Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mheshimu Yehova kwa Kuonyesha Heshima

Mheshimu Yehova kwa Kuonyesha Heshima

Mheshimu Yehova kwa Kuonyesha Heshima

“Utendaji [wa Yehova] ni utukufu na fahari.”—ZAB. 111:3.

1, 2. (a) Neno “utukufu” linamaanisha nini? (b) Ni maswali gani yatakayozungumziwa katika habari hii?

MADISON mwenye umri wa miaka 10 alipoulizwa afafanue neno “heshima” alijibu hivi mara moja, “Ni kuvalia vizuri.” Huenda binti huyo mdogo hakujua kwamba Biblia inasema kwamba Mungu ‘amevaa utukufu,’ au heshima, “na fahari.” (Zab. 104:1) Nyakati nyingine wanadamu wanaweza kuonyesha heshima kwa kuvalia vizuri. Kwa mfano, mtume Paulo alitaka wanawake Wakristo “wajipambe kwa mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili, si kwa mitindo ya kusuka nywele na dhahabu au lulu au mavazi yaliyo ghali sana.” (1 Tim. 2:9) Lakini kujiendesha kwa njia ya heshima inayokweza “utukufu na fahari” ya Yehova kunatia ndani mambo mengi zaidi.—Zab. 111:3.

2 Katika Biblia, neno la Kiebrania linalomaanisha “utukufu” linaweza pia kutafsiriwa kuwa “fahari,” “ukuu,” “adhama,” na “heshima.” Kamusi ya Kiswahili Sanifu inafafanua neno “utukufu” kuwa “hali ya kutukuka; taadhima, hadhi, heshima.” Na hakuna mtu anayestahili kuheshimiwa au kustahiwa sana kuliko Yehova. Kwa hiyo, tukiwa watumishi wake waliojiweka wakfu, tunapaswa kuongea na kutenda kwa njia inayomletea heshima. Hata hivyo, kwa nini wanadamu wanaweza kutenda kwa heshima? Utukufu na fahari ya Yehova inaonyeshwa jinsi gani? Utukufu wa Mungu unapaswa kuwa na uvutano gani kwetu? Yesu Kristo anaweza kutufunza nini kuhusu kuonyesha sifa hiyo? Na tunaweza kuonyesha jinsi gani heshima inayomtukuza Mungu?

Kwa Nini Tunaweza Kutenda kwa Heshima?

3, 4. (a) Tunapaswa kutenda jinsi gani kwa sababu ya heshima ambayo tumepewa? (b) Unabii wa Zaburi 8:5-9 unamhusu nani? (Ona maelezo ya chini.) (c) Yehova aliwapa nani heshima wakati uliopita?

3 Wanadamu wote wanaweza kutenda kwa heshima kwa sababu wameumbwa kwa mfano wa Mungu. Yehova alimheshimu mwanadamu wa kwanza kwa kumpa kazi ya kuitunza dunia. (Mwa. 1:26, 27) Hata baada ya mwanadamu kupoteza ukamilifu, Yehova alitaja tena daraka la mwanadamu kuhusiana na dunia. Hivyo, bado Mungu ‘anawavika wanadamu taji’ la utukufu, au heshima. (Soma Zaburi 8:5-9.) * Kwa kuwa tumetukuzwa au kuheshimiwa tunapaswa pia kumheshimu Yehova kwa kulisifu jina lake kuu kwa heshima na utukufu.

4 Yehova hasa ameweka kiasi fulani cha utukufu juu ya wale ambao wanamtolea utumishi mtakatifu. Mungu alimheshimu Abeli kwa kukubali dhabihu yake, lakini alikataa dhabihu iliyotolewa na Kaini, ndugu yake. (Mwa. 4:4, 5) Musa aliagizwa ‘atie sehemu ya utukufu wake’ juu ya Yoshua, ambaye angewaongoza Waisraeli baada yake. (Hes. 27:20) Biblia inasema hivi kumhusu Sulemani, mwana wa Daudi: “Yehova akaendelea kumfanya Sulemani kuwa mkuu zaidi mbele ya macho ya Israeli wote na kuweka juu yake heshima ya kifalme ambayo haikuwa imepata kuwa juu ya mfalme yeyote kabla yake juu ya Israeli.” (1 Nya. 29:25) Mungu ataweka heshima au utukufu wa pekee juu ya Wakristo watiwa-mafuta waliofufuliwa, ambao wametangaza kwa uaminifu “utukufu wa fahari ya ufalme wake.” (Zab. 145:11-13) Umati unaoongezeka wa “kondoo wengine” wa Yesu pia una daraka tukufu na takatifu la kumsifu Yehova.—Yoh. 10:16.

Utukufu na Fahari ya Yehova Inaonekana Wazi

5. Utukufu wa Yehova ni mkuu kadiri gani?

5 Katika wimbo unaoonyesha ukuu wa Mungu na udogo wa mwanadamu, mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Ee Yehova Bwana wetu, jina lako ni lenye utukufu kama nini katika dunia yote, wewe ambaye utukufu wako unasimuliwa juu ya mbingu!” (Zab. 8:1) Tangu kuumbwa kwa “mbingu na dunia” mpaka baada ya utimizo mkuu wa kusudi la Mungu la kuifanya dunia iwe paradiso na kuwainua wanadamu wote kufikia ukamilifu, tangu milele mpaka milele, Yehova Mungu peke yake ndiye aliye mkuu na mwenye utukufu zaidi katika ulimwengu wote.—Mwa. 1:1; 1 Kor. 15:24-28; Ufu. 21:1-5.

6. Kwa nini mtunga-zaburi alisema kwamba Yehova amevaa utukufu?

6 Hapana shaka kwamba mtunga-zaburi aliyemwogopa Mungu aliguswa moyo sana alipoona fahari kuu ya mbingu wakati wa usiku, huku nyota zenye kumetameta kama “vito” zikiwa zimetapakaa kotekote! Akiwa amestaajabishwa na jinsi Mungu ‘alivyozitandaza mbingu kama hema,’ mtunga-zaburi alisema kwamba Yehova amevaa utukufu na fahari kwa sababu ya uwezo Wake wa pekee sana wa kuumba. (Soma Zaburi 104:1, 2.) Utukufu na fahari ya Muumba huyo mweza yote ambaye haonekani, unaonekana wazi katika kazi zake zinazoonekana.

7, 8. Ni mambo gani yanayotuonyesha utukufu na fahari ya Yehova katika mbingu?

7 Kwa mfano, fikiria kikundi cha nyota cha Kilimia. Kikundi hicho ni kama bahari kubwa sana yenye nyota, sayari, na mfumo wa jua. Katika kikundi hicho, Dunia inaonekana kuwa ndogo sana kama chembe moja ya mchanga kwenye ufuo mkubwa sana wa bahari. Kikundi hicho kimoja tu cha nyota kina nyota zaidi ya bilioni 100! Ikiwa ungeweza kuhesabu nyota moja kila sekunde kwa saa 24 kwa siku bila kuacha, itakuchukua miaka zaidi ya 3,000 kuhesabu nyota bilioni 100.

8 Ikiwa kikundi cha Kilimia peke yake kina nyota zaidi ya bilioni 100, basi ulimwengu mzima una nyota ngapi? Wataalamu wa nyota wanakadiria kwamba mbali na kikundi cha Kilimia huenda kuna vikundi bilioni 50 kufikia bilioni 125 vya nyota. Kuna nyota ngapi katika ulimwengu wote? Bila shaka, hatuwezi kuhesabu idadi hiyo kubwa ajabu ya nyota. Hata hivyo, Yehova “anahesabu idadi ya nyota; zote anaziita kwa majina yake.” (Zab. 147:4) Unapoona jinsi Yehova anavyovaa fahari na utukufu, je, huchochewi kulisifu jina lake kuu?

9, 10. Uandalizi wa mkate unatukuza jinsi gani hekima ya Muumba wetu?

9 Baada ya kutazama mbingu zenye utukufu, acheni sasa tukazie fikira kitu cha kawaida kama mkate. Yehova ndiye “Mtengenezaji wa mbingu na dunia” na vilevile ndiye “anayewapa wenye njaa mkate.” (Zab. 146:6, 7) “Utukufu na fahari” ya Mungu inaonekana katika kazi zake kuu, kutia ndani mimea inayotokeza mkate. (Soma Zaburi 111:1-5.) Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii.” (Mt. 6:11) Mkate ulikuwa chakula kikuu cha watu wengi wa zamani, kutia ndani Waisraeli. Ingawa mkate unaonwa kuwa chakula rahisi, utaratibu wa kemikali wa hali ya juu sana unaunganisha vitu vichache vya msingi na kutokeza mkate mtamu.

10 Biblia ilipokuwa ikiandikwa, Waisraeli walikuwa wakitumia unga wa ngano au shayiri pamoja na maji kutengeneza mkate. Nyakati nyingine, chachu, au hamira, ilitumiwa kuoka mkate. Vitu hivyo vya msingi vinapochanganywa vinatokeza mchanganyiko wenye kustaajabisha ulio na kemikali mbalimbali ambazo zinaungana kwa njia ya pekee. Wanadamu hawaelewi kikamili jinsi kemikali hizo zinavyoungana. Zaidi ya hayo, mwili unasaga mkate kwa njia ya pekee ambayo pia inastaajabisha. Ndiyo sababu mtunga-zaburi aliimba hivi: “Jinsi kazi zako zilivyo nyingi, Ee Yehova! Zote umezifanya kwa hekima”! (Zab. 104:24) Je, wewe pia unachochewa vivyo hivyo kumsifu Yehova?

Utukufu na Fahari ya Mungu Inakuchochea Jinsi Gani?

11, 12. Kutafakari kuhusu kazi za Mungu za uumbaji kunaweza kuwa na matokeo gani kwetu?

11 Si lazima tuwe wataalamu wa nyota ili tustaajabie anga la usiku wala hatuhitaji kuwa wanakemia ili tufurahie mkate. Hata hivyo, ili tuthamini utukufu wa Muumba wetu, tunahitaji kutumia wakati kutafakari kuhusu kazi za mikono yake. Kutafakari kuhusu kazi hizo kunaweza kutusaidia jinsi gani? Kutafakari kuhusu kazi hizo kutatuchochea kama tunavyochochewa tunapotafakari kuhusu kazi nyingine za Yehova.

12 Daudi aliimba hivi kuhusu kazi nyingine kuu ambazo Yehova alitenda kwa ajili ya watu Wake: “Fahari tukufu ya utukufu wako na mambo ya kazi zako za ajabu nitayafanya yawe hangaiko langu.” (Zab. 145:5) Tunaonyesha kwamba tunahangaikia kazi hizo kwa kujifunza Biblia na kutumia wakati kutafakari yale tunayosoma. Kutafakari kwa njia hiyo kunaweza kuwa na matokeo gani juu yetu? Kunatufanya tuthamini hata zaidi utukufu na fahari ya Mungu. Hivyo basi, tunachochewa kujiunga na Daudi katika kumheshimu Yehova kwa kusema hivi: “Nitautangaza ukuu wako.” (Zab. 145:6) Kutafakari kuhusu kazi za ajabu za Mungu kunapaswa kutia nguvu uhusiano wetu pamoja na Yehova na kutuchochea kuwaambia wengine kumhusu kwa shauku na bidii. Je, unatangaza kwa bidii habari njema na kuwasaidia watu wathamini utukufu, fahari, na ukuu wa Yehova Mungu?

Yesu Anaonyesha Utukufu wa Mungu kwa Ukamili

13. (a) Kulingana na Danieli 7:13, 14, Yehova amempa Mwana wake nini? (b) Akiwa Mfalme, Yesu anawatendea jinsi gani raia wake?

13 Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alitangaza habari njema kwa bidii na kumletea heshima Baba yake wa mbinguni mwenye utukufu na ukuu. Yehova alimpa Mwana wake mzaliwa-pekee heshima ya pekee kwa kumpa ‘utawala na ufalme.’ (Soma Danieli 7:13, 14.) Hata hivyo, Yesu hana kiburi wala hawadharau wengine. Yuko tofauti sana—yeye ni Mtawala mwenye huruma ambaye anaelewa udhaifu wa raia wake na anawaheshimu. Kwa mfano, fikiria jinsi Yesu akiwa Mfalme Aliyechaguliwa alivyowatendea watu aliokutana nao, hasa wale waliodharauliwa na wale ambao hawakupendwa na wengine.

14. Wenye ukoma walionwa jinsi gani katika Israeli zamani?

14 Mara nyingi, watu wenye ukoma katika nyakati za zamani waliteseka sana kwa muda mrefu kabla ya kufa. Pole kwa pole, viungo vyao vya mwili viliambukizwa ukoma. Kumponya mtu mwenye ukoma kulionwa kuwa jambo gumu sana kama tu kumfufua mfu. (Hes. 12:12; 2 Fal. 5:7, 14) Watu wenye ukoma walitangazwa kuwa wasio safi na walichukiwa sana na kutengwa na jamii. Wenye ukoma walipokuwa wakiwakaribia watu, walipaswa kuwaonya hivi kwa sauti: “Si safi, si safi!” (Law. 13:43-46) Mtu mwenye ukoma alikuwa kama mtu aliyekufa. Maandishi ya marabi yanasema kwamba mwenye ukoma aliruhusiwa kusimama umbali wa mita 1.7 hivi kutoka kwa mtu yeyote. Iliripotiwa kwamba kiongozi fulani wa kidini alipomwona mwenye ukoma, hata kwa mbali, alimrushia mawe ili asimkaribie.

15. Yesu alimtendea jinsi gani mtu fulani mwenye ukoma?

15 Hata hivyo, jibu la Yesu kwa mwenye ukoma aliyemfikia na kumsihi amponye linagusa moyo. (Soma Marko 1:40-42.) Badala ya kumfukuza mtu huyo mwenye ukoma ambaye aliepukwa na watu, Yesu alimtendea kwa njia ya huruma na ya heshima. Yesu alimwona kuwa mwanadamu wa kusikitikiwa ambaye alihitaji kusaidiwa. Akichochewa kutoka moyoni, Yesu alimhurumia na kuchukua hatua ya haraka ya kumsaidia. Aliunyoosha mkono wake, akamgusa mtu huyo mwenye ukoma, na kumponya.

16. Umejifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyowatendea wengine?

16 Tukiwa wafuasi wa Yesu, tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani katika kuwaonyesha wengine heshima kama Baba yake? Njia moja ni kutambua kwamba wanadamu wote—bila kufikiria cheo chao, hali yao ya afya, au umri wao—wanastahili kuheshimiwa na kustahiwa. (1 Pet. 2:17) Wale walio na madaraka ya kusimamia, kama vile waume, wazazi, na wazee Wakristo wanahitaji hasa kuwaheshimu wale walio chini yao na kuwasaidia wajiheshimu. Biblia inasema hivi ili kukazia kwamba hilo ni takwa kwa Wakristo wote: “Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.”—Rom. 12:10.

Kuonyesha Heshima Katika Ibada

17. Tunaweza kujifunza nini kutokana na Maandiko kuhusu kuonyesha heshima tunapomwabudu Yehova?

17 Tunapaswa kujiendesha kwa heshima hasa tunapomwabudu Yehova. Andiko la Mhubiri 5:1 linasema hivi: “Linda miguu yako wakati wowote unapoenda kwenye nyumba ya Mungu wa kweli.” Musa na Yoshua waliamuriwa wavue viatu vyao waliposimama mahali patakatifu. (Kut. 3:5; Yos. 5:15) Walipaswa kufanya hivyo ili kuonyesha heshima au staha. Makuhani Waisraeli waliamuriwa wavae suruali za kitani “ili kuufunika mwili ulio uchi.” (Kut. 28:42, 43) Hilo liliwazuia wasionyeshe uchi wao walipotumikia kwenye madhabahu. Kila mshiriki wa familia ya kuhani alipaswa kufuata viwango vya Mungu vya heshima.

18. Tunaonyesha jinsi gani heshima katika ibada yetu kwa Yehova?

18 Kwa hivyo, tunapaswa kuonyesha heshima na staha katika ibada. Ili tustahili kuonyeshwa heshima na staha, ni lazima tutende kwa heshima. Hatupaswi kujifanya tu kuwa wenye heshima au kuwa na heshima kijuujuu tu. Haipaswi tu kuwa heshima inayoonwa na wanadamu, inapaswa kutoka moyoni ambamo Mungu anaweza kuona. (1 Sam. 16:7; Met. 21:2) Heshima inapaswa kuwa sehemu ya maisha yetu nayo inapaswa kuongoza tabia yetu, mtazamo wetu, uhusiano wetu na wengine, na hata jinsi tunavyohisi na kujiona. Kwa kweli, heshima inapaswa kuonekana nyakati zote na katika kila jambo tunalosema na kufanya. Tunaonyesha kwamba tunatii maneno haya ya mtume Paulo kupitia mwenendo wetu, mavazi na mapambo yetu, na jinsi tunavyowatendea wengine: “Sisi hatutoi sababu yoyote ya kukwaza kwa njia yoyote, ili huduma yetu isilaumiwe; bali katika kila njia tunajipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu.” (2 Kor. 6:3, 4) ‘Tunalipamba fundisho la Mwokozi wetu, Mungu, katika mambo yote.’—Tito 2:10.

Endelea Kuonyesha Heshima ya Kimungu

19, 20. (a) Ni njia gani bora ya kuwaonyesha wengine heshima? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini kuhusiana na heshima?

19 Heshima inaonyeshwa na Wakristo watiwa-mafuta, ambao ni “mabalozi walio badala ya Kristo.” (2 Kor. 5:20) “Kondoo wengine,” ambao wanawaunga mkono kwa ushikamanifu, ni wajumbe wenye heshima wa Ufalme wa Kimasihi. Balozi au mjumbe anaitetea serikali yake kwa ujasiri na kwa heshima. Kwa hivyo, tunapaswa kuitetea kwa heshima na kwa ujasiri serikali ya Mungu, Ufalme wake. (Efe. 6:19, 20) Na je, hatuwaonyeshi wengine heshima tunapowahubiria “habari njema za jambo bora”?—Isa. 52:7.

20 Tunapaswa kuazimia kumtukuza Mungu kwa kujiendesha wenyewe kwa njia inayomletea heshima. (1 Pet. 2:12) Acheni sikuzote tumheshimu sana, tuheshimu ibada yake, na kuwaheshimu waabudu wenzetu. Na Yehova, ambaye amevaa fahari na utukufu au heshima, atapendezwa na njia yetu ya heshima ya kumwabudu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Maneno ya Daudi katika Zaburi ya 8 ni ya kinabii pia na yalimhusu mwanadamu mkamilifu Yesu Kristo.—Ebr. 2:5-9.

Ungesema Nini?

• Kuthamini fahari ya utukufu wa Yehova kunapaswa kuwa na matokeo gani kwetu?

• Tunaweza kujifunza nini kuhusu heshima kutokana na jinsi Yesu alivyomtendea mtu fulani mwenye ukoma?

• Tunaweza kumheshimu Yehova kwa njia gani zinazoonyesha heshima?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Yehova alimheshimu Abeli jinsi gani?

[Picha katika ukurasa wa 14]

Kazi kuu za Yehova zinaonekana hata katika uandalizi wa mkate

[Picha katika ukurasa wa 15]

Umejifunza nini kuhusu heshima kutokana na jinsi Yesu alivyomtendea mtu fulani mwenye ukoma?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Tunamheshimu Yehova tunapoonyesha heshima katika ibada