Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni “Mwokoaji” Wetu

Yehova Ni “Mwokoaji” Wetu

Yehova Ni “Mwokoaji” Wetu

“Yehova atawasaidia na kuwaokoa.”—ZAB. 37:40.

1, 2. Ni ukweli gani wa msingi kumhusu Yehova ambao unatufariji na kututia nguvu?

KIVULI hakibaki palepale. Kadiri dunia inavyozunguka, vivuli vinavyosababishwa na jua vinasonga na kubadilika. Hata hivyo, Muumba wa dunia na jua, habadiliki. (Mal. 3:6) Biblia inasema, “naye habadiliki, kama kugeuka kwa kivuli.” (Yak. 1:17) Bila shaka, ukweli huo wa msingi kumhusu Yehova unatufariji na kututia nguvu, hasa tunapopatwa na majaribu na matatizo mazito. Kwa nini?

2 Kama tulivyoona katika habari iliyotangulia, Yehova alithibitika kuwa “Mwokoaji” katika nyakati za Biblia. (Zab. 70:5) Yehova habadiliki na sikuzote anatimiza ahadi zake; hivyo, waabudu wake leo wanaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba “atawasaidia na kuwaokoa.” (Zab. 37:40) Yehova amewaokoa jinsi gani watumishi wake leo? Anaweza kutuokoa jinsi gani sisi binafsi?

Kukombolewa Kutoka kwa Wapinzani

3. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba wapinzani hawataweza kuwazuia watu wa Yehova wasihubiri habari njema?

3 Hata Shetani akileta upinzani wa aina gani hawezi kamwe kuwazuia Mashahidi wa Yehova wasimwabudu Yehova kwa moyo wote kama anavyostahili kuabudiwa. Neno la Mungu linatuhakikishia hivi: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu.” (Isa. 54:17) Wapinzani wamejaribu kuwazuia watu wa Mungu wasihubiri lakini wameshindwa. Fikiria mifano miwili.

4, 5. Watu wa Yehova walipata upinzani gani mwaka wa 1918, na matokeo yalikuwa nini?

4 Mwaka wa 1918, watu wa Yehova walipata mateso mengi yaliyochochewa na makasisi ambao walitaka kuikomesha kazi ya kuhubiri. Mnamo Mei (Mwezi wa 5) 7, serikali ilitoa hati ya kumkamata J. F. Rutherford, ambaye alikuwa akisimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote wakati huo, na hati za kuwakamata ndugu wengine wa makao makuu. Kwa muda usiozidi miezi miwili, Ndugu Rutherford na washiriki wenzake walishtakiwa isivyo haki kwamba walipanga njama, kisha wakahukumiwa vifungo virefu vya gereza. Je, wapinzani walikuwa wamefanikiwa kutumia mahakama kukomesha kabisa kazi ya kuhubiri? Bila shaka hapana!

5 Kumbuka ahadi ya Yehova: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa.” Mambo yalibadilika ghafula Machi 26, 1919 (26/3/1919)—miezi tisa baada ya Ndugu Rutherford na washiriki wenzake kuhukumiwa—wakati ambapo ndugu hao waliachiliwa kwa dhamana. Mwaka uliofuata, Mei 5, 1920 (5/5/1920), mashtaka yaliyoletwa juu yao yalifutiliwa mbali. Ndugu hao walitumia uhuru wao kuendelea na kazi ya Ufalme. Matokeo yamekuwa nini? Tangu wakati huo kumekuwa na ongezeko kubwa sana! Yule “Mwokoaji” ndiye anayestahili kusifiwa kwa ajili ya ongezeko hilo.—1 Kor. 3:7.

6, 7. (a) Ni kampeni gani ya kuwaangamiza Mashahidi wa Yehova iliyoanzishwa katika Ujerumani ya Wanazi, na matokeo yalikuwa nini? (b) Historia ya watu wa Yehova leo inathibitisha jambo gani la hakika?

6 Sasa fikiria mfano wa pili. Mwaka wa 1934, Hitler aliapa kuwaangamiza kabisa Mashahidi wa Yehova huko Ujerumani. Halikuwa tishio tu, aliazimia kufanya hivyo. Mashahidi wengi walikamatwa na kufungwa gerezani. Maelfu ya Mashahidi waliteswa; mamia waliuawa katika kambi za mateso. Je, Hitler alifaulu katika kampeni yake ya kuwaangamiza Mashahidi? Je, alikomesha kabisa kazi ya kuhubiri habari njema huko Ujerumani? Alishindwa kabisa! Wakati wa mateso hayo, ndugu zetu waliendelea kuhubiri kisirisiri. Baada ya kuanguka kwa utawala wa Wanazi, walitumia uhuru wao kuendelea kuhubiri. Leo, kuna wahubiri wa Ufalme zaidi ya 165,000 nchini Ujerumani. Kwa mara nyingine tena, yule “Mwokoaji” ametimiza ahadi yake: “Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa.”

7 Historia ya Mashahidi wa Yehova leo inathibitisha kwamba Yehova hataruhusu kamwe watu wake waangamizwe wakiwa kikundi. (Zab. 116:15) Namna gani tukiwa mtu mmoja-mmoja? Yehova anatuokoa sisi binafsi jinsi gani?

Namna Gani Kuhusu Kulindwa Kimwili?

8, 9. (a) Tunajua jinsi gani kwamba Yehova hajaahidi kumlinda kila mmoja wetu kimwili kwa sasa? (b) Ni jambo la akili kukubali nini?

8 Tunajua kwamba Yehova hajaahidi kumlinda kila mmoja wetu kimwili kwa sasa. Msimamo wetu ni kama wa wale Waebrania watatu waaminifu ambao walikataa kuiinamia sanamu ya dhahabu ya Mfalme Nebukadneza. Vijana hao waliomwogopa Mungu hawakumtazamia Yehova awaokoe kimuujiza wasipate madhara ya kimwili. (Soma Danieli 3:17, 18.) Ingawa hivyo, Yehova aliwaokoa kutokana na miale ya moto wa tanuru. (Dan. 3:21-27) Lakini, hata katika nyakati za Biblia, ni watu wachache sana waliookolewa kimuujiza. Wapinzani waliwaua watumishi wengi waaminifu wa Yehova.—Ebr. 11:35-37.

9 Namna gani leo? Akiwa “Mwokoaji,” bila shaka Yehova anaweza kumwokoa mtu mmoja-mmoja kutoka katika hatari. Je, tunaweza kusema kwa uhakika kwamba Yehova amewaokoa au hakuwaokoa watu fulani? Hapana. Hata hivyo, mtu ambaye ameokoka hali ya hatari anaweza kuhisi kwamba Yehova alimsaidia. Lingekuwa jambo la kimbelembele kwa wengine kukataa maoni yake. Hata hivyo, ni jambo la akili kukubali pia kwamba Wakristo wengi waaminifu wamekufa kwa sababu ya kuteswa, kama ilivyokuwa wakati wa Wanazi. Wengine wamekufa katika misiba. (Mhu. 9:11) Tunaweza kuuliza hivi: ‘Je, Yehova alishindwa kuwa “Mwokoaji” wa watu waaminifu ambao waliuawa au kufa katika msiba?’ Hilo si kweli.

10, 11. Kwa nini wanadamu hawana uwezo wa kuzuia kifo, lakini Yehova anaweza kufanya nini kuelekea kifo?

10 Fikiria jambo hili: Mwanadamu hana uwezo wa kuzuia kifo, kwa kuwa hakuna mwanadamu anayeweza “kuiokoa nafsi yake katika mkono wa Kaburi.” (Zab. 89:48) Namna gani Yehova? Dada mmoja aliyeokoka nyakati zenye hatari za Wanazi anakumbuka maneno haya aliyoambiwa na mama yake Shahidi aliyekuwa akimfariji baada ya wapendwa wao kuuawa katika kambi za mateso: “Kama wanadamu wangekuwa watumwa wa kifo milele, basi kifo kingekuwa na nguvu kuliko Mungu, sivyo?” Ni wazi kwamba kifo hakina nguvu kuliko Mungu mwenye nguvu zote ambaye ndiye Chanzo cha uhai! (Zab. 36:9) Watu wote walio katika Kaburi, wako katika kumbukumbu ya Yehova, na atamwokoa kila mmoja wao.—Luka 20:37, 38; Ufu. 20:11-14.

11 Kwa sasa, Yehova anahusika moja kwa moja katika maisha ya waabudu wake waaminifu leo. Acheni sasa tuchunguze njia tatu ambazo zinaonyesha wazi kwamba yeye ni “Mwokoaji” wetu.

Tunalindwa Kiroho

12, 13. Kwa nini ulinzi wa kiroho ndio wa maana zaidi, na Yehova anatulinda kiroho jinsi gani?

12 Yehova anatupa ulinzi wa kiroho ambao ndio wa maana zaidi. Tukiwa Wakristo wa kweli, tunajua kwamba kuna kitu ambacho ni chenye thamani zaidi kuliko uhai wetu wa sasa. Uhusiano wetu mzuri pamoja na Yehova ndicho kitu chenye thamani zaidi tulicho nacho. (Zab. 25:14; 63:3) Kama hatungekuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova, uhai wetu wa sasa haungekuwa na maana yoyote na hatungekuwa na tumaini lolote la wakati ujao.

13 Tunathamini kwamba Yehova anatupa msaada wowote tunaohitaji ili kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Neno lake, roho yake takatifu, na kutaniko lake la ulimwenguni pote linatusaidia. Tunaweza kufanya nini ili tufaidike kabisa kutokana na maandalizi hayo? Tukijifunza Neno lake kwa bidii na kwa ukawaida, tutaitia nguvu imani yetu na tumaini letu. (Rom. 15:4) Tukisali kutoka moyoni ili tupate roho yake, atatusaidia kushinda kishawishi cha kujiendesha kwa njia isiyofaa. (Luka 11:13) Tukifuata mwongozo ambao jamii ya mtumwa mwaminifu inatoa kupitia vichapo vinavyotegemea Biblia, mikutano, na makusanyiko, tutalishwa ‘chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.’ (Mt. 24:45) Maandalizi kama hayo yanatulinda kiroho na kutusaidia kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu.—Yak. 4:8.

14. Simulia kisa kinachoonyesha jinsi Yehova anavyotulinda kiroho.

14 Ili kuonyesha jinsi Yehova anavyotulinda kiroho, kumbuka wale wazazi waliotajwa mwanzoni mwa habari iliyotangulia. Siku chache baada ya binti yao, Theresa, kuripotiwa kwamba amepotea, walipata habari zenye kuhuzunisha sana: Alikuwa ameuawa. * Baba yake anakumbuka hivi: “Nilimwomba Yehova amlinde. Alipopatikana akiwa ameuawa, nakubali kwamba mwanzoni nilijiuliza kwa nini sala zangu hazikujibiwa. Bila shaka, ninajua kwamba Yehova hajaahidi kuwalinda kimuujiza watu wake mmoja-mmoja kwa sasa. Niliendelea kusali ili nielewe jambo hilo. Nimefarijiwa kujua kwamba Yehova anawalinda watu wake kiroho—yaani, yeye anaandaa tunachohitaji ili kulinda uhusiano wetu pamoja naye. Ulinzi huo ndio wa maana zaidi, kwa kuwa wakati wetu ujao wa milele unategemea ulinzi huo. Katika maana hiyo, Yehova alimlinda Theresa; alimtumikia kwa uaminifu mpaka alipokufa. Nimepata amani kwa kujua kwamba matarajio yake ya kuishi wakati ujao yako mikononi mwa Yehova mwenye upendo.”

Kutegemezwa Tunapokuwa Wagonjwa

15. Yehova anaweza kutusaidia katika njia gani mbalimbali tunapolemewa na ugonjwa?

15 Yehova anaweza kututegemeza “katika kitanda cha ugonjwa,” kama alivyomtegemeza Daudi. (Zab. 41:3) Ingawa Yehova hatuponyi kimuujiza leo, anatusaidia. Jinsi gani? Kanuni zilizo katika Neno lake zinaweza kutusaidia kufanya maamuzi yenye hekima kuhusu matibabu na mambo mengine. (Met. 2:6) Tunaweza kupata mapendekezo mazuri sana na yenye faida katika habari zinazochapishwa katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zinazozungumza kuhusu ugonjwa wetu. Kupitia roho yake, Yehova anaweza kutupa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili tukabiliane na hali yetu na kudumisha utimilifu wetu katika hali zozote zile. (2 Kor. 4:7) Kwa msaada wake, tunaweza kuepuka kukazia fikira sana ugonjwa wetu na kupuuza mambo ya kiroho.

16. Ndugu mmoja amekabiliana jinsi gani na ugonjwa?

16 Mfikirie ndugu kijana aliyetajwa mwanzoni mwa habari iliyotangulia. Katika mwaka wa 1998, iligunduliwa kwamba ana ugonjwa wa mishipa ya fahamu (amyotrophic lateral sclerosis) ambao mwishowe ulimfanya apooze kabisa. * Amekabiliana jinsi gani na ugonjwa huo? Anaeleza hivi: “Mara kwa mara nimehisi uchungu na kuvunjika moyo na kuhisi kwamba kifo ndiyo njia pekee ya kupata kitulizo. Ninapojihisi kwamba nimelemewa, ninasali kwa Yehova na kumwomba vitu vitatu: moyo mtulivu, subira, na uvumilivu. Ninahisi kwamba Yehova amejibu sala zangu. Kuwa na moyo mtulivu kunaniwezesha kutafakari kuhusu mambo yenye kufariji, kama vile maisha katika ulimwengu mpya wakati ambapo nitaweza kutembea, kufurahia chakula kitamu, na kuzungumza na familia yangu tena. Subira inanisaidia kuvumilia hali ngumu na matatizo ya kupooza. Uvumilivu unaniwezesha kuendelea kuwa mwaminifu na kutopoteza usawaziko wangu wa kiroho. Kwa kweli ninaweza kusema kama mtunga-zaburi Daudi, kwa kuwa ninahisi kwamba Yehova amenitegemeza katika kitanda cha ugonjwa.”—Isa. 35:5, 6.

Tunaandaliwa Mahitaji ya Lazima

17. Yehova ameahidi atatufanyia nini, na ahadi hiyo inamaanisha nini?

17 Yehova anaahidi kwamba atatutunza kimwili. (Soma Mathayo 6:33, 34 na Waebrania 13:5, 6.) Hilo halimaanishi kwamba mahitaji yetu yatatoshelezwa kimuujiza au kwamba hatupaswi kufanya kazi. (2 The. 3:10) Ahadi hiyo inamaanisha hivi: Tukitafuta Ufalme wa Mungu kwanza katika maisha yetu na kuwa tayari kufanya kazi ili tupate riziki, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatusaidia kupata mahitaji ya lazima ya maisha. (1 The. 4:11, 12; 1 Tim. 5:8) Anaweza kutuandalia vitu tunavyohitaji kwa njia ambazo hatutazamii, labda anaweza kumtumia mwabudu mwenzetu kutusaidia au kutupa kazi ya kimwili.

18. Simulia jambo halisi linaloonyesha kwamba tunaweza kutunzwa tunapokuwa na uhitaji.

18 Mkumbuke yule mama asiye na mwenzi aliyetajwa mwanzoni mwa habari iliyotangulia. Wakati yeye na binti yake mdogo walipohamia eneo lingine, haikuwa rahisi kwake kupata kazi. Anaeleza hivi: “Nilienda kwenye utumishi wa shambani asubuhi, na kutafuta kazi kila siku wakati wa mchana. Ninakumbuka siku moja nilienda dukani kununua maziwa. Nilisimama na kuangalia mboga zilizokuwa dukani, lakini sikuwa na pesa za kutosha kununua mboga zozote. Sijawahi kamwe kushuka moyo hivyo katika maisha yangu. Niliporudi kutoka dukani siku hiyo, nilipata mifuko mingi yenye mboga za kila aina ikiwa imewekwa nyuma ya nyumba yangu. Tulipata chakula cha kututosha kwa miezi mingi. Nililia na kumshukuru Yehova.” Baadaye, dada huyo alipata habari kwamba mifuko hiyo ililetwa na ndugu mmoja wa kutaniko lao ambaye alipanda mboga katika shamba lake. Dada huyo alimwandikia hivi baadaye: “Hata ingawa nilikushukuru sana siku hiyo, nilimshukuru Yehova pia kwa sababu alitumia fadhili zako kunikumbusha kwamba ananipenda.”—Met. 19:17.

19. Watumishi wa Yehova watakuwa na uhakika gani wakati wa dhiki kuu, na tunapaswa kuazimia kufanya nini sasa?

19 Ni wazi kwamba yale ambayo Yehova alifanya katika nyakati za Biblia na pia katika siku zetu yanatufanya tumtegemee akiwa Msaidizi wetu. Hivi karibuni, wakati dhiki kuu itakapokuja juu ya ulimwengu wa Shetani, tutahitaji msaada wa Yehova kuliko wakati mwingine wowote. Hata hivyo, watumishi wa Yehova watamtegemea wakiwa na uhakika kamili. Watainua vichwa vyao na kushangilia, wakijua kwamba ukombozi wao unakaribia. (Luka 21:28) Hata tukipata majaribu gani sasa, acheni tuazimie kumtegemea Yehova, tukiwa na uhakika kabisa kwamba Mungu wetu asiyebadilika, kwa kweli, ni “Mwokoaji” wetu.

[Maelezo ya Chini]

Je, Unakumbuka?

• Yehova anaweza kuwaokoa jinsi gani wale ambao wameuawa au kufa katika misiba?

• Kwa nini ulinzi wa kiroho ndio wa maana zaidi?

• Ahadi ya Yehova ya kwamba atatutunza kimwili inamaanisha nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Ndugu Rutherford na washiriki wenzake walikamatwa mwaka wa 1918 na baadaye wakaachiliwa, na mashtaka yaliyoletwa juu yao yakafutiliwa mbali

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yehova anaweza kututegemeza katika “kitanda cha ugonjwa”