Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hujui Ni Wapi Itafanikiwa!

Hujui Ni Wapi Itafanikiwa!

Hujui Ni Wapi Itafanikiwa!

“Asubuhi panda mbegu zako na mpaka jioni usiache mkono wako upumzike; kwa maana hujui ni wapi hii itafanikiwa.”—MHU. 11:6.

1. Kwa nini kushuhudia ukuzi ni jambo la kustaajabisha na la kunyenyekeza?

MKULIMA anahitaji kuwa na subira. (Yak. 5:7) Baada ya kupanda mbegu, anahitaji kungoja ili ichipuke na kukua. Hatua kwa hatua, hali zinapokuwa nzuri, machipukizi yanaanza kutokea juu ya udongo. Kisha yanasitawi na kuwa mimea ambayo inatokeza masuke. Mwishowe, shamba la mkulima linakuwa tayari kuvunwa. Inastaajabisha kama nini kushuhudia muujiza huo wa ukuzi! Tunanyenyekezwa pia tunapotambua Chanzo cha ukuzi huo. Tunaweza kutunza mimea. Tunaweza kuimwagilia maji. Lakini ni Mungu tu ndiye anayeweza kuikuza.—Linganisha 1 Wakorintho 3:6.

2. Yesu alifundisha mambo gani kuhusu ukuzi wa kiroho katika mifano iliyozungumziwa kwenye habari inayotangulia?

2 Kama ilivyotajwa katika habari iliyotangulia, Yesu alilinganisha kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kazi ya mkulima anayepanda mbegu. Katika mfano wa udongo wa aina mbalimbali, Yesu alikazia kwamba hata ingawa mkulima anapanda mbegu nzuri, hali ya moyoni ya mtu inaamua ikiwa mbegu hiyo itakomaa au haitakomaa. (Marko 4:3-9) Katika mfano wa mpandaji anayelala usingizi, Yesu alikazia kwamba mkulima haelewi kikamili jinsi ukuzi unavyotukia, kwa sababu ukuzi unatokea kwa nguvu za Mungu, bali si kwa jitihada za wanadamu. (Marko 4:26-29) Acheni sasa tuzungumzie mifano mingine mitatu ya Yesu—mfano wa mbegu ya haradali, chachu, na wavu wa kukokota. *

Mfano wa Mbegu ya Haradali

3, 4. Mfano wa mbegu ya haradali unakazia mambo gani kuhusu ujumbe wa Ufalme?

3 Mfano wa mbegu ya haradali, ambao umeandikwa pia katika Marko sura ya 4, unakazia mambo mawili: kwanza, ukuzi mkubwa ajabu wa ujumbe wa Ufalme; pili, ulinzi ambao wale wanaokubali ujumbe huo wanapata. Yesu alisema hivi: “Tutaufananisha ufalme wa Mungu na nini, au tutauweka katika mfano gani? Kama mbegu ya haradali, ambayo ilipopandwa katika udongo ilikuwa ndiyo mbegu ndogo zaidi kuliko zote duniani—lakini baada ya kupandwa, humea na kuwa kubwa zaidi kuliko mboga nyingine zote na hutokeza matawi makubwa, hivi kwamba ndege wa mbinguni wanaweza kupata makao chini ya kivuli chake.”—Marko 4:30-32.

4 Mfano huo unaonyesha ukuzi wa “ufalme wa Mungu,” kama inavyothibitishwa na kuenea kwa ujumbe wa Ufalme na kukua kwa kutaniko la Kikristo kuanzia Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. na kuendelea. Mbegu ya haradali ni mbegu ndogo sana ambayo inaweza kuwakilisha kitu kidogo sana. (Linganisha na Luka 17:6.) Hata hivyo, mmea unaozaa haradali unaweza kufikia urefu wa mita 3 mpaka 5 na kuwa na matawi yenye nguvu, na hivyo unaweza kuonwa kuwa mti.—Mt. 13:31, 32.

5. Kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza lilipata ukuzi gani?

5 Kutaniko la Kikristo lilianza kukua polepole mwaka wa 33 W.K. wanafunzi 120 hivi walipotiwa mafuta kwa roho takatifu. Baada ya muda mfupi tu, kutaniko hilo dogo la wanafunzi likawa na maelfu ya waamini. (Soma Matendo 2:41; 4:4; 5:28; 6:7; 12:24; 19:20.) Katika muda wa miaka 30, hesabu ya wavunaji ilikuwa imeongezeka sana hivi kwamba mtume Paulo aliliambia kutaniko la Kolosai kuwa habari njema ilikuwa tayari ‘imehubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.’ (Kol. 1:23) Huo ulikuwa ukuzi mkubwa kama nini!

6, 7. (a) Kumekuwa na ukuzi gani kuanzia mwaka wa 1914? (b) Kutakuwa na ukuzi gani mwingine?

6 Tangu Ufalme wa Mungu uliposimamishwa mbinguni mwaka wa 1914, matawi ya “mti” wa haradali yamepanuka kwa njia isiyotazamiwa. Watu wa Mungu wameona unabii huu wa Isaya ukitimizwa kihalisi: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu.” (Isa. 60:22) Kikundi kidogo cha watiwa-mafuta walioshiriki katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme mwanzoni mwa karne ya 20 hakingewazia hata kidogo kwamba kufikia mwaka wa 2008, Mashahidi wapatao milioni saba wangekuwa wakifanya kazi hiyo katika nchi zaidi ya 230. Kwa kweli, huo ni ukuzi mkubwa ajabu kama ukuzi wa mbegu ya haradali katika mfano wa Yesu!

7 Lakini je, ukuzi huo unakomea hapo? Hapana. Mwishowe raia wa Ufalme wa Mungu watajaa katika dunia yote. Wapinzani wote watakuwa wameondolewa. Jitihada za wanadamu hazitaleta mabadiliko hayo, bali Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova ndiye atakayeingilia kati na kuleta mabadiliko hayo duniani. (Soma Danieli 2:34, 35.) Ndipo tutakapoona utimizo wa mwisho wa unabii mwingine ulioandikwa na Isaya: “Dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isa. 11:9.

8. (a) Ndege walio katika mfano wa Yesu wanawakilisha nani? (b) Hata sasa tunalindwa kutokana na nini?

8 Yesu anasema kwamba ndege wa mbinguni wanapata makao chini ya kivuli cha Ufalme huo. Ndege hao hawawakilishi maadui wa Ufalme ambao wanajaribu kula mbegu nzuri, kama wale ndege wanaotajwa kwenye mfano wa mtu aliyetawanya mbegu katika udongo wa aina mbalimbali. (Marko 4:4) Badala yake, katika mfano huu ndege wanawakilisha watu wenye mioyo minyoofu ambao wanatafuta ulinzi ndani ya kutaniko la Kikristo. Hata sasa, watu hao wanalindwa kutokana na mazoea mapotovu na yenye kuchafua kiroho ya ulimwengu huu mwovu. (Linganisha na Isaya 32:1, 2.) Vivyo hivyo, Yehova aliulinganisha Ufalme wa Kimasihi na mti na kusema hivi kinabii: “Kwenye mlima wa kilele cha Israeli nitakipandikiza, nacho hakika kitazaa matawi na kutokeza matunda na kuwa mwerezi mkubwa. Na chini yake hakika watakaa ndege wote wenye mabawa ya kila aina; watakaa katika uvuli wa majani yake.”—Eze. 17:23.

Mfano wa Chachu

9, 10. (a) Yesu alikazia jambo gani katika mfano wa chachu? (b) Katika Biblia, mara nyingi chachu inawakilisha nini, na tutazungumzia swali gani linalohusiana na jinsi Yesu alivyotumia neno chachu?

9 Nyakati nyingine wanadamu hawawezi kuona ukuzi. Katika mfano unaofuata, Yesu anakazia jambo hilo. Anasema hivi: “Ufalme wa mbinguni ni kama chachu, ambayo mwanamke alichukua na kuitia katika vipimo vikubwa vitatu vya unga, mpaka tonge lote likachacha.” (Mt. 13:33) Chachu hiyo inawakilisha nini, nayo inahusiana jinsi gani na ukuzi wa Ufalme?

10 Katika Biblia, mara nyingi chachu inatumiwa kuwakilisha dhambi. Mtume Paulo alionyesha maana hiyo ya chachu alipozungumza kuhusu uvutano mpotovu wa mtenda-dhambi fulani katika kutaniko la jiji la kale la Korintho. (1 Kor. 5:6-8) Je, Yesu alikuwa sasa akitumia chachu kuwakilisha ukuzi wa kitu kisichofaa?

11. Chachu ilitumiwa jinsi gani zamani katika Israeli?

11 Kabla ya kujibu swali hilo, tunahitaji kukumbuka mambo matatu ya kweli. Kwanza, ingawa Yehova hakuruhusu chachu itumiwe katika sherehe ya Pasaka, nyakati nyingine alikubali dhabihu ambazo zilikuwa na chachu. Chachu ilitumiwa katika matoleo ya ushirika ya kuonyesha shukrani, ambayo mtu alitoa kwa kupenda ili kumshukuru Yehova kwa sababu ya baraka zake nyingi. Mlo huo uliwaletea shangwe wale walioushiriki.—Law. 7:11-15.

12. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Biblia inavyotumia mifano?

12 Pili, ingawa nyakati nyingine kitu fulani katika Maandiko kinaweza kuwakilisha jambo lisilofaa, nyakati nyingine kitu hichohicho kinaweza kutumiwa kuwakilisha jambo linalofaa. Kwa mfano, katika 1 Petro 5:8, Shetani anafananishwa na simba, kuonyesha kwamba yeye ni hatari na mkatili. Lakini katika Ufunuo 5:5, Yesu anafananishwa na simba—“Simba ambaye ni wa kabila la Yuda.” Katika mfano huo wa pili, simba anatumiwa kuwakilisha haki yenye ujasiri.

13. Mfano wa Yesu wa chachu unaonyesha nini kuhusu ukuzi wa kiroho?

13 Tatu, katika mfano wa Yesu, hakusema kwamba chachu iliharibu tonge lote la unga, na kuufanya usiweze kutumiwa. Alikuwa tu akizungumzia njia ya kawaida ya kuoka mikate. Mwanamke huyo aliongeza kimakusudi chachu, na matokeo yakawa mazuri. Chachu hiyo ilitiwa katika tonge lote la unga. Hivyo, mwanamke huyo hangeweza kuona chachu hiyo ikifanya kazi. Hilo linatukumbusha mtu aliyepanda mbegu na kulala usingizi usiku. Yesu alisema kwamba “mbegu huota na hukua na kuwa ndefu, naye [mtu huyo] hajui ni jinsi gani hasa.” (Marko 4:27) Hiyo ni njia rahisi kama nini ya kuonyesha jinsi mtu anavyokua kiroho hatua kwa hatua kwa njia isiyoonekana! Huenda mwanzoni tusione ukuzi huo, lakini mwishowe matokeo yake yanaonekana wazi.

14. Ni jambo gani kuhusu kazi ya kuhubiri linalokaziwa na uhakika wa kwamba chachu inachachusha tonge lote?

14 Wanadamu hawaoni ukuzi huo, lakini unaenea duniani pote. Hilo ni jambo lingine linalokaziwa na mfano wa chachu. Chachu inachachusha tonge lote, ‘vipimo vyote vitatu vikubwa vya unga.’ (Luka 13:21) Kama chachu, kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme ambayo imetokeza ukuzi huo wa kiroho imepanuka hivi kwamba ujumbe wa Ufalme unahubiriwa sasa “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8; Mt. 24:14) Ni pendeleo kubwa kama nini kuchangia ukuzi huo wenye kustaajabisha wa kazi ya Ufalme!

Wavu wa Kukokota

15, 16. (a) Eleza kwa ufupi mfano wa wavu wa kukokota. (b) Wavu wa kukokota unawakilisha nini, na mfano huo unaonyesha jambo gani kuhusu ukuzi wa Ufalme?

15 Jambo la maana zaidi si hesabu ya wale wanaodai kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo bali ni ubora wa wanafunzi hao. Yesu anazungumzia jambo hilo kuhusu ukuzi wa Ufalme anapotoa mfano mwingine kuhusu wavu wa kukokota. Alisema hivi: “Tena ufalme wa mbinguni ni kama wavu wa kukokota ulioshushwa ndani ya bahari na kukusanya samaki wa kila aina.”—Mt. 13:47.

16 Wavu wa kukokota, ambao unawakilisha kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme, unakusanya samaki wa kila aina. Yesu anaendelea kusema hivi: “[Wavu wa kukokota] ulipojaa waliuvuta pwani na, baada ya kuketi, wakakusanya walio wazuri ndani ya vyombo, lakini wasiofaa wakawatupilia mbali. Hivyo ndivyo itakavyokuwa katika umalizio wa mfumo wa mambo: malaika watatoka kwenda na kuwatenga waovu kutoka katikati ya waadilifu nao watawatupa ndani ya tanuru ya moto. Humo ndimo watalia na kusaga meno yao.”—Mt. 13:48-50.

17. Kazi ya kutenganisha inayotajwa katika mfano wa wavu wa kukokota inatukia katika kipindi gani cha wakati?

17 Je, kazi hiyo ya kutenganisha inahusiana na hukumu ya mwisho ya kondoo na mbuzi ambayo Yesu alisema ingetukia wakati ambapo angekuja katika utukufu wake? (Mt. 25:31-33) Hapana. Hukumu hiyo ya mwisho itatukia Yesu atakapokuja wakati wa dhiki kuu. Kinyume chake, kazi ya kutenganisha inayotajwa katika mfano wa wavu wa kukokota inatukia wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo.” * Tunaishi katika kipindi hicho cha wakati—siku zinazotangulia dhiki kuu. Basi, kazi ya kutenganisha inafanywa jinsi gani leo?

18, 19. (a) Kazi ya kutenganisha inafanywa jinsi gani leo? (b) Ni lazima watu wenye mioyo minyoofu wachukue hatua gani? (Ona pia maelezo ya chini yaliyo kwenye ukurasa wa 21.)

18 Leo, kwa njia halisi, mamilioni ya samaki wa mfano kutoka katika bahari ya wanadamu wamevutwa kuingia katika kutaniko la Yehova. Wengine wao wanahudhuria Ukumbusho, wengine wanahudhuria mikutano yetu, na kuna wengine wanaokubali kujifunza Biblia. Lakini je, watu hao wote wanathibitika kuwa Wakristo wa kweli? Huenda ‘wanavutwa pwani,’ lakini Yesu anatuambia kwamba ni “walio wazuri” tu ndio wanaokusanywa ndani ya vyombo. Vyombo hivyo vinawakilisha makutaniko ya Kikristo. Samaki wasiofaa wanatupiliwa mbali, na mwishowe watatupwa katika tanuru ya moto ya mfano, inayofananisha uharibifu wa wakati ujao.

19 Kama samaki wasiofaa, watu wengi ambao walikuwa wakijifunza Biblia na watu wa Yehova wameacha kujifunza. Wengine ambao walizaliwa na wazazi Wakristo hawataki kamwe kufuata hatua za Yesu kwa ukaribu. Hawana nia ya kufanya uamuzi wa kumtumikia Yehova au wamemtumikia kwa muda kisha wakaacha. * (Eze. 33:32, 33) Hata hivyo, ni lazima watu wote wenye mioyo minyoofu wakusanywe ndani ya makutaniko ambayo ni kama vyombo kabla ya siku ya mwisho ya hukumu na waendelee kukaa mahali penye usalama.

20, 21. (a) Tumejifunza nini kwa kuzungumzia mifano ya Yesu kuhusu ukuzi? (b) Umeazimia kufanya nini?

20 Kwa hiyo, tumejifunza nini baada ya kuzungumzia kwa ufupi mifano ya Yesu kuhusu ukuzi? Kwanza, kama ukuzi wa mbegu ya haradali, kumekuwa na ongezeko kubwa duniani la watu wanaokubali ujumbe wa Ufalme. Hakuna kitu kinachoweza kuizuia kazi ya Yehova isienee! (Isa. 54:17) Zaidi ya hayo, wale ambao wametafuta “makao chini ya kivuli” cha mti huo wamelindwa kiroho. Pili, Mungu ndiye anayeikuza. Kama ile chachu isiyoonekana ilivyoenea katika tonge lote, nyakati nyingine ukuzi huo hauonekani waziwazi wala kueleweka, lakini unatukia! Tatu, si watu wote waliokubali ujumbe huo ambao wanathibitika kuwa wanafaa. Wengine wamekuwa kama samaki wasiofaa katika mfano wa Yesu.

21 Hata hivyo, inatia moyo sana kuona watu wengi wanaofaa wakivutwa na Yehova! (Yoh. 6:44) Hilo limetokeza ongezeko kubwa sana katika nchi mbalimbali. Utukufu wote unamwendea Yehova Mungu kwa ajili ya ukuzi huo. Kwa kuwa tunaona ukuzi huo, kila mmoja wetu anapaswa kuchochewa kutii himizo hili ambalo liliandikwa karne nyingi zilizopita: “Asubuhi panda mbegu zako . . . , kwa maana hujui ni wapi hii itafanikiwa, hapa au pale, au ikiwa zote mbili zitakuwa njema.”—Mhu. 11:6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Maelezo yafuatayo ni marekebisho ya maelezo ya wakati uliopita katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1992 (15/6/1992), ukurasa wa 17-22, na Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1976, (1/4/1976) ukurasa wa 149-154 au toleo la Kiingereza la Oktoba 1, 1975 (1/10/1975), ukurasa wa 589-608, au la Kifaransa la Januari 15, 1976, (15/1/1976) ukurasa wa 45-50.

^ fu. 17 Ingawa andiko la Mathayo 13:39-43 linazungumzia jambo tofauti kuhusu kazi ya kuhubiri juu ya Ufalme, linatimizwa wakati mmoja na mfano wa wavu wa kukokota, yaani, wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo.” Kutenganishwa kwa samaki wa mfano ni kazi inayoendelea, kama vile kazi ya kupanda na kuvuna inavyoendelea katika kipindi hicho chote cha wakati.—Mnara wa Mlinzi, Oktoba 15, 2000, ukurasa wa 25-26; Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli, ukurasa wa 178-181, fungu la 8-11.

^ fu. 19 Je, hilo linamaanisha kwamba malaika wamemtupilia mbali kila mtu ambaye ameacha kujifunza au kushirikiana na watu wa Yehova kana kwamba hafai? Hapana! Njia imefunguliwa kwa mtu yeyote anayetamani kwa moyo wote kumrudia Yehova.—Mal. 3:7.

Ungesema Nini?

• Mfano wa Yesu wa mbegu ya haradali unatufundisha nini kuhusu ukuzi wa Ufalme na ulinzi wa kiroho?

• Chachu katika mfano wa Yesu inawakilisha nini, na Yesu anakazia ukweli gani kuhusu ukuzi wa Ufalme?

• Mfano wa wavu wa kukokota unakazia jambo gani kuhusu ukuzi wa Ufalme?

• Tunaweza kuhakikisha jinsi gani kwamba tunaendelea kuwa kati ya wale ambao ‘wamekusanywa ndani ya vyombo’?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mfano wa mbegu ya haradali unatufundisha nini kuhusu ongezeko la Ufalme?

[Picha katika ukurasa wa 19]

Tunajifunza nini kutokana na mfano wa chachu?

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kazi ya kutenganisha samaki wazuri na samaki wasiofaa inawakilisha nini?