Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Hayuko Mbali Sana na Kila Mmoja Wetu”

“Hayuko Mbali Sana na Kila Mmoja Wetu”

Mkaribie Mungu

“Hayuko Mbali Sana na Kila Mmoja Wetu”

Matendo 17:24-27

WANAPOLINGANISHWA na ulimwengu huu mkubwa sana, wanadamu ni duni kwelikweli. Huenda umejiuliza, ‘Je, kweli wanadamu wanaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu Mweza-Yote?’ Ingewezekana ikiwa tu Mungu, ambaye jina lake ni Yehova, anataka tumkaribie. Je, anataka? Jibu lenye kufariji linapatikana katika maneno yanayopendeza ambayo Paulo aliwaambia wanaume wenye elimu wa Athene. Maneno hayo yamerekodiwa katika Matendo 17:24-27. Ona mambo manne anayotaja Paulo kumhusu Yehova.

Kwanza, Paulo anasema kwamba Mungu ‘aliufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo.’ (Mstari wa 24) Uzuri na unamna-namna unaofanya maisha yapendeze sana unathibitisha kwamba Mtengenezaji wetu anatufikiria na kutupenda. (Waroma 1:20) Ungekuwa upumbavu kufikiri kwamba Mungu kama huyo angechagua kuwa mbali sana na viumbe anaopenda.

Pili, Yehova “huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.” (Mstari wa 25) Yehova ndiye Mtegemezaji wa uhai. (Zaburi 36:9) Hewa, maji, na vyakula ambavyo ni muhimu kwa uhai ni zawadi kutoka kwa Muumba wetu. (Yakobo 1:17) Je, inapatana na akili kuamini kwamba Mungu wetu mkarimu angejitenga nasi, na hivyo kutunyima zawadi ya kumjua na kumkaribia?

Tatu, Mungu “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu.” (Mstari wa 26) Yehova si mwenye ubaguzi hata kidogo. (Matendo 10:34) Je, tungetarajia awe na ubaguzi? Alimuumba “mtu mmoja,” Adamu ambaye watu wa mataifa na jamii zote wametoka kwake. “Mapenzi [ya Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe.” (1 Timotheo 2:4) Kwa hiyo, una nafasi ya kumkaribia haidhuru rangi yako ya ngozi, taifa, au kabila.

Mwishowe, Paulo anataja kweli yenye kutia moyo sana: Yehova “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Mstari wa 27) Ingawa ametukuzwa sana, sikuzote wale wanaotaka kumkaribia Yehova kwa unyoofu wanaweza kumpata. Neno lake linatuhakikishia kwamba hayuko mbali sana, bali “yuko karibu na wote wanaomwitia.”—Zaburi 145:18.

Kutokana na maneno ya Paulo, ni wazi kwamba Mungu anataka tumkaribie. Hata hivyo, Paulo anaeleza kwamba wale tu ambao Mungu anawaruhusu wamkaribie ni watu walio tayari ‘kutafuta’ na hata “kupapasa-papasa” ili wampate. (Mstari wa 27) Kichapo kimoja cha marejeo ya watafsiri wa Biblia kinasema kwamba “vitenzi vyote viwili vinaeleweka kuwa vinaonyesha jambo linalowezekana . . . au tamaa inayoweza kutoshelezwa.” Kwa mfano: Unapoingia katika chumba unachofahamu kukiwa na giza, huenda ukapapasa-papasa ukitafuta swichi ya taa au mlango, lakini unajua kwamba utapata unachotafuta. Vivyo hivyo, tukimtafuta Mungu kwa unyoofu na kupapasa-papasa ili kumpata, tunaweza kuwa na hakika kwamba jitihada zetu zitafanikiwa. Paulo anatuhakikishia kwamba ‘kwa kweli tutampata.’—Mstari wa 27.

Je, unatamani kumkaribia Mungu? Ikiwa kwa imani utaanza ‘kumtafuta Mungu’ na “kupapasa-papasa” ili kumpata, hutakatishwa tamaa. Si vigumu kumpata Yehova, kwa kuwa “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”