Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Noa na Ile Gharika si Mambo ya Kuwaziwa Tu

Noa na Ile Gharika si Mambo ya Kuwaziwa Tu

Noa na Ile Gharika si Mambo ya Kuwaziwa Tu

JE, UNATAMANI kuwe na ulimwengu bora, ulimwengu ambamo watu wanaishi kwa amani? ulimwengu ambamo hakuna vita, uhalifu, wala ukandamizaji? Ikiwa ndivyo, basi unaweza kutiwa moyo na simulizi la kihistoria ambalo huenda unalifahamu vizuri. Ni simulizi la Noa, mtu mzuri sana ambaye alijenga safina iliyomwokoa pamoja na familia yake kupitia gharika ya ulimwenguni pote iliyowaangamiza waovu.

Si hadithi nyingi zinazojulikana kuliko simulizi hilo. Rekodi ya mambo yaliyompata Noa inapatikana katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo, sura ya 6 hadi 9, na imerudiwa katika Kurani na katika hekaya za watu wengi duniani pote. Je, kweli Gharika ilitokea, au ni hekaya tu ya kuwatia moyo watu wafanye mambo mema? Wanatheolojia na wanasayansi wamejadiliana kuhusu swali hilo kwa karne nyingi. Hata hivyo, Biblia, Neno la Mungu, linasema wazi kabisa kwamba simulizi hilo ni jambo hakika, si la kuwaziwa. Fikiria hili:

Simulizi la Mwanzo linatuambia mwaka, mwezi, na siku hususa ambayo Gharika ilianza, wakati na mahali hususa ambapo safina ilitua, na wakati ambapo dunia ilikauka. Vilevile mambo mengi kuhusu safina yameelezwa kwa njia hususa—muundo, vipimo, na vifaa vilivyotumiwa kuijenga. Kinyume na hilo, kwa kawaida hekaya hazitoi ufafanuzi hususa.

Kuna rekodi mbili za nasaba katika Biblia zinazothibitisha kuwa Noa alikuwa mtu halisi. (1 Mambo ya Nyakati 1:4; Luka 3:36) Ezra na Luka, ambao walikusanya nasaba hizo, walikuwa wachunguzi waangalifu. Luka alichunguza nasaba ya Yesu Kristo kurudi nyuma kufikia Noa.

Nabii Isaya na Ezekieli na vilevile mitume Wakristo Paulo na Petro walitaja kuhusu Noa au Gharika.—Isaya 54:9; Ezekieli 14:14, 20; Waebrania 11:7; 1 Petro 3:19, 20; 2 Petro 2:5.

Yesu Kristo alitaja kuhusu Gharika, akisema hivi: “Sawa na vile ilivyotukia katika siku za Noa, ndivyo itakavyokuwa pia katika siku za Mwana wa binadamu: walikuwa wakila, walikuwa wakinywa, wanaume walikuwa wakioa, wanawake walikuwa wakiolewa, mpaka siku ile ambayo Noa aliingia katika safina, na gharika ikafika na kuwaangamiza wote.” (Luka 17:26, 27) Ikiwa Gharika haikutukia, basi maneno ya Yesu kuhusu “siku za Mwana wa binadamu” hayangekuwa na umuhimu wowote.

Mtume Petro alitabiri kwamba kungekuwa na “wadhihaki” ambao wangepuuza kinachosemwa katika Biblia. “Kulingana na kupenda kwao,” akaandika Petro, “hawalioni jambo hili, kwamba . . . ulimwengu wa wakati [wa Noa] uliangamia kwa gharika ya maji.” Je, tunapaswa kukosa kuona ‘jambo hilo’? Hatupaswi! Petro akaongeza hivi: “Mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zinahifadhiwa mpaka ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.”—2 Petro 3:3-7.

Kwa mara nyingine tena, Mungu atawaharibu waovu, na kwa mara nyingine tena, kutakuwa na waokokaji. Kwa kuiga mfano wa Noa, tunaweza kuwa kati ya waadilifu ambao wataokolewa kuingia katika ulimwengu bora.