Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tulitumie Jina la Mungu Ikiwa Hatujui Linavyopaswa Kutamkwa?

Kwa Nini Tulitumie Jina la Mungu Ikiwa Hatujui Linavyopaswa Kutamkwa?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Kwa Nini Tulitumie Jina la Mungu Ikiwa Hatujui Linavyopaswa Kutamkwa?

Leo, hakuna mtu anayeweza kujua kabisa jinsi jina la Mungu lilivyotamkwa katika Kiebrania cha kale. Hata hivyo, ni jambo muhimu kujua kwamba jina la kibinafsi la Mungu linapatikana mara 7,000 hivi katika maandishi ya Biblia. Yesu alijulisha jina la Mungu alipokuwa duniani na akawafundisha wanafunzi wake wasali kwamba jina hilo litakaswe. (Mathayo 6:9; Yohana 17:6) Hivyo, ni wazi kwamba ni muhimu sana kwa Wakristo kutumia jina la Mungu. Kwa nini basi haijulikani kabisa jinsi ambavyo jina hilo lilitamkwa awali? Kuna sababu mbili kuu.

Kwanza, miaka elfu mbili hivi iliyopita, kulitokea ushirikina miongoni mwa Wayahudi kwamba ni kosa kulitamka jina la Mungu. Msomaji alipopata jina hilo katika Biblia alisema “Bwana.” Katika njia hiyo, baada ya karne nyingi za kutotumia jina hilo, watu walisahau jinsi ya kutamka jina la Mungu.

Pili, Kiebrania cha kale kiliandikwa bila vokali, kama tu maneno yanavyofupishwa katika Kiswahili na katika lugha nyingine. Mtu alipokuwa akisoma maandishi, angejiingizia vokali. Baada ya muda, mfumo ulianzishwa ili kuzuia watu wasisahau kabisa jinsi ya kutamka maneno ya Kiebrania. Alama zilitiwa mahali ambapo vokali zilipaswa kuwa kwenye kila neno katika Biblia ya Kiebrania. Hata hivyo, mahali ambapo jina la Mungu lilipatikana, alama za vokali hazikutiwa mahali hapo au alama za vokali za jina “Bwana” ziliongezwa ili kumkumbusha msomaji atamke neno hilo la badala.

Hivyo, kile kilichobaki ni konsonanti nne zinazoitwa Tetragramatoni, ambazo kamusi moja inazifafanua kuwa “herufi nne za Kiebrania ambazo kwa kawaida hutoholewa kuwa YHWH au JHVH zinafanyiza jina la kibiblia la Mungu.” Inaeleweka kwa nini herufi YHWH, zikiwa na alama za vokali, zinakuwa “Yehova,” jina ambalo linajulikana sana na kukubaliwa katika Kiswahili.

Hata hivyo, wasomi fulani wanapendekeza kwamba jina hilo litamkwe “Yahweh.” Je, matamshi hayo yanakaribia kupatana na yale ya awali? Hakuna mtu anayejua kwa hakika. Kwa kweli, wasomi wengine wametoa sababu fulani za kuepuka matamshi hayo. Bila shaka, majina ya Biblia, yanapotamkwa katika lugha za kisasa, huenda hayatamkwi kama Kiebrania cha awali, na hakuna mtu anayelalamika. Ni kwa sababu tumezoea kuyatumia majina hayo na tunaweza kuyatambua kwa urahisi. Ndivyo ilivyo na jina Yehova.

Wakristo wa karne ya kwanza waliitwa watu kwa ajili ya jina la Mungu. Waliwahubiria watu kuhusu jina hilo na kuwatia moyo waliitie. (Matendo 2:21; 15:14; Waroma 10:13-15) Ni wazi kwamba Mungu analiona kuwa jambo muhimu kutumia jina lake katika lugha yoyote tunayozungumza, tutambue maana yake, na kuishi kupatana na kinachowakilishwa na jina hilo.

[Blabu katika ukurasa wa 31]

Ni jambo muhimu kujua kwamba jina la kibinafsi la Mungu linapatikana mara 7,000 hivi katika maandishi ya Biblia