Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fikiria ‘Mwisho Baadaye’

Fikiria ‘Mwisho Baadaye’

Fikiria ‘Mwisho Baadaye’

TUNAKABILIWA na maamuzi mengi maishani. Bila shaka, ni jambo la hekima kutaka kujua barabara fulani itakuongoza wapi kabla ya kuanza kuifuata. Watu fulani wamejutia sana maamuzi waliyofanya. Huenda hata wewe umewahi kusema, ‘Laiti ningejua jinsi mambo yangekuwa, ningefanya mambo kwa njia tofauti.’

Msafiri mwenye uzoefu unataka kujua mahali ambapo kila barabara inaelekeza. Huenda akachunguza ramani na kuzungumza na watu wanaofahamu eneo analozuru. Atahakikisha kwamba anatazama vibao anavyopata njiani. Hata hivyo, katika safari ya maisha ni jinsi gani unaweza kuwa na hakika kuhusu njia unayopaswa kufuata? Kuhusu Waisraeli wa kale, Mungu alisema hivi wakati mmoja kupitia Musa: “Laiti wangalikuwa wenye hekima! Ndipo wangalifikiria hili kwa uzito. Wangaliufikiria mwisho wao baadaye.”—Kumbukumbu la Torati 32:29.

Mashauri Bora

Hatuhitaji kukisia kuhusu ‘mwisho baadaye’ wa njia ya maisha. Mungu ndiye anayefaa zaidi kuwashauri wanadamu kuhusu barabara bora. Ameona njia mbalimbali ambazo wanadamu wamepitia na ameona matokeo yake. Biblia inasema: “Njia za mwanadamu ziko mbele za macho ya Yehova, naye anayatafakari mapito yake yote.”—Methali 5:21.

Yehova anawajali wale wanaompenda. Kupitia Neno lake, Biblia, anaonyesha njia inayofaa. Tunasoma hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” Kwa hiyo, kabla ya kuanza safari yoyote, ni jambo la hekima kutafuta mashauri ya Yehova, kama alivyofanya Mfalme Daudi wa Israeli la kale aliyesali hivi: “Unijulishe njia ninayopaswa kuitembea.”—Zaburi 32:8; 143:8.

Ukifuata njia unayoonyeshwa na msafiri anayetegemeka na mwenye uzoefu, unaweza kuwa na uhakika na kuhisi salama. Huhitaji kuwa na wasiwasi kuhusu unakoelekea. Daudi aliomba na kufuata mwongozo wa Yehova. Kwa sababu hiyo, alifurahia amani ya akili inayoelezewa kwa njia yenye kupendeza katika Zaburi ya 23 inayojulikana sana. Daudi aliandika hivi: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote. Ananilaza katika malisho yenye majani mengi; ananiongoza kando ya mahali pa kupumzika palipo na maji ya kutosha. Anaiburudisha nafsi yangu. Ananiongoza katika mapito ya uadilifu kwa ajili ya jina lake. Hata ingawa ninatembea katika bonde lenye kivuli kizito, siogopi chochote kibaya.”—Zaburi 23:1-4.

Watakuwa na Wakati Ujao wa Aina Gani?

Msafiri mmoja kwenye barabara ya maisha alikiri kwamba ‘karibu ageuke kando’ kutoka kwa njia inayofaa. Huenda mtunga-zaburi huyo alikuwa Asafu au mmoja wa wazao wake. Ni nini kilichokuwa kimetokea? Alikuwa ameona ufanisi wa watu wasio wanyoofu na wenye jeuri na alionea wivu “amani ya watu waovu.” Kwa maoni yake walionekana kuwa “waliostarehe mpaka wakati usio na kipimo.” Jambo baya hata zaidi, mtunga-zaburi huyo alikuwa ameanza kushuku hekima ya kufuata njia ya uadilifu ambayo alikuwa amechagua.—Zaburi 73:2, 3, 6, 12, 13.

Kisha mtunga-zaburi huyo akaingia katika patakatifu pa Yehova na kusali akifikiria mwisho wa waovu. “Nilitaka kuutambua wakati wao ujao,” akasema. Alitafakari mambo ambayo yangewapata watu aliokuwa akiwaonea wivu. Wangekuwa na wakati ujao wa aina gani? Alitambua kwamba watu kama hao walikuwa “kwenye udongo unaoteleza” na ‘wangemalizwa kwa matisho ya ghafula!’ Namna gani kuhusu barabara ambayo mtunga-zaburi alikuwa akifuata? Alisema hivi: “Baadaye [Yehova] utanipeleka kwenye utukufu.”—Zaburi 73:17-19, 24.

Kufikiria kuhusu matokeo ya matendo ya wale wanaopata ufanisi kwa njia zisizo halali au zinazotiliwa shaka kulimhakikishia mtunga-zaburi kuwa alikuwa kwenye njia inayofaa. Alifikia mkataa huu: “Lakini mimi, kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.” Sikuzote, kumkaribia Yehova Mungu kunaleta faida zenye kudumu.—Zaburi 73:28.

“Fikiria Njia Utakayochukua”

Leo tunaweza kukabili maamuzi kama hayo. Huenda ukapewa kandarasi yenye kupendeza ya biashara, ukapandishwa cheo, au ukaalikwa kuwa mshiriki katika biashara yenye faida. Bila shaka, hakuna biashara mpya isiyokuwa na hatari zake. Hata hivyo, je, huoni umuhimu wa kufikiria ‘mwisho baadaye’ wa uamuzi utakaofanya? Huenda kukawa na matokeo gani? Je, utahitajika kuwa mbali na nyumbani, na hivyo kumfanya mwenzi wako au wewe mwenyewe ufadhaike? Je, utashirikiana na wafanyakazi, wahudumu wa hoteli, au watu wengine wasio na tabia nzuri? Kwa kuchunguza kwa makini njia unayotaka kufuata, utaweza kufanya uamuzi wenye hekima. Tii shauri hili la Sulemani: “Fikiria njia utakayochukua.”—Methali 4:26, Biblia Habari Njema.

Sisi sote tunapaswa kutafakari shauri hilo, lakini vijana hasa ndio wanaopaswa kufanya hivyo. Kijana mmoja alikodi video ambayo alijua ilikuwa na picha zenye kuamsha hamu ya ngono. Baadaye alisimulia kwamba alipotazama video hiyo, hamu yake ya ngono iliamshwa sana hivi kwamba akamwendea kahaba aliyekuwa akiishi karibu na kwao. Hatimaye alisumbuka moyoni, alikuwa na dhamiri iliyochafuka, na wasiwasi kuhusu uwezekano wa kupatwa na magonjwa. Kilichotukia kinalingana na ufafanuzi huu wa Biblia: “Ghafula kijana huyo akamfuata, kama ng’ombe-dume anayeenda machinjoni.” Laiti angefikiria ‘mwisho baadaye’!—Methali 7:22, 23.

Fuata Vibao Barabarani

Watu wengi wanakubali kwamba si jambo la hekima kupuuza vibao barabarani. Hata hivyo, inasikitisha kwamba watu fulani wanapuuza vibao hivyo katika barabara ya maisha ikiwa hawakubaliani na mwongozo unaotolewa. Fikiria kisa cha Waisraeli fulani katika siku za Yeremia. Taifa hilo lilihitaji kufanya uamuzi na Yehova Mungu aliwashauri hivi: ‘Ulizeni kuhusu barabara za zamani za kale, mahali ambapo sasa pana njia nzuri; na mtembee ndani yake.’ Lakini watu hao walisema kwa ukaidi kuwa ‘hawatatembea’ katika njia hiyo. (Yeremia 6:16) Ni nini uliokuwa ‘mwisho baadaye’ wa kufuata njia hiyo ya uasi? Mnamo 607 K.W.K., Wababiloni walikuja na kuharibu kabisa jiji la Yerusalemu na kuwapeleka wakaaji wake Babiloni kuwa mateka.

Hatutafaidika kamwe tukipuuza vibao ambavyo Mungu ameweka. Maandiko yanatuhimiza hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”—Methali 3:5, 6.

Baadhi ya maonyo ya Mungu ni kama ishara zinazosema “Usiingie.” Kwa mfano, Biblia inasema: “Usiingie katika pito la waovu, wala usitembee na kuingia moja kwa moja katika njia ya wabaya.” (Methali 4:14) Moja kati ya njia zinazodhuru ni ile inayofafanuliwa katika Methali 5:3, 4: “Midomo ya mwanamke mgeni hudondoka-dondoka kama sega la asali, nalo kaakaa lake ni laini kuliko mafuta. Lakini matokeo yake ni machungu kama pakanga; ni makali kama upanga wenye makali kuwili.” Kwa watu fulani, kufanya ngono na kahaba au mtu mwingine asiye mwenzi wao ni jambo la kusisimua. Lakini kupuuza ishara zinazosema “Usiingie” zinazoelekeza mwenendo wa maadili kunaweza kusababisha msiba.

Kabla ya kuchukua hatua ya kwanza kufuata barabara yenye ishara “Usiingie,” jiulize, ‘Inanielekeza wapi?’ Kufikiria jinsi ‘mwisho baadaye’ unavyoweza kuwa kunatosha kukuzuia usifuate njia inayoweza kuwa na matokeo mabaya. UKIMWI na magonjwa mengine ya zinaa, mimba zisizotakikana, utoaji-mimba, mahusiano yaliyoharibika, na dhamiri zilizochafuka ni matokeo mabaya yanayowapata wale wanaopuuza ishara hizo. Mwisho wa barabara kwa wanaojihusisha katika ukosefu wa maadili unaelezwa waziwazi na mtume Paulo. “Hawataurithi ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10.

“Hii Ndiyo Njia”

Nyakati nyingine ni vigumu kuona mahali njia fulani inatuelekeza. Hivyo, tunamshukuru Mungu kwa kutujali kwa upendo na kutupa mwongozo ulio wazi! “Hii ndiyo njia,” Yehova amesema, “tembeeni ndani yake.” (Isaya 30:21) Njia ambayo Yehova anatuonyesha inaelekeza wapi? Ingawa barabara hiyo ni nyembamba na yenye magumu, Yesu alisema kwamba inaongoza kwenye uzima wa milele.—Mathayo 7:14.

Tenga wakati ufikiri kuhusu njia unayotumia. Je, ndiyo njia inayofaa? Inaelekea wapi? Sali ili upate mwongozo wa Yehova. Chunguza ‘ramani,’ yaani, Biblia. Huenda pia ukaona uhitaji wa kuzungumza na msafiri mwenye uzoefu ambaye amekuwa akijitahidi kutembea katika njia ya Mungu. Ukiona uhitaji wa kubadili mwelekeo, fanya hivyo haraka.

Mara nyingi msafiri anatiwa moyo anapoona kibao kinachomhakikishia kwamba anafuata barabara inayofaa. Ukijichunguza na uone kwamba unatembea katika njia ya uadilifu, endelea kufanya hivyo. Sehemu ya safari inayothawabisha zaidi iko karibu.—2 Petro 3:13.

Kila njia inaongoza mahali fulani. Utakapofika mwisho wa njia uliyochagua, utakuwa wapi? Hutafaidika ukianza kusema, ‘Laiti ningalichagua njia nyingine!’ Kwa hiyo, kabla ya kupiga hatua nyingine maishani, jiulize, ‘Ni nini utakaokuwa “mwisho baadaye”?’

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Ni Nini Utakaokuwa ‘Mwisho Baadaye’?

Mara nyingi vijana wanakabiliwa na vishawishi na mikazo ya kufanya mambo yanayofanywa na wengi. Haya ni baadhi ya mambo yanayoweza kutokea.

Kijana mmoja anakuambia huna ujasiri wa kuvuta sigara.

Mwalimu mwenye nia nzuri anakuhimiza ufuatilie elimu ya juu katika chuo kikuu.

Unaalikwa kwenye karamu itakayokuwa na vileo na huenda dawa za kulevya zitapatikana kwa wingi pia.

“Mbona usiweke anwani na maelezo ya kibinafsi kwenye Intaneti?” mtu fulani anakudokezea.

Rafiki anakualika ukatazame sinema yenye jeuri au ukosefu wa maadili.

Ikiwa utakabiliwa na hali kama hizo, utafanya nini? Je, utakubali tu au utafikiria kwa uangalifu ‘mwisho baadaye’ utakuwa jinsi gani? Litakuwa jambo la hekima kujiuliza hivi: “Je, mtu anaweza kukusanya moto kifuani pake na mavazi yake yasiungue? Au je, mtu anaweza kutembea juu ya makaa ya moto na miguu yake mwenyewe isiungue?”—Methali 6:27, 28.