Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Katika barua yake kwa Waebrania, mtume Paulo alisema kuhusu “kuwekewa mikono.” Je, alikuwa akizungumza kuhusu kuweka rasmi wazee au alikuwa akizungumzia jambo lingine tofauti?—Ebr. 6:2.

Ingawa hatuwezi kusema kwa uhakika, inaelekea Paulo alikuwa akizungumza kuhusu kuwawekea waamini mikono ili wapate zawadi za roho.

Biblia inasema kuhusu kuwekewa mikono kuhusiana na mtu kuwekwa rasmi katika mapendeleo ya kitheokrasi. Musa ‘aliweka mkono wake juu ya’ Yoshua alipomweka Yoshua rasmi achukue nafasi yake. (Kum. 34:9) Katika kutaniko la Kikristo, wanaume waliokuwa na sifa za kustahili waliwekwa rasmi kwa kuwekewa mikono. (Mdo. 6:6; 1 Tim. 4:14) Paulo alishauri kutomwekea mtu yeyote mikono haraka-haraka.—1 Tim. 5:22.

Hata hivyo, Paulo aliwahimiza Wakristo Waebrania ‘wasonge mbele kuelekea ukomavu’ kwa kuwa sasa walikuwa wameliacha “fundisho la msingi.” Kisha, alitaja “kutubu matendo yaliyokufa, na imani kwa Mungu, fundisho juu ya mabatizo na kuwekewa mikono.” (Ebr. 6:1, 2) Je, kuwekwa rasmi kwa wazee kungekuwa jambo la msingi ambalo Wakristo wangepaswa kusonga mbele ili kulifikia? Hapana. Kuwa mzee wa kutaniko ni lengo ambalo ndugu wakomavu wanapaswa kujitahidi kulifikia na kisha kulithamini.—1 Tim. 3:1.

Hata hivyo, watu waliwekewa mikono katika hali nyingine. Katika karne ya kwanza, Yehova aliwakataa Waisraeli wa asili kuwa watu wake naye akawachagua Waisraeli wa kiroho, kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta. (Mt. 21:43; Mdo. 15:14; Gal. 6:16) Zawadi za kimuujiza za roho, kama vile kusema kwa lugha, zilithibitisha wazi badiliko hilo. (1 Kor. 12:4-11) Kornelio na watu wa nyumba yake walipogeuka na kuwa waamini, wapya hao walipokea roho takatifu, kama ilivyoonekana wazi ‘waliposema katika lugha.’—Mdo. 10:44-46.

Nyakati nyingine, zawadi za kimuujiza zilitolewa kwa kuwawekea watu mikono. Filipo alipohubiri habari njema huko Samaria, watu wengi walibatizwa. Baraza linaloongoza lilimtuma mtume Petro na Yohana huko. Kwa nini? Tunasoma hivi: “Ndipo [wawili hao] wakaanza kuweka mikono yao juu ya [watu waliobatizwa hivi karibuni], nao wakaanza kupokea roho takatifu.” Hilo lilimaanisha kwamba walipokea zawadi za roho, yaani, uwezo mbalimbali ambao ulionekana waziwazi. Tunajua hilo kwa sababu Simoni, ambaye hapo awali alikuwa akifanya ufundi wa uchawi, aliona uwezo huo wa roho na kwa pupa akajaribu kununua uwezo wa kuwawekea wengine mikono ili wapate roho takatifu na hivyo kuwawezesha kufanya miujiza. (Mdo. 8:5-20) Baadaye, watu 12 huko Efeso walibatizwa. Tunasoma hivi: “Paulo alipoweka mikono yake juu yao, roho takatifu ikaja juu yao, nao wakaanza kusema katika lugha na kutoa unabii.”—Mdo. 19:1-7; linganisha na 2 Timotheo 1:6.

Hivyo, kwenye Waebrania 6:2, inaelekea Paulo alikuwa akizungumza kuhusu kuwawekea waamini wapya mikono ili wapate zawadi za roho.