Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Barua kwa Wagalatia, Waefeso, Wafilipi, na Wakolosai

Mambo Makuu Katika Barua kwa Wagalatia, Waefeso, Wafilipi, na Wakolosai

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Barua kwa Wagalatia, Waefeso, Wafilipi, na Wakolosai

BAADA ya kusikia kwamba Wakristo fulani walikuwa wakipotoshwa na wafuasi wa dini ya Kiyahudi ili waiache ibada safi, mtume Paulo anaandika barua kali kwa “makutaniko ya Galatia.” (Gal. 1:2) Barua hiyo iliyoandikwa mwaka wa 50-52 W.K., ina mashauri ya moja kwa moja na himizo zito.

Miaka kumi hivi baadaye, akiwa “mfungwa wa Kristo Yesu” huko Roma, Paulo anayaandikia makutaniko yaliyo Efeso, Filipi, na Kolosai, na kuwapa mashauri mazuri na kuwatia moyo kwa upendo. (Efe. 3:1) Sisi leo tunaweza kufaidika kwa kukazia uangalifu ujumbe ulio katika vitabu vya Biblia vya Wagalatia, Waefeso, Wafilipi, na Wakolosai.—Ebr. 4:12.

“KUTANGAZWA KUWA WAADILIFU”—JINSI GANI?

(Gal. 1:1–6:18)

Kwa kuwa wafuasi wa dini ya Kiyahudi wanajaribu kwa ujanja kumvunjia Paulo heshima, anatetea utume wake kwa kueleza habari fulani kuhusu maisha yake. (Gal. 1:11–2:14) Akipinga mafundisho yao ya uwongo, Paulo anasema hivi: “Mtu hutangazwa kuwa mwadilifu, si kwa sababu ya matendo ya sheria, bali tu kupitia imani kumwelekea Kristo Yesu.”—Gal. 2:16.

Paulo anasema kwamba Kristo ‘aliwaachilia huru kwa kuwanunua wale walio chini ya sheria’ na kuwaweka huru ili wafurahie uhuru wa Kikristo. Anawapa Wagalatia himizo hili lenye uzito: “Simameni imara, na msijiache wenyewe kufungwa tena katika nira ya utumwa.”—Gal. 4:4, 5; 5:1.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

3:16-18, 28, 29—Je, bado agano la Kiabrahamu ni halali? Ndiyo. Agano la Sheria halikuchukua mahali pa agano ambalo Mungu alifanya pamoja na Abrahamu, bali liliongezwa kwenye agano hilo. Hivyo, agano la Kiabrahamu liliendelea kuwapo baada ya Sheria ‘kufutwa.’ (Efe. 2:15) Ahadi zake zinapitishwa kwa “uzao” wa kweli wa Abrahamu, yaani, Kristo Yesu, ambaye ndiye sehemu ya msingi, na kwa wale “wa Kristo.”

6:2—“Sheria ya Kristo” ni nini? Sheria hiyo inahusisha mambo yote ambayo Yesu alifundisha na kuamuru. Inatia ndani hasa amri ya ‘kupendana.’—Yoh. 13:34.

6:8—Ni kwa njia gani ‘tunapanda kwa roho’? Tunafanya hivyo kwa kuishi kwa njia inayoiwezesha roho ya Mungu kutenda kazi kwa uhuru ndani yetu. Kupanda kwa roho kunatia ndani kushiriki kwa moyo wote katika shughuli zinazoiwezesha roho hiyo kutenda kazi kwa uhuru.

Mambo Tunayojifunza:

1:6-9. Matatizo yanapotokea katika kutaniko, wazee Wakristo wanapaswa kuchukua hatua ya haraka. Kwa kutoa hoja zenye kusadikisha na kutumia Maandiko, wanaweza kupinga haraka habari za uwongo.

2:20. Fidia ni zawadi ya Mungu kwa kila mmoja wetu. Tunapaswa kuiona hivyo.—Yoh. 3:16.

5:7-9. Mashirika mabaya yanaweza ‘kutuzuia tusiendelee kuitii kweli.’ Ni jambo la hekima kuyaepuka.

6:1, 2, 5Wale walio na “sifa za kustahili kiroho” wanaweza kutusaidia kubeba mzigo mzito, kama vile jambo lenye kutaabisha au tatizo zito ambalo limetokea baada ya sisi kujikwaa kwa kufanya kosa bila kujua. Lakini ni lazima sisi wenyewe tujibebee mzigo wa madaraka ya Kikristo.

‘KUKUSANYA VITU VYOTE KATIKA KRISTO’

(Efe. 1:1–6:24)

Akikazia kichwa cha umoja wa Kikristo katika barua yake kwa Waefeso, Paulo anazungumzia “usimamizi wa mambo kwenye kikomo kamili cha nyakati zilizowekwa rasmi . . . kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani.” Kristo ametoa “zawadi katika wanadamu” ili kuwasaidia wote ‘kuufikia umoja katika imani.’—Efe. 1:10; 4:8, 13.

Ili kumheshimu Mungu na kuendeleza umoja, Wakristo wanapaswa “kuvaa utu mpya” na ‘kujitiisha kwa mmoja na mwenzake katika kumwogopa Kristo.’ Wanahitaji pia “kusimama imara kupinga hila za Ibilisi” kwa kuvaa mavazi kamili ya silaha za kiroho.—Efe. 4:24; 5:21; 6:11.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:4-7—Ni kwa njia gani Wakristo watiwa-mafuta waliagizwa kimbele muda mrefu kabla hawajazaliwa? Waliagizwa kimbele au kuamuliwa kimbele wakiwa kikundi, si mtu mmoja-mmoja. Hilo lilitukia kabla ya wanadamu wenye dhambi kuzaliwa. Unabii ulio katika Mwanzo 3:15, uliotangazwa kabla ya mimba ya mwanadamu yeyote mwenye dhambi kutungwa, unatia ndani kusudi la Mungu la kwamba wafuasi fulani wa Kristo watawale pamoja naye mbinguni.—Gal. 3:16, 29.

2:2—Ni kwa njia gani roho ya ulimwengu ni kama hewa, na mamlaka yake inaonekana jinsi gani? “Roho ya ulimwengu”—roho ya kujitegemea na ya kutotii—iko kila mahali kama hewa tunayopumua. (1 Kor. 2:12) Mamlaka au nguvu za roho hiyo zinaonekana waziwazi kwa kuwa inashawishi, inatenda kazi daima, na ina uvutano mwingi sana juu ya watu.

2:6—Ni kwa njia gani Wakristo watiwa-mafuta wanaweza kuwa “mahali pa kimbingu” wakiwa bado duniani? Katika mstari huo, maneno “mahali pa kimbingu” hayamaanishi urithi wao wa kimbingu ambao wameahidiwa. Badala yake, yanamaanisha msimamo wao wa kiroho uliokwezwa ambao wanapata ‘wanapotiwa muhuri kwa roho takatifu iliyoahidiwa.’—Efe. 1:13, 14.

Mambo Tunayojifunza:

4:8, 11-15. Yesu Kristo “alichukua mateka,” yaani, aliwatoa wanadamu waliokuwa chini ya mamlaka ya Shetani ili awatumie wakiwa zawadi kwa kusudi la kulijenga kutaniko la Kikristo. Tunaweza ‘kukua kwa upendo katika mambo yote ndani ya Kristo’ kwa kutii na kujitiisha kwa wale wanaoongoza kati yetu na kuunga mkono mipango ya kutaniko.—Ebr. 13:7, 17.

5:22-24, 33. Zaidi ya kujitiisha kwa mume wake, mke anapaswa pia kumheshimu. Mke anaonyesha hilo kupitia “roho ya utulivu na ya upole” na kujitahidi kumheshimu kwa kusema mambo mazuri kuhusu mume wake na kazi zake na kujitahidi kufanikisha maamuzi yake.—1 Pet. 3:3, 4; Tito 2:3-5.

5:25, 28, 29. Mume anapaswa kumwandalia mke wake—kimwili, kihisia, na kiroho—kama ‘anavyojilisha’ mwenyewe. Pia, anapaswa kuonyesha kwamba anamthamini kwa kutumia wakati wa kutosha pamoja naye na kumwonyesha fadhili kwa maneno na matendo.

6:10-13. Ili kupinga majeshi ya roho waovu, tunahitaji kujitahidi kwa moyo wote kuvaa mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu.

‘ENDELEA KUTEMBEA KWA UTARATIBU’

(Flp. 1:1–4:23)

Katika barua yake kwa Wafilipi, Paulo anakazia upendo. Anasema hivi: “Hili ndilo ninaloendelea kusali, kwamba upendo wenu uwe mwingi hata zaidi na zaidi pamoja na ujuzi sahihi na utambuzi kamili.” Anawasaidia kuepuka mtego wa kujiamini kupita kiasi, kwa kuwahimiza hivi: “Endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.”—Flp. 1:9; 2:12.

Paulo anawatia moyo wale waliokomaa wafuatilie “kuelekea ule mradi kwa ajili ya tuzo la mwito wa Mungu.” Anasema hivi: “Kwa kadiri ambavyo tumefanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika kawaida hiyohiyo.”—Flp. 3:14-16.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:23—Paulo alikuwa chini ya mkazo kutokana na ‘mambo gani mawili,’ na ni “kufunguliwa” gani ambako alitamani? Kwa sababu ya hali zake, Paulo alikuwa chini ya mkazo wa mambo haya mawili yaliyomkabili: uhai au kifo. (Flp. 1:21) Ingawa hataji kile ambacho angechagua, anataja kile ambacho alitamani—“kufunguliwa na kule kuwa pamoja na Kristo.” (Flp. 3:20, 21; 1 The. 4:16) “Kufunguliwa” huko wakati wa kuwapo kwa Kristo kungemwezesha Paulo kupata thawabu ambayo Yehova alikuwa amemtayarishia.—Mt. 24:3.

2:12, 13—Mungu anatuwezesha kwa njia gani ‘kuwa na nia na kutenda’? Roho takatifu ya Yehova inaweza kutenda katika moyo wetu na akili yetu ili kuongeza hamu yetu ya kufanya yote tuwezayo katika utumishi wake. Hivyo, hatuachwi bila msaada ‘tunapoendelea kuufanyia kazi wokovu wetu.’

Mambo Tunayojifunza:

1:3-5. Ingawa walikuwa maskini kimwili, Wafilipi walituwekea mfano bora wa kuonyesha ukarimu.—2 Kor. 8:1-6.

2:5-11. Kama kielelezo cha Yesu kinavyoonyesha, kuwa mnyenyekevu hakuonyeshi kwamba mtu ni dhaifu bali kunaonyesha kwamba ana nguvu za kufanya mambo yanayofaa. Zaidi ya hilo, Yehova anawakweza wanyenyekevu.—Met. 22:4.

3:13. “Mambo ya nyuma” yanaweza kuwa mambo kama vile kazi yenye mshahara mnono, usalama wa kuwa katika familia tajiri, au hata dhambi nzito za zamani ambazo tumetubu na ‘kuoshwa na kuwa safi.’ (1 Kor. 6:11) Tunapaswa kuyasahau mambo hayo, yaani, kuacha kuyahangaikia, na “kujinyoosha kwenda mbele kuelekea mambo yaliyo mbele.”

“KUIMARISHWA KATIKA IMANI”

(Kol. 1:1–4:18)

Katika barua yake kwa Wakolosai, Paulo anafichua maoni yasiyofaa ya walimu wa uwongo. Anasema kwamba wokovu hautokani na matakwa ya Sheria, bali unatokana na ‘kuendelea katika imani.’ Paulo anawatia moyo Wakolosai ‘waendelee kutembea katika muungano na Kristo, wakiwa wametia mizizi na kujengwa katika yeye na kuimarishwa katika imani.’ Wanapaswa kutenda jinsi gani baada ya kuimarishwa?—Kol. 1:23; 2:6, 7.

Paulo anaandika hivi: “Zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano. Pia, acheni amani ya Kristo itawale mioyoni mwenu.” Mtume huyo anawaambia hivi: “Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kama kwa wanadamu.” Anasema hivi kuhusu wale walio nje ya kutaniko: “Endeleeni kutembea kwa hekima” kuwaelekea.—Kol. 3:14, 15, 23; 4:5.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:8—Ni ‘mambo gani ya msingi ya ulimwengu’ ambayo Paulo alionya juu yake? Hayo ni mambo ya ulimwengu wa Shetani—mambo au kanuni za msingi zinazouongoza au kuuchochea. (1 Yoh. 2:16) Mambo hayo yanatia ndani falsafa, kupenda vitu vya kimwili, na dini za uwongo za ulimwengu huu.

4:16—Kwa nini barua kwa Walaodikia si sehemu ya Biblia? Huenda ni kwa sababu barua hiyo haikuwa na habari zilizofaa siku zetu. Au huenda ilirudia mambo yaliyotajwa katika barua nyingine zilizokubalika kuwa sehemu ya Maandiko.

Mambo Tunayojifunza:

1:2, 20. Fidia, ambayo ni uandalizi wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu, inaweza kusafisha dhamiri yetu kutokana na hatia na kutupa amani ya akili.

2:18, 23. “Unyenyekevu wa kujifanya,” yaani, kujifanya kuwa mnyenyekevu ili kuwapendeza wengine labda kwa kujinyima vitu vya kimwili au kuutendea mwili kwa ukali kunaonyesha kwamba mtu ‘anajivuna kutokana na hali yake ya akili ya kimwili.’