika nchi zenye matibabu ya hali ya juu, mara nyingi kuwa na tumaini kunasaidia sana ili kupata matibabu yatakayomsaidia mgonjwa apate nafuu. Michelle, ambaye amekuwa akimsaidia mama yake ambaye amepata kansa mara tatu, anasema hivi: “Mama anapotaka kujaribu matibabu mengine au kupata ushauri wa daktari mwingine, ninamsaidia kufanya utafiti. Nimetambua kwamba ninahitaji kuona mambo kihalisi lakini kusema mambo ambayo hayatamvunja moyo.”

Namna gani ikiwa hakuna tumaini la kupata dawa? Kumbuka kwamba mtu mwenye ugonjwa usioweza kupona anahitaji kuzungumza waziwazi kuhusu kifo. Georges, mwangalizi Mkristo aliyenukuliwa mapema, anasema: “Ni muhimu sana kutoficha ukweli wa kwamba mgonjwa huyo atakufa karibuni. Hilo linamwezesha mgonjwa kufanya mipango inayofaa na kujitayarishia kifo.” Matayarisho hayo yanaweza kumsaidia mgonjwa kuona kwamba ametimiza mambo aliyotaka na kwamba hatakuwa mzigo kwa wengine.

Bila shaka, si rahisi kuzungumzia mambo hayo. Lakini kuzungumzia mambo waziwazi kunakuwezesha kueleza kwa undani jinsi unavyohisi. Huenda mtu anayekaribia kufa akataka kusuluhisha hali ya kutoelewana, kusema mambo anayojutia, au kuomba msamaha. Mambo kama hayo yanaweza kuboresha uhusiano wako pamoja na mtu huyo.

Mfariji Katika Siku Zake za Mwisho

Unaweza kumfariji jinsi gani mtu anayekaribia mwisho wa maisha yake? Dakt. Ortiz, aliyenukuliwa awali, anasema: “Acha mgonjwa ataje maombi yake ya mwisho. Sikiliza kwa makini. Ikiwezekana, jaribu kufanya mambo ambayo mgonjwa anataka. Ikiwa huwezi kutimiza maombi ya mgonjwa, mwambie waziwazi.”

Huenda mgonjwa anayekaribia kufa akahitaji kuendelea kushirikiana na wapendwa wake. Georges anasema, “Msaidie mgonjwa kushirikiana nao hata ikiwa watazungumza kwa muda mfupi kwa sababu ya mgonjwa kuchoka.” Wanaweza kutiana moyo na kusali pamoja hata ikiwa wanazungumza kwa simu tu. Christina, mwanamke kutoka Kanada ambaye alipoteza wapendwa watatu mfululizo, anasema hivi: “Kadiri walivyokaribia mwisho wa maisha yao, ndivyo walivyotegemea zaidi sala za marafiki wao Wakristo.”

Je, unapaswa kuogopa kulia mbele ya mpendwa wako? Hapana. Ukitokwa na machozi, unampa mgonjwa nafasi ya kukufariji. Kitabu kimoja (The Needs of the Dying) kinasema hivi: “Inagusa moyo sana kufarijiwa na mtu anayekaribia kufa, na ni muhimu sana kwa mgonjwa kuwafariji wengine.” Anapowafariji wengine, mtu ambaye ametunzwa kwa muda mrefu anaweza kuona kwamba bado ana daraka la kuwa rafiki, baba, au mama anayejali.

Ni kweli kwamba hali zinaweza kukuzuia usiwe pamoja na mpendwa wako katika dakika za mwisho za maisha yake. Hata hivyo, ikiwa unaweza kuwa pamoja na rafiki yako hospitalini au nyumbani, jitahidi kushika mkono wake mpaka anapokufa. Dakika hizo za mwisho ni nafasi ya kusema mambo ambayo kwa kawaida hungeyasema. Usiruhusu hali yake ya kupoteza fahamu ikuzuie usimpe kwaheri na kumwambia kwamba unampenda na unatumaini kumwona tena katika ufufuo.—Ayubu 14:14, 15; Matendo 24:15.

Ukitumia dakika hizo za mwisho vizuri, inaelekea hutajuta baadaye. Kwa kweli, unaweza kufarijika sana wakati ujao unapokumbuka pindi hizo zenye hisia nyingi. Utakuwa umethibitika kuwa rafiki wa kweli “wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Ukikazia fikira mgonjwa badala ya ugonjwa, wewe mwenyewe na mpendwa wako mnafaidika

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29]

Jinsi ya Kumheshimu Mgonjwa

Katika nchi nyingi, jitihada zinafanywa ili kuhakikisha kwamba mtu mwenye ugonjwa usioweza kupona ana haki ya kufa kwa amani na kwa heshima. Hati za mwelekezo wa mapema kuhusu matibabu ni muhimu katika kutetea haki hizo na zinawaruhusu wagonjwa kufia nyumbani au katika makao ya kuwatunzia wagonjwa mahututi.

Hati ya mwelekezo wa mapema kuhusu matibabu inatimiza mambo haya:

• Inawawezesha madaktari na watu wa ukoo kuwasiliana

• Inaondolea familia daraka la kufanya maamuzi

• Inapunguza uwezekano wa mgonjwa kupewa matibabu yasiyotakikana, yasiyofaa, yenye kuumiza, na yaliyo ghali

Hati nzuri ya mwelekezo wa mapema inatia ndani habari inayofuata:

• Jina la mwakilishi wako wa kitiba

• Matibabu ambayo huenda ukakubali au kukataa ikiwa huwezi kupata nafuu

• Ikiwezekana, jina la daktari anayejua maamuzi yako

[Picha katika ukurasa wa 26]

Badala ya kukazia fikira hali ya sasa ya mgonjwa, kazia fikira maisha na historia yake