Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Tazama! Kijakazi wa Yehova!”

“Tazama! Kijakazi wa Yehova!”

Igeni Imani Yao

“Tazama! Kijakazi wa Yehova!”

MARIA alitazama juu akiwa amekodoa macho, mgeni alipoingia nyumbani kwao. Mgeni huyo hakumwuliza kuhusu baba wala mama yake kwani alikuwa amekuja kumwona yeye! Alikuwa na hakika kwamba mgeni huyo hakuwa mkaaji wa Nazareti. Katika mji mdogo kama huo, ilikuwa rahisi kuwatambua wageni. Mgeni huyu angetambuliwa kwa urahisi mahali popote pale. Alimsalimu Maria kwa njia isiyo ya kawaida, alipomwambia hivi: “Siku njema, uliyependelewa sana, Yehova yuko pamoja nawe.”—Luka 1:28.

Hivyo ndivyo Biblia inavyoanza kutueleza kumhusu Maria, binti ya Heli, aliyeishi katika mji wa Nazareti huko Galilaya. Anapotajwa kwa mara ya kwanza, anakabili maamuzi muhimu. Amechumbiwa na seremala anayeitwa Yosefu ambaye ingawa si tajiri, ana imani yenye nguvu. Hivyo, ni kana kwamba tayari alikuwa amejipangia maisha yake. Alikuwa aishi maisha ya hali ya chini akiwa mke anayefanya kazi ili kumsaidia Yosefu kulea watoto wao. Lakini, ghafula, mgeni huyo anampa mgawo kutoka kwa Mungu ambao ungebadili maisha yake.

Huenda ukashangaa kujua kwamba Biblia haisemi mengi kumhusu Maria. Inasema machache sana kuhusu malezi yake, machache zaidi kuhusu utu wake, na haisemi chochote kuhusu sura yake. Lakini, yale ambayo Neno la Mungu linasema kumhusu yanafunua mengi.

Ili kumfahamu Maria vizuri, hatupaswi kuamini tu mambo yanayofundishwa katika dini mbalimbali kumhusu. Kwa sasa, tusifikirie picha na mifano mingi iliyotengenezwa ya Maria. Pia na tuondoe akilini mafundisho ya kidini yanayomkweza sana mwanamke huyo wa hali ya chini kwa kumwita majina kama vile “Mama ya Mungu” na “Malkia wa Mbinguni.” Badala yake acha tukazie fikira mambo ambayo Biblia inafunua hasa kumhusu. Inatufunulia mambo muhimu sana kuhusu imani yake na jinsi tunavyoweza kuiiga.

Malaika Anamtembelea

Huenda unajua kwamba mgeni wa Maria hakuwa mwanadamu bali ni malaika Gabrieli. Alipomwita ‘aliyependelewa sana,’ Maria ‘alishtushwa sana’ na maneno hayo na kushangazwa na salamu hizo zisizo za kawaida. (Luka 1:29) Alipendelewa sana na nani? Maria hakutarajia kupendelewa sana miongoni mwa wanadamu. Lakini malaika alikuwa akizungumza kuhusu kupendelewa na Yehova Mungu. Hilo lilikuwa muhimu kwake. Lakini Maria hakukata kauli kwa kiburi kwamba anapendelewa na Mungu. Tukijitahidi kupata kibali cha Mungu, bila kujivuna tukifikiri kwamba tayari tumekipata, tutajifunza somo muhimu ambalo Maria alielewa kabisa. Mungu anawapinga wenye majivuno, lakini anawapenda na kuwategemeza watu wa hali ya chini na wanyenyekevu.—Yakobo 4:6.

Maria angehitaji kuwa mnyenyekevu hivyo, kwa sababu malaika alimtolea pendeleo la ajabu. Alimwambia kwamba angemzaa mtoto ambaye angekuwa mwanadamu muhimu zaidi ya wote. Gabrieli alisema hivi: “Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:32, 33) Bila shaka Maria alijua ahadi ambayo Mungu alikuwa amempa Daudi miaka zaidi ya elfu moja mapema, kwamba mmoja wa wazao wake angetawala milele. (2 Samweli 7:12, 13) Hivyo, mwana wake angekuwa masihi aliyekuwa akitarajiwa na watu wa Mungu kwa karne nyingi!

Zaidi ya hayo, malaika alimwambia Maria kwamba mwana wake ‘angeitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi.’ Mwanamke wa kibinadamu angeweza jinsi gani kuzaa Mwana wa Mungu? Kwa kweli, Maria angeweza jinsi gani kuzaa mwana? Alikuwa amechumbiwa na Yosefu lakini hawakuwa wameoana. Maria aliuliza swali hilo waziwazi kwa maneno haya: “Hilo litawezekanaje, kwa kuwa silali na mwanamume?” (Luka 1:34) Ona kwamba alizungumza kuhusu ubikira wake bila kuona aibu hata kidogo. Kinyume na hilo, alijivunia kuwa bikira. Leo, vijana wengi wako tayari kutupilia mbali ubikira wao na wanawadhihaki wale ambao bado ni mabikira. Bila shaka ulimwengu umebadilika. Hata hivyo, Yehova hajabadilika. (Malaki 3:6) Kama ilivyokuwa katika siku za Maria, bado Yehova anawathamini wale wanaoshikilia viwango vyake vya maadili.—Waebrania 13:4.

Ingawa alikuwa mtumishi mwaminifu wa Mungu, Maria alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu. Hivyo basi, angeweza jinsi gani kuzaa mtoto mkamilifu, Mwana wa Mungu? Gabrieli alieleza: “Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu za Aliye Juu Zaidi zitakufunika. Kwa sababu hiyo pia kile kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35) Kitu kitakatifu ni kitu “safi” na “kilichotakata.” Kwa kawaida, watoto wanarithi hali ya kutokamilika kutoka kwa wazazi wao. Lakini katika kisa hiki, Yehova angefanya muujiza wa pekee. Angehamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la Maria, kisha nguvu zake za utendaji, au roho takatifu, ‘ingemfunika’ Maria ili kumzuia kabisa mtoto huyo asipate dhambi. Je, Maria aliamini ahadi ya malaika? Aliitikia namna gani?

Itikio la Maria kwa Gabrieli

Ni jambo ngumu kwa watu wenye mashaka, kutia ndani wanatheolojia wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, kuamini kwamba bikira anaweza kuzaa. Hata ingawa wana elimu nyingi, wameshindwa kuelewa kweli fulani rahisi. Kama alivyosema Gabrieli, “kwa Mungu hakuna tangazo lolote lisilowezekana.” (Luka 1:37) Maria alikubali maneno ya Gabrieli kuwa ya kweli, kwa sababu alikuwa mwanamke mwenye imani kubwa. Hata hivyo, Maria hakuamini tu alichoambiwa bila uthibitisho kamili. Kama mtu yeyote anayefikiri, Maria alihitaji uthibitisho ambao ungetegemeza imani yake na Gabrieli alikuwa tayari kumpa uthibitisho zaidi. Alimwambia kuhusu Elisabeti, mtu wa ukoo wake, aliyezeeka na kwa muda mrefu alijulikana kuwa tasa. Mungu alikuwa amemwezesha achukue mimba kimuujiza!

Sasa Maria angefanya nini? Alikuwa amepewa mgawo na kuthibitishiwa kwamba Mungu angetimiza mambo yote aliyosema Gabrieli. Tusifikiri kwamba pendeleo hilo halikutokeza mahangaiko au matatizo yoyote. Kwanza, alihitaji kufikiria kuhusu uchumba wake na Yosefu. Je, bado Yosefu angekubali kumwoa baada ya kugundua kwamba ana mimba? Pia, huenda mgawo wenyewe ulionekana kuwa mzito sana. Alipaswa kubeba uhai wa kiumbe chenye thamani zaidi kati ya viumbe vyote vya Mungu, yaani, Mwana mpendwa wa Mungu! Angemtunza akiwa kitoto kichanga kisicho na uwezo na kumlinda katika ulimwengu mbovu. Kwa kweli huo ulikuwa mgawo mzito sana!

Biblia inaonyesha kwamba nyakati nyingine hata wanaume waaminifu na wenye nguvu walisita kukubali migawo migumu waliyopewa na Mungu. Musa alisema kwamba hangeweza kuzungumza kwa ufasaha vya kutosha ili kutumiwa akiwa msemaji wa Mungu. (Kutoka 4:10) Yeremia alisema kwamba alikuwa “mvulana tu,” mchanga sana asiweze kukubali mgawo aliopewa na Mungu. (Yeremia 1:6) Naye Yona aliukimbia mgawo wake! (Yona 1:3) Lakini Maria alitenda jinsi gani?

Maneno yake ya unyenyekevu na utii yamekumbukwa kwa miaka mingi. Alimwambia Gabrieli hivi: “Tazama! Kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.” (Luka 1:38) Kijakazi ndiye aliyekuwa mtumishi wa chini zaidi kati ya watumishi wote kwani maisha yake yalikuwa mikononi mwa bwana wake. Hivyo ndivyo alivyohisi Maria kumwelekea Bwana wake, Yehova. Alijua kwamba alikuwa salama mikononi mwake, kwamba ni mshikamanifu kwa wale walio washikamanifu kwake, na Yehova angembariki ikiwa angejitahidi kutimiza mgawo huo mgumu.—Zaburi 18:25.

Nyakati fulani Mungu anatuambia tufanye jambo linaloonekana kuwa gumu, hata lisilowezekana machoni petu. Hata hivyo, katika Neno lake anatupa sababu nzuri za kumtegemea, yaani, kujiweka mikononi mwake kama alivyofanya Maria. (Methali 3:5, 6) Je, tutafanya hivyo? Tukifanya hivyo atatuthawabisha, na kutupa sababu za kuimarisha imani yetu kwake hata zaidi.

Kumtembelea Elisabeti

Aliyosema Gabrieli kumhusu Elisabeti yalikuwa muhimu sana kwa Maria. Kati ya wanawake wote duniani, ni nani angeelewa vema zaidi hali yake? Kwa haraka, Maria alifunga safari ambayo ingechukua siku tatu au nne kuelekea nchi yenye milima ya Yuda. Alipokuwa akiingia nyumbani kwa Elisabeti na kuhani Zekaria, Yehova alimthawabisha Maria kwa kumpa uthibitisho mwingine wenye nguvu ili kuimarisha imani yake. Aliposikia tu salamu za Maria, Elisabeti alihisi mtoto mchanga aliyekuwa katika tumbo lake la uzazi akiruka kwa shangwe. Alijawa na roho takatifu na kumwita Maria “mama ya Bwana wangu.” Mungu alimfunulia Elisabeti kwamba mwana wa Maria angekuwa Bwana wake, Masihi. Zaidi ya hilo, aliongozwa na roho kumpongeza Maria kwa sababu ya kutii kwa uaminifu aliposema: “Mwenye furaha pia ni yule aliyeamini.” (Luka 1:39-45) Ndiyo, mambo yote ambayo Yehova alimwahidi Maria yangetimia!

Kisha Maria akazungumza pia. Yale aliyosema yamehifadhiwa kwa uangalifu katika Luka 1:46-55. Hayo ndiyo maneno mengi zaidi aliyowahi kusema Maria kurekodiwa katika Biblia, na yanafunua mengi kumhusu. Yanaonyesha shukrani na uthamini wake, anapomsifu Yehova kwa kumbariki na pendeleo la kuwa mama ya Masihi. Yanaonyesha kina cha imani yake, anaposema kwamba Yehova anawashusha wenye majivuno na wenye nguvu na kuwasaidia watu wa hali ya chini na maskini wanaotaka kumtumikia. Pia yanafunua kiwango cha ujuzi wa Maria. Kulingana na kadirio moja, alirejelea Maandiko ya Kiebrania zaidi ya mara 20!

Kwa wazi, Maria alifikiria kwa uzito kuhusu Neno la Mungu. Lakini, aliendelea kuwa mnyenyekevu, na badala ya kujitungia maneno aliacha Maandiko yaeleze hali yake. Siku moja, mtoto aliyekuwa ndani ya tumbo lake la uzazi angeonyesha roho hiyohiyo, akisema: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.” (Yohana 7:16) Ni vizuri kujiuliza: ‘Je, ninaliheshimu sana Neno la Mungu kwa njia hiyo? Au je, ninapendelea maoni na mafundisho yangu mwenyewe?’ Jibu la Maria ni wazi.

Maria aliendelea kukaa na Elisabeti kwa miezi mitatu, hapana shaka akipokea na kuandaa kitia moyo kingi. (Luka 1:56) Wanawake hao wawili wanatukumbusha umuhimu wa urafiki. Tukitafuta marafiki ambao kwa kweli wanampenda Mungu wetu, Yehova, bila shaka tutaimarika kiroho na kumkaribia zaidi. (Methali 13:20) Hatimaye, ulifika wakati wa Maria kurudi nyumbani. Yosefu angesema nini akigundua kwamba ana mimba?

Maria na Yosefu

Inaelekea kwamba Maria hakusubiri mimba yake ionekane. Bila shaka lazima angezungumza na Yosefu. Kabla ya kufanya hivyo, huenda alijiuliza mwanamume huyo mzuri, aliyemwogopa Mungu angesema nini kuhusu yale ambayo angemwambia. Hata hivyo, alimfikia na kumwambia yote yaliyokuwa yamempata. Kama unavyoweza kuwazia Yosefu alihangaishwa sana na jambo hilo. Ingawa alitaka kumwamini msichana huyo mpendwa, alilomwambia halikuwa limewahi kutukia tena. Biblia haielezi kuhusu mawazo yake au jinsi alivyofikiria. Lakini inatuambia kwamba aliamua kumtaliki kwa sababu wakati huo watu waliochumbiana walionwa ni kama wameoana. Hata hivyo, aliamua kumtaliki kwa siri kwa sababu hakutaka kumwaibisha hadharani au kumfanya aadhibiwe. (Mathayo 1:18, 19) Lazima Maria alihuzunishwa kumwona mwanamume huyo mwenye fadhili akihangaishwa na hali hiyo isiyo ya kawaida. Hata hivyo, Maria hakukasirika.

Yehova hakumwacha Yosefu achukue hatua aliyoona kuwa bora. Katika ndoto, malaika wa Mungu alimwambia kwamba mimba ya Maria ilikuwa kwa kweli ya kimuujiza. Lazima hilo lilimtuliza kama nini! Sasa Yosefu alifanya kama Maria alivyofanya tangu mwanzoni, yaani, alitenda kupatana na mwelekezo wa Yehova. Alimwoa Maria, na akajitayarisha kutimiza wajibu wa pekee wa kumlea Mwana wa Yehova.—Mathayo 1:20-24.

Inafaa wenzi wa ndoa na wale wanaotarajia kufunga ndoa wajifunze kutokana na wenzi hao wachanga walioishi miaka 2,000 iliyopita. Alipokuwa akimtazama mke wake mchanga akitimiza majukumu yake akiwa mama, bila shaka Yosefu alifurahi kwamba malaika wa Yehova alikuwa amemwelekeza. Lazima Yosefu alikuwa ameona umuhimu wa kumtegemea Yehova wakati wa kufanya maamuzi mazito. (Zaburi 37:5; Methali 18:13) Hapana shaka kwamba akiwa kichwa cha familia aliendelea kuwa mwangalifu na mwenye fadhili alipofanya maamuzi.

Kwa upande mwingine, tunaweza kukata kauli gani kutokana na nia ya Maria ya kuolewa na Yosefu? Ijapokuwa mwanzoni ilikuwa vigumu kwa Yosefu kuelewa kisa chake, Maria alingojea akiwa na tumaini kwamba mwanamume huyo angekuwa kichwa cha familia yao. Kwa wazi hilo lilikuwa somo zuri kwake, nalo ni somo zuri kwa wanawake Wakristo leo. Mwishowe, matukio hayo yaliwafundisha Yosefu na Maria mengi kuhusu umuhimu wa kuzungumza kwa unyoofu na waziwazi.

Bila shaka wenzi hao walianzisha ndoa yao juu ya msingi bora zaidi. Wote wawili walimpenda Yehova Mungu na zaidi ya hilo walitamani kumpendeza wakiwa wazazi wanaotegemeka na wanaojali. Bila shaka wangepata baraka nyingi sana—na matatizo mengi pia. Walitarajia kumlea Yesu, ambaye angekuwa mtu mkuu zaidi kuwahi kuishi duniani.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kumpenda Mungu ndio msingi bora zaidi wa ndoa